Vijana Wanauliza...
Vipi Juu ya Kuzurura-zurura?
MADUKA ya vidio, mikahawa ya vyakula vyepesi, kona za barabara za mitaa, maduka madogo ya karibu yanayofunguliwa kwa muda mrefu—katika mitaa ya matajiri na maskini—zimekuwa sehemu ambazo vijana wanapenda kuzurura-zurura.
Madukani hasa ndizo sehemu zinazopendwa za kuzurura-zurura katika United States. Huko, vikundi vya vijana mara nyingi vinaweza kuonwa vikizurura kwa muda wa saa nyingi. “Nyakati zote madukani ndiyo sehemu za kutembelewa,” adai msichana mmoja tineja, “kwa sababu kuna mambo mengi yanayoendelea huko, na nyakati zote kuna kitu cha kuvuta akili yako—kama vile wavulana!”
Kama hakuna maduka karibu? Basi sehemu iliyo tupu au kona ya barabara itafaa. Tari mwenye umri wa miaka 15 asema hivi: “Rafiki zangu nami huenda kwa gari hadi kwenye sehemu kubwa za kuegesha magari katika bustani ya karibu na kukaa kwenye sehemu za mbele za gari na kuongea kwa muda wa saa nyingi.”—Gazeti ’Teen, Septemba 1990.
Bila shaka, hakuna jambo jipya hasa kuhusu kuzurura-zurura. Biblia yatuambia juu ya watu wa nyakati za kale ambao walikuwa wakikusanyika katika sehemu za umma na “walikuwa hawana nafasi kwa neno lolote ila kutoa habari na kusikiliza habari za jambo jipya.” (Matendo 17:21) Lakini ni kwa nini kipisha wakati hiki kimekuja kupendwa sana na vijana siku hizi?
Kulingana na kitabu The Adolescent, cha F. Philip Rice, vijana “hutambua kwa kadiri yenye kuongezeka mahitaji yao ya kuwa wa kikundi fulani. Wanataka wapendwe na marika zao.” Hivyo, kuzurura-zurura na marafiki zao huonekana kuwa inajazia uhitaji wa kuwa na mwenzi na utegemezo.
Vijana wengine huiona kuwa njia tu ya kuondoa uchovu. Aeleza kijana Michelle: “kukaa nyumbani usiku kunachosha. Unataka uende nje na kufurahia kwa sababu usipoenda nje utakuwa na jioni yenye kuchosha.” Ed mwenye umri wa miaka kumi na sita anadai kwamba kuzurura-zurura “ni jambo linalofaa kufanywa na kwa njia fulani kunakuepusha na matatizo.” Lakini kweli kunafanya hivyo?
Watu Wanapozurura-zurura
Biblia haishutumu kujifurahisha na marafiki zako. Hata hivyo, inaonya hivi: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Sasa, ni vijana wangapi kati ya wale wanaosimama-simama kwenye kona za barabara bila kitu cha kufanya wanaoweza kusemwa kuwa watu wenye hekima—wale wanaostahi kanuni za Biblia? Huenda wasiwe watu wenye matata, lakini kikundi kikubwa cha vijana wachovu, wasiokuwa na usimamizi pamoja na kuwa na wakati mwingi wa bure kinaweza kwa urahisi kuleta matatizo.
Kwa sababu hiyo Biblia haipendekezi kuzurura-zurura. Fikiria wakati mtume Paulo na Sila walipozuru jiji la Thesalonike. Wapinzani wa ujumbe wa Kikristo ‘walijitwalia watu kadha wa kadha katika watu ovyo wasio na sifa njema [“wazururaji wasiofaa kitu,” Today’s English Version], nao wakakutanisha mkutano, wakafanya ghasia mjini.’ (Matendo 17:5) Kulingana na Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words, wazururaji hao walikuwa watu mmoja mmoja “waliokuwa sokoni daima na hivyo kuzurura-zurura huko bila kitu cha kufanya.” Je! waona ufanano? Kwa vyovyote vile, yaelekea wazururaji hao hawakupendezwa na ujumbe wa Paulo, lakini wakiwa hawana kitu cha kufanya, wangeweza kwa urahisi kushawishiwa wafanye ghasia.
Ukorofi na Jeuri
Sasa, fikiria uwezekano wa matatizo kutokea wakati kikundi cha vijana wasiokuwa na jambo la kufanya wanapokuwa pamoja. Si kwamba kuna yeyote anayepanga kuwe na jeuri. “Hakuna mambo mengi yanayoendelea,” adai kijana mwenye umri wa miaka 16 anayeitwa Ken anayependa kuketi tu kupiga gumzo katika sehemu ya kuegesha magari ya shule. “Tunakalia magari yetu na kusimulia mizaha ya upuuzi au tunazungumza tu juu ya urafiki wetu na watu wa jinsia tofauti.” Naam, kuzungumza juu ya michezo, muziki, na juu ya mtu wa jinsia tofauti huenda kukafurahisha kila mmoja kwa muda. Lakini, mara nyingi, vijana huchoka upesi na mazungumzo tu.
Watafiti Mihaly Csikszentmihalyi na Reed Larson waripoti hivi: “Tena na tena, [vijana] walisimulia pindi hizo [za kuzurura-zurura] kwa maneno kama ‘kuwa wenye ghasia,’ wenye makelele, wenye kichaa, na wakaidi. . . . Kuna kitu fulani kuhusu kukutana kwa kikundi cha marika kinachotokeza ghasia, hata ikiwa vijana mmoja mmoja wanaohusika hawana mwelekeo wa kufanya hivyo. . . . Matendo yenye ghasia yalitia ndani kuendesha gari huku na huku, kutupa mikebe katika nyua za watu, na kupigana.” (Italiki ni zetu.)—Being Adolescent.
Ni kweli, huenda usiwe na mwelekeo wa kufanya jambo la upumbavu kwa sababu tu marafiki zako wanalifanya. Lakini unaweza kujitia chini ya mkazo mwingi wa kufanya mabaya ukiwa miongoni mwa watenda mabaya. (1 Wakorintho 15:33, NW) Hata kama unaepuka kujiingiza katika ghasia, kuwapo kwako hapo kwaweza kufanya wengine wakudhanie vibaya. Hilo ndilo jambo lililompata msichana mchanga Dina, binti ya Yakobo, mzee wa ukoo wa kale Mwebrania.
Dina alilelewa kuwa mwabudu wa Yehova Mungu, ingawa familia yake iliishi katika nchi ya Kanaani—nchi iliyojawa na upotovu wa kingono na ibada ya sanamu. Basi, baba yake Yakobo alijaribu sana kupunguza uhusiano na Wakanaani wenye kukosa maadili kwa kupiga hema yake nje ya jiji la Shekemu na kuweka ugavi wa maji tofauti. (Mwanzo 33:18; Yohana 4:12) Na bado, Dina ‘akawa anatoka kuwaona binti za nchi,’ labda kwa ukawaida. (Mwanzo 34:1) Huenda Dina alikuona kuzurura-zurura na Wakanaani kuwa raha isiyodhuru. Lakini wanawake wa Kanaani walikuwa na sifa ya kukosa maadili. Kwa hiyo, wakati mtu mmoja Mkanaani aliyeitwa Shekemu alipomwona Dina akiwa pamoja na wanawake kama hao, ‘alimtwaa, akalala naye, akambikiri.’—Mwanzo 34:2.
Kwa njia iyo hiyo, kuzurura-zurura na kikundi kisichofaa kunaweza kukuweka katika matatizo makubwa. Kijana mmoja anayeitwa Leonard akumbuka kwamba ajapolelewa akiwa Mkristo, alianza “kuzurura-zurura na kikundi chenye uasi. Tulikuwa tukizurura-zurura na kunywa pombe pamoja—hata ingawa sikuwa na umri wa kukubaliwa kunywa pombe. Kufikia umri wa miaka 18, nilikuwa nikivuta bangi.”
Matumizi Bora Zaidi ya Wakati
Uchunguzi mmoja ulipata kwamba asilimia 44 ya vijana waliochunguzwa walitumia muda wa saa tatu hadi tano kila wakati walipoenda madukani; asilimia 14 walikuwa wakitumia muda wa saa sita. Lakini badala ya kuwa na tabia ya kupoteza wakati kwa kukosa kitu cha kufanya, kijana mwenye hekima ‘hukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu.’—Waefeso 5:15, 16.
Je! kazi zako za shule na za nyumbani hubaki bila kufanywa kwa sababu ya wakati unaotumia kuzurura-zurura na vijana wengine? Vipi juu ya utendaji wako wa kiroho—funzo la binafsi la Biblia, mikutano ya Kikristo, kazi ya kutolea wengine ushahidi? Je! unapuuza madaraka kama hayo? Ukiwa na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana,” haielekei kwamba utakuwa na wakati ambao utakosa kitu cha kufanya.—1 Wakorintho 15:58, NW.
Mambo ya Badala Yanayofaa
Tafrija ni sehemu ya maana ya maisha. (Mhubiri 3:4) Lakini kuzurura-zurura si njia pekee ya kujifurahisha. “Ninafurahia kuwa peke yangu,” asema mwanamke mchanga anayeitwa Lucy. “Ninapenda kusoma, na hilo limenisaidia kusitawisha kupendezwa na historia, tamaduni, na lugha za nchi za nje. Mimi huzuru majumba ya hifadhi ya vitu vya kale na hifadhi za picha, mimi hushona na kupika. Pia mimi hufurahia kuchora na kuandika barua, mimi hata hujaribu shairi kidogo mara moja-moja.” La, si lazima kuwa peke yako kuchoshe.
Familia yenu yaweza kuwa chanzo kingine cha tafrija inayofaa. Sasa, kabla ya kukataa wazo hilo, ebu msikilize kijana mmoja anayeitwa Jack. Yeye akumbuka: “Kila wakati wazazi wangu walikuwa wametupangia kitu cha kufanya. Tulikuwa tukienda kuteleza juu ya barafu na kwenda kwenye mchezo wa kwenda kwa kutumia viatu vyenye magurudumu; tulikuwa tukienda katika bustani, makao ya wanyama ambao wamefungiwa, na majumba ya hifadhi. Hata kufanya usafi katika ua au nyumba kulifurahisha wakati tulipofanya hivyo tukiwa familia.” Labda familia yako imeacha kufanya mambo pamoja. Na kama ni hivyo, mbona usifikirie mambo fulani ya kufanya pamoja na familia mnapoenda kwenye tafrija? Unaweza kufurahia zaidi ya ulivyotarajia!
Jambo hilo halimaanishi kwamba huwezi kufurahia kushirikiana na marika zako—kutia ndani nyakati mnapozungumza tu juu ya mambo ya kufurahisha au kustarehe tu pamoja. Lakini, uwe mteuzi kwa aina ya marafiki unaochagua. Kijana mmoja anayeitwa Enrique asema hivi: “Nilikuwa nikipenda kuzurura-zurura na vijana wa kilimwengu, lakini mara nilipoweka maisha yangu wakfu kumtumikia Yehova, nilishirikiana na vijana kundini. Tulienda kuhubiri pamoja, kucheza mpira pamoja—nilijitahidi kufanya mambo pamoja nao kwa kadiri nilivyoweza.”
Shelleace vilevile alikuwa akipenda kuzurura-zurura na vikundi visivyofaa. Yeye akumbuka hivi juu ya marafiki zake wa zamani: “Maisha zao zilikosa kusudi na mwongozo. Ilinichukua muda kujiondoa kutoka kwao, lakini nilipofanya hivyo, nilijipatia washirika wazuri. Ndipo tu nilipofanya maendeleo kiroho.”
Kwa hiyo, ingawa kuzurura-zurura kwaweza kufurahisha au hata kusisimua nyakati nyingine, hakutakusaidia kiroho, na inaelekea kutakudhuru. Uwe mwerevu. Tafuta njia bora zaidi za kutumia wakati wako.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Je! kuzurura-zurura ndiyo njia bora zaidi ya kutumia wakati wako?