Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 11/15 kur. 522-526
  • Ni “Ishara” Gani Wanayoitazamia Wakristo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni “Ishara” Gani Wanayoitazamia Wakristo?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUEPUKA MATARAJA YASIYOFAA
  • KRISTO ANATAWALA KWA KITAMBO KABLA YA UTAWALA WA MIAKA ELFU
  • “KUJA” AU “KUWAPO”​—JAMBO JIPI?
  • HAJA YA KUWA MACHO
  • Kuangaza Nuru Juu ya Kuwapo kwa Kristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Je! Kristo Angeweza Kurudi Pasipo Kuonekana?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Kuja kwa Yesu au Kuwapo kwa Yesu—ni Kupi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Kristo Yupo!
    Amkeni!—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 11/15 kur. 522-526

Ni “Ishara” Gani Wanayoitazamia Wakristo?

Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi

1-3. “Wakristo” wengine wametazamia nini kwa habari ya kuja kwa Kristo katika mamlaka, nayo maoni yao yanalinganaje na yale ya waandishi na Mafarisayo?

KWA karne kumi na tisa Wakristo wamekutazamia kuja kwa Kristo katika mamlaka.

2 Wengine wametazamia kuonekana kwa ghafula na kwa mwujiza angani, au wakaamini kwamba wale ‘wanaozaliwa mara ya pili’ kama ndugu za kiroho wa Kristo watatoweka kwa ghafula na kwa mwujiza watoke usoni pa dunia, wakipelekwa mbinguni.

3 Maoni haya yanalingana na yale ya waandishi na Mafarisayo wa kidini wa karne kumi na tisa zilizopita. Wao walitaka ishara kutoka kwa Yesu Kristo, iwasadikishe kwamba yeye alikuwa ndiye Masihi. Walitaka aonekane angani, akiwa na mamlaka kuu na utukufu, ili wote waweze kuona kwa macho yao ya asili. Lakini yeye alikataa.​—Mt. 12:38; linganisha Danieli 7:13, 14; Mathayo 26:64.

KUEPUKA MATARAJA YASIYOFAA

4. Kwa sababu gani ni jambo la akili na linalolingana na Maandiko kuamini kwamba wale wanaotazamia kuja kwa Kristo kwa njia ya kuonekana wanakosea?

4 Twaweza kukosea kwa kuwa na taraja kama hilo, tukitazamia mwujiza, upate kutusadikisha. Hii inatofautiana na maneno ya mtume kwamba “twaenenda kwa imani, si kwa kuona.” (2 Kor. 5:7) Kama vile kulivyokuwa na mashuhuda mengi wakati Yesu alipokuwa duniani kwa waliokuwa na imani katika Yehova Mungu kuweza kumkubali Yesu kama Masihi, ndivyo na leo kulivyo na uhakikisho wa kutosha wa kutenda kwake sasa katika mambo ya dunia. Mtume anasema hivi: “Imani . . . ni bayana ya mambo yasiyoonekana.” (Ebr. 11:1) Kwa hiyo vitu vinavyoimarisha imani si vitu vionekanavyo sikuzote, na huenda hata yakawa mambo yaliyo tofauti sana na yale ambayo tumeongozwa na maoni au tamaa za kipekee tuyatazamie.

5, 6. Kwa sababu gani tupendezwe na utawala wa miaka elfu wa Kristo, na ni nini kinachoonyesha kwamba unakaribia?

5 Kwa hiyo, ni vema kuchunguza kwa makini tuone yanayosemwa na Biblia kuwa mashuhuda ya kuwapo kwa Kristo na kukaribia kwa utawala wake wa miaka elfu juu ya dunia.

6 Utawala wa Ufalme wa Kristo wa miaka elfu unaahidi hali zilizo bora​—hali wasizopata kuziona wanadamu. Kwa hiyo, imempasa kila mtu atazamie mashuhuda ya kukaribia kwake kwa kupendezwa na kwa shauku nyingi. Kitabu cha Biblia cha Ufunuo (sura 20 na 21) kinafunua mengi ya mambo mema yatakayoletwa na utawala wa miaka elfu. Kinatuambia pia kwamba utawala huu wa miaka elfu lazima utanguliwe muda mfupi tu na vita yenye maangamizi makubwa zaidi kuliko zote katika historia ya kibinadamu. Twaweza kuwaona watawala wa kisiasa au “wafalme wa ulimwengu wote” wakikusanywa, chini ya majeshi yenye uwezo upitao ule wa wanadamu, kwa ajili ya Vita ya vita vyote, penye mahali paitwapo Har–​Magedoni.​—Ufu. 16:13-16.

KRISTO ANATAWALA KWA KITAMBO KABLA YA UTAWALA WA MIAKA ELFU

7. Habari katika Ufunuo zinaonyeshaje kwamba Kristo Yesu anaanza kutawala kama Mfalme kabla ya utawala wa miaka elfu pamoja na warithi wenzake kuanza?

7 Ukiusimulia mpango wa vita hiyo, Ufunuo unafunua kwamba Kiongozi wa majeshi ya kimbinguni ya Yehova atakuwa upande wa Mungu Mwenye Nguvu Zote. Yeye anaitwa Mwaminifu na Wakweli, Neno la Mungu. Anaonyeshwa kama aliyeanza kutawala tayari kama Mfalme kabla ya vita penye Har–​Magedoni kuanza. Habari zinamsimulia Kristo akielekea vitani: “Naye ana jina limeandikwa katika vazi lake na paja lake, MFALME WA WAFALME, NA BWANA WA MABWANA.” (Ufu. 19:11-16; linganisha Ufunuo 12:5, 10-12.) Hivyo yeye anatawala kama Mfalme kabla ya kuingia katika hicho kipindi cha miaka elfu cha kutawala pamoja na warithi wenzake wa Kikristo 144,000.​—Ufu. 14:1-4; 20:4-6.

8, 9. Njozi ya Yohana katika Ufunuo sura ya 6 inaonyeshaje kwamba Kristo anatawala kama Mfalme kabla ya utawala wa miaka elfu?

8 Uhakikisho zaidi unatolewa, katika mfano mwingine, kwamba Kristo ‘angekuwapo,’ katika maana ya kuelekeza fikira zake na kutumia mamlaka yake ya kifalme juu ya dunia. (Linganisha ‘kushuka’ kwa Yehova katika Mika 1:3; 2 Samweli 22:10.) Katika sura ya sita ya Ufunuo mtume Yohana anaandika njozi yake ambamo alimwona Mwana-Kondoo wa Mungu, Yesu Kristo, akianza kuzifungua muhuri saba akiwa amekishika “kitabu” kilichokunjwa alichokuwa amekipokea mkononi mwa Mungu. Yohana anaandika hivi: “Kisha nikaona hapo Mwana-Kondoo alipofungua moja ya zile muhuri saba, nikasikia mmoja wa wale wenye uhai wanne akisema, kama kwa sauti ya ngurumo, Njoo! Nikaona, na tazama, farasi mweupe, na yeye aliyempanda ana uta, akapewa taji, naye akatoka, ali akishinda tena apate kushinda. Na alipoifungua muhuri ya pili, nikamsikia yule mwenye uhai wa pili akisema, Njoo! Akatoka farasi mwingine, mwekundu sana, na yeye aliyempanda alipewa kuiondoa amani katika nchi, ili watu wauane, naye akapewa upanga mkubwa.”​—Ufu. 6:1-4.

9 Mfano huu wa unabii unayafananisha mambo yaliyotukia duniani kuanzia na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza mwaka wa 1914 C.E. Yesu Kristo anaonyeshwa akitawazwa kama Mfalme, akipanda farasi mweupe wa vita yenye haki. Mpanda farasi mwekundu sana anafananisha mfululizo wa vita vya kidunia, ambavyo vimeiharibu dunia sana tangu mwaka huo wa 1914 C.E.

10. Mtunga zaburi aonyeshaje kwamba kuwapo kwa Kristo kama Mfalme kunatangulia utawala wa miaka elfu?

10 Pia, mtunga zaburi aliyeongozwa kwa roho alitabiri waziwazi kwamba Yesu Kristo angeanza kutawala kama Mfalme wakati fulani kabla “wafalme wa ulimwengu” hawajaharibiwa na kabla hajaanza utawala wake wa miaka elfu. Kwa unabii, aliandika hivi: “Mbona mataifa wanafanya ghasia, na makabila wanatafakari ubatili? Wafalme wa dunia wanajipanga, na wakuu wanafanya shauri pamoja, juu ya [Yehova], na juu ya masihi wake [Kristo wake, Septuagint Version ya Kigiriki], Na tuvipasue vifungo vyao, na kuzitupia mbali nasi kamba zao. Yeye aketiye mbinguni anacheka, Bwana anawafanyia dhihaka. Ndipo atakaposema nao kwa hasira yake, na kuwafadhaisha kwa ghadhabu yake. Nami nimemweka mfalme wangu juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu.”​—Zab. 2:1-6; linganisha Matendo 4:24-30.

11. Twajuaje kwamba kuwapo kwa Kristo katika mamlaka ya kifalme ni kuwapo kwa kutokuonekana?

11 Kwa hiyo, baada ya mwanzo wa kuwapo kwa Kristo katika mamlaka ya Ufalme na utukufu, kutakuwako kipindi ambamo atakuwa mwenye shughuli nyingi akifanya hukumu ya hii taratibu ya mambo na mwishowe aiharibu kabisa. (Zab. 2:8-12; 110:2-6) Wakati huu atakuwa asiyeonekana kwa macho ya kibinadamu, kwa maana sasa yeye ni “chapa ya nafsi” ya Mungu asiyeonekana, ambaye ‘hakuna mtu aliyemwona wakati wo wote.’ Kristo sasa “amekaa katika nuru isiyoweza kukaribiwa,” na “hakuna mwanadamu aliyemwona, wala awezaye kumwona.”​—Ebr. 1:3; Yohana 1:18; 1 Tim. 6:16.

12. Yesu aliwafanyia wanafunzi wake nini, kwa sababu parousia yake au kuwapo kungekuwa kusikoonekana?

12 Kwa kuwa Kristo alipaswa asionekane kwa macho ya kibinadamu wakati wa kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme tangu mwaka wa 1914 C.E. na kuendelea, kwa huruma aliwapa wanafunzi wake “ishara” ambayo kwayo wangeweza kujua na kuelewa wakati huo ukifika. Aliitabiri “ishara” hii mara tu baada ya alipoutabiri uharibifu wa hekalu katika Yerusalemu. Wakati wa kuisimulia “ishara” ulikuwa muda mfupi baada ya alipokuwa amewaambia hivi viongozi wa kidini wa Kiyahudi waliomkataa: “Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa. Kwa maana nawaambia, Hamtaniona kamwe tangu sasa, hata mtakaposema, Amebarikiwa ajaye kwa jina la [Yehova].”​—Mt. 23:38, 39.

13. Twaonaje kwamba maneno ya Yesu katika Mathayo 23:38, 39 hayakutimizwa penye hekalu la halisi Yerusalemu?

13 Maneno haya makali ya Yesu yalionyesha kwamba alikuwa akienda, na kwamba wangekuwako wale ambao wangeyatumia maneno ya unabii ya Zaburi 118:26 na kusema: “Na abarikiwe yeye ajaye kwa jina la [Yehova].” Lakini maneno haya yasingesemwa penye hekalu hilo lililoonekana katika Yerusalemu. Hii ilionyeshwa wazi na maneno yaliyofuata ya Yesu. Habari zinasema hivi: “Yesu akaenda zake, akatoka hekaluni; wanafunzi wake wakamwendea ili kumwonyesha majengo ya hekalu. Naye akajibu akawaambia, Hamyaoni haya yote? Amin, nawaambieni, Halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa.”​—Mt. 24:1, 2.

“KUJA” AU “KUWAPO”​—JAMBO JIPI?

14-16. Mitume wa Yesu walimwuliza ulizo gani, nao walikuwa wakiuliza nini?

14 Halafu Yesu na mitume wake kumi na wawili wakatoka Yerusalemu wakapanda Mlima wa Mizeituni uliokuwa karibu. Wakiwa wamekaa mahali ambapo wangeweza kuuona mwundo wote wa hekalu vizuri, walivutwa sana. Mwishowe wanne kati ya mitume wake wakatoa ulizo lililowapendeza wote. Kulingana na tafsiri ya New World Translation, ulizo lao lilikuwa hili: “Tuambie, Mambo haya yatakuwa lini, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako [pa·rou·siʹa Kigiriki] na ya mwisho wa taratibu ya mambo?”​—Mt. 24:3; Marko 13:3, 4.

15 Tafsiri nyingine za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zinalitambua neno hili pa·rou·siʹa kama likimaanisha “kuwapo.” Young’s Literal Translation of the Holy Bible yasema hivi: “Tuambie, mambo haya yatakuwa lini? nayo ni nini ishara ya kuwapo kwako, na ya mwisho kamili wa kizazi?” Rotherham’s The Emphasised Bible yasema hivi: “Tuambie mambo haya yatakapokuwa,​—na ishara ya kuwapo kwako na mwisho wa kizazi ni nini.”

16 Angalia kwamba mitume waliuliza juu ya Parousia ya Bwana Yesu Kristo. Je! walikuwa wakiuliza juu ya “kuja” kwake au “majilio,” kama wengine wanavyokuita? Sivyo. Liangalie neno lililotumiwa kwa kuja kwa Kristo na Mkristo aliyeuawa kwa sababu ya imani yake Stefano alipoihutubia Sanhedrin ya Kiyahudi: “Ni yupi katika manabii ambaye baba zenu hawakumwudhi? nao waliwaua wale waliotabiri habari za kuja [eʹleu·sis, Kigiriki] kwake yule Mwenye Haki; ambaye ninyi sasa mmekuwa wasaliti wake, mkamwua.” (Matendo 7:52) Angalia kwamba neno eʹleu·sis, si neno pa·rou·siʹa, lilitumiwa. Ni maneno mawili ya Kigiriki yaliyo tofauti katika namna na asili, na pia katika maana.

17-19. Eleza maana ya neno la Kigiriki parousia.

17 Ni nini maana ya neno la Kigiriki pa·rou·siʹa? Linamaanisha kwa halisi “kuwa kando ya,” usemi huu ukiwa umetolewa katika preposition ya Kigiriki paraʹ (“kando ya”) na ousía (“kuwa”). Ebu na tuone wanavyosema wabuni kamusi.

18 Liddell na Scott’s A Greek-English Lexicona inaonyesha neno la Kiingereza “presence” (“kuwapo”) kama ufafanuzi wa kwanza wa parousia. Inaonyesha “arrival” (“kufika”), kama ufafanuzi wa pili, kisha inaongeza: “Hasa ziara ya mtu wa kifalme au aliye mashuhuri.”

19 Kupatana na hili, Theological Dictionary of the New Testament (iliyochapwa na Gerhard Friedrich)b inaonyesha neno la Kiingereza “Presence” kama “Maana ya Jumla.” Halafu, kama “Matumizi ya Ustadi ya Maneno,” katika Kigiriki, inaonyesha “1. Ziara ya Mtawala.” Inasema kuhusu “Matumizi ya Ustadi ya páreimi [kiarifa] na parousía katika Agano Jipya.”: “Katika Agano Jipya maneno hayo hayatumiwi kamwe kuonyesha kuja kwa Kristo katika mwili, na parousía halimaanishi kurudi kamwe. Wazo la zaidi ya parousía moja laonekana katika Kanisa la baadaye tu.”

20. Kwa kuuangalia ufafanuzi wa wabuni kamusi juu ya parousia, twaonaje wanafunzi walilotaka kujua hasa?

20 Kwa hiyo, wanafunzi wa Yesu walikuwa wakiuliza juu ya muda wa baada ya kufika kwake, si juu ya “kufika” kwake kwa wakati ujao. Na ikiwa, badala ya kutumia neno “kuwapo,” twafuata “matumizi ya ustadi ya maneno” katika Kigiriki, wanafunzi wataeleweka kuwa walimwuliza Yesu hivi: “Ni nini itakayokuwa ishara ya [ziara yako kama mtu wa kifalme] na ya mwisho wa taratibu ya mambo?” “Ziara” inatia mengi zaidi kuliko “kufika” tu. Inatia na “kuwapo.”

21. Je! ufafanuzi uliotajwa juu wa parousia ni wenye msingi mzuri?

21 Katika linaloitwa Agano Jipya neno la Kigiriki parousía linaonekana mara 24, mara zote linapoonekana humo, si New World Translation of the Holy Scriptures peke yake inayolitafsiri neno hilo kila mara kama “kuwapo,” bali pia tafsiri nyingine zinafanya hivyo, kama vile Young’s Literal Translation of the Holy Bible, ya 1862 C.E.; Wilson’s The Emphatic Diaglott, ya 1857-1863 C.E.; na Rotherham’s The Emphasised Bible, ya 1897 C.E. Twaona namna “kuwapo” na “kutokuwapo” yanavyotofautishwa kwa kufaa, katika Wafilipi 2:12, ambapo mtume Paulo asema hivi: “Kama vile mlivyotii sikuzote, si wakati mimi nilipokuwapo tu, bali sasa zaidi sana mimi nisipokuwapo.”

22. Kwa sababu gani kuwapo kwa Kristo kusingaliweza kutokea mwaka wa 70 C.E.?

22 “Kuwapo” kwa Kristo, walikouliza wanafunzi wake, kusingaliweza kutokea wakati wa kuharibiwa kwa Yerusalemu na Warumi mwaka wa 70 C.E. Kwa sababu gani sivyo? Ijapokuwa ni kweli kwamba taratibu ya mambo ya Kiyahudi ilikoma wakati huo, taratibu ya mambo iliyo kuu zaidi iliyofananishwa kwa unabii na taratibu hiyo ya Kiyahudi haikukoma wakati huo. Hii ilipaswa itokee wakati wa pa·rou·siʹa, iliyopaswa kufikia upeo katika “dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.” (Mt. 24:21) Dhiki ya Yerusalemu mwaka wa 70 C.E. ilikuwa mbaya kupita zote alizopata kuziona, lakini bila shaka haikuwa mbaya zaidi kuliko gharika ya dunia nzima ya siku za Nuhu nayo haikuwa na maangamizi makuu kuliko ambayo mwisho wa hii taratibu nzima ya mambo ya ulimwengu utakuwa nayo.

HAJA YA KUWA MACHO

23, 24. Jibu la Yesu lilikuwa la kadiri gani, na kwa sababu gani tulifikirie kwa makini?

23 Kwa hiyo, pa·rou·siʹa au “kuwapo” kwa Bwana Yesu Kristo ni kuwapo kwake au kuzuru kama Mfalme, kwa kutokuonekana, katika mamlaka ya kifalme na utukufu. Kwa hiyo “ishara” inahitajiwa ili watu duniani waweze kufahamu kuwapo huko. Kulingana na njia yake ya kawaida ya kuyasikiliza kwa upole maulizo yote yaliyoulizwa na wanafunzi wake, Yesu aliwapa jibu lenye maelezo mengi zaidi hata kuliko walivyotazamia. Sura zote za Mathayo 24 na 25, pamoja na habari zinazolingana katika Marko sura ya 13 na Luka sura ya 21, zinatoa sehemu nyingi za “ishara” ya kuwapo kwake.

24 Kwa hiyo, inafaa tuyafikirie kwa makini mambo ambayo Yesu alionyesha yangetoa uhakikisho wa kutosha juu ya kuwapo kwake kwa kutokuonekana. “Ishara” hii pamoja na sehemu zake nyingi, kama ilivyoonyeshwa na Yesu, siyo ishara ya kuonyesha kwamba anakuja, bali kwamba yeye yupo, akielekeza fikira zake na mamlaka isiyoonekana duniani.

25. Wakristo watatofautianaje na watu wa kidini wa Kristendomu katika shauri la kutazamia ishara?

25 Wale walio na ufahamu, wakitumia ‘macho ya moyoni,’ wataufahamu uhakika huo. Kama vile nabii Danieli alivyoandika: “wao walio na hekima ndio watakaoelewa.” (Dan. 12:10) Kama Kristo akitokea kwa namna ya kuonekana kwa mng’ao, au kwa kufanya matukio ya mwujiza ulimwenguni pote, hekima ingehitajiwaje? Kwa hiyo, Wakristo wa kweli hawatakuwa kama wale walio na taraja lisilofaa; bali watakuwa na hekima na ufahamu, nao ‘watainua vichwa vyao, kwa kuwa ukombozi wao umekaribia.’​—Luka 21:28, 36.

​—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.

[Maelezo ya Chini]

a Volume ya 2, ukurasa 1343.

b Volume ya 5, kurasa 859, 865.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki