Kuangaza Nuru Juu ya Kuwapo kwa Kristo
“Wakati Mwana wa Mtu atakapokuja katika utukufu wake . . . atawatenganisha watu.”—MATHAYO 25:31, 32, Habari Njema kwa Watu Wote.
1. Makasisi wa Jumuiya ya Wakristo wamefasirije maana ya yale maneno kwenye Mathayo 24:3?
SIKU tatu kabla ya kifo cha Yesu, wanne kati ya wanafunzi wake walimkaribia na kumwuliza hivi kwa hamu: “Tuambie, mambo hayo yatakuwa lini? Nayo ni nini dalili ya kuja [Kigiriki, pa·rou·siʹa (paruusia)] kwako, na ya mwisho wa dunia?” Kwa karne nyingi, makasisi na waandishi wa Jumuiya ya Wakristo wamefasiri maneno hayo yaliyonenwa kwa Yesu kwenye Mathayo 24:3 (Union Version) kumaanisha kwamba angeweza kuonekana tena katika mwili ili aweze kuonwa na ainabinadamu yote. Kwa hiyo, wao wamefundisha kwamba kurudi kwa Kristo kungekuwa kwa wonyesho mkuu na sherehe yenye kuonekana. Wao hurejezea jambo hilo kuwa kuja kwa pili kwa Kristo. Lakini je! dhana zao ni za kweli?
2, 3. (a) Buku 2 la Studies in the Scriptures lilionyesha tofauti gani kati ya maneno “kuja” na “kuwapo”? (b) Watu wa Yehova walikuja kuelewa nini kuhusu maana ya pa·rou·siʹa ya Kristo?
2 Kufikia 1889, wakiwa wachukuaji nuru wa karne ya 19, wapakwa kwa roho wa Yehova walikuwa tayari wamepokea sahihisho kuhusiana na kurudi kwa Kristo. Katika Buku 2 la Studies in the Scriptures, kurasa 158 hadi 161, Charles T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Bible and Tract Society, aliandika: “Parousia . . . humaanisha kuwapo, na halipaswi kamwe kutafsiriwa kuja, kama vile katika Biblia ya Kiingereza ya kawaida . . . ‘Emphatic Diaglott,’ [ambayo ni] tafsiri yenye thamani sana ya Agano Jipya, hufasili parousia inavyofaa, kuwapo . . . si katika maana ya kuja, kana kwamba yuko njiani, bali kuwapo, kama inavyokuwa baada ya kufika [Yesu] asema, ‘Kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa parousia [kuwapo, NW] kwake Mwana wa Adamu.’ Angalia kwamba, ulinganisho si kati ya kuja kwa Nuhu na kuja kwa Bwana wetu . . . Basi, tofauti iliyoko, ni kati ya wakati wa kuwapo kwa Nuhu miongoni mwa watu ‘kabla ya gharika,’ na wakati wa kuwapo kwa Kristo katika ulimwengu, wakati wa majilio yake ya pili, ‘kabla ya moto’—ile taabu kubwa mno ya Siku ya Bwana [Yehova] ambayo kizazi hiki huishia.”—Mathayo 24:37.
3 Kwa hiyo watu wa Yehova wa karne ya 19 walielewa ifaavyo kwamba pa·rou·siʹa [kuwapo] kwa Kristo kungekuwa kusikoonekana. Wao pia walikuwa wamepata kuelewa kwamba mwisho wa Nyakati za Wasio Wayahudi ungetukia katika vuli ya 1914. Mnurisho wa kiroho ulipoendelea, walielewa baadaye kwamba Yesu Kristo alitawazwa mbinguni kuwa Mfalme wa Ufalme mwaka huohuo, 1914.—Mithali 4:18; Danieli 7:13, 14; Luka 21:24; Ufunuo 11:15.
“Kuwapo kwa Bwana Wetu”
4. “Kuwapo kwa Bwana wetu Yesu Kristo” hurejezea nini?
4 Basi, katika siku yetu, ni nini kinachomaanishwa na usemi wa Kibiblia “kuwapo kwa Bwana wetu Yesu Kristo”? (1 Wathesalonike 5:23, NW) Mamlaka moja husema kwamba neno “kuwapo,” pa·rou·siʹa, “lilikuja kuwa neno rasmi la ziara ya mtu wa cheo kikubwa, hasa ya wafalme na wamaliki waliozuru mkoa fulani.” Kwa hiyo usemi huo hurejezea kuwapo kifalme kwa Bwana Yesu Kristo akiwa Mfalme, kuanzia na baada ya 1914, kufuatia kutawazwa kwake mbinguni. Yeye yupo bila kuonekana ili ‘awe na enzi katikati ya adui zake,’ akitawala sasa akiwa Mfalme na kutimiza amri hiyo ya kiunabii. (Zaburi 110:2) Kwa muda wa miaka 79 hivi, wanadamu duniani wamekuwa wakiona matokeo ya kuwapo kifalme kwa Kristo kusikoonekana.
5. Ni matukio gani wakati wa pa·rou·siʹa yatakayozungumziwa katika makala tatu ya mafunzo ya gazeti hili?
5 Katika mfululizo huu wa makala tatu, tutapitia uthibitisho wenye kuvutia wa utimizo mbalimbali wa Ufalme wa Kristo wakati wa kipindi hiki. Kwanza, tutatokeza unabii kadhaa wa Biblia unaotabiri matukio kadhaa ambayo tayari yametukia au yanaendelea kutukia hata sasa. Pili, tutaeleza ile kazi kubwa inayotimizwa na jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili ambayo Yesu anatumia katika kipindi hiki chote cha kuwapo kwake kifalme. (Mathayo 24:45-47) Makala ya tatu itatusimulia umalizio mkuu, kipindi cha “dhiki kubwa.” Huo ndio wakati ambapo Yesu aja akiwa Mfishaji wa Yehova ili kuharibu wanadamu wasio waadilifu na kuokoa waadilifu. (Mathayo 24:21, 29-31) Wakati huo wa uharibifu unasimuliwa na mtume Paulo kuwa wenye “kuwalipa ninyi mteswao raha pamoja na sisi; wakati wa kufunuliwa kwake Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika na uweza wake; katika mwali wa moto; huku akiwalipiza kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana wetu Yesu.”—2 Wathesalonike 1:7, 8.
Ile Ishara
6. Ni ishara gani yenye mambo mengi inayosimuliwa katika Mathayo sura ya 24 na 25?
6 Miaka mia kumi na tisa iliyopita, wanafunzi wa Yesu wachukuaji nuru walimwomba ishara, au uthibitisho, wa kuwapo kwake wakati ujao katika uwezo wa Kifalme. Jibu lake, ambalo limerekodiwa katika sura za 24 na 25 za Mathayo, liliandaa ishara yenye mambo mengi, ambayo sehemu zayo zote zinatimizwa sasa ulimwenguni pote. Utimizo wa ishara hiyo huonyesha kwamba huo ungekuwa wakati wa taabu na wa kutahini sana. Yesu alionya hivi: “Angalieni, mtu asiwadanganye. Kwa sababu wengi watakuja kwa jina langu, wakisema, Mimi ni Kristo; nao watadanganya wengi. Nanyi mtasikia habari za vita na matetesi ya vita; angalieni, msitishwe; maana hayo hayana budi kutukia; lakini ule mwisho bado.”—Mathayo 24:4-6.
7. Ni sehemu zipi za ishara ambazo tumeona zikitimizwa tangu 1914?
7 Yesu aliendelea kutoa unabii kwamba kungekuwako vita vya kiwango kisicho na kifani. Katika utimizo, viwili kati ya vita hivyo vimeitwa vita vya ulimwengu, moja kuanzia 1914 hadi 1918 na ya pili kuanzia 1939 hadi 1945. Zaidi ya hayo, alisema kwamba kungekuwako upungufu wa chakula na matetemeko ya dunia mahali mahali. Wakristo wa kweli wangenyanyaswa sana. Sawa na unabii huo, Mashahidi wa Yehova, wachukuaji nuru wa ki-siku-hizi, wamepatwa na mnyanyaso katika miongo minane ambayo imepita wanapohubiri habari njema za Ufalme wa Mungu “katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:7-14) Kila Kitabu-Mwaka cha Mashahidi wa Yehova huongezea uthibitisho huo kwamba sehemu hizo za ishara zinatimizwa.
8, 9. (a) Kuwapo kwa Yesu kifalme kunatia ndani nini? (b) Unabii wa Yesu kuhusu Makristo wawongo unaonyesha nini kuhusu mahali na jinsi ya kuwapo kwake?
8 Kwa kuwa umaliki wa Yesu unatia ndani dunia yote, ibada ya kweli inapanuliwa kwenye mabara yote. Kuwapo (pa·rou·siʹa) kwake kifalme ni wakati wa ukaguzi wa tufeni pote. (1 Petro 2:12) Lakini, je, kuna jiji kuu au kitovu ambako Yesu aweza kuendewa? Yesu alijibu hilo kwa kutabiri kwamba wakati wa kutazamia kuwapo kwake, Makristo wawongo wangetokea. Yeye alionya: “Basi wakiwaambia, [Kristo] Yuko jangwani, msitoke; yumo nyumbani, msisadiki. Kwa maana kama vile umeme utokavyo mashariki ukaonekana hata magharibi, hivyo ndivyo kutakavyokuwa kuja [kuwapo, NW, pa·rou·siʹa] kwake Mwana wa Adamu.”—Mathayo 24:24, 26, 27.
9 Yesu, “Mwana wa Adamu,” alijua vema zaidi ya mtu mwingine yeyote duniani, mahali ambapo angekaa wakati wa kuwapo kwake. Hangekaa ama hapa ama hapa au mahali popote pale duniani. Hangepatikana katika mahali fulani pasipo na watu, “jangwani,” ili kwamba wale ambao wangemtafuta Mesiya wangeweza kumjia huko wakiwa mbali wasiweze kuonwa na mamlaka za kiserikali za nchi, mahali ambapo wafuasi wangeweza kujizoeza chini ya uongozi wake, wakijitayarisha kufanya ushambulizi wa kisiasa na kumweka yeye kuwa Mtawala wa Kimesiya wa ulimwengu. Zaidi ya hayo, yeye hangejificha mahali fulani “nyumbani,” pakijulikana na watu wachache tu aliowachagua, kwamba humo, bila kuonekana na bila kutambulika, ndimo angeweza kufanya njama na mipango ya kisiri na waandamani wake ili kupindua serikali za ulimwengu kisha apakwe mafuta awe Mesiya aliyeahidiwa. La hasha!
10. Meme za kweli ya Biblia zimemwekaje tufeni pote?
10 Kinyume cha hivyo, hakungekuwa na chochote cha kuficha kuhusu kuja kwa Yesu akiwa Mfalme, mwanzoni mwa kuwapo kwake kifalme. Kama vile Yesu alivyotabiri, meme za kweli ya Biblia zinaendelea kumweka (kumulika) kwenye maeneo mapana kutoka sehemu za mashariki hadi sehemu za magharibi, tufeni pote. Kweli kweli, wakiwa wachukuaji nuru wa ki-siku-hizi, Mashahidi wa Yehova wanathibitika kuwa ‘nuru ya mataifa, ili wapate kuwa wokovu [wa Yehova] hata miisho ya dunia.’—Isaya 49:6.
Utendaji wa Kimalaika
11. (a) Majeshi ya kimalaika yanatumiwa katika njia gani katika kuangaza nuru ya Ufalme? (b) Washiriki wa jamii ya ngano wamekusanywa wakati gani na katika kikundi gani?
11 Maandiko mengine yanayohusu kuwapo kwa Yesu humsimulia akiwa ameandamana na, au ‘akiwatuma’ majeshi ya kimalaika. (Mathayo 16:27; 24:31) Katika kielezi cha ngano na magugu, Yesu alisema kwamba “lile konde ni ulimwengu” na kwamba “mavuno ni mwisho wa dunia [mfumo wa mambo, NW]; na wale wavunao ni malaika.” Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba, wakati wa kuwapo kwake katika uwezo na utukufu wa Ufalme, yeye atumia tu wajumbe wa kimalaika katika shughuli za kidunia. Kuanzia 1919, malaika chini ya mwelekezo wa Yesu walitenganisha jamii ya ngano ya wapakwa kwa roho waliozaliwa kwa roho waliokuwa wametawanywa na matukio ya Vita ya Ulimwengu 1, nao wakatayarishwa kwa ajili ya utendaji zaidi katika jina la Mfalme. (Mathayo 13:38-43) Katika miaka ya 1920 maelfu mengine ya wanadamu walichukua msimamo wao kwa ajili ya Ufalme wa Mungu uliosimamishwa nao wakapakwa kwa roho ya Mungu. Wapakwa kwa roho hao waliongezwa kwa matokeo mazuri kwenye idadi za mabaki wa kwanza. Wakiwa pamoja, wao hufanyiza jamii ya mtumwa mwaminifu mwenye akili wa siku yetu.
12. Malaika wameshiriki katika usafishaji gani, na kukiwa na tokeo gani kwa dunia?
12 Kielelezo kingine cha ushiriki wa kimalaika wakati wa kuwapo kwa Yesu baada ya kutawazwa kwake katika 1914 kimerekodiwa kwenye Ufunuo 12:7-9: “Mikaeli [Yesu Kristo] na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake; nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni. Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.” Hivyo, mbingu zilizo juu sasa zimesafishwa, zikiacha milki ya kidunia tu ya Ufalme ije kusafishwa kikamili kwa utakaso wa jina la Yehova. Katika mwaka huu wa 1993, onyo la kimungu laendelea kutumika: “Ole wa nchi . . . kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.”—Ufunuo 12:12.
Ufufuo wa Kimbingu
13, 14. (a) Ni nini ambalo Maandiko huonyesha limekuwa likiendelea tangu 1918 na baada ya hapo? (b) Paulo na Yohana wanafunua nini kuhusu mabaki wapakwa kwa roho leo?
13 Tukio jingine la ajabu katika wakati wa kuwapo kwa Kristo ni mwanzo wa ufufuo wa kimbingu. Mtume Paulo alionyesha kwamba wale Wakristo wapakwa kwa roho waliolala usingizi kwa muda mrefu makaburini mwao wangekuwa wa kwanza kuhuishwa na kuishi na Yesu Kristo katika milki ya roho. Kwa muda wa miaka uthibitisho umetolewa kuonyesha kwamba hilo laonekana lilitukia kuanzia 1918 na kuendelea. Paulo aandika: “Katika Kristo wote watahuishwa. Lakini kila mmoja mahali pake; limbuko ni Kristo; baadaye walio wake Kristo, atakapokuja [wakati wa kuwapo kwake, NW, pa·rou·siʹa].” (1 Wakorintho 15:22, 23) Ufufuo wa wapakwa kwa roho wakati wa kuwapo kwa Kristo kunathibitishwa kwenye 1 Wathesalonike 4:15-17: “Kwa kuwa twawaambieni haya kwa neno la Bwana [Yehova, NW], kwamba sisi tulio hai, tutakaosalia hata wakati wa kuja kwake [kuwapo kwake, NW, pa·rou·siʹa] Bwana, hakika hatutawatangulia wao waliokwisha kulala mauti . . . Nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza. Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani.” Kuna 144,000 ambao ni mali ya Kristo wakiwa wapakwa kwa roho ambao hatimaye watapokea zawadi hiyo zuri ajabu.—Ufunuo 14:1.
14 Kama vile Paulo anavyoonyesha, wale mabaki wapakwa kwa roho walio hai leo hawaingii ndani ya Ufalme mbele ya wale Wakristo mashahidi-wafia-imani wapakwa kwa roho na wanafunzi waaminifu wa mapema. Mtume Yohana anasimulia kirefu zaidi kuhusu wale wapakwa kwa roho wanaokufa leo kama ifuatavyo: “Wenye furaha ni wale wafu ambao hufa katika muungano pamoja na Bwana kutoka wakati huu na kuendelea. Ndiyo, yasema roho, acheni wao wapumzike kazi zao ngumu, kwa kuwa vitu walivyofanya huenda moja kwa moja pamoja nao,” yaani katika kuishi kwao baada ya ufufuo. (Ufunuo 14:13, NW) Na Paulo asema hivi: “Angalieni, nawaambia ninyi siri; hatutalala sote, lakini sote tutabadilika, kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa parapanda ya mwisho; maana parapanda italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu, nasi tutabadilika.” (1 Wakorintho 15:51, 52) Loo! huo ni muujiza wenye kustaajabisha jinsi gani!
15, 16. (a) Yesu alitoa kielezi kipi kwenye Luka 19:11-15, na kwa sababu gani? (b) Unabii huo umekuwa ukitimizwaje?
15 Wakati mmoja Yesu alipokuwa akihubiria kikundi cha wafuasi wake kuhusu Ufalme wa Mungu, alitumia kielezi ili kuwasaidia wasahihishe mawazo yao yasiyokuwa sahihi. Habari hiyo inasomwa hivi: “Wao walidhani ya kuwa ufalme wa Mungu utaonekana mara. Basi akasema, Mtu mmoja, kabaila, alisafiri kwenda nchi ya mbali, ili ajipatie ufalme na kurudi. Akaita watu kumi katika watumwa wake, akawapa mafungu kumi ya fedha, akawaambia, Fanyeni biashara hata nitakapokuja. . . . Ikawa aliporudi, ameupata ufalme wake, aliamuru waitwe wale watumwa aliowapa fedha, ili ajue faida aliyopata kila mtu kwa biashara yake.”—Luka 19:11-15.
16 Yesu alikuwa ndiye “mtu” huyo aliyeenda mbinguni, “nchi ya mbali” ambako angepokea ufalme. Ufalme huo aliupata katika 1914. Punde baadaye, Kristo akiwa Mfalme alifanya hesabu na wale waliodai kuwa wafuasi wake ili kuona yale ambayo walikuwa wamefanya katika kutunza masilahi ya Ufalme waliyopewa. Waaminifu wachache walichaguliwa kupokea pongezi la bwana mkubwa wao: “Vema, mtumwa mwema; kwa vile ulivyokuwa mwaminifu katika neno lililo dogo, uwe na mamlaka juu ya miji kumi.” (Luka 19:17) Kipindi hicho cha kuwapo kwa Kristo kilihusisha utendaji mkubwa wenye kuendelea wa kuhubiriwa kwa Ufalme, kutia ndani kujulishwa rasmi kwa hukumu za Mungu dhidi ya waovu, na uangalizi wa kazi hiyo ulitiwa ndani katika mamlaka iliyopewa yule “mtumwa mwema.”
Kuhubiri Ulimwenguni Pote
17. Ni shangwe gani inayotia alama pa·rou·siʹa?
17 Ni nini kingine kingetukia wakati wa pa·rou·siʹa hiyo? Ungekuwa wakati wa shangwe kuu katika kazi ya kuhubiri na kusaidia wapya wajitayarishe kwa ajili ya wokovu kupitia dhiki kubwa inayokuja. Wale wa “mkutano mkubwa,” wanaosaidia mabaki, wanakuwa “barua zenye sifa [za pendekezo, NW].” (Ufunuo 7:9; 2 Wakorintho 3:1-3) Paulo anataja shangwe ya kazi hiyo ya kuvuna anaposema hivi: “Maana tumaini letu, au furaha yetu, au taji ya kujionea fahari, ni nini? Je! si ninyi, mbele za Bwana wetu Yesu, wakati wa kuja kwake [kuwapo kwake, NW, pa·rou·siʹa]?”—1 Wathesalonike 2:19.
Endelea Kuwa Safi Bila Lawama
18. (a) Ni sala gani ya Paulo inayohusu pa·rou·siʹa? (b) Ni lazima sisi sote tuonyeshe roho gani wakati huu, na katika njia zipi?
18 Paulo alisali pia kwa ajili ya utakaso wa wale walio hai katika wakati huu wa kuwapo kwa Kristo: “Mungu wa amani mwenyewe awatakase kabisa; nanyi nafsi zenu na roho zenu na miili yenu mhifadhiwe mwe kamili, bila lawama, wakati wa kuja kwake [kuwapo kwake, NW, pa·rou·siʹa] Bwana wetu Yesu Kristo.” (1 Wathesalonike 5:23) Naam, leo, iwe sisi ni sehemu ya wapakwa kwa roho au ni sehemu ya ile hesabu kubwa ya kondoo wengine, roho ya ushirikiano hutufungamanisha pamoja kwa uaminifu-mshikamanifu ili tuendelee kuwa safi na bila lawama katika wakati huu wa pekee. Vivyo hivyo, tunahitaji kujizoeza saburi. Yakobo aliandika: “Kwa hiyo ndugu, vumilieni, hata kuja kwake [kuwapo kwake, NW, pa·rou·siʹa] Bwana. . . . Mthibitishe mioyo yenu, kwa maana kuja kwake [kuwapo kwake, NW, pa·rou·siʹa] Bwana kunakaribia.”—Yakobo 5:7, 8.
19. Petro alitoa onyo gani kuhusu pa·rou·siʹa, na twapaswa kuitikiaje?
19 Mtume Petro pia alikuwa na jambo la kutuambia sisi tulio hai katika kipindi hiki cha sasa. Yeye alituonya dhidi ya wadhihaki, walio wengi katika pande zote za dunia. Petro husema hivi: “Mkijua kwanza neno hili ya kwamba katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe, na kusema, Iko wapi ahadi ile ya kuja [kuwapo, NW, pa·rou·siʹa] kwake? kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.” (2 Petro 3:3, 4) Kujapokuwa wadhihaki wengi wakati wa kuwapo kwa Kristo, watu wa Yehova wanaendelea kung’aa wakiwa nuru ya ulimwengu, kwa wokovu wa wengi.
Maswali ya Kupitia
◻ Watu wa Yehova walitiwaje nuru hatua kwa hatua kuhusu pa·rou·siʹa?
◻ Mathayo 24:4-8 limekuwa likitimizwaje?
◻ Malaika wamekuwa wakishirikianaje na Kristo aliyetawazwa?
◻ Ni muujiza upi wenye kustaajabisha unaoonekana kuandamana na pa·rou·siʹa?
◻ Ni shangwe gani inayoonwa wakati huu, na ni nani wanaoshiriki katika shangwe hiyo?