Je! Uhai Una Kusudi?
“‘Kwa nini tupo hapa?’ ndilo swali la maana sana ambalo binadamu anakabili. . . . Mimi naamini kuwa uhai una maana kujapokuwa kifo kisicho na maana ambacho nimeona. Kifo hakina maana, uhai unayo.”
MANENO hayo yaliandikwa na Elie Wiesel, mwandikaji anayejulikana sana aliyeokoka kambi za mateso za Nazi. Alikuwa mmoja wa wengi waliojibu swali lililotokezwa na gazeti Life: “Kwa nini tupo hapa?” Yeye alikuwa ameona maisha yalipokuwa katika hali yayo mbaya sana, hata hivyo alikuwa na usadikisho kwamba uhai una maana.
Ingawa hivyo, si kila mtu alikubaliana na hayo. Dereva mmoja wa teksi aitwaye José Martínez alijibu swali ilo hilo kwa njia hii: “Tupo hapa ili tufe, ni kuishi na kufa tu. Mimi huendesha teksi. Huvua samaki, humpeleka rafiki-msichana wangu matembezini, hulipa kodi, husoma kidogo, halafu ninajitayarisha kufa . . . Uhai ni udanganyifu mkubwa.” Kwa wazi, uhai hauna maana wala kusudi kwa José.
Kwa kushangaza, idadi fulani ya watu wenye elimu wanaonekana wakikubaliana na dereva huyo wa teksi kuliko kukubaliana na yule mwandikaji. Wanamageuzi Richard E. Leakey na Roger Lewin, wanadokeza hivi katika kitabu chao Origins: “Labda jamii ya kibinadamu ni kosa kubwa la kibayolojia, baada ya [jamii hiyo] kugeuka kupita kiasi ambacho ingeweza kusitawi kwa upatano wayo yenyewe na ulimwengu unaoizunguka.” Angalau kwa hao, uhai wa kibinadamu hauna maana.
Vivyo hivyo, mwanamageuzi Stephen Jay Gould aliandika: “Tupo hapa kwa sababu kikundi kimoja cha samaki kilicho tofauti na vingine vyote kilikuwa na mfanyizo wa pezi usio wa kawaida ambao ungeweza kugeuka kuwa miguu ya viumbe vya barani; . . . kwa sababu jamii dhaifu iliyo ndogo, iliyoibuka katika Afrika robo milioni ya miaka iliyopita, kufikia sasa, imeweza kuendelea kuwako kwa njia moja au nyingine. Tunaweza kutamani kupata jibu la ‘juu zaidi’—lakini hakuna lolote.” Uhai wa kibinadamu ni aksidenti isiyo na maana kwa Gould.
Gould hakosei katika angalau jambo moja. Wengi hutamani jibu la “juu zaidi” kuliko lile atokezalo. Katika nyakati za mikasa, wengi hufikiri kama vile Jason mwenye miaka 11. Mvulana huyu mchanga aliandika hivi kuhusu kifo cha rafiki yake mchanga: “Rafiki yangu Kim alipokufa kwa ugonjwa wa kansa nilimwuliza mama yangu kwamba ikiwa Mungu angemruhusu Kim afe hali alikuwa mwenye miaka 6 tu, kwa nini alimfanya azaliwe kwa vyovyote?” Kiasili, Jason alihisi kwamba uhai una kusudi, na kifo cha huzuni cha rafiki yake mchanga kilionekana kuwa kikipinga kusudi hilo.
Umaana wa Swali Hilo
Je! ni jambo la maana kujua kama uhai una kusudi au hauna? Je! hilo ni swali la kifalsafa tu, au lapasa kukuhangaisha? Wengi wameishi muda wa maisha yao bila kufikiria jambo hilo. Na ikiwa José Martínez hakosei, njia yao huenda ikawa ndiyo ya hekima kufuatwa.
Hata hivyo, ikiwa Elie Wiesel hakosei na uhai una kusudi, bila shaka tunapaswa kujaribu tujue ni nini. Ama sivyo, tungekosa jambo la maana sana la ono la kuishi. Ingekuwa kama kutembea ndani ya jumba la sanaa bila kutazama picha au kuketi katika mkahawa bila kuagiza mlo.
Tunaweza kujuaje iwapo uhai una kusudi au la? Tutazungumzia mambo fulani ya hakika yanayosaidia kutatua tatizo hilo katika makala ifuatayo.