Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 4/8 kur. 11-14
  • Kazi Yangu Ilikuwa Kuvunja Nyumba Usiku

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kazi Yangu Ilikuwa Kuvunja Nyumba Usiku
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sikuzaliwa Nikiwa Mhalifu
  • Kwa Nini Nilichagua Maisha ya Uhalifu
  • Nimepata Kweli!
  • Kutoa Ushahidi Gerezani
  • Kuachiliwa na Kuazimia
  • Utoro Wangu Kuelekea Kweli
    Amkeni!—1994
  • Simba Angurumaye awa Kondoo Mpole
    Amkeni!—1999
  • Jinsi Ukweli Ulivyonibadili Nisiwe Mhalifu Niwe Mkristo
    Amkeni!—1990
  • Kumtumikia Mungu Nyakati za Magumu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 4/8 kur. 11-14

Kazi Yangu Ilikuwa Kuvunja Nyumba Usiku

NGO-ONG! Nyundo ya hakimu ikavuma katika chumba cha mahakama. Maneno yake yaliyofuata yalisikika kama mgurumo mkubwa kwangu, ingawa aliyasema kwa sauti nyororo. “Ninakuhukumu wewe kifungo cha miaka 15.” Sitasahau kamwe maneno hayo wala matukio yaliyofuata. Ofisa wa polisi alinipeleka kwa haraka kutoka chumba cha mahakama hadi kwenye seli iliyokuwa imekuwa makao yangu kwa muda wa miezi mitatu iliyopita.

Mapema asubuhi iliyofuata, nilichukuliwa kutoka seli yangu, nikapelekwa kupitia ujia mwembamba hadi kwenye chumba kidogo, ambapo nilivalishwa mshipi wa ngozi uliokuwa wa sentimeta 13 upana na ukafungwa imara kwa nyuma. Upande wa mbele ulikuwa na vyuma viwili vya mviringo ambavyo mikono yangu ilifungiwa. Wale maofisa wawili walipomaliza utaratibu huo, walinipeleka kupitia kijia kingine, ambapo nilijiunga na kikundi cha wanaume waliofungwa pingu za mikono kama mimi. Wanaume hao walikuwa wamesimama katika mistari miwili, mmoja kando ya mwenzake. Nilipelekwa hadi kwenye nafasi yangu katika mstari mmoja, na mnyororo uliopita kati ya mistari hiyo miwili uliinuliwa na kufungwa kwenye chuma cha tatu cha mviringo, kilichokuwa kwenye upande mmoja wa mshipi huo wa ngozi.

Baadaye, maofisa sita walitupeleka hadi kwenye mtambo wa kupandisha vitu ambao ungetuchukua hadi kwenye basi iliyoundwa kwa njia ya kipekee. Ebu wazia nilikuwa nimeketi kando ya muuaji na mbele ya wachuuzi wa dawa za kulevya, wanajisi-watu, na majambazi. Sote tukielekea mahali pamoja—gerezani!

Huenda ukauliza, ni nini kilichoongoza kwenye hali hizo? Acha nikueleze juu ya maisha yangu ya mapema na matukio yaliyonipeleka gerezani.

Sikuzaliwa Nikiwa Mhalifu

Wazazi wangu walifunga ndoa baada tu ya Vita ya Ulimwengu ya 2, na katika 1947 kaka yangu akazaliwa. Miaka miwili baadaye mimi nilizaliwa, nikifuatwa na ndugu yangu mwingine miezi 18 baadaye. Hivyo wakiwa na watoto watatu, wazazi wangu walifunga safari ndefu ya magharibi kutoka Richmond, Virginia, U.S.A., kuelekea jimbo la Oregon katika Pwani ya Pasifiki. Halafu tukafunga safari ndefu kaskazini kuelekea Jimbo la Washington na kukaa katika mji wa Bellevue. Wakati huo, maisha yalionekana kuwa ya kawaida kwangu. Ingawa hatukuwa familia iliyounganika sana, tulikuwa na tafrija pamoja mara kwa mara na tulihudhuria kanisa la Kilutheri la mahali hapo. Lilikuwa jambo la kawaida kwa familia yenye kutoka Virginia kuwa na heshima kwa Mungu, Yesu, na Biblia. Katika Januari 1960 dada yangu mchanga alizaliwa. Jinsi mama yangu alivyofurahi kupata hatimaye kisichana hicho kidogo alichokuwa ametamani sana!

Hata hivyo, jambo fulani lilitukia miezi sita hivi baadaye lililobadili njia yetu ya maisha. Tulihama tena, wakati huu katika mji wenye miti mingi wa Bonde la Maple. Tuliacha kwenda kanisa, kulikuwa hakuna tena tafrija za familia, na baba yangu akaanza kunywa pombe sana. Mimi bado huhuzunika nikumbukapo kuhama kwetu. Tulishuka moyo muda mrefu sana baadaye. Ninaamini kwamba hilo lilichangia kwenye maisha yangu mapotovu nilipokuwa tineja.

Kwa Nini Nilichagua Maisha ya Uhalifu

Bonde la Maple, kama unavyoweza kuwazia kwa jina lenyewe tu, halikuwa sehemu ya kupendeza kwa tineja mwenye fujofujo wa miaka ya 1960. Hivyo ningetafuta mapendezi ya kujifurahisha mwenyewe. Hiyo ilikuwa rahisi kwangu kwa sababu ya ushirika mbaya niliokuwa nao shuleni. Shughuli za baada ya shule zingegeuka kuwa karamu za ulevi, zikifuatwa na vita vya ngumi na dawa za kulevya. Mara kadhaa katika visa kama hivi, ningejikokota nyumbani kama saa tisa au kumi za usiku—nikiwa nimelewa. Au singerudi nyumbani kwa siku kadha, nikikaa na marafiki zangu. La kushangaza ni kwamba, nilijua nilikuwa nafanya mabaya, na bado wazazi wangu hawakuonekana kuwa waliyaona hayo.

Nyakati nyingine, tungeiba ili kuona tu kama tungepatikana. Wakati mmoja, niliiba gari na kuliendesha ili kujifurahisha tu. Lakini nilikamatwa nikakaa zaidi ya mwaka mmoja katika shule ya kurekebi watoto watundu, iitwayo Green Hill.

Kufikia wakati nilipoachiliwa kutoka Green Hill, nilikuwa katika shule ya sekondari. Humo nikafikiri kwamba ningefanya yale “niliyojifunza” kutoka ‘shule ya uhalifu’ ya watoto. Sikutambua kamwe kwamba msemo wa Kibiblia unaosema, “Mashirika mabaya yanaharibu mazoea yenye mafaa,” ulikuwa unapata matokeo yake.—1 Wakorintho 15:33, New World Translation.

Nilikuwa na umri wa miaka 16 hivi nilipokutana na mtu tofauti, mwanaume mchanga Jim Carley. Hivi majuzi yeye na familia yake walikuwa wamehamia mji wa kwetu kutoka Idaho. Ni watu wachache sana waliomjua kwa jina Jim; alijulikana zaidi kwa jina Spud, jina la kupangiwa kutokana na kiazi kinachojulikana sana cha Idaho. Alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Jim nami tulienda shule ile ile moja. Kwa kumchunguza, ningeweza kuona kwamba alikuwa tofauti na marafiki zangu wengine. Yeye alikuwa na uhusiano mzuri na kila mtu lakini hakushiriki katika matendo yao maovu. Hili lilinivutia. Ninakumbuka akinieleza wazi kwa nini mfumo mwovu huu utakwisha karibuni na kubadilishwa na ulimwengu mpya wa amani chini ya utawala wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu.

Nilitaka nisikie mengi zaidi, hivyo nikahudhuria mara kadha “kanisa” lao, lililoitwa Jumba la Ufalme. Hiyo ilikuwa katika 1967. Yale niliyoyasikia huko yalikuwa ya kuvutia, lakini nilihisi kwamba ulimwengu huo mpya ulikuwa jambo la wakati ujao ulio mbali sana. Isitoshe, nilikuwa ninajifurahisha sasa. Nilikuwa katika biashara ya kutosheleza “maagizo” ya chochote kilichohitajiwa na yeyote—vifaa vya kazi, sehemu za gari, sterio, televisheni. Bila shaka, “maagizo” hayo yalitoshelezwa kwa wivi na ujanja. Kwa nini niende kwenye kanisa ambalo lililaumu “biashara” yangu yenye kufurahisha?

Nilipokuwa na umri wa miaka 19, niliacha kwenda shule nikaoa aliyekuwa mpenzi wangu katika shule ya sekondari. Mwaka mmoja baadaye nilikuwa baba ya mtoto msichana, Rhonda Jean. Nikiwa na jukumu hili la ziada, nilihisi nikiwa na uhitaji wa kuwaandalia lakini kupitia tu njia zisizo za unyofu.

Nimepata Kweli!

Nilikuwa ningali katika “biashara” ya kutumia na kuuza madawa ya kulevya, kuiba magari, na kuvunja nyumba usiku, lakini hatimaye “biashara” hiyo iliniletea hasara. Nilikamatwa na upesi nikajipata katika ile hali ya kufungwa pingu za mikono iliyoelezwa mbeleni na kuelekea gerezani. Ebu wazia, nilikuwa mwenye umri wa miaka 20, mwenye mke na msichana mchanga wa miezi sita. Na sasa nilikuwa naenda gerezani kwa miaka 15! Nikang’amua kwamba ilinipasa kufanya jambo fulani ili kudhibiti maisha yangu. Nikaanza kufikiria yale Spud aliyosema kuhusu Biblia.

Nilipokuwa gerezani, nikaanza kusoma Biblia pamoja na vitabu visivyo vya kidini vya kujielimisha. ‘Kusoma vitabu hivi kutanisaidia nikue,’ nikafikiri. Havikusaidia. Hakuna chochote kilichosaidia mpaka mfungwa mwingine katika Kituo cha Kurekebi Tabia katika Shelton, Washington, alipouliza kama ningependa kuwako kwenye mazungumzo ya Biblia pamoja na baadhi ya Mashahidi wa Yehova kutoka kundi la mahali hapo. Nilifahamishwa kuwa walikuja kwenye gereza kila juma. Nikakubali. Tangu nilipokutana kwa mara ya kwanza na Mashahidi hao wawili, nilijua kwamba nilichokuwa najifunza kutoka kwenye Biblia na kitabu cha mafunzo Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele kilikuwa kweli. Nilikuwa nimeipata kweli!

Kutoa Ushahidi Gerezani

Mara nyingine idadi kubwa ya wafungwa hata 15 wangejiunga nami katika mafunzo yangu ya Biblia pamoja na Mashahidi kila juma. Katika kipindi hiki mke wangu akaamua kuwa nilikuwa nimekuwa kichaa gerezani, na akaanza kutafuta talaka. Jambo hilo lilijaribu sana imani yangu mpya.

Nikaamua kuimarisha imani yangu kwa kula chakula cha kiroho zaidi. Nilianza kwa kusoma Biblia nzima pamoja na vichapo vya Kibiblia, kutia ndani makala za magazeti ya wakati uliopita za Mnara wa Mlinzi na Amkeni!. Nilikuwa ninakuza imani yenye nguvu. Pia, nilianza kuhubiria yeyote aliyesikiliza. Upesi nikaanza kuepukwa na wengi wa wafungwa. Ninapofikiria, ninaona kwamba hilo lilikuwa ni ulinzi halisi kwangu.

Hata hivyo, nilikuwa na mazungumzo mengi ya kupendeza pamoja na wengine gerezani. Moja lilikuwa ni pamoja na padri Mkatoliki, aliyesema kwamba nilikuwa ninafunzwa mambo yaliyopotolewa na kwamba watu wangeweza kufanya Biblia iseme chochote walichotaka. Ili kuthibitisha dai lake, alisema angenionyesha kwamba Biblia husema kwamba hakuna Mungu. Nilikubali anionyeshe. Alifungua Biblia yake kwenye kitabu cha Zaburi na kuweka mkono wake hivi kwamba kidole chake shahada kingeweza kufunika sehemu fulani ya mstari huo. Nikasema: “Tafadhali sogeza kidole chako niweze kusoma mstari wote.” Yeye akajibu: “Soma tu kilicho chini ya kidole changu.” Nilifanya hivyo, na kwa mshangao wangu ilisema: “Hakuna Mungu!” “Unaona,” yeye akasema, “uthibitisho ndio huo. Hakuna Mungu!” Mara nyingine nikamwomba nione mstari wote. Wakati huu aliondoa mkono wake. Na hapo ilisema: “Mpumbavu amesema moyoni, Hakuna Mungu.”—Zaburi 14:1.

Kuachiliwa na Kuazimia

Kwa sababu ya mtazamo na tabia yangu iliyobadilika, baada tu ya miaka miwili ya kufungwa niliachiliwa na kuahidi kwamba singetoroka. Hiyo ilikuwa mwishoni-mwishoni mwa 1971. Labda wengine walifikiri nilikuwa ‘nimekuwa wa dini’ ili tu kupumbaza kamati inayotoa idhini ya kurudi nyumbani. Lakini sasa nilikuwa huru na mwenye kuazimia kuliko wakati mwingine wowote kutoshirikiana tena na mashirika mabaya. Nilichagua kwa makusudi kuishi katika eneo ambamo nilijua washiriki wangu wa kwanza hawangekuwa. Nilijua halingekuwa jambo la hekima kuwasiliana na yeyote wa washiriki wangu wa zamani. Wao pia waliniepa kwa sababu walikuwa wamesikia kwamba nilikuwa nimekuwa kama “padri” na nilikuwa ninamhubiri kila mtu.

Niliendelea na mafunzo yangu ya Biblia na nikaanza kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya Kundi la Covington katika Kent, Washington. Kazi ya kuhubiri ikawa sehemu ya maana sana katika maisha yangu, na katika Juni 1972, nikabatizwa. Nilikuwa ninajaribu kuwa na usawaziko katika mambo ya kawaida na wakati ule ule nikimtumikia Mungu na kumfunza binti yangu Biblia. Alikuwa sasa anakaribia umri wa miaka mitatu na alikuwa anaishi na mama yake, mke wangu wa hapo kwanza. Lilithibitika kuwa jaribu la miaka 16 yenye mahangaiko. Nitakubali, kwamba kulikuwa na nyakati ambapo ningehisi kwamba mambo hayakuwa yanaenda kwa mwendo wa kasi kunitosheleza. Ndipo ningekumbuka shauri la Kimaandiko: “Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote. . . . Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana [Yehova, NW].”—Warumi 12:18, 19.

Siku nyingi nilikuwa nikilia na kusali. Ulimwengu wangu wa wakati huo ulikuwa kama hali ya hewa ya sehemu ya Puget Sound, isiyo na uangavu wa kuchangamsha, ikiwa na mwangaza wa jua mara kwa mara tu. ‘Mwangaza wangu wa jua’ uliangaza katika maana ya shughuli za kitheokrasi, kama vile mikutano na makusanyiko ambapo mtu aweza kupata marafiki wapya na kuwapata tena wale wa zamani. Katika moja la makusanyiko hayo, nilikutana na mmoja ambaye angenivutia sana, na baada ya miaka miwili ya kufahamiana, Mary Hughes nami tukaoana katika Agosti 1974.

Katika Julai ya mwaka uliofuata, tulipata mwana tuliyemwita Trey (kutokana na Tom wa 3). Nilijua kwamba katika ndoa hii, Mungu angekuwa wa kwanza nyakati zote, hasa kwa kuwa hivi majuzi tu nilikuwa nimewekwa kuwa mtumishi wa huduma katika kundi la Kikristo. Kwa sababu ya pendeleo hilo, niling’amua kwamba mlango mpya wa fursa ulikuwa wazi kwangu kwa utumishi wangu kwa Yehova. Niliazimia kuutumia kikamili na kuendelea kumtumikia. Nilijibidiisha, nyakati zote nikimtegemea Mungu anifunze jinsi ya kukua kiroho. Wakati wowote nilipoombwa kushughulikia mgawo fulani, ningekubali, nikimtumaini anipe hekima iliyohitajika. Halafu, katika 1987, nilipendekezwa kuwa mzee.

Baada ya kupita kwa miaka nimejifunza kwamba kufanya mambo kwa njia ya Yehova huwa ndio mwendo wa hekima zaidi nyakati zote. Usikose subira. Jambo hilo lilidhihirika kwangu zaidi wakati, katika masika ya 1990, binti yangu Rhonda, wakati huo akiwa na umri wa miaka 20, alipokuja nyumbani kuishi nasi na akawa Shahidi aliyebatizwa. Niliweza kukumbushwa tena jinsi kweli ilivyo na nguvu. Kwa sababu za utunzi wa kisheria, nilikuwa sijawasiliana naye kwa miaka minane iliyopita. Yehova alibariki jitihada zangu za miaka iliyopita nilipopanda mbegu za kweli ya Biblia katika binti yangu wakati wa ziara fupi zilizokubaliwa na mahakama.

Ilikuwa ni kama Rhonda alikumbuka karibu kila kitu ambacho Mary nami tulikuwa tumemfunza kuhusu Biblia. Maisha yetu ya familia yalikuwa yamemvutia wee! Tangu siku hiyo ya masika, Rhonda amefanya maendeleo ya haraka sana katika maarifa ya Biblia.

Ninapotazama nyuma kwenye aina ya maisha niliyokuwa nayo halafu nitazame jinsi yalivyo sasa, lazima niseme kwamba kuwa mwenye shughuli sana katika kumtumikia Mungu ndio ulinzi bora zaidi kutokana na mitego ya Shetani. Badala ya kuwa na ule mshipi wa ngozi wenye kuzuia niliouchukia sana, sasa ninaona uhuru mkubwa, uhuru kutoka kifungo hadi kwenye uhuru wa kuwa mhudumu wa Mungu mwenye kuendeleza amani.—Kama ilivyosimuliwa na Tom McDaniel.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nilipokuwa mfungwa nambari 626023 katika kituo cha kurekebi tabia cha Jimbo la Washington

[Picha katika ukurasa wa 13]

Familia ya McDaniel—Mary, Tom, binti Rhonda, na mwana wao Trey

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki