Maoni ya Biblia
Kristo Yupo!
“MANDELA anakuja! Mandela anakuja!” wakaimba watoto wa Soweto, Afrika Kusini. Kufunguliwa kwa Mandela kutoka jela mnamo Februari 11, 1990, kulitazamiwa sana kuwa mwanzo wa mabadiliko katika Afrika Kusini. Hata hivyo, kwa miaka mingi kabla hajafunguliwa, kuwapo kwake kulihisiwa. Akiwa angali katika jela, alikuwa “ameendeleza kwa bidii vita vya kukomesha ubaguzi wa rangi.” Kama vile gazeti moja la kimataifa lilivyotaja, miaka 27 ya kufungwa kwake gerezani “hakukupunguza kuwapo kwake—wala vita vyake.” Kufunguliwa kwake kutoka jela kwaonyesha vyema tofauti kati ya kuja na kuwapo.
Hali kadhalika, wakirejezea Yesu Kristo akichukua mamlaka ya kifalme, waandikaji wa Biblia wa karne ya kwanza walitofautisha kati ya kuja kwake na kuwapo kwake. Kuwapo kwa Kristo Yesu katika mamlaka ya kifalme kungehisiwa na kutambuliwa miaka mingi kabla ya yeye ‘kuja juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na utukufu mwingi.’ (Mathayo 24:30) Kuwapo kwa Kristo kusikoonekana (Kigiriki, pa·rou·si΄a) kungetangulia kuja huku (Kigiriki, er΄kho·mai) kutekeleza hukumu dhidi ya kizazi kikaidi na kipotovu.
Pa·rou·si΄a—Inamaanisha Nini?
Neno la Kigiriki pa·rou·si΄a lamaanisha kihalisi “kuwa kando ya” na “likawa neno rasmi la ziara ya mtu mkuu, hasa ya wafalme na watawala wanaozuru mkoa fulani.” Theological Dictionary of the New Testament chaeleza hivi: “[parousia] hasa yaonyesha kuwapo kwenye utendaji.” Na kuhusu kuwapo kwa Kristo Yesu, kitabu The Parousia chaeleza hivi: “Maandiko hayaelezi kamwe juu ya ‘parousia ya pili.’ Hata asili yayo iwe ingekuwa nini, ingekuwa ni jambo la pekee, ambalo halingekuwa limetukia kabla ya wakati huo, na ambalo halingetukia tena. Kungekuwa ni kuwapo ambako ni tofauti na kwa hali ya juu zaidi kuliko madhihirisho mengine yake kwa wanadamu.”
Akitoa maelezo juu ya maneno ya kiunabii ya Yesu alipokuwa akijibu maswali yaliyoulizwa na mitume katika Mlima wa Mizeituni, Profesa A. T. Robertson katika kitabu Word Pictures in the New Testament aandika kwamba Yesu alikuwa “akitumia uharibifu wa hekalu na Yerusalemu uliotukia katika kizazi hicho katika 70 W.K., kuwa mfano wa kuja kwake mwenyewe kwa pili na wa mwisho wa ulimwengu . . . au ukamilisho wa enzi hii.” Hayo yalikuwa ni maswali gani, na Yesu aliyajibuje?
Ishara ya Kuwapo kwa Kristo
Kama ilivyoandikwa katika Mathayo 24:3, mitume waliuliza hivi: “Tuambie, mambo hayo yatakuwa lini? Nayo ni nini dalili ya kuja [kuwapo, NW] kwako, na ya mwisho wa dunia?” Akijibu, Yesu aliwapa wanafunzi ishara ambayo ingekuwa uthibitisho wenye kuonekana wa kuwapo kwake kusikoonekana katika mamlaka ya Ufalme. Ishara kamili ilitia ndani vita vingi, ukosefu wa chakula wenye kuenea, matetemeko ya ardhi yenye uharibifu mwingi, magonjwa ya kipuku, ongezeko la uhalifu na woga. Kuwapo kwa Kristo kungekuwa wakati wa msukosuko na hangaiko la duniani pote. Serikali za kibinadamu na viongozi wa kilimwengu wangeshindwa kukabiliana kwa mafanikio na mfumo unaozorota.—Mathayo 24:7, 12; Luka 21:11.
Akithibitisha uhakika wa maneno ya Yesu ya kiunabii, profesa wa masomo ya kisiasa, John Meisel, alisema: “Muhula mkubwa unakwisha, ubadilishwe na ule ambao bado muundo wao hautambuliki vizuri.” Baada ya kueleza juu ya kifo cha Ukomunisti, kushindwa kwa Usosholisti, na kutofaa kwa ubepari, Profesa Meisel aliendelea kusema hivi: “Magumu mengi yanayowapata wanadamu yanashinda sayansi ya kijamii na yanahitaji njia nyinginezo za kuyatatua.” Jambo hilo lamaanisha nini? “Mawazo makuu yanayoaminiwa na ulimwengu wa sasa yanaporomoka na yanahitaji kubadilishwa.”
Kuwapo Kwenye Utendaji kwa Kristo
Zijapokuwa hali mbaya sana za ulimwengu unaozidi kuzorota, kuwapo kwa Yesu katika mamlaka ya kifalme kulianza zaidi ya miaka 75 iliyopita na kumehisiwa kwa njia yenye kuonekana na iliyo wazi.a Ujapokuwa ule uharibifu uliosababishwa na vile vita vikuu viwili vya ulimwengu, Mfalme aliyetawazwa Kristo Yesu, ameshiriki kwa vitendo katika kutokeza taifa jipya la watu—watu kwa ajili ya jina la Yehova “wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.” Kuwapo kwenye utendaji kwa Kristo kumechochea programu ya ulimwenguni pote ya kuhubiri na kufundisha ambayo imegusa mioyo ya mamilioni ya watu wenye maelekeo mema. Wamesukumwa na mioyo yao wachukue msimamo wao upande wa Ufalme wa Yehova ulio mikononi mwa Kristo Yesu.—Ufunuo 7:9, 10.
Kwa sababu ya ushuhuda unaongezeka kila siku wa ishara yenye sehemu nyingi ya kuwapo kwa Kristo, ni wazi kwa Mkristo aliye macho kwamba tunakabili mwisho wa muhula. Sasa ndio wakati wa ‘kumzingatia kwa makini zaidi’ Mfame aliyetawazwa, Kristo Yesu. (Waebrania 2:1, Habari Njema kwa Watu Wote). Yeye atuonya kwa upole hivi: “Basi, kesheni, ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.”—Luka 21:36.
[Maelezo ya Chini]
a Utawala wa kifalme wa Yesu Kristo ulianza katika 1914. Kwa maelezo marefu zaidi juu ya jambo hilo, ona sura 16 hadi 18 za kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichotangazwa katika 1982 na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.