Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g93 6/22 kur. 21-24
  • Sayansi—Jitihada Inayoendelea ya Ainabinadamu ya Kutafuta Kweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sayansi—Jitihada Inayoendelea ya Ainabinadamu ya Kutafuta Kweli
  • Amkeni!—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mipaka ya Sayansi
  • Tendo la Haraka Lahitajiwa
  • Ni Nani Anayeweza Kusuluhisha Tatizo Hilo?
  • Maisha Katika Wakati Ujao Ulio Karibu
  • Waweza Kuitumaini Sayansi Kadiri Gani?
    Amkeni!—1998
  • Sayansi—Jitihada Inayoendelea ya Ainabinadamu ya Kutafuta Kweli
    Amkeni!—1993
  • Chanzo cha Ulimwengu na Uhai Ni Nini?
    Amkeni!—2002
  • Jinsi Sayansi Inavyoathiri Maisha Yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1993
g93 6/22 kur. 21-24

Sehemu ya 6

Sayansi—Jitihada Inayoendelea ya Ainabinadamu ya Kutafuta Kweli

Kuyakabili Magumu ya Karne ya 21

TISA, nane, saba, na kuendelea kuhesabu! Je! twahesabu kuelekea wakati wa kurushwa kwa roketi angani? La, badala ya hiyo twahesabu miaka ambayo ingali inabaki kabla binadamu kuingizwa katika mambo yasiyojulikana ya karne ya 21.a

Wakiona matimizo ya kisayansi ya karne iliyopita, wengi wanaweza kuamini kwa unyoofu kwamba sayansi inaweza kukabili ugumu wowote ambao karne ya 21 yaweza kuleta.b Huenda wakahisi kama alivyohisi mwandikaji mmoja wa Ufaransa katika mwanzo wa karne ya 20. “Sayansi inaelekea kutawala ulimwengu leo,” akaandika. “Kutoka sasa utawala wa ulimwengu si wa Mungu, bali ni wa sayansi, ni wa sayansi ikiwa mfadhili na mkombozi wa ainabinadamu.”

Ili sayansi itimize mataraja hayo ni lazima iondoe matatizo mengi ambayo imechangia kuleta.

Ule uharibifu wa mazingira ambao sayansi imesababisha ni mkubwa sana. Kitabu 5000 Days to Save the Planet chakazia hivi: “Tukiendelea na mwendo wetu wa sasa wa kuharibu mazingira, swali si kama jamii ya kisasa itaokoka karne inayofuata, bali ni kama itatoweka kwa kishindo [kinyukilia] au kwa ukimya [kimazingira]?”

Huo hauonekani kuwa uchaguzi unaokubalika.

Mipaka ya Sayansi

“Wanasayansi wengi wa karne ya 19 . . . mara nyingi walihisi kwamba siku moja wangepata kweli kamili na uelewevu wa hakika,” chasema kitabu The Scientist. “Waandamizi wao,” kitabu hicho chaendelea kusema, “huzungumzia tu kufikia ‘uelewevu wa kiasi’, wa kufuata kweli kwa kuendelea lakini bila kuielewa kabisa.” Ukosefu huo wa ujuzi kamili unaweka mipaka sana kwa mambo ambayo sayansi inaweza kufanya.

Mambo hakika ya sayansi hayajabadilika kwa miaka ambayo imepita, lakini nadharia za kisayansi zimebadilika—tena mara kwa mara. Kwa kweli, nyakati nyingine nadharia zimetoka upande mmoja hadi upande ule mwingine. Kwa mfano, kuna wakati wanasayansi wa kitiba walipodhani kwamba kutoa damu mwilini mwa mtu mgonjwa mahututi kulikuwa njia ya kisayansi ya kutibu. Baadaye walidhani kwamba kumtia damu ndiyo utibabu. Sasa wengine wanaanza kuona hekima ya kutotoa damu wala kutotia damu na hivyo kutafuta utibabu mwingine usio hatari.

Kwa wazi, mambo ambayo wanasayansi wanajua ni madogo sana yakilinganishwa na mambo wasiyojua. The World Book Encyclopedia chasema hivi: “Bado wanabotania hawaelewi kabisa jinsi mfumo wa usanidimwanga (fotosinthesi) unavyofanya kazi. Wanabiolojia na wanabiokemia bado hawajapata jibu la swali la jinsi uhai ulivyoanza. Waastronomia bado hawajapata maelezo yanayoridhisha ya chanzo cha ulimwengu wote mzima. Wanasayansi wa kitiba na wafisiolojia hawajui kisababishi wala ponyo la kansa au jinsi ya kutibu aina mbalimbali za magonjwa ya vairasi. . . . Wanasaikolojia hawajui visababishi vyote vya magonjwa ya akili.”

Sayansi ina mipaka pia kwa njia ya kwamba haiwezi kufanya vizuri zaidi ya watu wanaoifanya. Kwa maneno mengine ukosefu wa ujuzi wa mwanasayansi unaongezwa na kutokamilika kwake. Waandikaji wa kitabu 5000 Days to Save the Planet waligundua kwamba “mara kwa mara . . . mashirika yenye kusudi la pekee yamegeuza utafiti, yakapotoa uchanganuzi wa gharama na faida ya vifaa na kukandamiza habari ili wauze bidhaa zinazodhuru au kuendelea na utendaji mbalimbali unaoharibu mazingira.”

Hata ikiwa wanasayansi wengi zaidi ni wanyoofu, bado hiyo si sababu ya kuwastahi au kustahi mno utendaji wao. “Wao ni kama mtu mwingine yeyote,” atoa hoja Edward Bowen aliyezaliwa Uingereza, yeye mwenyewe akiwa mwanasayansi. “Wote wana mapungufu yao. Wengine wamejitoa, wengine ni wapotovu, wengine wana akili nyingi, wengine wamezubaa kama zuzu. Nimejua baadhi ya watu mashuhuri wa sayansi, watu ambao wamefanyia ulimwengu mambo mazuri ajabu. Na ingawa sijui mwanasayansi ambaye amepata kufungwa, nimejua wengine ambao wanastahili kabisa kufungwa.”

Kwa wazi, kwa sababu ya mipaka yayo mingi, sayansi ya kisasa haiwezi kukabili ifaavyo magumu ya karne ya 21. Hasa imeshindwa kulinda mazingira, na badala ya kusaidia kuondoa vita duniani, imesaidia kutengeneza silaha zenye uharibifu mkubwa.

Tendo la Haraka Lahitajiwa

Kila mmoja anakubali kwamba ni lazima jambo fulani lifanywe haraka. Novemba uliopita, kikundi cha wanasayansi 1,575, kutia ndani washindi 99 wa tuzo la Nobeli, kilitoa taarifa yenye kichwa “Onyo la Wanasayansi wa Ulimwengu kwa Binadamu” ambayo ndani yayo waliandika hivi: “Ni mwongo mmoja tu au miongo michache ya miaka inayobaki kabla ya nafasi ya kuondoa matisho yanayotukabili kutoweka na mataraja ya binadamu kudidimia sana.” Wao walikazia hivi: “Ainabinadamu na ulimwengu wa asili wako kwenye mwendo wa kugongana.”

Maonyo kama hayo yametolewa hapo awali. Kwa kweli, katika 1952, Bertrand Russell, mwanafalsafa mwingereza wa karne ya 20 na mwenyewe akitetea sayansi, alisema hivi: “Ikiwa uhai wa kibinadamu utaendelea sayansi ijapokuwapo, ainabinadamu italazimika kujifunza kutia nidhamu hisia zayo, jambo ambalo halijahitajika katika wakati ambao umepita. Watu watalazimika kutii sheria hata kama wanafikiria sheria hiyo si ya haki na haifai. . . . Mambo yasipotendeka hivyo, jamii yote ya kibinadamu itaangamia, na itaangamia kwa sababu ya sayansi. Uchaguzi wa wazi ni lazima ufanywe kabla ya miaka hamsini ijayo, uchaguzi kati ya Kutumia Akili ama Kifo. Na kwa maneno ‘Kutumia Akili’ namaanisha utayari wa kutii sheria inayotangazwa na mamlaka ya kimataifa. Nahofu kwamba ainabinadamu huenda ikachagua Kifo. Natumaini sivyo.”

Ukweli ni kwamba watu wanaotaka kutii viwango vya uadilifu ni wachache sana siku hizi. Yule kiongozi wa kutetea haki za kibinadamu aliyekufa Martin Luther King alisema hivi kwa usahihi: “Uwezo wetu wa kisayansi umepita uwezo wetu wa kiroho. Tuna silaha zenye kuelekezwa kwenye shabaha na tuna watu wasio na shabaha.” Lakini Russell aligundua pasipo kujua suluhisho kwa matatizo ya ainabinadamu aliposema kwamba ainabinadamu italazimishwa “kutii sheria inayotangazwa na mamlaka ya kimataifa.”

Ni Nani Anayeweza Kusuluhisha Tatizo Hilo?

Ni kweli, Bertrand Russell hakuwa akirejezea mamlaka ya kimungu alipozungumzia sheria inayotangazwa na mamlaka ya kimataifa. Lakini kutii sheria zenye mamlaka kama hizo ndiko kunahitajika hasa. Kwa wazi, sheria za kibinadamu na mamlaka za kibinadamu si suluhisho. Haziwezi kubadili ulimwengu na hivyo kuepuka msiba. Rekodi mbaya ya historia yathibitisha kwamba wanadamu wanahitaji utawala wa kimungu.c

Kwa kweli, ni Mungu Mwenye Uwezo Wote pekee, anayeitwa Yehova, ndiye anayeweza kuandaa mamlaka ya kimataifa yenye nguvu na uwezo wa kukabili magumu ya karne ya 21. (Zaburi 83:18) Hiyo mamlaka ambayo ni lazima wote watii ikiwa watapokea uhai ni Ufalme wa Mungu, ambao ni serikali ya ulimwengu ya kimbingu iliyosimamishwa na Muumba, Yehova Mungu.

Zamani sana Biblia ilitabiri hivi kuhusu serikali hii: “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume; na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; naye ataitwa jina lake . . . Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe.” (Isaya 9:6, 7) Bikira Mariamu alitungwa mimba kimwujiza, kisha mtoto huyo aliyetabiriwa, Yesu Kristo, akazaliwa Bethlehemu ya Yudea.—Luka 1:30-33.

Alipokuwa duniani Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali juu ya serikali ya Mungu aliposema hivi: “Basi ninyi salini hivi; . . .Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Ni roho takatifu, au kani ya utendaji, yenye nguvu ya Yehova pekee inayoweza kusaidia watu wenye nia kufanya mabadiliko yanayohitajika katika maisha zao kwa kupatana na sheria za uadilifu za serikali yake. Sayansi haiwezi. Maelfu ya miaka ya mabishano na vurugu yathibitisha kwamba haiwezi.

Yehova Mungu, ambaye ana ujuzi sahihi mwingi sana wa kisayansi, atahakikisha kwamba dunia inafurahia hali za Paradiso, kama zilivyokuwa katika shamba la Edeni, alipoumba wanadamu wawili wa kwanza. Wakati huo aliwaagiza hivi: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha.” (Mwanzo 1:28) Ingawa hawakuwa watiifu na hawakutekeleza mgawo huo, Yehova Mungu atahakikisha kwamba kusudi lake la awali la dunia kuwa paradiso litatimizwa. “Nimenena, nami nitatekeleza,” yeye asema. (Isaya 46:11) Lakini kusudi la awali la Mungu kwa ajili ya dunia litatimizwa lini?

Yesu Kristo na mitume wake walieleza hali ambazo zingekuwapo duniani katika “siku za mwisho,” kabla tu ya Ufalme wa Mungu kuchukua mahali pa serikali zote za kibinadamu. (2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:3-14, 37-39; 2 Petro 3:3, 4) Mtu anaposoma unabii mbalimbali wa Biblia unaotajwa hapo na kuulinganisha na matukio ya ulimwengu, inakuwa wazi kwamba tunaishi katika wakati ambapo Ufalme wa Mungu utachukua hatua inayotajwa katika Biblia kwenye Danieli 2:44: “Na katika siku za wafalme hao [serikali za kibinadamu zinazotawala sasa] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”

Maisha Katika Wakati Ujao Ulio Karibu

Ebu wazia jambo hilo litamaanisha nini kwa wakati ujao ulio karibu! Ni mambo mazuri ajabu kama nini yanayongojea ainabinadamu katika wakati wa karne inayokuja, ikiwa si hata kabla ya wakati huo! Matokeo mabaya ya maelfu ya miaka ya utawala wa kibinadamu usiokamilika, dini yenye unafiki, biashara yenye pupa, na sayansi ya ulimwengu huu vitaondolewa na mahali pavyo pachukuliwe na utawala wa kimungu, ambao utabariki binadamu kupita hata matarajio yao makubwa zaidi.

Hivi ndivyo Biblia inavyosimulia matukio ambayo kwa hakika yatakuwapo katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu: “Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4.

Kwa hiyo, jambo muhimu kabisa kwako kujua ni lile la kuendelea kuhesabu ambako kutakwisha hivi karibuni kwenye uharibifu wa mfumo wa ulimwengu ambao uko chini ya mtawala mwenye nguvu, asiyeonekana, Shetani Ibilisi. (Yohana 12:31; 2 Wakorintho 4:3, 4) Ni muhimu kwamba ujifunze mapenzi ya Mungu na kuyafanya, kwa sababu Biblia inaahidi hivi: “Dunia [Ulimwengu, NW] inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.”—1 Yohana 2:17.

Basi, kadiri wakati unavyoruhusu, na unufaike ifaavyo kwa hekima kutokana na maandalizi ya Yehova kwa ajili ya kuokolewa. Kisha utakuwa na pendeleo la kufurahia maisha wakati ujao, naam, katika karne ya 21 inayokuja—na vilevile katika karne za 22, 23, na nyinginezo baadaye.

[Maelezo ya Chini]

a Tukisema kihalisi, karne ya 21 itaanza mnamo Januari 1, 2001. Hata hivyo, matumizi ya kawaida huona karne ya 1 kuwa yaanzia mwaka wa 1 hadi wa 99 (hakukuwa na mwaka 0); karne ya 2, kutoka mwaka wa 100 hadi wa 199; na kufuatana na hiyo, karne ya 21, yaanzia mwaka wa 2000 hadi wa 2099.

b Hii ni sehemu ya mwisho katika Amkeni! ya mfululizo wenye sehemu sita juu ya sayansi.

c Kutokufaa kwa serikali za kibinadamu kulionyeshwa katika mfululizo wa sehemu kumi katika Amkeni! (Machi 8 hadi Desemba 8, 1991) wenye kichwa “Utawala wa Kibinadamu Wapimwa Katika Mizani.”

[Sanduku katika ukurasa wa 23]

Kujapokuwako Habari Mbaya, Kuna Habari Njema

Yajapokuwa maendeleo ya kisayansi, watoto wengi wenye njaa kali na watu wazima wenye kudhoofika bado wanapatikana. Lakini hivi karibuni chini ya Ufalme wa Kimesiya wa Mungu, ‘kutakuwapo wingi na nafaka; katika ardhi juu ya milima.’—Zaburi 72:16.

Yajapokuwa maendeleo ya kisayansi, mamilioni bado wanadhulumiwa na kupatwa na jeuri. Lakini hivi karibuni Mfalme wa Ufalme wa Kimesiya wa Mungu ‘atamwokoa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atawakomboa nafsi zao na kuonewa na udhalimu.’—Zaburi 72:12-14.

Yajapokuwa maendeleo ya kisayansi, idadi ya watu wasio na makao, wakiwa hawana nyumba na chakula cha kutosha, inaendelea kupanda ulimwenguni pote. Lakini hivi karibuni chini ya Ufalme wa Kimesiya wa Mungu, watu “watajenga nyumba na kukaa ndani yake . . . Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine.”—Isaya 65:21, 22.

Yajapokuwa maendeleo ya kitiba, magonjwa yanayoweza kuzuiwa yanaendelea kuua mamilioni. Lakini hivi karibuni chini ya Ufalme wa Kimesiya wa Mungu, “hapana mwenyeji atakayesema, mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Maisha yatakuwa yenye kufurahisha kila mahali duniani

[Hisani]

Kwa hisani ya Hifadhi ya Nyoka na Wanyama ya Hartebeespoortdamy

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki