Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • pr seh. ya 1 kur. 3-6
  • Je! Uhai Una Kusudi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Uhai Una Kusudi?
  • Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Hali Zilizo Ngumu Zaidi
  • Yale Ambayo Wao Husema
  • Matokeo
  • Yehova Mungu wa Kusudi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Kufuatia Kusudi Lenye Maana Maishani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Mungu Ana Kusudi Gani kwa Wanadamu?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • Je! Uhai Una Kusudi?
    Amkeni!—1992
Pata Habari Zaidi
Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?
pr seh. ya 1 kur. 3-6

Sehemu ya 1

Je! Uhai Una Kusudi?

Wakati mmoja au mwingine, karibu kila mtu hujiuliza uhai una kusudi gani. Je! ni kufanya kazi kwa bidii ili kuboresha maisha zetu, kuandalia riziki familia zetu, kufa baada ya miaka labda 70 au 80, na kisha kukoma kuwako milele? Kijana mmoja aliyehisi hivyo alisema kwamba uhai hauna kusudi jingine kuliko “kuishi, kuzaa watoto, kufurahi na kisha kufa.” Lakini je, hiyo ni kweli? Na je, kwa kweli kifo ndicho mwisho wa mambo yote?

2 Watu wengi katika nchi za Mashariki na Magharibi pia, huhisi kwamba kusudi kubwa la kuishi ni kujipatia mali za kimwili. Wanaamini kwamba hilo laweza kufanya maisha yawe yenye furaha, na yenye maana. Lakini vipi watu ambao tayari wana mali za kimwili? Mwandikaji Mkanada Harry Bruce alisema: “Idadi kubwa ajabu ya watu walio matajiri husisitiza kwamba hawana furaha.” Yeye aliongeza hivi: “Uchunguzi wa maoni ya watu unaonyesha kwamba hali ya kutazamia balaa imekumba vibaya Amerika Kaskazini . . . Je! kuna mtu yeyote mwenye furaha ulimwenguni? Ikiwa ndivyo, siri ni nini?”

3 Aliyekuwa rais wa U.S. Jimmy Carter alisema hivi: “Tumegundua kwamba kumiliki vitu na kuvitumia hakuridhishi tamaa yetu ya kupata maana. . . . Kurundika mali za kimwili hakuwezi kujazia utupu wa uhai usio na tumaini na kusudi.” Na kiongozi mwingine wa kisiasa alisema hivi: “Kwa miaka kadhaa sasa nimejishughulisha na utafutaji mkubwa wa kweli juu yangu mimi na uhai wangu; watu wengine wengi ninaojua wanafanya ivyo hivyo. Watu wengi zaidi kuliko wakati mwingine wowote wanauliza, ‘Sisi ni nani? Kusudi letu ni nini?’”

Hali Zilizo Ngumu Zaidi

4 Wengi huwa na shaka kama uhai una kusudi wanapoona kwamba maisha yamekuwa magumu zaidi. Kotekote ulimwenguni watu zaidi ya bilioni moja ni wagonjwa sana au hawana chakula cha kuwatosha, ikitokeza vifo vya watoto wapatao milioni kumi kila mwaka katika Afrika pekee. Idadi ya watu wote duniani, inayokaribia bilioni 6, inaendelea kuongezeka kwa zaidi ya watu milioni 90 kwa mwaka, asilimia 90 ya ongezeko hilo likiwa katika nchi zinazositawi. Idadi hiyo inayoendelea kupanda hufanya kuwe na uhitaji mkubwa wa chakula, makao, na viwanda, mambo ambayo huendeleza uharibifu wa ardhi, maji, na hewa kutokana na vichafuzi vya viwanda na vitu vinginevyo.

5 Kichapo World Military and Social Expenditures 1991 charipoti hivi: “Kila mwaka eneo la msitu lililo sawa na lile la nchi yote ya [Uingereza] huharibiwa. Kwa miendo ya sasa (ya kukatwa kwa miti), kufikia mwaka 2000, tutakuwa tumeondolea mbali asilimia 65 ya misitu katika maeneo ya kitropiki yenye unyevu.” Kulingana na shirika la UM, miti 10 hukatwa kwa kila 1 unaopandwa; katika Afrika uwiano ni zaidi ya 20 kwa 1. Kwa hiyo maeneo ya jangwa huongezeka, na kila mwaka eneo lenye ukubwa kama ule wa Ubelgiji hupotezwa isifae kilimo.

6 Pia, kwa sababu ya vita, karne hii ya 20 imekuwa na vifo vingi mara nne zaidi ya karne nne zilizotangulia zikiwekwa pamoja. Kila mahali, uhalifu unaongezeka, hasa uhalifu wa kutumia nguvu. Kuvunjika kwa familia, utumizi wa dawa za kulevya, UKIMWI, magonjwa yanayopitishwa kingono, na mambo mengine yasiyofaa pia yanafanya maisha yawe magumu zaidi. Na viongozi wa ulimwengu hawajaweza kuandaa suluhisho kwa matatizo mengi yanayokumba familia ya kibinadamu. Hivyo, inaeleweka ni kwa nini watu huuliza, Uhai una kusudi gani?

7 Swali hilo limeshughulikiwaje na wasomi na viongozi wa kidini? Baada ya karne hizi nyingi za wakati, je, wameandaa jibu lenye kuridhisha?

Yale Ambayo Wao Husema

8 Msomi Mkonfusho Tu Wei-Ming alisema hivi: “Kusudi kuu la uhai limo katika kuwako kwetu kwa kibinadamu, ambako ni kwa kawaida.” Kulingana na maoni hayo, binadamu wangeendelea kuzaliwa, wang’ang’ane ili waishi, kisha kufa. Mtazamo kama huo hauna tumaini. Na je, hata ni wa kweli?

9 Elie Wiesel, mwokokaji wa kambi za kifo za Nazi katika Vita ya Ulimwengu 2, alionelea hivi: “‘Kwa nini tupo hapa?’ ndilo swali la maana sana ambalo binadamu apaswa alikabili. . . . Mimi naamini kuwa uhai una maana kujapokuwa kifo kisicho na maana ambacho nimeona.” Lakini yeye hakuweza kusema kusudi la uhai ni nini.

10 Mhariri Vermont Royster alisema hivi: “Tunapomfikiria mwanadamu mwenyewe, . . . cheo chake katika huu ulimwengu wote mzima, tumesonga mbele kidogo sana kuliko muda ule ambao wakati ulianza. Tungali na maulizo ya kutaka kujua sisi ni akina nani na kwa sababu gani tunaishi na ni wapi tunakoelekea.”

11 Mwanasayansi wa mageuzi Stephen Jay Gould aliandika hivi: “Huenda tukatamani kupata jibu la ‘juu zaidi’—lakini hakuna lolote.” Kwa wanamageuzi mithili ya hao, uhai ni mng’ang’ano wa kuendelea kuishi kwa walio na nguvu zaidi, mwisho wao ukiwa kifo. Maoni hayo pia hayana tumaini. Na tena, je, hayo ni ya kweli?

12 Viongozi wengi wa kidini husema kwamba kusudi la uhai ni kuwa na maisha mazuri ili mtu akifa, nafsi yake iende mbinguni na kukaa huko milele. Njia tofauti na hiyo ambayo watu wabaya hupewa ni kuteswa milele katika moto wa helo. Na bado, kulingana na itikadi hiyo, duniani kungeendelea kuwa na uhai usioridhisha ambao umeendelea kuwapo katika historia yote. Lakini ikiwa kusudi la Mungu lilikuwa watu waishi mbinguni kama malaika, kwa nini yeye hakuwaumba tu kwa njia hiyo kwanza, kama alivyoumba malaika?

13 Hata makasisi huona vigumu kuelewa maoni hayo. Dakt. W. R. Inge, aliyekuwa kiongozi wa Kathedro ya St. Paul katika London, alisema hivi wakati mmoja: “Katika maisha yangu yote nimejitahidi sana kupata kusudi la kuishi. Nimejaribu kupata majibu ya masuala matatu ambayo wakati wote huonekana kuwa ya msingi: tatizo la umilele; tatizo la utu wa kibinadamu; na tatizo la uovu. Nimeshindwa. Sijaweza kutatua lolote la hayo.”

Matokeo

14 Ni nini matokeo ya mawazo mengi mbalimbali ya wasomi na viongozi wa kidini juu ya swali la kusudi la uhai? Wengi huitikia kama alivyofanya mwanamume mzee-mzee aliyesema: “Kwa muda mrefu katika maisha yangu, nimekuwa nikijiuliza ni kwa nini nipo hapa. Ikiwa kuna kusudi, mimi sijali tena.”

15 Idadi kubwa ya wale wanaochunguza maoni tele ya dini za ulimwengu hutoa mkataa kwamba kwa kweli si kitu hata mtu aamini nini. Wanahisi kwamba dini ni kitulizo cha akili, jambo linaloandaa amani kidogo ya akili na utoshelezo ili mtu aweze kukabiliana na matatizo ya maisha. Wengine huhisi kwamba dini si jambo jingine ila ushirikina tu. Wanahisi kwamba kukisia kwa dini kwa karne nyingi hakujajibu swali la kusudi la uhai, wala hakujaboresha maisha za makabwela. Kwelikweli, historia huonyesha kwamba dini za ulimwengu huu mara nyingi zimezuia ainabinadamu isifanye maendeleo na zimekuwa visababishi vya chuki na vita.

16 Hata hivyo, je, bado ni jambo la maana kupata kweli kuhusu kusudi la uhai? Mtaalamu wa afya ya akili Viktor Frankl alijibu hivi: “Jitihada ya kupata maana ya uhai wa mtu ndiyo kani kuu yenye kuchochea katika binadamu. . . . Mimi nathubutu kusema kwamba, ulimwenguni hamna kitu ambacho kingesaidia mtu afaulu kuziokoka hata hali zilizo mbaya zaidi, kama vile anavyoweza kusaidiwa kwa kujua kwamba kuna kusudi katika uhai wa mtu.”

17 Kwa kuwa falsafa za kibinadamu na dini hazijatoa maelezo ya kuridhisha juu ya ni nini kusudi la uhai, sisi tunaweza kwenda wapi ili kupata maana ya uhai? Je! kuna chanzo cha hekima bora kinachoweza kutuambia kweli kuhusu jambo hili?

Isipokuwa imeonyeshwa vingine, manukuu ya maandiko yametoka katika Biblia ya Union Version ya Kiswahili

[Maswali ya Funzo]

1. Ni swali gani ambalo huulizwa mara nyingi kuhusu kusudi la uhai, na mtu mmoja alitoa maelezo gani kulihusu?

2, 3. Kwa nini kujipatia mali za kimwili hakutoshi kuwa kusudi la kuishi?

4. Kwa nini wengine huwa na shaka kama uhai una kusudi?

5. Ni nini kinachopata mimea duniani?

6, 7. Ni nini baadhi ya matatizo ambayo viongozi wa kibinadamu wameshindwa kutatua, kwa hiyo ni maswali gani yanayohitaji kujibiwa?

8, 9. (a) Msomi mmoja wa Uchina alisema nini kuhusu kusudi la uhai? (b) Mwokokaji mmoja wa kambi ya kifo ya Nazi alisema nini?

10, 11. (a) Mhariri mmoja alionyeshaje kwamba mwanadamu hana majibu? (b) Kwa nini maoni ya mwanasayansi mmoja wa mageuzi hayaridhishi?

12, 13. Ni nini yaliyo maoni ya viongozi wa kidini, na je, hayo yanaridhisha zaidi ya yale ya wachunguzi walimwengu?

14, 15. Maoni hayo yenye kutofautiana yana matokeo gani juu ya watu wengi?

16. Kupata kusudi la uhai kwaweza kuwa kwa maana jinsi gani?

17. Ni maswali gani ambayo sasa tunahitaji kuuliza?

[Picha katika ukurasa wa 4]

“Kila mwaka eneo la msitu lililo sawa na lile la nchi yote ya [Uingereza] huharibiwa”

[Picha katika ukurasa wa 5]

“Kwa muda mrefu katika maisha yangu, nimekuwa nikijiuliza ni kwa nini nipo hapa”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki