Je! Kristo Angeweza Kurudi Pasipo Kuonekana?
KWA SABABU gani ulizo hilo Iitokezwe? Kwa sababu tu Yesu mwenyewe aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Ndipo itakapoonekana ishara yake Mwana wa Adamu mbinguni; ndipo mataifa yote ya ulimwengu watakapoomboleza, nao watamwona Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na utukufu mwingi.” (Mathayo 24:30) Walakini baadaye alipokuwa akila chakula cha jioni chake cha mwisho pamoja na wanafunzi wake, yeye alisema: “Bado kitambo kidogo na ulimwengu haunioni tena; bali ninyi [mtaniona]. Na kwa sababu mimi ni hai, ninyi nanyi mtakuwa hai.” (Yohana 14:19) Jambo hilo linaloonekana kuwa kupingana linafanywa liwe gumu zaidi na ufunuo aliopewa mtume Yohana miongo sita baadaye. Unasema hivi: “Tazama, yuaja na mawingu; na kila jicho litamwona, na hao waliomchoma; na kabila zote za dunia wataomboleza kwa ajili yake.”—Ufunuo 1:7.
Je! huko ‘kuona’ kunapasa kuchukuliwa kwa njia halisi? Au je! kwaweza kuwa na maana kubwa zaidi? Umaana wa maulizo hayo unaonyeshwa na yale yaliyotokea katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu, wakati Wayahudi wengi walipokuwa wakimtazamia Masihi wao.
JE! ANGEWEZA KUTOKEA, LAKINI ASITAMBULIWE?
Huenda ulizo la kwanza kabisa huko nyuma lilikuwa, ‘Je! Masihi, au Kristo; angeweza kutokea pasipo kutambuliwa?’ Bila shaka angeonekana kama mtu, lakini je! Wayahudi wangeweza kumtofautisha kuwa Yule aliyetumwa na Mungu?
Maandishi ya Biblia yanaonyesha waziwazi namna wengi kati ya umati wa watu walivyoitikia. Alipoingia Yerusalemu kwa ushindi, wao walikuwa wakipaza sauti hivi: “Hosana, Mwana wa Daudi; ndiye mbarikiwa, yeye ajaye kwa jina la [Yehova].” Wengine walipouliza hivi “Ni nani huyu?” umati wa watu uliendelea kusema: “Huyu ni yule nabii, Yesu, wa Nazareti ya Galilaya.” Ilionekana kwao kama kwamba mwanamume huyo mwenye kufanya miujiza angechukua hatua na kuwaweka huru Wayahudi na nira ya Warumi. Walakini mambo hayakuwa hivyo. Yesu hakuwa mleta mapinduzi wa kisiasa, bali, mahali pake, alisitawisha uhuru wa kiroho na usafi wa kidini. Oo, wenye kutazamia kutukuza taifa huko nyuma walishuka moyo kama nini! “Masihi” huyo hakufaa wazo walilotangulia kuwa nalo la mwokozi wa Israeli. Ilikuwa tofauti kama nini kati ya umati wa watu wenye urafiki Nisani 9 (Jumapili) na genge la watu wenye kiu ya kutaka kumwaga damu Nisani 14 (Ijumaa)! “Wakasema wote, [Atundikwe]. . . . Damu yake na iwe juu yetu, na juu ya watoto wetu.”—Mathayo 21:9-11; 27:22-25.
Kwa sababu ya kukosa ufahamu, wengi kati ya Wayahudi walikosa pendeleo tukufu la kuwa wafalme pamoja na Kristo katika ufalme wake wa kimbinguni. Mawazo yao ya kisiasa na ya kutukuza taifa yaliwapofusha wasione baraka za kiroho ambazo zingewaletea mema. Wao walitaka masihi wa kizazi chao tu kwa ajili ya lile tatizo lao moja—kukaliwa kwa nchi yao na Warumi. Walishindwa kumtambua Masihi wa kweli ajapoonyesha sifa zake zote za kumtambulisha.—Mathayo 1:21—2:6.
JE! KUNA UFANANI WA KISASA?
Je! yawezekana kwamba jambo kama hilo limetokea katika karne yetu ya 20? Je! yawezekana kwamba mamilioni kwa kukosea wanatazamia kumwona Kristo akija kwa njia halisi juu ya mawingu?
Katika onyo ambalo Yesu aliwapa wafuasi wake, tuna kionyesho kilicho karibu cha kujibu maulizo hayo: “Mtu akiwaambia, Tazama, Kristo yupo hapa, au yuko kule, msisadiki. Kwa maana watatokea makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu; wapate kuwapoteza, kama yamkini, hata walio wateule. Tazama, nimekwisha kuwaonya mbele.” (Mathayo 24:23-25) Jambo hilo linaonyesha kwamba kuwapo kwa Kristo hakutaonekana katika sehemu hii wala hii ya dunia. Kwa hiyo, wale wanaodai kuwa ndio Kristo aliyerudi, au kuwa walimwona “hapa” au “kule,” ama wamedanganywa au wao ni mabandia.
Ufunguo wa kufahamu jambo hilo unapatikana katika ulizo ambalo wanne kati ya wanafunzi wa Kristo walimwuliza Bwana yao walipokuwa wakitazama Yerusalemu na hekalu lake wakiwa juu ya Mlima wa Mizeituni uliokuwa karibu. Yesu alikuwa amewashtua kwa kutabiri kwamba hekalu hilo, makao makuu yenyewe ya ibada ya Wayahudi wakati huo, lingeharibiwa kabisa. Kwa hiyo walimwuliza hivi “Tuambie, Mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo [Kigiriki, parousia] kwako na ya umalizio wa taratibu ya mambo?”
Sasa, pengine ungependa kulinganisha andiko hilo, ambalo limeandikwa kulingana na tafsiri ya New World, na tafsiri yako mwenyewe ya Biblia. Kulingana na Union Version, andiko hilo linasema hivi: “Ni nini dalili ya kuja kwako, na ya mwisho wa dunia?” Habari Njema kwa Watu Wote inasema hivi: “Ni ishara gani itakayoonyesha kuja kwako na mwisho wa dunia?”—Mathayo 24:3.
Tafsiri hizo mbalimbali zilizoonyeshwa hapo zimeondosha watu kwenye njia kuhusiana na maana ya kweli na matumizi ya jibu ambalo Yesu aliwapa wanafunzi wake. Ni jambo tofauti matukio kuonyesha kwamba mtu fulani anakuja au anarudi, na ni jambo tofauti kabisa matukio kuthibitisha kwamba mtu aliyekuwa akingojewa tayari amekwisha kurudi. Pengine umekwisha kujionea jambo hilo kwenye uwanja wa ndege au kwenye kituo cha gari-moshi. Kuna tofauti iyo hiyo ambayo ni ngumu kuiona kati ya kurudi kwa Kristo na “kuwapo” kwake akiwa tayari yupo. Je! jambo hilo linakushangaza?
Lakini tunawezaje kujua tafsiri yenye kutoa maana kabisa—“kuwapo” au “kuja”? Ebu tugeuke kwenye andiko jingine linalotumia neno ilo hilo la Kigiriki parousia na tuone namna linavyotafsiriwa katika Biblia fulani zilizotangulia kutajwa. Kwa mfano, katika Wafilipi 2:12 tunasoma hivi: “Basi, wapendwa wangu, kama vile mlivyotii sikuzote, si wakati mimi nilipokuwapo [Kigiriki, parousia] tu, bali sasa zaidi sana mimi nisipokuwapo, utimizeni wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.” (Union Version) Hapo sasa Habari Njema kwa Watu Wote inasema hivi: “Wapenzi wangu, nilipokuwa nanyi mlinitii daima, na hata sasa niwapo mbali nanyi endeleeni kutii.” Linganisha Wafilipi 1:26, ambapo parousias linatumiwa.a
Ni maneno gani yanayotumiwa hapa kuwa tafsiri ya parousia? Ni ‘kuwapo’ na ‘kuwa nanyi.’ “Kufika” au “kuja” hayawezi kufaa. Inakuwa kwamba neno lenyewe la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “kuja,” eleusis, lilitumiwa na mfia-imani Mkristo Stefano alipotokeza ulizo hili la moja kwa moja katika kujitetea mbele ya mahakama ya Kiyahudi ya Sanhedrin: “Ni yupi katika manabii ambaye baba zenu hawakumwudhi? nao waliwaua wale waliotabiri habari za kuja [Kigiriki, eleuseos] kwake yule Mwenye Haki.”—Matendo 7:52.
ANGEONEKANA AU HANGEONEKANA?
Sasa ulizo ni hili, Ikiwa Yesu alitoa ishara zenye kuonekana za kuonyesha kuwapo kwake, kurudi kwake, basi je! angeonekana au hangeonekana? Mahali pa kukubali mawazo ya kidesturi juu ya jambo hilo, na tuongozwe na yale yanayoonyeshwa na Maandiko. Kwa mfano, mtume Petro aliandika hivi katika barua yake ya kwanza iliyoongozwa na Mungu: “Kwani, hata Kristo alikufa mara moja tu kuhusu dhambi, mtu mwenye haki kwa ajili ya wasio haki, ili apate kuongoza ninyi kwa Mungu, yeye akiuawa katika mwili, lakini akifanywa hai katika roho.” (1 Petro 3:18, NW) Mtume Paulo anaongeza ushuhuda, kwa kusema: “Hata imekuwa, sisi tangu sasa hatumjui mtu awaye yote kwa jinsi ya mwili. Ingawa sisi tumemtambua Kristo kwa jinsi ya mwili, lakini sasa hatumtambui hivi tena.”—2 Wakorintho 5:16.
Kama Yesu angerudi katika mwili, je! hilo lingefaidi wanadamu kweli, au halingetufaidi sana? Kwa kweli, lingetilia shaka ubora wa dhabihu yake na kusudi la kuja kwake kwa kwanza duniani. Kristo mwenyewe alisema hivi: “Mimi ndimi chakula chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni; mtu akila chakula hiki, ataishi milele. Na chakula nitakachotoa mimi [si kwa muda tu] ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.” (Yohana 6:51) Dhabihu yake ndiyo msingi wa kukombolewa kwa wanadamu, na kufufuliwa kwake kwenye uzima wa roho kunamaanisha tuna mtetezi mwenye huruma wa kututetea. Kwa hiyo Paulo aliandika hivi, “Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.” Wanadamu hawangefaidika na cho chote kama Kristo angeacha cheo hicho ili aonekane akiwa na mwili duniani.—Warumi 8:34.
Basi ni kwa njia gani nyingine Kristo anaweza kuja mara ya pili bila mwili? Kwa kusema kwa njia rahisi, ni kuwapo kwake, au parousia, akiwa Mwana wa Mungu asiyeonekana, akiwa amepewa uwezo wa Ufalme na kuelekeza fikira zake juu ya dunia. Ndiyo, sababu yeye alitupa ishara zenye kuonekana, ambazo zingethibitisha kuwapo kwake kusikoonekana.—Mathayo 24:3—25:46.
JINSI ‘ANAVYOONEKANA’
Tukiwa tunakumbuka mambo hayo makuu, na turudi kwenye maandiko yaliyotajwa mwanzoni mwa makala hii. Mojalapo lilikuwa Yohana 14:19, ambapo Yesu alisema hivi: “Bado kitambo kidogo na ulimwengu haunioni tena, bali ninyi [mtaniona]. Na kwa sababu mimi ni hai, ninyi nanyi mtakuwa hai.” Ndiyo, wafuasi wake, walakini si watu wote kwa ujumla, walimwona pindi mbalimbali baada ya kufufuliwa kwake. Hiyo si kusema kwamba yeye alikuwa ameutwaa kwa mara nyingine mwili wake uliotolewa dhabihu, bali kwamba alijivika miili ya nyama kulingana na mahitaji ya pindi iliyokuwapo, kama malaika walivyokuwa wametangulia kufanya. (Luka 1:11, 26, 27; 2:9-14) Katika pindi mbili, yeye aliwatokea wanafunzi wake walipokuwa pamoja katika chumba kimoja ingawa ‘milango ilikuwa imefungwa.’ Kwa hakika hakuna kiumbe wa kawaida mwenye mwili na damu angaliweza kutokea na kutokomea katika hali za namna hiyo.—Yohana 20:19, 26; 1 Wakorintho 15:3-8.
Bila shaka, kuna maana kubwa zaidi ya maneno ya Yesu ‘mtaniona’ kuliko tu kutokea mbalimbali alikofanya akiwa Kristo aliyefufuliwa. Yeye mwenyewe alikuwa ametangulia kusema hivi: “Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo.” Huo ulikuwa wonyesho ulio wazi kwamba wafuasi wake waliotiwa mafuta wangeshiriki pamoja naye makao yake ya kimbinguni na kumwona wakiwa na uzima wa namna hiyo.—Yohana 14:2, 3.
Lakini tunapaswaje kufahamu Ufunuo 1:7, ambapo panaonyesha kwamba hata wasioamini ‘wangemwona’? Andiko hilo linasema hivi: “Tazama, yuaja na mawingu; na kila jicho litamwona, na hao waliomchoma; na kabila zote za dunia wataomboleza kwa ajili yake.” Je! hayo yanapasa kuchukuliwa kwa njia halisi? Kristo akipanda mawingu ya halisi, kila jicho linawezaje kumwona? Kama angeonekana Australia, bila shaka hangeweza kuonekana wakati huo huo katika Afrika na sehemu nyingi nyingine za dunia, hata awe juu kadiri gani. Uhakika wa kwamba kuwapo kwa Kristo kunashirikishwa na matumizi ya mfano ya mawingu katika maandiko mbalimbali unatusaidia kufahamu kwamba kuwapo kwake lazima kuwe kusikoonekana, kwa kuwa mawingu hayawezeshi mtu aone, kama ajuavyo kila rubani wa ndege au mtu anayeongoza ndege ikiwa angani.
Sasa, ni kina nani waliomchoma? Kwa halisi, askari Warumi walimchoma, walakini kwa muda mrefu wamekuwa wafu. (Yohana 19:23, 32-34) Kwa hiyo lazima maneno hayo yawe na maana nyingine. Yesu mwenyewe anatoa kijulisho cha jambo hilo katika mfano wake wa ‘kondoo na mbuzi’ anaposema hivi: “Kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi.” (Mathayo 25:31-46) Kwa hiyo, yale mataifa na watu mmoja mmoja wanaoonea au ‘kuchoma’ wanafunzi wa Kristo waliopo duniani katika hii karne ya 20 wanahesabiwa kuwa ‘wanamchoma’ Kristo wakati huu wa kuwapo kwake kusikoonekana. Na watalazimishwa wajue uzito wa yale ambayo wamefanya na ni nani anayewahukumu. Ndiyo, ‘‘kabila zote za dunia” ‘zitamwona,’ au kufahamu kwa akili, kuwapo na kufunuliwa kwa Kristo kwa sababu ya badiliko la hali litakalowapata ghafula. Watatambua Kristo anatawala akihukumu, bali si kwa hukumu ya kuwapendelea. Watakuwa na sababu nzuri ya kujipiga wenyewe kwa huzuni.
Kwa upande mwingine, mamilioni ya watu kuzunguka ulimwengu wametambua kuwapo kwa Kristo tangu mwaka wenye matukio mengi wa 1914. Ingawa wanajua kwamba vita, njaa na matetemeko ya ardhi yamekuwa mambo ya kawaida katika vizazi vingine, wao wanatambua kwamba hakuna kizazi kingine cho chote kilichopata kujionea hata vita ya ulimwengu moja, acha mbili. Kati ya vizazi vyote vilivyotangulia hakuna kizazi ambacho kimekuwa na nguvu za kuweza kuharibu jamii yote ya kibinadamu. Lakini kizazi cha leo kina nguvu za kufanya hivyo. Ingawa watu wanajua kwamba unabii wa Kristo ulitimizwa kwa njia ndogo kabla ya kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka 70 W.K., vilevile wao wanatambua kwamba maneno ya unabii huo yalielekeza kwenye jambo kubwa zaidi. Sehemu zile nyingi za ishara aliyotabiri Yesu ziko wazi sasa, na wengine wa kizazi kilichoona mwanzo wa misiba hiyo katika mwaka 1914 wangali pamoja nasi.—Mathayo 24:34.
WEWE UTAFANYA NINI?
Kwa hiyo sasa ulizo ni hili, Utakuwa na maoni gani kuelekea kuwapo kwa Kristo kusikoonekana, parousia yake? Katika kipindi hiki ambapo watu wanazidi kutokujali wengi wamechagua kuwa wenye ubaridi au kudhihaki. Lakini je! unaweza kutaka kufanya hivyo unaposhughulika na kusudi la Mungu la kuokoa wanadamu? Je! ni jambo la hekima kusukuma mbali kwa wepesi mahakikisho na mipango ya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova ya wakati ujao wa jamii ya kibinadamu? Onyo la Petro linafaa katika jambo hilo: “Ninyi mwajua hili kwanza, kwamba katika siku za mwisho watakuja wadhihaki pamoja na dhihaka yao, wakiendelea kulingana na tamaa zao wenyewe na kusema: ‘Ku wapi huku kuwapo kwake kulikoahidiwa? Kwani, tangu ile siku mababu zetu walipolala usingizi wa mauti, mambo yote yaendelea sawasawa kama yalivyokuwa tangu mwanzo wa kuumba.’”—2 Petro 3:3, 4, NW.
Wakati ukifika wa Kristo kudhihirishwa au wa kuchukua tendo la hukumu juu ya ulimwengu, hakutakuwako nafasi ya kudai hawakujua wala kuwa na ubaridi kwa ajili ya hali. Yesu mwenyewe alilitaja jambo hilo wazi, kwa kusema: “Ndipo itakapoonekana ishara yake Mwana wa Adamu mbinguni; ndipo mataifa yote ya ulimwengu watakapoomboleza, nao watamwona Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na utukufu mwingi.” Wakati wa utambuzi huo wa kuwapo kwa Kristo utakuwa ni kuchelewa mno wasiweze kufaidika. Hiyo itamaanisha uharibifu wa wale ambao hawajatii.—Mathayo 24:30; Ufunuo 1:7; 11:18.
Kwa hiyo unaweza kufanya nini ili upokee baraka za Mungu sasa? Kwa unyenyekevu mtafute Yehova maadamu anapatikana. Soma na kujifunza Biblia ukiwa na kusudi la kujua jinsi Kristo alivyokuwa dhabihu kamilifu yenye kukomboa wakati wa kuja kwake kwa kwanza, na jinsi alivyo mfalme aliye roho mwenye utukufu katika kuwapo kwake, ambako sasa ndio wakati huu. Hayo yanaweza kukuletea uzima na furaha. Wapashe habari Mashahidi wa Yehova kwenye Jumba la Ufalme bila kuchelewa. Kwa furaha watakusaidia ufahamu Biblia yako, bila malipo. Iwapo huwajui Mashahidi katika eneo lako, basi jione huru kuwaandikia wachapaji wa gazeti hili kwa kutumia anwani ya karibu nawe iliyoonyeshwa katika ukurasa wa 2.—Sefania 2:3.
[Maelezo ya Chini]
a Ikiwa ungependa kuchunguza zile mara 24 zote ambapo parousía inaonekana, ni kama ifuatavyo: Mathayo 24:3, 27, 37, 39; 1 Wakorintho 15:23; 16:17; 2 Wakorintho 7:6, 7; 10:10; Wafilipi 1:26; 2:12; 1 Wathesalonike 2:19; 3:13; 4:15; 5:23; 2 Wathesalonike 2:1, 8, 9; Yakobo 5:7, 8; 2 Petro 1:16; 3:4, 12; 1 Yohana 2:28. Vilevile inapendeza kuangalia kwamba, kati ya wale waandikaji watano wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo waliotumia neno parousía, watatu walikuwa katika kile kikundi kilichomwuliza Yesu lile ulizo juu ya Mlima wa Mizeituni.—Marko 13:3.
[Blabu katika ukurasa wa 7]
Ikiwa Yesu alitoa ishara zenye kuonekana za kuonyesha kuwapo kwake, basi je! angeonekana au hangeonekana?
[Picha katika ukurasa wa 5]
Ingawa hapo kwanza umati wa watu ulimshangilia Yesu, yeye hakuwa aina ya masihi ambaye wengi walimtazamia
[Picha katika ukurasa wa 6]
Kutazamia kufika kwa mtu ni tofauti na huyo mtu akiwapo