Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Kulea Watoto Nikiwa mwalimu wa shule ya msingi, nathamini sana makala zenu juu ya “Watoto wako—Kufanya Yaliyo Bora Zaidi Kwao.” (Septemba 22, 1992, Kiingereza) Mojapo magumu makubwa zaidi ambayo walimu hukabili leo ni kushughulika na watoto ambao wazazi wao ni wenye shughuli mno wasipendezwe nao kihalisi. Katika mkutano mmoja wa karibuni wa Usiku wa Wazazi unaofanywa kila mwaka, nilishiriki na wengine baadhi ya mambo yaliyokuwa katika toleo hilo. Wazazi waliona mazungumzo yetu kuwa ya mwono wa ndani na yenye kuchochea kufikiri.
M. P., United States
Mlifanya vizuri sana. Hizo zilikuwa makala bora zaidi ambazo nimepata kusoma. Hamkuonyesha tu mifano mibaya bali mlitaja pia masuluhisho.
M. R., Ujerumani
Makala hizo ziliandikwa vizuri, lakini ni lazima nitaje juu ya urejezo wenu wa utumizi mbaya wa watoto kwa njia ya waziwazi sana. Ulinishtua sana.
F. M., Kanada
Kwa kweli inashtua kusoma juu ya utumizi mbaya unaofanywa na watu wazima kwa watoto wasio na hatia, wasioweza kujikinga. Ingawa tunajua kwamba baadhi ya wasomaji wetu huenda wasipende kusoma mambo kama hayo, wazazi wanahitaji kujulishwa juu ya kila hatari halisi ambayo watoto wao wanakabili leo. (Linganisha 2 Wakorintho 2:11.) Kwa hiyo tuliona ni lazima tutaje mambo hayo waziwazi, tukifanya hivyo kwa njia inayofaa kadiri iwezekanavyo.—Mhariri.
Dansi za Uhitimu Nilipata makala ya “Vijana Wanauliza . . . Je! Niende Kwenye Dansi ya Uhitimu?” (Machi 8, 1993) kuwa na habari yenye kuarifu na yenye msaada. Hata hivyo, je, mlikuwa mkitia moyo Wakristo wawe na vikusanyiko vikubwa rasmi vya kujitumbuiza?
N. P., United States
Makala hiyo haikuwa ikitia moyo kupanga vitumbuizo vikubwa vya kirafiki. Tulitaja tu kwamba kuhitimu kutoka shule ya sekondari ni tukio la maana. Baadhi ya vijana Wakristo na wazazi wao wanaweza kuchagua kufurahia pindi hiyo pamoja na wengine. Kitia moyo kilitolewa cha kuweka kila utendaji wa kirafiki kuwa ‘wenye kiasi, wa ukubwa unaofaa, na kupangwa vizuri.’ Ona “Mnara wa Mlinzi” la Agosti 15, 1992.—Mhariri.
Mafuta ya Zeituni Asanteni sana kwa makala yenu nzuri ya “Mafuta ya Zeituni Yenye Kutumika Kwa Njia Nyingi” katika toleo la Oktoba 8, 1992, Kiingereza. Ninafanya kazi katika hospitali nikiwa mshauri wa ulaji, na ninashauri watu juu ya ulaji usiokuwa na mafuta mengi. Makala hiyo ilikuwa sahihi na yenye kunifaa sana katika kufundisha watu.
D. S., United States
Lugha Chafu Binti yangu, anayekaribia miaka 15, alitoka shuleni na kuniambia kwamba alikuwa na tatizo kwa sababu watoto wengi katika shule yao hutumia lugha chafu kwa kawaida. Alitaka kujua kuna ubaya gani hasa katika kutumia maneno machafu katika usemi wa kila siku. Tulijaribu kueleza lakini tukahisi hatukufanya vizuri sana. Jioni hiyo, nilipopata toleo la Amkeni! la Desemba 8, 1992, Kiingereza, nilishangaa kuona makala “Maoni ya Biblia—Kwa Nini Wakristo Wasitumie Lugha Chafu.” Nilienda nayo katika chumba cha kulala cha binti yangu mara hiyo na tukaisoma pamoja. Sasa yeye anahisi anaweza kujibu yeyote amwulizaye ni kwa nini hatumii maneno machafu.
P. P., Uingereza
Ulimwengu Mpya Ule mfululizo “Ulimwengu Mpya Unaowaridhisha Wote” (Oktoba 22, 1992) ulikuwa mojapo makala bora zaidi juu ya jambo hilo katika miaka ya karibuni. Maandiko yaliyotajwa na picha zilizo nzuri ziliamsha ndani yangu hisia ya uthamini wa kina kirefu. Nina hakika utagusa mioyo ya wasomaji wengi.
I. Z., Italia