Kutoka Kuwa Dhaifu Kimwili Hadi Kuwa Mtukuza Mungu
Mashahidi wa Yehova wawili waliokuwa wakishiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba katika Februari 1984 walizungumza na mwanamke mmoja katika kijiji cha Corcovada, Añasco, Puerto Rico. Walisikia sauti kutoka ndani na kumwuliza mwanamke huyo kama kulikuwa na mtu mgonjwa.
“Ndiyo,” akaitikia, “ni mume wangu. Amekuwa mgonjwa kwa miaka 14 na hatoki kamwe nje ya chumba hicho ila aweze kuoga na kula.”
Mashahidi hao wawili waliuliza kama wangeweza kuzungumza na mume wake. Mke huyo akasema kuwa mume wake hakupenda kuzungumza na mtu yeyote, lakini kama wale Mashahidi wangependa kuingia ili wamwone, wangeweza.
Mmoja wa Mashahidi hao aeleza, “Tuliingia chumbani, na kumpata mtu huyo kitandani. Tulipoona hali yake, tulimhurumia. Yeye alikuwa dhaifu sana hivi kwamba alitetemeka. Tulimweleza juu ya Ufalme wa Mungu na tumaini la kuishi katika ulimwengu usio na magonjwa au hata kifo. Machozi yalitiririka usoni pake. Nilimwuliza kama angependa kuishi katika ulimwengu huo mpya ambapo hakuna yeyote angekuwa mgonjwa.”—Ufunuo 21:3, 4.
“Ndiyo,” yeye akajibu. “Tulimwuliza turudi tena na kujifunza Biblia naye. Kwa kibali chake tulirudi, na funzo likafanywa akiwa amelala kitandani.
“Baada ya ziara chache, nilidokeza aketi kitandani ili iwe rahisi zaidi kwake kujifunza. Yeye alijitahidi kufanya hivyo, ingawa mwanzoni angeketi kwa muda mfupi tu kwa kuwa angepatwa na kizunguzungu. Baada ya mafunzo kadhaa, alipozidi kupata nguvu, nilidokeza kwamba tufanye funzo hilo kwenye chumba cha kulia. Yeye alikubali, na kila juma tungemsaidia kutembea hadi humo.
“Mtu huyo alifanya maendeleo mazuri katika mafunzo yake, hata ingawa hangeweza kuona vizuri na mikono yake ilitetemeka sana hivi kwamba ilikuwa vigumu kwake kushika lenzi kuzi. Yeye alituambia kuwa katika miaka 14 aliyokuwa mgonjwa, alikuwa hajamwona daktari kwa sababu alishindwa kutembea. Kwa hiyo tulifanya mipango ya kumpeleka kwa daktari.
“Upasuaji wa macho yake ulifanywa kwa mafanikio, na upesi alikuwa anasoma Biblia bila msaada wa lenzi kuzi. Hata mikono yake iliacha kutetemeka. Alianza kutembea-tembea nyumbani kwa ukawaida, na hatimaye angeenda kitandani kulala usiku tu. Muda baada ya hapo yeye alianza kuhudhuria mikutano yetu ya Kikristo kwenye Jumba la Ufalme.
“Kwa wakati, kumpenda Yehova Mungu na ahadi Zake kwa huyu aliyekuwa dhaifu kimwili kulimsukuma kusema na wengine kuhusu mambo aliyokuwa amejifunza. Punde kidogo, aliungana nasi katika huduma ya nyumba kwa nyumba, jambo ambalo lilishangaza sana majirani na marafiki zake. Afya yake ilifanya maendeleo sana hivi kwamba hata alianza kufanya kazi shambani mwake.”
Katika Novemba 1988 ono hilo lilisimuliwa kwenye kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova, na mtu huyo, Pedro Martínez, akatokea jukwaani. Mwishowe, katika Novemba 1989, alionyesha wakfu wake kwa Yehova kwa ubatizo wa maji.