Ni Nani Atakayeiona “Ishara Yake Mwana wa Adamu”?
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1, 2. Nabii Danieli aliona njozi gani juu ya Mfalme wa Kimasihi?
MMOJAWAPO wa unabii wenye kushtusha zaidi alioutoa Yesu Kristo ulikuwa na matumizi yake mwenyewe juu ya njozi ya Danieli nabii katika Danieli 7:13, 14. Nabii alipewa maono ya mfano ya serikali za ulimwengu kuanzia na Babeli (aliyoishi chini yake wakati huo) mpaka mwisho wa serikali zote za kibinadamu na kuchukuliwa kwa mahali pazo na utawala wa Kimasihi. Kwa habari ya Mfalme wa Kimasihi, Danieli aliandika hivi:
2 “Nikaona katika njozi za usiku, na tazama, mmoja aliye mfano wa mwanadamu akaja pamoja na mawingu ya mbingu akamkaribia huyo mzee wa siku, wakamleta karibu naye. Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie.”—Dan. 7:13, 14.
3. Wayahudi walidai Yesu awaonyeshe nini kuhakikisha Umasihi wake?
3 Yesu Kristo ndiye anayeelezwa hapa akiwa kama “aliye mfano wa mwanadamu.” (Linganisha Luka 5:24; 7:34.) Wayahudi walidai kwamba awaonyeshe kweli yeye alikuwa ndiye Masihi kwa njia ya kuonekana akiwa katika mawingu ya mbingu, kulingana na maoni yao juu ya unabii na utimizo wake. Lakini Yesu aliwaambia wasingepokea ishara hiyo. (Mt. 12:38, 39; 16:1-4; Marko 8:11, 12) Badala yake Maandiko yaonyesha kwamba “ishara yake Mwana wa Adamu” katika mamlaka na utukufu ingeonekana baadaye.
4. Ni nani ‘atakayekuona’ kuwapo kwa Mwana wa Adamu, na kwa njia gani?
4 Basi, ni nani atakayeiona “ishara yake Mwana wa Adamu” ajapo “juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na utukufu mwingi”? Yesu alionyesha kwamba watu wote duniani wangeiona. Alisema hivi: “Ndipo mataifa yote ya ulimwengu watakapoomboleza, nao watamwona Mwana wa Adamu.” (Mt. 24:30) Kwa kuwa Kristo ni mtu wa kiroho asiyeonekana sasa, macho ya kibinadamu hayawezi kumwona kwa halisi, lakini yaweza kufahamu kuwapo kwake kwa mambo yanayotukia. (1 Tim. 6:16) Wengine watakufahamu kuwapo kwake kusikoonekana mapema; wengine wanaoelezwa kama wakiomboleza hawatakufahamu mpaka aanzapo kuchukua hatua ya kuharibu vitu vifanyizavyo taratibu iliyopo ya mambo ya ulimwengu.
5. Kutakuwa na mfuatano gani wa matukio wakati wa “dhiki kubwa”?
5 Yesu alisema hatua hii kwa upande wake ingekuwa na maana ya dhiki isiyo na kifani kwa dunia “tangu mwanzo wa ulimwengu.” (Mt. 24:21) Sehemu ya kwanza ya dhiki hiyo itakuwa uharibifu wa ‘Babeli Mkuu’—wa dini zote za kilimwengu, zaidi ukiwa juu ya matengenezo ya kidini yaitwayo ‘ya Kikristo’ yanayojidai kumfuata Kristo, lakini kwa kweli yakimwakilisha vibaya. (Ufu. 17:1, 2, 16-18; 18:21) Baada ya hili kutakuwa na pigano la nguvu kati ya wakuu wa kisiasa, wa kibiashara na wa kijeshi wa ulimwengu huu na “MFALME WA WAFALME,” Yesu Kristo.—Ufu. 19:11-21.
SIKU ‘ZAFUPIZWA’
6. Kwa sababu gani Yerusalemu uliharibiwa mwaka wa 70 C.E.?
6 Taifa la Israeli wa kale lilijidai kuwa watu wa Mungu. Wao walikuwa na Maandiko ya Kiebrania yaliyoongozwa na Mungu. Lakini walizoea ibada ya uongo na kumtesa Yesu Kristo na wafuasi wake. Wao walikuwa rafiki za ulimwengu, si za Mungu. Walimkataa Yesu, yeye aliyetiwa mafuta na Mungu na kuwakilisha taifa la Kiyahudi kama Mfalme. Badala yake walipaza sauti wakati wa kujaribiwa kwa Yesu mbele ya gavana wa Kirumi Pontio Pilato, “Sisi hatuna mfalme ila Kaisari.” (Yohana 19:12-16) Mungu aliwatupilia mbali watoke kwake na kuuharibu Yerusalemu kwa kutumia majeshi ya Kirumi mwaka wa 70 C.E., kwa sababu ya uasi wao.
7. Kristendomu amekuwaje sawa na Yerusalemu wa kale?
7 Kristendomu amekuwa kama Yerusalemu wa kale. Anayo Biblia naye ajidai kuwa wakili wa pekee wa Mungu wa kweli. Lakini yeye amekanusha dai lake kwa kuwatesa wale watangazao ufalme wa Mungu wa Kimasihi. Yeye ameshiriki kabisa katika ulimwengu huu, akijiingiza katika siasa zake. (Yohana 17:14; Yak. 4:4) Kwa hiyo Mungu atamharibu, kama vile alivyouharibu Yerusalemu wa kale.
8, 9. Siku ‘zilifupizwaje’ kwa sababu ya “wateule” wakati wa mazingiwa ya Yerusalemu mwaka wa 70 C.E.?
8 Katika uharibifu wa Yerusalemu wa karne ya kwanza mazingiwa yalikuwa ya muda mfupi, siku 142 tu. Wakati huo Wayahudi 1,100,000 waliuawa na 97,000 wakaokoka na kuuzwa utumwani. Yesu alikuwa amekwisha sema hivi kwa unabii: “Kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo.”—Mt. 24:22.
9 Katika maneno ya Yesu juu ya kufupizwa kwa siku, “wateule” kwanza walikuwa Wakristo waliokuwa wanaishi katika Yerusalemu na Uyahudi, waliokuwa wa kwanza kuifahamu hukumu ya unabii ya Yehova iliyokuwa karibu kuupata Yerusalemu, na waliotoka nje, wakakimbilia usalama kupita Mto Yordani. Kwa sababu ya kuwatoa hawa mapema, Mungu angeweza kufanya kazi ya kuuharibu Yerusalemu kwa haraka kwa kulitumia jeshi la Kirumi. Ilikuwa rehema kwa upande wake kutofutilia mbali kila nafsi.
10, 11. Ni mambo gani yanayofanana na yanayotofautiana katika watu waliookolewa Yerusalemu na watu watakaookolewa katika “dhiki kubwa” itakayokuja nyakati za kisasa?
10 Kwa njia iyo hiyo, “wateule” wa Mungu, ndugu za Yesu Kristo waliotiwa mafuta na kuzaliwa kwa roho ambao wangali duniani wakati huu, wanaingia katika mahali pa usalama. Wanafahamu kutokana na mambo yanayoshuhudiwa, matukio ya nyakati zetu, kwamba Mwana wa Adamu yupo kwa kutoonekana na kwamba uharibifu wa taratibu hii ya mambo u karibu. Wao hawajitengi na watu kwa kimwili, kama walivyofanya Wakristo Yerusalemu. Bali wanapata kimbilio kwa Yehova chini ya mfalme wake wa Kimasihi, wanayemkubali na kumtumikia. Wanautumaini ufalme wake, si jitihada za wanadamu, ulete amani na usalama duniani. Uaminifu wao umeonekana na “mkutano mkubwa” wa watu wengine wajiungao nao katika ibada.—Ufu. 7:9-17.
11 “Wateule” na wenzi wao waishapo kujulikana waziwazi na kuwekwa chini ya ulinzi usioonekana wa Mfalme, ndipo uharibifu uwezapo kuendelea. Si lazima iwe dhiki iliyorefushwa, bali yaweza ‘kufupizwa.’ Kwa njia hii watu fulani wataokolewa. Watu hawa wataokolewa waingie katika taratibu mpya ya Mungu, si wauzwe utumwani, kwa sababu ya kuonyesha imani katika ufalme wa Kimasihi na kufahamu kuwapo kwa Kristo kusikoonekana. Kwa hiyo, ingawa wataokolewa na kifo kama waokokaji wale 97,000 katika Yerusalemu, “wateule” na “mkutano mkubwa” ‘hawafananishwi’ na wasio haki hao wa huko nyuma. Ulinganifu uliopo tu ni katika uhakika wa kwamba, nyakati zote mbili, watu waliokolewa; na pia katika rehema ya Yehova ya kutowafutilia mbali Wayahudi wote huko, si watu wote watakaofutiliwa mbali wakati huu.
HAWADANGANYWI NA MASIHI WA UONGO
12, 13. Yesu alitoa onyo gani juu ya masihi wa uongo?
12 Alipokuwa akisimulia yatakayoupata Yerusalemu, Yesu aliwaonya wanafunzi wake juu ya masihi wa uongo katika siku zao, na pia mambo ambayo yangekuwa ya lazima Wakristo wayaangalie watazamiapo pa·rou·siʹa yake au “kuwapo” katika mamlaka ya Ufalme. Alisema hivi:
13 “Wakati huo mtu akiwaambia, Tazama, Kristo yupo hapa, au yuko kule, msisadiki. Kwa maana watatokea makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu; wapate kuwapoteza, kama yamkini, hata walio wateule. Tazama, nimekwisha kuwaonya mbele. Basi wakiwaambia, Yuko jangwani, msitoke; yumo nyumbani, msisadiki. Kwa maana kama vile umeme utokavyo mashariki ukaonekana hata magharibi, hivyo ndiyo kutakavyokuwa kuja [“kuwapo,” NW], kwake Mwana wa Adamu. Kwa kuwa po pote ulipo mzoga, ndipo watakapokusanyika tai.”—Mt. 24:23-28.
14. (a) Ni kwa njia gani kuwapo kwa Kristo kusingekuwa “jangwani” wala katika ‘vyumba’ vya ndani? (b) Kungekuwaje kama umeme?
14 Wakati ambapo Kristo angerudi katika kuwapo kusikoonekana asingekuja kama mwanadamu duniani. Kwa hiyo Wakristo wasimtafute “jangwani,” ili waweze kujizoeza pamoja naye wakiwa pembeni kufanya maasi. Wala asingekuwamo katika ‘chumba’ cha ndani cha siri ambamo angeweza kufanya shauri la kufanya mabaya juu ya serikali za ulimwengu akiwa na wafuasi wake. Sivyo, kuwapo kwake ungekuwa kama umeme, si kwa kutokea kwa ghafula na bila kutazamiwa, bali kwa kuonekana katika eneo kubwa, waziwazi, kila mtu apate kuona. (Luka 17:24; linganisha Zaburi 97:4.) Wafuasi wake wasingeficha habari za kuwapo kwake kusikoonekana wakijua, bali wangezitangaza kote.—Mt. 10:26, 27.
15. Ni kwa njia gani “wateule” wangekuwa kama tai wanaokusanyika kwenye mzoga?
15 Yesu alisema “wateule” wasingedanganywa na kukatishwa tamaa na Makristo wa uongo. Kwa njia ya mfano wao ni kama “tai” kwa kuwa wenye busara nyingi ya kiroho. Kama vile tai ajuavyo ulipo mzoga atakaoula, ndivyo na “wateule” wenye busara wangekusanyika pamoja kwa Masihi anayetazamiwa, Yesu, wapate kula chakula cha kiroho katika mahali pa Kimasihi, kwa maana wangemfahamu Kristo wa kweli.—Luka 17:37.
USEMI ‘MARA BAADA YA’
16. Matukio ambayo Yesu alisema yangetokea ‘mara baada ya’ mambo aliyokuwa ametangulia kuyataja yalipaswa yatokee wakati gani?
16 Yesu alitoa maonyo haya yaliyokuwa na matumizi kwa Yerusalemu kwanza na watu wake, kisha kwa Wakristo wakati wa karne zilizofuata uharibifu wa Yerusalemu. Kufuata onyo hili alitumia usemi mara, “baada ya dhiki ya siku zile.” (Mt. 24:29) Usemi huu ulifanyiza mgawanyiko, kwa habari ya wakati. Aliyosema tangu wakati huo na kuendelea yalitumika kwa Njia moja tu, yaani, katika nyakati za kisasa, si kwa Yerusalemu huko nyuma. Hii yawezaje kusemwa kwa kufaa?
17, 18. (a) Neno “mara” lilitumiwaje katika karne ya kwanza? (b) Twajuaje Yesu hakumaanisha mambo ambayo yangetukia huko nyuma kwa usemi ‘mara baada ya’?
17 Matumizi ya karne ya kwanza ya neno lililotafsiriwa “mara” (Kigiriki, euthéōs) yalikuwa tofauti na matumizi yetu ya Kiswahili leo. Neno la Kigiriki halikumaanisha kwa lazima kwamba kusingepita muda. Dr. A. T. Robertson’s Word Pictures in the New Testament chataja neno linalofanana na hilo kinapoeleza jambo hili (ingawa neno tofauti la Kigiriki latumiwa), kikisema hivi: “Matumizi ya en tachei [“upesi”] katika Ufu. 1:1 yamepaswa yamfanye mtu atue kabla hajaamua. Hapa tunayo sura ya unabii inayofanana na ile yenye maono yaliyofupizwa.” Pia, twaweza kuona muda mrefu unaotiwa ndani katika neno linalotumiwa na mtume Paulo: “Mungu wa amani atamseta Shetani chini ya miguu yenu upesi.”—Rum. 16:20.
18 Kwa kweli, Yesu aliweka nafasi ya karne nyingi za wakati kwa usemi ‘mara baada ya,’ kwa maana mambo aliyoyaeleza baada ya hapo hayakuonekana katika karne ya kwanza. Maandishi ya kihistoria hayaonyeshi kwamba Warumi wenye kuzingira Yerusalemu na ‘mataifa mengine ya dunia’ waliomboleza kwa kumwona Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu akiwa na “nguvu na utukufu mwingi.”
19. Yesu alisema ni nini kingetokea kwanza ‘mara baada ya’ sehemu ya kwanza ya unabii huu?
19 Badala yake, mambo aliyoyasema Kristo kwa unabii yanatimia wakati wetu. Alisema kwa unabii juu ya hali zenye kuhuzunisha ulimwenguni, kana kwamba jua lilikuwa limezimika na nyota zikaanguka kutoka mbinguni, kusiwe na matumaini maangavu mbele. Mambo haya yametukia tangu mwaka wa 1914, wakati Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipoonyesha mahali pa kugeuka kwa mambo ya ulimwengu, ikaleta kipindi chenye huzuni zaidi kupita vyote katika historia ya wanadamu.
20. Ni nini kitakachotukia hasa badala ya uharibifu wa dunia unaoogopwa kwa njia ya vita ya atomiki?
20 Lakini sayari hii au idadi yake yote ya watu haitaharibiwa kamwe na vita ya kutumia silaha za atomiki, wala kwa njia yo yote yenye kuongozwa na wanadamu. Kwa maana ‘ishara yake Mwana wa Adamu’ itaonekana mbinguni wakati wa huzuni nyingi zaidi sana ya dunia, na “ndipo mataifa yote ya ulimwengu watakapoomboleza, nao watamwona Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na utukufu mwingi.”—Mt. 24:30.
21. (a) “Kuja” kwa Mwana wa Adamu juu ya mawingu ya mbinguni kunamaanisha kipindi gani cha wakati? (b) Anakujaje “juu ya mawingu ya mbinguni”? (c) Ni kwa sababu gani ‘mataifa ya dunia’ yataomboleza?
21 Hii yamaanisha, si mwanzo wa pa·rou·siʹa au kuwapo kusikoonekana kwa Kristo, bali “kuja” kwake (Kigiriki, er·khoʹme·non) katika “dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.” Wakati atakapokuja “na mawingu; na kila jicho litamwona” yeye atakuwa haonekani kwa macho ya kimwili. (Ufu. 1:7) Kwa kawaida “mawingu” yangemficha ye yote aliyemo, kwa hiyo usemi huo waonyesha kwamba yeye ‘anayekuja’ hawezi kuonekana mwenyewe. Kwa kuchunguza afanyayo Mwana wa Adamu wakati huo, si kwa macho ya kimwili kwa njia halisi, kila mtu ataona kwamba yatukiayo hayatokani na wanadamu, bali yatoka mbinguni. ‘Mataifa ya dunia’ ambao wamepinganishwa na Mungu na dini ya uongo na matengenezo ya kibiashara na ya kisiasa ‘yataomboleza’ yaionapo mamlaka ipitayo uwezo wa kibinadamu ya Mwana wa Adamu ikitumiwa juu ya majeshi yao na taratibu zao.
22. “Wateule” wamekusanywaje wakati wa kuwapo kwa Kristo, na ni nani wametokea watumikie pamoja nao?
22 Wakati wa pa·rou·siʹa, ya Kristo inayotangulia “kuja” kwake kufikiliza hukumu, ujumbe wa Ufalme na kusimamishwa kwake umetangazwa kama mpulizo mkubwa wa tarumbeta kuelekea “pepo nne”—katika kila upande—kukusanya “wateule” wa Yehova waliotiwa mafuta na kuzaliwa kwa roho katika umoja wa ibada. (Mt. 24:31) Pia, wengine wamesikia na kusikiliza wakiwa na tamaa ya kumtumikia Mungu, nao wanatumikia pamoja na “wateule.”
KUTIMIA KATIKA KIZAZI HIKI
23. (a) Wakristo wa kweli wanawezaje kuiona “ishara” ya kuwapo kwa Kristo sasa? (b) Ni mfano gani alioutoa Kristo uonyeshao hivi?
23 Si jambo moja, bali mambo mengi yanayotukia sasa yanaungana kuhakikisha kwamba tu karibu na siku na saa ya kuonekana huko kwa wakati ujao kwa “ishara yake Mwana wa Adamu” kwa watu wote, hata wasioamini. Lakini kabla yake, wale waliaminio Neno la Mungu wanaiona “ishara” iliyopo tayari ya kuwapo kusikoonekana kwa Kristo sasa, kwa kuyaona yanayotukia tangu mwaka wa 1914 C..E. Maneno ya Yesu aliyowaambia wafuasi wake baada ya hapo yaonyesha kwamba hatawaruhusu wapatikane wakifuatana na taratibu ya mambo ya kilimwengu katika matumaini yake, mipango yake na matendo yake yenye kuvunja moyo. Alisema hivi: “Basi kwa mtini jifunzeni mfano; tawi lake likiisha kuchipuka na kuchanue majani, mwatambua ya kuwa wakati wa mavuno u karibu; nanyi kadhalika, myaonapo hayo yote, tambueni ya kuwa yu karibu, milangoni. Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia.”—Mt. 24:32-34.
24. Kwa sababu gani ni faraja kujua kwamba mambo yote aliyoyasema Kristo katika unabii huu mkuu yatatukia katika kizazi chetu wenyewe?
24 Kwa kuwa ufalme wa “Mwana wa Adamu” ni “mamlaka ya milele, ambayo haitapita kamwe,” inafariji kujua kwamba mambo haya yatatukia katika kizazi chetu wenyewe. (Dan. 7:13, 14; 2:44) Kwa maana Yeye huyu atatawala kwa kumwogopa Yehova Mungu wake, naye atatawala, si awatumie watu kwa faida yake mwenyewe kama wanadamu walivyofanya, bali ili wapate amani na furaha.—Isa. 11:1-5; 32:18.
25. Tukiuona utimizo wa mambo aliyoyaeleza Yesu, yatupasa tufanye mambo gani zaidi?
25 Ikiwa wasomaji wa makala hii wanaona kwa ufahamu mambo ambayo Yesu alieleza kama yakitokea sasa, wanaweza kujihesabu kama waliopendelewa sana kuwa na macho yaliyo wazi kuiona “ishara” ya kuwapo kwa Kristo. Sasa wanayo nafasi ya kuchukua hatua za kujifunza mengi zaidi juu ya kusudi la Yehova kwa dunia hii na kurekebisha njia zao zote watembee kwa njia inayompendeza Mungu. Kwa njia hiyo wanaweza kutazamia ulinzi wa Mungu waionapo “ishara yake Mwana wa Adamu” ‘ajapo’ kufikiliza hukumu juu ya taratibu hii ya mambo.
—Kutoka Kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached.