Je! Mungu Anasikiliza Sala Zako?
MAMILIONI kwa mamilioni ya sala zimepelekwa kwa Mungu tangu Yesu alipowapa wanafunzi wake ile Sala ya Kielelezo. Wengi wanairudia sala hiyo neno kwa neno. Lakini mahali pengi watu wanaona kwamba sala nyingi hazijibiwi. Je! bado Mungu anasikiliza sala zetu? Ni jambo gani linalofanya sala ikubalike kwake?
Kwanza, ni lazima tuamini kwamba Mungu atajibu sala zetu. “Yeye anayemkaribia Mungu yampasa aamini kwamba yuko na kwamba anakuwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii nyingi.”—Waebrania 11:6, NW.
Halafu ni lazima tuelekeze sala zetu kwa Mungu tukiwa na unyofu wa kweli kweli. Je! hiyo inasikika kama ajabu? Ijaposikika hivyo, Yesu alionya hivi: “Tena msalipo, msiwe kama wanafiki; kwa maana wao wapenda kusali hali wamesimama katika masinagogi na katika pembe za njia, ili waonekane na watu. Amin, nawaambia, Wamekwisha kupata thawabu yao.” (Mathayo 6:5) Kwa hiyo, sala ndefu-ndefu za kuvuta sa-u-u-u-ti zinazotolewa hadharani ili kujionyesha mbele ya wasikilizaji hazimpendezi Mungu. Yeye hasikilizi sala za namna hiyo.
Tena, haitupasi kumfikia Mungu tukidai kutambuliwa (kupewa utukuzo). Mungu anasikia sala za wanyenyekevu wanaotaka kufanya yanayofaa na wanaokubali udhambi wao.—Luka 18:9-14; 1 Petro 3:12.
Je! tunaposali ni lazima mwili wetu uwe katika kikao fulani cha pekee? Kulingana na maandishi ya Biblia watumishi wa Mungu walikuwa na vikao vya namna mbalimbali wakati wa kusali; hata hivyo sala zao zilisikiwa. Wengine walipiga magoti; wengine walisimama. Nehemia alisali angali amesimama mbele ya mfalme wa Uajemi. Yona alipiga kelele akiwa katika tumbo la samaki mkubwa sana, na ni vigumu kueleza alikuwa katika kikao gani wakati huo. (Danieli 6:10; 1 Wafalme 8:22; Nehemia 2:1-5; Yona 2:1, 2) Kwa hiyo ingawa huenda tukataka kuwa katika kikao kitakachotusaidia kukaza fikira kwenye sala zetu, jambo la maana ni kuwa na tamaa ya unyofu wa moyo ya kumfikia Mungu katika sala. Tunaweza kufanya hivyo wakati wo wote, katika mahali po pote na chini ya hali zo zote.—Waefeso 6:18.
Njia Inayofaa Kupitishia Sala
Yehova Mungu amethibitisha njia ya kupitia ili kumfikia yeye. Yesu alieleza hivi: “Mimi ndimi njia . . . ; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.”—Yohana 14:6.
Wengi wanaamini kwa unyofu kwamba wakisali kwa jina la “mtakatifu” fulani, au hata kwa jina la mama wa kidunia wa Yesu, Mariamu, watapata matokeo mazuri. Lakini kama kweli tunataka “Baba yetu” ajibu sala zetu, kwa uhakika tunapaswa kupitia njia ambayo yeye ameweka. Hiyo tu ndiyo njia yetu ya kumfikia Mungu. Ni kama vile Yesu alivyosema: “Mkimwomba Baba neno lo lote atawapa kwa jina langu.”—Yohana 16:23.
Si za Kurudia-rudia Yale Yale Tu
Wakati Yesu alipoisema Sala ya Kielelezo, je! alikusudia wafuasi wake wawe wakirudia maneno yale yale aliyotumia kila wakati walipopelekea Mungu sala? Yeye aliianza sala hiyo kwa kusema: “Basi ninyi salini hivi” wala si ‘kwa kutumia maneno haya.’ (Mathayo 6:9) Wakati mwingine wafuasi wa Yesu walimwambia hivi: “Bwana, tufundishe sisi kusali.” Kwa kujibu, Yesu alitoa sala yenye mawazo yanayofanana na yale yaliyo katika Sala ya Kielelezo, lakini akatumia maneno tofauti. Alisema: “Baba, Jina lako litakaswe, Ufalme wako uje, Utupe siku kwa siku riziki yetu. Utusamehe dhambi zetu, kwa kuwa sisi nasi tunamsamehe kila tumwiaye. Na usitutie majaribuni.” Kwa hiyo, Sala ya Kielelezo ilikuwa kiolezo cha njia tunayopaswa kusali kwayo. Inatuonyesha namna ya mambo tunayopaswa kuomba na ubora unaotofautiana wa mambo hayo.—Luka 11:1-4.
Kulingana na hayo, je! Mungu atasikia sala zinazosomwa katika kitabu cha sala? Kama wewe una mtoto, je! ungependezwa akisema nawe kwa kutumia maneno aliyosoma katika kitabu fulani, yakiwa yametayarishwa na mtu mwingine? Au ungependelea yeye aseme yaliyo katika moyo wake mwenyewe? Kwa uhakika Yehova Mungu anapendelea tuseme naye kutokana na yaliyo moyoni mwetu, si kutokana na kitabu cha sala. Mfalme Daudi alisema hivi: “Mbele zake [Mungu] mwageni moyo wenu.” (Zaburi 62:8, NW) Kuongezea hilo, Yesu alituonya hivi: “Mkiwa katika kusali, msipayuke-payuke.”—Mathayo 6:7.
Kupatana na Mapenzi ya Mungu
Mtume Yohana alituandikia hivi: “Huu ndio ujasiri tulio nao kwake [Mungu], ya kuwa, tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake, atusikia.” (1 Yohana 5:14) Hilo hapo ni takwa jingine tunalopaswa kutimiza ili sala zetu zisikiwe na Mungu. Sala zetu zinapasa kupatana na mapenzi ya Mungu. Zaidi ya hilo, tukiisha kusali inatupasa tuhakikishe tunatenda kupatana na sala zetu.
Kornelio, aliyekuwa afisa wa kijeshi Mwitalia wa karne ya kwanza ‘alipelekea Mungu dua kwa kuendelea.’ Yehova alisikia sala zake na kumpa msaada ili ajifunze mengi zaidi juu ya mapenzi ya kimungu. Je! Wewe unataka Mungu asikie sala zako? Basi soma Biblia ujue mapenzi ya Mungu ni nini ili sala zako ziweze kupatana nayo. Wakiwa chini ya mwelekezo wa Mungu, Mashahidi wa Yehova watapendezwa sana kukupa msaada wa namna ile ile ambayo mtume Petro alimpa Kornelio kuhusiana na jambo hilo.—Matendo 10:2-5.
“Katika kila neno kwa kusali . . . haja zenu na zijulikane na Mungu.” (Wafilipi 4:6, 7) Endelea kuomba—kwanza mambo yanayohusiana na Mungu: jina lake, ufalme wake na mapenzi yake. Halafu omba mambo yanayohusu mahitaji yako ya kibinafsi na ya wanadamu wenzako. Fanya hivyo kupatana na aliyosema Yesu katika ile Sala ya Kielelezo. Jifuatanishe na matakwa ya Mungu yanayohusu sala, kisha Yehova na azisikilize sala zako kwa kuzikubali.