Kulea Familia Ulimwenguni Pote Kulea Katika Upendo, Nidhamu, Mfano, na Kanuni za Kiroho
WAZAZI kutoka nchi kadhaa wamepeleka ripoti juu ya mafanikio ya kulea watoto wao kuanzia utoto kupitia miaka ya utineja. Wote hao ni Mashahidi wa Yehova, na hivyo ripoti zao zakazia uhitaji wa uangalifu katika sehemu nne zilizoorodheshwa katika kichwa kilicho juu. Teuzi zilizotolewa hapa zarejezea namna chache tu za malezi ya familia waliyofuata.
Kutoka Hawaii
“Kama Biblia ituambiavyo, upendo ndio sifa iliyo ‘kuu zaidi.’ Ni lazima upendo katika pande zake zote za thamani uangaze kotekote katika makao na familia. Carol na mimi tumeshiriki sifa hii ya kimungu katika ndoa yetu. Sisi tuna ukaribu. Tunapenda kuwa pamoja. Siwezi kukazia kupita kiasi kuamini kwangu kwamba ufunguo mkubwa wa malezi ya mtoto yenye mafanikio ni wenzi wa ndoa wenye furaha.
“Nakumbuka mpaka leo hii hisia zenye nguvu zilizojaza moyo wangu wakati wa siku na majuma baada ya mtoto wetu wa kwanza kuzaliwa. Kulikuwa na mshangao juu ya mwanzo wa kiumbe kipya. Nakumbuka nikimwona Carol akiwa mwenye furaha sana na mwenye uradhi alipokuwa akimyonyesha mtoto Rachel. Nilimfurahia, lakini pia nilihisi uchungu kidogo, wivu kidogo. Carol alikuwa na kifungo sana na Rachel, lakini nilikuwa wapi? Nilihisi kana kwamba nilikuwa nimesukumwa—kwa upole sana lakini hata hivyo kusukumwa—nje ya kitovu cha familia yetu. Kwa msaada wa Yehova niliweza kueleza hisia zangu na hangaiko langu kwa Carol, na akanionyesha huruma na utegemezo mwingi.
“Baada ya hapo niliweza kuwa na ukaribu na mtoto wetu mpya kwa kusaidia katika kazi zote za mtoto, kutia ndani zile zisizopendeza—kuosha nepi chafu ni mwono wa kipekee kweli kweli! Tumekuwa na watoto wengine watano baada ya Rachel. Rebecca ndiye wa mwisho, sasa akiwa na umri wa miaka minane. Tumeongoza mafunzo ya Biblia ya kibinafsi, na kila mmoja wa watoto wetu.
“Jambo moja zaidi kuhusu malezi ya mtoto ya mapema. Carol na mimi tulifurahia kuongea na watoto wetu tangu wakati walipozaliwa. Tuliongea kuhusu mambo ya aina yote. Wakati mwingine tuliongea kuhusu Yehova na kazi zake nzuri ajabu. Wakati mwingine tuliongea kuhusu mambo ya kijinga, ya kimchezo, yenye kuchekesha. Bila shaka, tulikuwa tunajaribu kuwafundisha jambo, lakini zaidi ya hilo tulikuwa tukiwa na wakati mzuri tu, wenye mapumziko. Naamini mazungumzo kama hayo yalichangia kwa kadiri kubwa kifungo cha mzazi na mtoto. Hakuna shaka kwamba yalisaidia katika kufanyiza uwasiliano mzuri ambao tumekuwa nao katika familia yetu.
“Yehova ametufundisha kanuni kubwa zaidi ya mambo ya kiroho, ya kujitoa sisi wenyewe. Carol na mimi hatujawa kamwe na wingi wa vitu vya kimwili, lakini kwa kweli hatujapata kamwe kuvitafuta au kuvikosa. Ikiwa tungalitumia wakati wetu mwingi tukiwa watumwa wa utajiri, hatungalikuwa na wakati wa kutosha wa kujitolea kwa Yehova na familia yetu. Tulifanya uchaguzi unaofaa.” (Maelezo ya Carol yafuata.)
“Nafikiri kuwalea watoto wako husaidia sana katika kufunganisha watoto kwa mama zao. Unatumia wakati mwingi sana ukimpakata na kumbeba mtoto wako hivi kwamba hamna budi kuwa na ukaribu. Mama hawezi kamwe kumwacha mtoto kwa zaidi ya saa mbili au nne. Siku zote Ed na mimi tumekuwa wenye kutunza sana juu ya kutoacha watoto wetu watunzwe na akina yaya. Nilitaka kuwafundisha watoto wangu na kuwaangalia wakuavyo sikuzote. Kwa hiyo wakati walipokuwa wadogo, sikuenda kazi. Nafikiri hilo liliwasaidia watambue jinsi walivyokuwa na umaana kwetu. Njia kuu ya kukaribia watoto wako ni kutumia wakati pamoja nao. Hakuna lolote linalochukua mahali pa kuwa kwako hapo binafsi. Mambo yote ya kimwili hayatachukua mahali pako.
“Miaka ya utineja ilikuwa migumu kwa sababu tu nilihitaji kujirekebisha kulingana na ukuzi wa watoto. Ilikuwa vigumu kukubali hilo, kutambua kwamba hawakunihitaji sana na walikuwa wanaanza kujitegemea. Ni wakati wenye kuogopesha, na inatahini kazi yako yote ya kufundisha, kutia nidhamu na kurekebisha ambako umefanya. Ni kuchelewa kweli kweli kuanza wakiwa matineja. Ni kuchelewa mno kujaribu wakati huo kuwafundisha maadili, upendo kwa ainabinadamu, na hasa upendo kwa Yehova. Mambo haya ni lazima yakazwe kikiki tangu kuzaliwa na kuendelea.
“Una miaka 12 ya kufanya kazi yako kabla ya miaka ile migumu ya utineja. Lakini ikiwa umefanya bidii kutumia kanuni za Biblia, ni wakati wa kuvuna shangwe na amani wanapoamua wanataka kumtumikia Yehova kutoka moyoni.”—Edward na Carol Owens.
Kutoka Zimbabwe
“Watoto ni ‘urithi kutoka kwa Yehova.’ Ndivyo isemavyo Biblia kwenye Zaburi 127:3. Kuwa na hili akilini imetusaidia sisi tukiwa wazazi tufanye yote tuwezayo katika kutunza urithi huu. Moja ya jitihada za msingi katika familia yetu ilikuwa ni kufanya mambo pamoja—kusali pamoja, kujifunza Biblia pamoja, kuabudu pamoja, kufanya kazi pamoja, kutembelea marafiki pamoja, kucheza pamoja.
“Nidhamu ilihitajiwa wakati mwingine. Wakati mmoja mwana wetu, aliyekuwa katika utineja wake wa mapema, alichelewa kuja nyumbani. Tulikuwa na wasiwasi. Hakusema waziwazi. Tuling’amua kwamba kulikuwa na kasoro fulani, lakini tuliamua kuweka kando jambo hilo hadi asubuhi. Karibu usiku wa manane tulisikia mbisho kwenye mlango wa chumba chetu cha malazi. Alikuwa mwana wetu, akiwa na machozi machoni pake.
“‘Baba, mama, nimeshindwa kulala kwa muda wa saa nne zilizopita, kwa sababu tu sikusikiliza mliponishauri kutokana na Biblia juu ya mashirika mabaya. Baada ya shule leo watoto wengine walinikaza niende kuogelea pamoja nao, na mmoja wa wavulana hao akanivuruta chini ya maji. Kama mvulana mwingine asingalinisaidia, ningalikufa majini. Walinichekelea na kuniita mwoga. Nikaja moja kwa moja hadi nyumbani, lakini niliketi nje ya nyumba kwa sababu nilihisi nikiwa na hatia. Ninasikitika sikuwasikiliza mliponionya juu ya mashirika mabaya, kama inavyoonyeshwa katika Biblia.’—1 Wakorintho 15:33.
“Alilia na hata sisi pia. Tulipendezwa kwamba alikuwa amejifunza somo, lakini tulitia nidhamu ili kukazia jambo hilo hata zaidi. Kutoka 34:6, 7, NW, huonyesha kwamba Yehova ni mwenye rehema na husamehe makosa, lakini bado ‘hatakosa kwa vyovyote kuadhibu.’”—David na Betty Mupfururirwa.
Kutoka Brazili
“Mimi ni mjane na ilinilazimu nimlee mvulana wangu peke yangu. Wakati ule ule, ninafanya kazi nikiwa mwalimu. Si rahisi kufundisha na kuadhibu watoto. Linalohitajiwa ni mafundisho yenye kuambatana, nidhamu yenye usawaziko, na mfano mzuri kwa upande wa wazazi. Ilikuwa vigumu kwangu kuwa mkali na wakati ule ule kuwa mwenye huruma. Nilihitaji kujifunza ustadi wa kusikiliza, hasa kusikiliza kwa moyo wangu. Ni jambo la maana kuwasiliana, si kuzungumza tu, bali husisha mtoto, mfanye aitikie kwa kihisia-moyo. Nilijaribu kumfanya ahisi kuwa sehemu ya familia kwa kumhusisha katika mpango wa matumizi ya fedha ya familia. Bili ya taa au ya maji ilipofika, au bei ya mavazi au ya viatu ilipopanda, tulizungumzia mambo hayo pamoja.
“Ni jambo la maana kupongeza kwa moyo mweupe mambo yafanywapo vizuri. Kadiri nafasi zilipojitokeza, ningemwonyesha kanuni ya kufuata sheria na kanuni za Mungu. Katika pindi moja, baada ya kumshauri mara kadha, ilinilazimu kutumia fimbo halisi. Jinsi jambo hilo lilivyokuwa ligumu kwangu, lakini, wee, matokeo yalikuwa yenye kufurahisha kama nini! Katika kipindi cha ubalehe tuna hali zetu za furaha na huzuni, lakini tunaweza kuona kanuni ya mafundisho na nidhamu. Huniambia matatizo yake ya kibinafsi na maelekeo yake.
“Ni lazima niwe chonjo ili nisitawishe uwasiliano mzuri. Kwa hiyo najaribu kutojiingiza sana katika kazi yangu ya kimwili ili sikuzote niwe na wakati kwa ajili ya mwanangu. Tunapokuwa na matatizo, najaribu kusikiliza kwa makini, na kwa msaada wa Yehova, tunayashinda. Ninamjulisha kwamba hata mimi hufanya makosa pia. Katika pindi moja nilikasirika sana, na nikamwambia ‘afunge mdomo wake.’ Aliniambia kwamba kumwambia mtu ‘afunge mdomo wake’ kulionyesha ukosefu wa upendo. Alisema kweli. Alasiri hiyo tulikuwa na maongeo marefu kweli kweli.”—Yolanda Moraes.
Kutoka Jamhuri ya Korea
“Nilitumia kanuni za Biblia kwa bidii katika maisha ya familia yangu. Hasa Kumbukumbu la Torati 6:6-9 lilikuwa ndani ya moyo wangu. Kwa hiyo nilijaribu kuwa na watoto wangu mara nyingi iwezekanavyo, ili niwe karibu nao, ili nikaze kikiki kanuni za Neno la Mungu ndani ya akili zao na mioyo yao. Pia niliwaalika wamishonari na washiriki wa familia ya Betheli wa wakati wote kwenye makao yetu ili wawapatie watoto wangu hisi ya utumishi wa wakati wote.
“Jambo la kwanza ambalo wazazi wanapaswa kufanya wakati watoto wanaposababisha matatizo ni kuonyesha matunda ya roho. Ni rahisi kuudhika na watoto na kukasirika. Hata hivyo, sisi wazazi, ni lazima tuwe wenye subira na tuonyeshe mfano wa mwenendo mzuri. Ni jambo la maana kuwaheshimu watoto na kuwapatia fursa ya kueleza hali. Ikiwa hakuna uthibitisho ulio wazi wa kosa, basi watumaini na kuwajenga sikuzote. Unapoadhibu mtoto, kwanza toa sababu pamoja naye, mwonyeshe kosa alilofanya, na umwonyeshe jinsi kosa lake lilivyomchukiza Yehova na wazazi wake. Halafu tia nidhamu. Kwa kawaida wanangu wangesema hivi baada ya kutiwa nidhamu: ‘Baba, sielewi ni kwa nini nilikuwa mwasi. Nilikuwa mpumbavu sana.’ Wanathamini wazazi wanaojali sana kuwatia nidhamu.
“Wazazi wanahitaji kuwa chonjo kwa mwanzo wa mwenendo mbaya. Mwanangu mkubwa alipokuwa katika shule ya upili katika kidato cha tatu, nilisikia sauti kubwa ya muziki wa roki ikitoka kwenye chumba chake. Niligundua kwamba amejiunga na kikundi cha wanafunzi wa kutia nidhamu (wanafunzi wa umri mkubwa ambao walikuwa wakishauri wengine), na alikuwa amejiachilia akavutwa na mavutano ya kilimwengu. Nilisikia kwamba chini ya mkazo wenye kuendelea kutoka kwa wanakikundi na kwa ajili ya udadisi alikuwa amevuta sigareti. Tulitoa sababu pamoja juu ya hatari za uvutaji sigareti, na mwanangu aliamua yeye mwenyewe kwamba alipaswa ajiuzulu kutoka kwenye kikundi hicho, jambo ambalo alifanya. Ili kujaza nafasi ilioachwa baada ya kuacha utendaji mbalimbali wa shule usiofaa, tulipanga tafrija inayofaa pamoja na familia na washiriki wa kundi.
“Hatimaye, nataka kusema kwamba jambo la maana zaidi ni kwa wazazi kuweka mfano mwema. Kila mara nilikuwa ninawaambia wavulana wangu wawili kwamba nilitaka kumtumikia Mungu kwa wakati wote nikiwa mhudumu anayehubiri habari njema. Mvulana wangu wa pili alipomaliza shule, nilistaafu kazi katika kiwanda cha hariri na nikawa mhudumu wa wakati wote. Wavulana wangu wawili waliona azimio langu na wakalifuata. Baada ya kutumikia katika gereza kwa sababu ya suala la kutokuwemo, wote wawili waliingia katika utumishi wa wakati wote na wanaendelea hadi leo hii.”—Shim Yoo Ki.
Kutoka Sweden
“Tumelea watoto saba, wavulana watano na wasichana wawili. Sasa wakiwa wamekua, wote wanahubiri habari njema za ufalme wa Mungu kwa bidii nyingi. Kuanzia umri wa mapema, watoto walihudhuria mikutano ya kundi na kwenda pamoja nasi katika huduma ya shambani. Hatua kwa hatua walijifunza kazi ya kuhubiri—kupiga kengele ya mlango, kuamkua, kusema jina lao, na kutolea kikaratasi cha kukaribisha, trakti, au gazeti. Walipokuwa wangali wachanga kidogo, walitoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.
“Nyakati nyingine matatizo makubwa yalihitaji uangalifu wa pekee. Kuonyesha upendo na saburi ni kwa maana—hakuna kufoka au kuteta. Matatizo yalitatuliwa kwa kutoa sababu juu ya mambo na kukazia maoni ya Yehova. Tuliwafundisha juu ya mambo ya kifedha. Walipokuwa wakubwa, walifanya kazi kwa kugawanya magazeti ya habari, kuvuna piti, kazi ya bustani, na kadhalika. Kuwatembelea babu na nyanya yao mbali kutoka nyumbani kuliwafanya wajue matatizo ya watu wazee na kuwa na huruma kuwaelekea.
“Katika kusherehekea mwaka wa 30 wa ndoa yetu, tulipokea barua inayofuata:
“‘Kwa Wazazi Wetu Wapendwa:
“‘ASANTENI KWA YOTE! Upendo mchangamfu mliotutolea kwa ukarimu, imani halisi mliyoingiza ndani yetu, tumaini nzuri ajabu mlilotupatia—hili haliwezi kufananishwa na maneno au thamani ya pesa. Hata hivyo, tunatumaini kwamba kupitia kumbukumbu hili dogo, mtaelewa jinsi tunavyohisi juu yenu, baba na mama yetu wapenzi. [Ilitiwa sahihi] Watoto wenu.’
“Tukikumbuka ile ‘miradi ya miaka 20 yote,’ tunahisi shukrani nyingi sana kwa Yehova, Baba yetu wa kimbingu, ambaye amekuwa mwenye huruma nyingi kutuelekea.”—Bertil na Britta Östberg.
Michanganyiko ya Habari Kutoka kwa Wazazi
“Mama anyonyeshaye ni njia ya Yehova ya kumleta mtoto karibu kimwili na mama, lakini baba anaweza kuuzidisha kwa kiti cha kubembeza. Nilifurahia kuwapakata watoto wetu mikononi mwangu na kuwabembeza ili walale karibu kila usiku.”
“Nikiwa baba yao, sikuwa na uwezo wa kuwanyonyesha watoto wetu, lakini nilikuwa na ukaribu wa kimwili pamoja nao kwa kuwaosha kila usiku. Ulikuwa wakati wa furaha, kwangu na hata kwao.”
“Mara kwa mara, nimechukua mmoja wa watoto wetu, kila mtu peke yake, ili kula nami peke yangu. Wanapenda kipindi hiki cha kuwa pamoja na baba peke yao.”
“Miaka ilipopita, hatua kwa hatua tuliwaamini na kuwapa uhuru zaidi na madaraka. Spring’i iliyobanwa mkononi mwa mtu ni lazima iachiliwe polepole ili kuzuia kuruka kwayo ghafula bila kuzuiwa.”
“Onyesha shauku nyingi. Hakuna mtoto yeyote aliyekufa kwa sababu ya makumbatio na busu—lakini hisia zao zaweza kufa bila hizo.”
“Kuwa mwenye subira, usiwakandamize. Usiwakemee kila mara. Waache wasitawishe kujistahi. Kwa kila uchambuzi wape sifa nne!”
“Wape yaliyo bora zaidi, kuwafanya wawe bora zaidi.”
[Picha katika ukurasa wa 9]
Watoto wachanga kama Rebecca wanahitaji shauku ya kweli
[Picha katika ukurasa wa 10]
Kuchukua wakati ili kufanya mambo pamoja kutachangia kifungo imara cha familia