Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 8/15 kur. 9-14
  • Kuja kwa Yesu au Kuwapo kwa Yesu—ni Kupi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuja kwa Yesu au Kuwapo kwa Yesu—ni Kupi?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Walikuwa Wakiuliza Nini?
  • Yale Aliyoyaandika Mathayo —Katika Kigiriki
  • Sehemu Mbalimbali Katika Lugha ya Kiebrania
  • Kungojea Upeo wa Kuwapo Kwake
  • Kuangaza Nuru Juu ya Kuwapo kwa Kristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Kristo Yupo!
    Amkeni!—1993
  • Ni “Ishara” Gani Wanayoitazamia Wakristo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Kuwapo kwa Mesiya na Utawala Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 8/15 kur. 9-14

Kuja kwa Yesu au Kuwapo kwa Yesu—ni Kupi?

“Itakuwa ni nini ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”—MATHAYO 24:3, NW.

1. Maswali yalikuwa na fungu gani katika huduma ya Yesu?

KUTUMIA maswali kwa ustadi kwa Yesu kulifanya wasikilizaji wake wafikiri, hata waone mambo kwa njia mpya. (Marko 12:35-37; Luka 6:9; 9:20; 20:3, 4) Twaweza kushukuru kwamba alijibu maswali pia. Majibu yake hudhihirisha kweli ambazo labda hatungejua au kuelewa kwa njia nyingine.—Marko 7:17-23; 9:11-13; 10:10-12; 12:18-27.

2. Tuelekeze uangalifu wetu kwenye swali jipi sasa?

2 Kwenye Mathayo 24:3, twapata mojapo maswali ya maana zaidi ambayo Yesu alipata kujibu wakati wowote. Mwisho wa uhai wake wa kidunia ukiwa karibu, Yesu alikuwa ametoka tu kuonya kwamba hekalu la Yerusalemu lingeharibiwa, hilo likitia alama mwisho wa mfumo wa Kiyahudi. Simulizi la Mathayo laongeza hivi: “Alipokuwa ameketi juu ya Mlima wa Mizeituni, wanafunzi walimkaribia kwa faragha, wakisema: ‘Tuambie, Ni wakati gani mambo haya yatakuwa, nayo itakuwa ni nini ishara ya kuwapo [“kuja,” Habari Njema kwa Watu Wote] kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?’”—Mathayo 24:3, NW.

3, 4. Kuna tofauti gani ya maana katika jinsi ambavyo Biblia hutafsiri neno kuu moja kwenye Mathayo 24:3?

3 Mamilioni ya wasomaji wa Biblia wamejiuliza, ‘Kwa nini wanafunzi waliuliza swali hilo, na jibu la Yesu lapaswa liniathirije?’ Katika jibu lake Yesu alisema kuhusu kutokea kwa majani kukionyesha kwamba wakati wa kiangazi “umekaribia.” (Mathayo 24:32, 33, HNWW) Kwa sababu hiyo, makanisa mengi hufundisha kwamba mitume walikuwa wakiuliza kuhusu ishara ya “kuja” kwa Yesu, ishara inayothibitisha kwamba kurudi kwake kulikuwa karibu sana. Wao wanaamini kwamba “kuja” huko kutakuwa wakati hasa achukuapo Wakristo mbinguni kisha alete mwisho wa ulimwengu. Je, unaamini kwamba hilo ni sahihi?

4 Badala ya ufasiri “kuja,” tafsiri fulani za Biblia, kutia ndani New World Translation of the Holy Scriptures, hutumia neno “kuwapo.” Je, yawezekana kwamba swali ambalo wanafunzi waliuliza na lile alilosema Yesu kwa kujibu latofautiana na yale ambayo hufundishwa katika makanisa? Swali kwa kweli lilikuwa nini? Na ni jibu gani alilotoa Yesu?

Walikuwa Wakiuliza Nini?

5, 6. Twaweza kufikia mkataa gani kuhusu kufikiri kwa mitume walipouliza lile swali tunalosoma kwenye Mathayo 24:3?

5 Kwa sababu ya yale aliyosema Yesu kuhusu hekalu, yaelekea wanafunzi walikuwa wakifikiria mfumo wa mambo wa Kiyahudi walipokuwa wakiomba ‘ishara ya kuwapo [au “kuja”] kwake na umalizio wa mfumo wa mambo [kihalisi, “enzi”].—Linganisha “ulimwengu” kwenye 1 Wakorintho 10:11 na Wagalatia 1:4, King James Version.

6 Kufikia wakati ule mitume hawakuyaelewa sana mafundisho ya Yesu. Mapema walikuwa wamewazia kwamba “ufalme wa Mungu utaonekana mara.” (Luka 19:11; Mathayo 16:21-23; Marko 10:35-40) Na hata baada ya yale mazungumzo juu ya Mlima wa Mizeituni, lakini kabla ya kutiwa mafuta kwa roho takatifu, walimuuliza Yesu ikiwa alikuwa akirudishia Israeli Ufalme wakati ule.—Matendo 1:6.

7. Kwa nini mitume wangemuuliza Yesu kuhusu fungu lake la wakati ujao?

7 Hata hivyo, walijua bila shaka kwamba yeye angeondoka, kwani majuzi alikuwa amewaambia hivi: “Nuru ingaliko pamoja nanyi muda kidogo. Enendeni maadamu mnayo nuru hiyo.” (Yohana 12:35; Luka 19:12-27) Kwa hiyo yawezekana sana kwamba walijiuliza, ‘Ikiwa Yesu ataondoka, tutatambuaje kurudi kwake?’ Alipotokea akiwa Mesiya, wengi hawakumtambua. Na zaidi ya mwaka mmoja baadaye, maswali yaliendelea kuhusu kama yeye angetimiza mambo yote ambayo Mesiya alitazamiwa kufanya. (Mathayo 11:2, 3) Kwa hiyo mitume walikuwa na sababu ya kuuliza kuhusu wakati ujao. Lakini, tena, je, walikuwa wakiuliza kuhusu ishara ionyeshayo kwamba angekuja karibuni au walikuwa wakiuliza kuhusu jambo jingine tofauti?

8. Yaelekea mitume walikuwa wakisema lugha gani pamoja na Yesu?

8 Ebu wazia kwamba wewe ulikuwa ndege aliyekuwa akisikiliza mazungumzo hayo juu ya Mlima wa Mizeituni. (Linganisha Mhubiri 10:20.) Labda ungalisikia Yesu na mitume wakisema Kiebrania. (Marko 14:70; Yohana 5:2; 19:17, 20; Matendo 21:40) Hata hivyo, yaelekea walijua pia lugha ya Kigiriki.

Yale Aliyoyaandika Mathayo —Katika Kigiriki

9. Tafsiri za kisasa zilizo nyingi za Mathayo zinategemea nini?

9 Maandishi ya tangu karne ya pili W.K. yaonyesha kwamba mwanzoni Mathayo aliandika Gospeli yake katika Kiebrania. Yaonekana kwamba baadaye aliiandika katika Kigiriki. Hati nyingi katika Kigiriki zimefikia wakati wetu na zimetumikia zikiwa msingi wa kutafsiri Gospeli yake katika lugha za leo. Mathayo aliandika nini katika Kigiriki kuhusu mazungumzo hayo juu ya Mlima wa Mizeituni? Aliandika nini kuhusu kule “kuja” au “kuwapo” ambako wanafunzi waliuliza juu yako na ambako Yesu alieleza juu yako?

10. (a) Mara nyingi Mathayo alitumia neno gani la Kigiriki kwa neno “kuja,” nalo laweza kuwa na maana zipi? (b) Ni neno jingine gani la Kigiriki lililo lenye upendezi?

10 Katika sura 23 za kwanza za Mathayo, mara zaidi ya 80 twapata neno la kawaida la Kigiriki linalotumiwa kwa neno “kuja,” ambalo ni erʹkho·mai. Hilo mara nyingi hutoa wazo la kukaribia au kwenda karibu na, kama kwenye Yohana 1:47: “Yesu akamwona Nathanaeli anakuja kwake.” (Italiki ni zetu.) Kwa kutegemea jinsi kinavyotumiwa, kitenzi erʹkho·mai chaweza kumaanisha “wasili,” “enda,” “pata,” “fika,” au “mtu kushika njia yake.” (Mathayo 2:8, 11; 8:28; Yohana 4:25, 27, 45; 20:4, 8; Matendo 8:40; 13:51) Lakini kwenye Mathayo 24:3, 27, 37, 39, Mathayo alitumia neno tofauti, nomino isiyopatikana kwingineko katika Gospeli: pa·rou·siʹa. Kwa kuwa Mungu alipulizia uandikaji wa Biblia, kwa nini alimchochea Mathayo kuchagua neno hilo la Kigiriki katika mistari hiyo alipokuwa akiandika Gospeli yake katika Kigiriki? Linamaanisha nini, na kwa nini tutake kujua?

11. (a) Maana ya pa·rou·siʹa ni nini? (b) Vielelezo kutoka katika maandishi ya Yosefo huonyeshaje wazi uelewevu wetu wa pa·rou·siʹa? (Ona kielezi-chini.)

11 Moja kwa moja, pa·rou·siʹa humaanisha “kuwapo.” Kamusi ya Expository Dictionary of New Testament Words ya Vine yasema hivi: “PAROUSIA, . . . [kihalisi], kuwapo, para, pamoja, na ousia, kuwa (kutoka eimi, kuwa), huonyesha kuwasili na kuwapo pamoja kunakofuata. Kwa mfano, katika barua fulani ya mafunjo, mwanamke asema juu ya umuhimu wa parousia yake mahali fulani ili ashughulikie mambo yanayohusu mali yake.” Kamusi nyingine hueleza kwamba pa·rou·siʹa, huonyesha ‘ziara ya mtawala.’ Basi, halimaanishi muda wa kuwasili tu, bali kuwapo kunakoendelea tangu kuwasili. Kwa kupendeza, hivyo ndivyo mwanahistoria Myahudi Yosefo, aliyeishi wakati uleule wa mitume, alivyotumia pa·rou·siʹa.a

12. Biblia yenyewe hutusaidia kuthibitishaje maana ya pa·rou·siʹa?

12 Hiyo maana “kuwapo” inaonyeshwa wazi na fasihi za kale, hata hivyo Wakristo wanapendezwa hasa na jinsi Neno la Mungu hutumia pa·rou·siʹa. Jibu ni lilelile—kuwapo. Twaona hivyo kutokana na vielelezo katika barua za Paulo. Kwa mfano, aliwaandikia Wafilipi hivi: “Kama vile mlivyotii sikuzote, si wakati mimi nilipokuwapo tu, bali sasa zaidi sana mimi nisipokuwapo, utimizeni wokovu wenu wenyewe.” Alisema pia juu ya kukaa nao ili waweze kuchachawa “kwa sababu ya kuwapo [pa·rou·siʹa] [kwake] pamoja [nao] tena.” (Wafilipi 1:25, 26; 2:12) Tafsiri nyingine husema “kuwa kwangu pamoja nanyi tena” (Weymouth; New International Version); “ninapokuwa pamoja nanyi tena” (Jerusalem Bible; New English Bible); na “mnapokuwa nami miongoni mwenu mara nyingine tena.” (Twentieth Century New Testament) Kwenye 2 Wakorintho 10:10, 11, Paulo alitofautisha ‘kuwapo kwake mwenyewe’ na ‘kutokuwapo.’ Katika vielelezi hivi yeye bila shaka hakuwa akisema juu ya kukaribia au kuwasili kwake; alitumia pa·rou·siʹa kwa maana ya kuwapo.b (Linganisha 1 Wakorintho 16:17.) Namna gani kuhusu marejezo kwenye pa·rou·siʹa ya Yesu? Je, yana maana ya “kuja” kwake, au yanaonyesha kuwapo kunakoendelea?

13, 14. (a) Kwa nini tufikie mkataa kwamba pa·rou·siʹa huendelea kwa wakati fulani? (b) Ni jambo gani ambalo lazima lisemwe kuhusu urefu wa pa·rou·siʹa ya Yesu?

13 Wakristo watiwa-mafuta kwa roho katika siku ya Paulo walipendezwa na pa·rou·siʹa ya Yesu. Lakini Paulo aliwaonya ‘wasidanganywe.’ Kwanza lazima “mtu wa kuasi” aonekane, ambaye amethibitika kuwa makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. Paulo aliandika kwamba “yule [mtu wa kuasi] ambaye kuja [“kuwapo,” “NW”] kwake ni kwa mfano wa kutenda kwake Shetani, kwa uwezo wote, na ishara na ajabu za u[w]ongo.” (2 Wathesalonike 2:2, 3, 9, italiki ni zetu.) Kwa wazi, pa·rou·siʹa, au kuwapo, kwa yule “mtu wa kuasi” hakukuwa kuwasili kwa muda tu; kungeendelea kwa wakati fulani, ambapo katika huo ishara za uwongo zingetokezwa. Kwa nini hili ni jambo la maana?

14 Fikiria mstari unaotangulia tu: “Ndipo atakapofunuliwa yule asi, ambaye Bwana Yesu atamwua kwa pumzi ya kinywa chake, kumwangamiza kwa ufunuo wa kuwapo kwake.” (Italiki ni zetu.) Sawa na vile kuwapo kwa “mtu wa kuasi” kungekuwa kwa kipindi fulani cha wakati, kuwapo kwa Yesu kungeendelea kwa muda fulani na upeo wako ungekuwa uangamizo wa yule “mwana wa uharibifu.”—2 Wathesalonike 2:8.

Sehemu Mbalimbali Katika Lugha ya Kiebrania

15, 16. (a) Ni neno gani hasa linalotumiwa katika tafsiri nyingi za Mathayo katika Kiebrania? (b) Neno bohʼ hutumiwaje katika Maandiko?

15 Kama ilivyoonyeshwa, yaonekana kwamba mwanzoni Mathayo aliandika Gospeli yake katika Kiebrania. Kwa hiyo, ni neno gani la Kiebrania alilotumia kwenye Mathayo 24:3, 27, 37, 39? Tafsiri za Mathayo zinazotafsiriwa katika Kiebrania cha kisasa zina namna ya kitenzi bohʼ, katika swali la mitume na pia katika jibu la Yesu. Hilo lingeweza kuongoza kwenye usomaji mbalimbali kama huu: “Itakuwa ni nini ishara ya [bohʼ] kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” na “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo [bohʼ] kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” (NW) Neno bohʼ humaanisha nini?

16 Kijapokuwa na maana mbalimbali, kitenzi cha Kiebrania bohʼ humaanisha kwa msingi “kuja.” Kamusi ya Theological Dictionary of the Old Testament yasema hivi: ‘Likionekana mara 2,532, neno bohʼ ndicho kimojapo vitenzi vinavyotumiwa mara nyingi zaidi katika Maandiko ya Kiebrania na ndicho kitenzi kikuu kinachotumiwa kuonyesha mwendo. (Mwanzo 7:1, 13; Kutoka 12:25; 28:35; 2 Samweli 19:30; 2 Wafalme 10:21; Zaburi 65:2; Isaya 1:23; Ezekieli 11:16; Danieli 9:13; Amosi 8:11) Ikiwa Yesu na mitume wangetumia neno lenye maana nyingi hivyo, maana ingeweza kubishaniwa. Lakini je, walitumia hilo?

17. (a) Kwa nini si lazima iwe kwamba tafsiri za Mathayo katika Kiebrania cha kisasa huonyesha yale ambayo Yesu na mitume wake walisema? (b) Ni wapi kwingine tuwezako kupata kidokezo cha neno ambalo yawezekana Yesu na mitume walitumia, na ni sababu gani nyingine inayofanya chanzo hicho kiwe chenye upendezi kwetu? (Ona kielezi-chini.)

17 Kumbuka kwamba tafsiri za Kiebrania cha kisasa ni tafsiri ambazo huenda zisionyeshe barabara yale aliyoandika Mathayo katika Kiebrania. Jambo la hakika ni kwamba yawezekana sana Yesu alitumia neno jingine badala ya bohʼ, moja ambalo lilifaana na maana ya pa·rou·siʹa. Twaona jambo hilo kutoka katika kile kitabu cha 1995 cha Hebrew Gospel of Matthew, cha Professor George Howard. Kitabu hicho kilikazia maandishi fulani yenye ubishi dhidi ya Ukristo ya karne ya 14 yaliyoandikwa na tabibu Myahudi Shem-Tob ben Isaac Ibn Shaprut. Hati hiyo ilikuwa na maandishi ya Kiebrania ya Gospeli ya Mathayo. Kuna uthibitisho kwamba badala ya kutafsiriwa kutoka Kilatini au Kigiriki katika wakati wa Shem-Tob, maandishi hayo ya Mathayo yalikuwa mazee sana na awali yalikuwa yametungwa katika Kiebrania.c Kwa njia hiyo hayo yaweza kutuleta karibu zaidi na yale yaliyosemwa kwenye Mlima wa Mizeituni.

18. Shem-Tob atumia neno jipi la Kiebrania lenye upendezi, nalo lamaanisha nini?

18 Kwenye Mathayo 24:3, 27, 39, maandishi ya Mathayo ya Shem-Tob hayatumii kitenzi bohʼ. Badala ya hivyo, yanatumia nomino bi·ʼahʹ inayolingana nayo. Nomino hiyo huonekana katika Maandiko ya Kiebrania kwenye Ezekieli 8:5 pekee, ambapo inamaanisha ‘mahali pa kuingilia.’ Badala ya kuonyesha tendo la kuja, hapo bi·ʼahʹ hurejezea mwingilio wa jengo; unapokuwa mahali pa kuingilia au mlangoni, umo katika jengo. Pia, hati za kidini zisizo za Kibiblia miongoni mwa Hati-Kunjo za Bahari Iliyokufa mara nyingi hutumia bi·ʼahʹ kuhusiana na kuwasili au kuanza kwa nyadhifa za kikuhani. (Ona 1 Mambo ya Nyakati 24:3-19; Luka 1:5, 8, 23.) Na tafsiri ya 1986 katika Kiebrania ya Peshitta ya Kisiria (au, Kiaramu) cha kale hutumia bi·ʼahʹ kwenye Mathayo 24:3, 27, 37, 39. Kwa hiyo kuna uthibitisho kwamba katika nyakati za kale yawezekana nomino bi·ʼahʹ ilikuwa na maana iliyotofautiana kwa njia fulani na kitenzi bohʼ kinachotumiwa katika Biblia. Kwa nini hilo ni lenye upendezi?

19. Ikiwa Yesu na mitume walitumia bi·ʼah,ʹ ni mkataa gani huenda tukafikia?

19 Katika swali la mitume na katika jibu la Yesu yawezekana walitumia nomino hii bi·ʼah.ʹ Hata ikiwa mitume walikuwa wakifikiria tu wazo la kuwasili kwa Yesu wakati ujao, yawezekana kwamba Kristo alitumia bi·ʼahʹ ili kutia ndani mengi zaidi kuliko yale waliyokuwa wakifikiria. Huenda ikawa Yesu alikuwa akielekezea kuwasili kwake ili kuanza wadhifa mpya; kuwasili kwake kungekuwa mwanzo wa fungu lake jipya. Hilo lingelingana na maana ya pa·rou·siʹa, ambalo Mathayo alitumia baadaye. Kwa kueleweka, kutumia bi·ʼahʹ jinsi hiyo kungepaswa kuunga mkono yale ambayo Mashahidi wa Yehova wamefundisha kwa muda mrefu, kwamba ile “ishara” yenye kutia ndani mambo mengi aliyotoa Yesu ilipaswa ionyeshe kwamba alikuwapo.

Kungojea Upeo wa Kuwapo Kwake

20, 21. Twaweza kujifunza nini kutokana na elezo la Yesu kuhusu siku za Noa?

20 Kujifunza kwetu juu ya kuwapo kwa Yesu kwapaswa kuwa na uvutano wa moja kwa moja juu ya maisha yetu na matazamio yetu. Yesu aliwasihi sana wafuasi wake wabaki wakiwa macho. Yeye aliandaa ishara ili kuwapo kwake kuweze kutambuliwa, ingawa wengi wasingejali: “Kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu [“Noa,” NW], ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu. Kwa kuwa kama vile siku zile zilizokuwa kabla ya Gharika watu walivyokuwa wakila, na kunywa, wakioa na kuolewa, hata siku ile aliyoingia Nuhu katika safina, wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu.”—Mathayo 24:37-39.

21 Katika siku za Noa, watu walio wengi wa kizazi hicho waliendelea tu na shughuli zao za kawaida. Yesu alitabiri kwamba ingekuwa vivyo hivyo kwa habari ya “kuja [“kuwapo,” NW] kwake Mwana wa binadamu.” Yawezekana kwamba watu waliomzunguka Noa walihisi kwamba hakuna jambo lolote ambalo lingetendeka. Unajua kilichotendeka kwa kweli. Siku hizo, zilizoenea kipindi fulani, zilielekea kwenye upeo, “Gharika ikaja, ikawachukua wote.” Luka hutoa simulizi kama hilo ambalo katika hilo Yesu alilinganisha “siku za Nuhu [“Noa,” NW]” na “siku zake Mwana wa Adamu.” Yesu alionya kwa upole hivi: “Ndivyo itakavyokuwa siku ile atakayofunuliwa Mwana wa Adamu.”—Luka 17:26-30.

22. Kwa nini tupendezwe hasa na unabii wa Yesu katika Mathayo sura ya 24?

22 Hayo yote yana maana ya pekee kwetu kwa sababu tunaishi wakati ambapo twatambua matukio aliyotabiri Yesu—vita, matetemeko ya dunia, magonjwa ya kuambukiza, upungufu wa chakula, na mnyanyaso wa wanafunzi wake. (Mathayo 24:7-9; Luka 21:10-12) Hali hizo zimedhihirika tangu lile pambano lenye kubadili historia lililoitwa kwa kufaa Vita ya Ulimwengu 1, ingawa watu walio wengi huona mambo hayo kuwa sehemu za kawaida za historia. Hata hivyo, Wakristo wa kweli huona umaana wa matukio hayo makubwa, sawa na vile watu walio macho huelewa kutokana na mtini wenye kutoa majani, kwamba wakati wa kiangazi umekaribia. Yesu alishauri hivi: “Nanyi kadhalika, mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.”—Luka 21:31.

23. Maneno ya Yesu katika Mathayo sura ya 24 yana maana ya pekee kwa nani, na kwa nini?

23 Juu ya Mlima wa Mizeituni, Yesu alielekeza sehemu kubwa ya jibu lake kwa wafuasi wake. Wao ndio waliopaswa kushiriki katika ile kazi ya kuokoa uhai ya kuhubiri habari njema duniani pote kabla ya mwisho kuja. Wao ndio wangeweza kulitambua lile “chukizo la uharibifu . . . [likiwa] limesimama katika patakatifu.” Wao ndio wangeitikia kwa ‘kukimbia’ kabla ya dhiki kubwa. Na wao ndio wangeathiriwa hasa na maneno haya yaliyoongezwa: “Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo.” (Mathayo 24:9, 14-22) Lakini maneno hayo ya kufikiriwa yanamaanisha nini hasa, na kwa nini yaweza kusemwa kwamba yanatuandalia msingi wa kuwa na furaha, uhakika, na bidii iliyoongezeka sasa? Funzo lifuatalo la Mathayo 24:22 litaandaa majibu.

[Maelezo ya Chini]

a Vielelezo kutoka kwa Yosefo: Kwenye Mlima Sinai umeme na ngurumo “zilitangaza kwamba Mungu alikuwapo [pa·rou·siʹa] hapo.” Udhihirisho wa kimuujiza katika tabenakulo “ulionyesha kuwapo [pa·rou·siʹa] kwa Mungu.” Kwa kumwonyesha mtumishi wa Elisha yale magari yenye kuzunguka-zunguka, Mungu “alidhihirisha kwa mtumishi wake nguvu [zake] na kuwapo [pa·rou·siʹa] kwake.” Ofisa Mroma Petronius alipojaribu kuwatuliza Wayahudi, Yosefo alidai kwamba ‘Mungu alimwonyesha Petronius kuwapo [pa·rou·siʹa] kwake kwa kutuma mvua. Yosefo hakutumia pa·rou·siʹa kumaanisha kukaribia tu au kuwasili kwa muda. Lilimaanisha kuwapo kwenye kuendelea, hata kusikoonekana. (Kutoka 20:18-21; 25:22; Mambo ya Walawi 16:2; 2 Wafalme 6:15-17)—Linganisha Antiquities of the Jews, Kitabu cha 3, sura ya 5, fungu la 2 [80]; sura ya 8, fungu la 5 [202]; Kitabu cha 9, sura ya 4, fungu la 3 [55]; Kitabu cha 18, sura ya 8, fungu la 6 [284].

b Katika kamusi ya A Critical Lexicon and Concordance to the English and Greek New Testament, E. W. Bullinger huonyesha kwamba pa·rou·siʹa humaanisha ‘kuwa au kupata kuwapo, basi, kuwapo, kuwasili; kuja kunakotia ndani wazo la kukaa kwa kudumu kuanzia kuja huko na kuendelea.’

c Uthibitisho mmoja ni kwamba mara 19, yana ule usemi wa Kiebrania “Lile Jina,” ukiwa umeandikwa mzima au kwa ufupi. Profesa Howard aandika hivi: “Kusoma Jina la Kimungu katika hati ya Kikristo iliyonukuliwa na mwandishi Myahudi wa makala zenye ubishi ni jambo la kutokeza. Ikiwa hii ingekuwa tafsiri ya Kiebrania ya hati ya Kikristo ya Kigiriki au ya Kilatini, mtu angetazamia kupata adonai [Bwana] katika maandishi, si ufananisho wa lile jina tukufu la kimungu YHWH. . . . Jambo la kwamba aliongeza jina hilo tukufu halielezeki. Uthibitisho hudokeza kwa nguvu kwamba Shem-Tob alipokea nakala yake ya Mathayo ikiwa tayari na Jina la Kimungu katika maandishi na kwamba labda alilihifadhi badala ya kujasiri kuwa na hatia ya kuliondoa.” Biblia ya New World Translation of the Holy Scriptures—With References hutumia maandishi ya Mathayo (J2) ya Shem-Tob kuwa utegemezo wa kutumia jina la kimungu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

Ungejibuje?

◻ Kwa nini ni jambo la maana kuona tofauti kati ya jinsi Biblia kadhaa hutafsiri Mathayo 24:3?

◻ Maana ya pa·rou·siʹa ni nini, na kwa nini hilo ni jambo la kufikiriwa?

◻ Ni ulinganifu gani unaoweza kuwako kwenye Mathayo 24:3 katika Kigiriki na katika Kiebrania?

◻ Twahitaji kujua jambo gani kuhusu wakati katika kuelewa Mathayo sura ya 24?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mlima wa Mizeituni, ulio karibu na Yerusalemu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki