Sala za Kurudia-Rudia-au za Kutoka Moyoni?
NDEGE moja kubwa ya abiria ilikuwa inaenda juu hewani karibu meta 12,420. Chini kulikuwa maji baridi ya Pasifiki. Kwa ghafula, injini moja ikazima. Halafu, zile nyingine tatu zikapoteza nguvu. Ndege hiyo ikashuka mara moja kilometa tisa kwa dakika mbili! Lakini ilipobaki karibu meta 2,727 ifike chini, ilipata nguvu tena na ikasafiri salama hadi San Francisco. Akahema msafiri mmoja: “Nilisali kwa nguvu zaidi ya wakati mwingine wowote wa maisha yangu.”
Katika nyakati za maafa, hatari, au huzuni nyingi, watu wengi, hata wasio wanadini, humwendea Mweza Yote kupata msaada. Kinyume cha hilo, wanadini, mara nyingi hurudia sala kikawaida katika makanisa na mahekalu au nyumbani. Kwa msaada wa rosari, wengi husema Sala ya Bwana na zile za Kusalimu Mariamu. Wengine hutumia vitabu vya sala. Mamilioni ya watu nchi za Mashariki huzungusha upesi magurudumu yaliyo na sala ndani yayo kama njia ya kurudia-rudia sala kwa haraka sana.
Umepata kujiuliza, ‘Ni jinsi gani tunapaswa kusali? Je, sala zapaswa kurudiwa-rudiwa au zapasa zitoke moyoni?’
Jinsi Sala Ilivyo
Wazia baba umpendaye sana, anayeishi nchi nyingine, akuhimiza umpigie simu wakati wowote upendao—bila malipo. Je, hungempigia simu mara nyingi? Je, hungefurahishwa kudumisha, hata kujenga kifungo cha thamani? Je, hungeweza kuzungumzia mahangaiko yako na kuonyesha shukrani nyingi sana kwa msaada wowote na kitia-moyo ambacho amekupa muda wote wa maisha yako? Huo uhusiano wa kibinafsi unaweza kuwa hazina kubwa kwako, sivyo?
Katika simu zako, huenda ukataja mambo fulani mara kwa mara, lakini hungeweza kujieleza mwenyewe kwa kusoma kutoka katika kitabu au kurudia-rudia kikawaida, au sivyo? Wala, hata sala ya Mkristo haingeweza kuwa hivyo. Kwa kweli, Kristo Yesu alisema kwamba sala hazipaswi kuwa namna hiyo.
Kristo Yesu Alisema Nini?
“Nanyi mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke, kama watu wa mataifa; maana wao hudhani ya kuwa watasikiwa kwa sababu ya maneno yao kuwa mengi.”a (Mathayo 6:7) Tafsiri nyinginezo huonyesha hivi: “Katika sala zenu msipayuke-payuke kama wapagani.” (NE) “Katika kusali kwenu msijaze maneno matupu kama wafanyavyo wasio Wayahudi.”—Revised Standard Version.
Watu wengine hufikiri kwamba kutumia maneno mengi ndiko kumcha Mungu, kusema kwa ufasaha kuwa ndio ujitoaji, kurudia-rudia maneno na kutoa sala ndefu kuwa ndiko kupata itikio hakika. Hata hivyo, Mungu hapimi thamani ya sala kwa yadi au meta. Ni wazi, Yesu hakutaka wafuasi wake watumie sala zisizobadilika au kukariri sala. Kwa sababu hiyo, rosari, vitabu vya sala, au magurudumu ya sala ni yenye thamani gani ya kudumu?
Baada ya kusema yaliyoko juu, Yesu aliwapa wanafunzi wake sala ya kielelezo—ile Sala ya Bwana ijulikanayo sana. (Mathayo 6:9-13) Je, alikusudia watamke maneno hayo kwa kurudia kama kasuku? La hasha. Kwa kweli alipoyasema tena maneno hayo, zaidi ya mwaka mmoja baadaye, hata Yesu mwenyewe hakutumia maneno yaleyale. (Luka 11:2-4) Je, kuna rekodi yoyote ya Wakristo wa mapema kufanya hivyo au kurudia-rudia sala nyinginezo za kikawaida? Tena, la.
Je, hiyo yamaanisha kwamba hatuwezi kutaja jambo lilelile au kuomba mara nyingi? Hasha, kwa sababu Yesu pia alisema: “Fulizeni kuomba, nanyi mtapewa; fulizeni kutafuta sana, nanyi mtapata.” (Mathayo 7:7, NW) Mara nyingi ni lazima kwetu kufanya ombi lilelile mara nyingi. Kwa hiyo Yehova huona jinsi juhudi zetu zilivyo katika maombi yetu na jinsi hisia zetu za ndani zilivyo kuhusu mambo yetu.
Kwa mfano, katika karne ya tano K.W.K., Nehemia aliyekuwa mcha Mungu aliishi akiwa mshiriki wa jamii ya Wayahudi waliokuwa uhamishoni katika Babiloni. Alikuwa mnyweshaji wa mfalme wa Uajemi. Alipoambiwa kuwa jamii yake, wakaaji wa Yudea, waliendelea vibaya, alisali “mchana na usiku” ili wapate kitulizo. (Nehemia 1:6) Sala zake zilipata kusikiwa vya kufaa. Yehova alimsukuma mtawala wa Uajemi mwenye huruma amruhusu Nehemia afunge safari hadi Yerusalemu kunyoosha mambo. Alifanya hilo, ikitokeza furaha kwa watu wake na imani yao ikahifadhiwa.—Nehemia 1:3–2:8.
Jinsi Sala ya Kuhisiwa Moyoni Husaidia
Ijapokuwa yeye ndiye Mwenye Nguvu Kupita Wote wa ulimwengu wote mzima, Yehova huwaalika “watoto” wake wamfikie kwa moyo wote. “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi,” asema mwanafunzi wa Yesu Yakobo. (Yakobo 4:8) Lakini jinsi gani? Ni lazima tusali kupitia jina la Yesu. (Yohana 14:6, 14) Zaidi ya hiyo, kama vile Paulo alivyoshauri: “Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”—Waebrania 11:6.
Wale walio na matatizo, hata wale ambao wamefanya kosa zito, wanaweza kuomba na kupokea msaada wa msamaha. Yesu alitoa kielezi cha hilo kwa hadithi ya kiongozi wa kidini mmoja ambaye, alipokuwa akisali, alishukuru Mungu kwamba alikuwa mtakatifu zaidi ya wengine; lakini mtoza ushuru mmoja (aliyechukiwa na kuonwa kuwa mtenda dhambi nzito wakati ule) alisema tu: “Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi.” Kwa kweli, sala hiyo sahili, na ya kuhisiwa moyoni haikutoka katika kitabu. Na Yesu aliwakemea wanadini wanafiki lakini akasema kwa yule mwingine: “Naye ajidhiliye atakwezwa.”—Luka 18:10-14.
Mielekeo mibaya ya ulimwengu hufanya wengi wawe na wasiwasi na kushuka moyo. Huenda Wakristo hata wakawa na wasiwasi kuhusu msimamo wao mbele za Mungu. Lakini kumwendea Yehova kwa ukawaida, mara nyingi, na kutoka moyoni ili kupata msaada kwaweza kutokeza maajabu. Paulo aliandika: “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba [“kusihi,” NW], pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.”—Wafilipi 4:6, 7.
Kusihi kunamaanisha kuomba kwa bidii, kuomba Mungu msaada, kumwaga yaliyo moyoni kwake kama vile mtoto angefanya kwa mzazi ambaye ana upendo na uelewevu. Sala za aina hiyo hazitoki kwenye vitabu, wala hazirudiwi-rudiwi kwa mtindo wa kikasuku. Zinatoka katika mioyo inayohitaji msaada na imani thabiti kwa Yehova, ‘Msikiaji wa sala.’—Zaburi 65:2, NW.
[Maelezo ya Chini]
a Neno lililofasiriwa ‘kupayuka-payuka’ (bat-ta-lo-geʹo) linatumiwa mara moja tu katika Biblia na linamaanisha “‘kububujika’ katika kujaribu kufanikiwa katika sala kwa kurudia-rudia kwingi.”—Theological Dictionary of the New Testament.