Wazazi Wenye Kuwatenda Watoto Vibaya—Wasababishaji Wakubwa wa Mkazo wa Akili
“Kwa sababu [watoto] wana habari chache nje ya familia, mambo wanayojifunza nyumbani kujihusu na kuhusu wengine yanakuwa mambo ya kweli yanayokazwa akilini mwao.” —Dakt. Susan Forward.
MFINYANZI anaweza kuchukua rundo la udongo, atie kiasi cha maji kinachohitajika, na kuufanyiza chombo kinachopendeza. Vivyo hivyo, wazazi hufanyiza maoni ya mtoto, yake mwenyewe na yale ya ulimwengu. Kukiwa na upendo, mwongozo, na nidhamu, mtoto hukua awe mtu mzima aliyeimarika.
Hata hivyo, mara nyingi zaidi maoni kwenye akili na moyo wa mtoto huundwa na wazazi wenye kutenda vibaya. Kutendwa vibaya kihisia-moyo, kimwili, na kingono hutokeza kufikiri kubaya ambako huja kukwama akilini na kuwa vigumu kubadilishwa.
Kutendwa Vibaya Kihisia-Moyo
Maneno yanaweza kuumiza zaidi ya ngumi. “Sikumbuki siku ambayo [mama yangu] hakuniambia kwamba afadhali nisingezaliwa,” asema Jason. Karen asema: “Sikuzote nilifanywa nione kwamba nilikuwa mbaya au sikufaa.”
Kwa kawaida watoto wataamini lolote linalosemwa dhidi yao. Mvulana akiitwa mjinga mara nyingi, basi hatimaye anaweza kujihisi kuwa mjinga. Ukimwambia msichana hastahili, huenda ataamini hivyo tu. Watoto wana ufahamu wa kadiri na mara nyingi hawawezi kutambua lililo sawa kutokana na linalosemwa vibaya kwa kutiwa chumvi au uongo.
Kutendwa Vibaya Kimwili
Joe akumbuka baba yake mwenye kutenda vibaya: “Angeanza kunipiga ngumi mpaka anirushe ukutani. Angenitwanga mpaka nipumbazike . . . Jambo lenye kuogopesha zaidi lilikuwa ni kutojua kamwe kilichoamsha hasira zake!”
Jake alikuwa akipigwa kwa ukawaida na baba yake. Alipopigwa wakati mmoja jinsi hiyo, alipokuwa na umri wa miaka sita, mkono wake ulivunjika. “Singelia yeye akiniona au dada zangu au Mama yangu wakiniona,” akumbuka Jake. “Hiyo tu ndiyo staha niliyokuwa nimebaki nayo.”
Kitabu Strong at the Broken Places chasema kwamba kutendwa vibaya kimwili utotoni ni kama “kuwa katika aksidenti ya gari kila siku, kila juma au kila mwezi.” Kutendwa vibaya huko humfundisha mtoto kwamba ulimwengu si salama na kwamba hakuna yeyote wa kutumainiwa. Kwa kuongezea, mara nyingi jeuri hutokeza jeuri. “Watoto wasipolindwa kutokana na wanaowatenda vibaya,” gazeti Time laonya, “basi itabidi siku moja umma ulindwe kutokana na watoto.”
Kutendwa Vibaya Kingono
Kulingana na kadirio moja, msichana 1 kati ya wasichana 3 na mvulana 1 kati ya wavulana 7 wamelazimishwa kufanya ngono wanapofika umri wa miaka 18. Wengi wao huteseka kwa ukimya. “Kama wanajeshi wanaopotea vitani,” chasema kitabu The Child in Crisis, “[watoto] hao hupotea kwa miaka mingi katika msitu wao wa woga na hatia.”
“Jinsi nilivyomchukia baba yangu kwa kunitenda vibaya na jinsi nilivyohisi kuwa na hatia kumchukia,” asema Louise. “Nilihisi aibu hiyo kwa sababu mtoto anapaswa kupenda wazazi wake na sikuwapenda wazazi wangu kamwe.” Hisia zenye kutatanisha kama hizo zaeleweka hasa ikiwa mtunzi wa mtoto anageuka kuwa mtenda mabaya. Beverly Engel auliza hivi katika kitabu The Right to Innocence: “Twaweza kukubalije kwamba mzazi wetu mwenyewe, yule ambaye alipaswa kutupenda na kututunza, hangetujali?”
Kutendwa vibaya kingono kwaweza kubadili maoni ya mtoto ya maisha kabisa. “Kila mtu mzima ambaye alitendwa vibaya akiwa mtoto huwa na hisia sana za kuwa asiyefaa, asiyestahili, na mbaya kabisa,” aandika Dakt. Susan Forward.
Hayapotei
“Si mwili tu wa mtoto ambao unaumizwa au kukataliwa,” mtafiti Linda T. Sanford aandika. “Familia zenye matatizo huumiza akili ya mtoto.” Mtoto anapotendwa vibaya iwe ni kihisia-moyo, kimwili, au kingono, huenda akakua akihisi kutopendwa au kutostahili.
Jason, aliyetajwa mwanzoni, alikosa kujistahi akiwa mtu mzima hivi kwamba alionwa kuwa mtu aliye katika hatari ya kujiua. Akijiweka mwenyewe katika hali za kutisha maisha yake bila sababu, alikadiria maisha yake kama vile mama yake alimfundisha: ‘Laiti hungezaliwa wewe.’
Akifikiria matokeo ya kutendwa vibaya akiwa mtoto, Joe anasema: “Hayapotei kamwe kwa sababu unatoka nyumbani au unaoa. Sikuzote mimi huogopa jambo fulani, na ninajichukia kwa sababu ya kuwa mwoga.” Mkazo wa nyumba za watoto wenye kutendwa vibaya husababisha watoto wengi wakue wakitazamia kutendewa vibaya na kujiwekea himaya kali ambayo huwafunga badala ya kuwalinda.
Kwa Connie, ngono ya maharimu ilimfanya aone vibaya sana, jambo lililoimarika akiwa mtu mzima: “Bado ninafikiria sana wakati ambao watu wanaweza kutazama ndani yangu na kuona jinsi nilivyochafuka.”
Aina zote za kutendwa vibaya zaweza kumfundisha mtoto masomo mabaya sana ambayo yanaweza kuimarika sana kufikia wakati wa utu mzima. Ni kweli, ulilojifunza laweza kubadilishwa kuwa jambo lisilo la kujifunza. Waokokaji wengi zaidi ambao wamepona kutokana na kutendwa vibaya utotoni wameshuhudia jambo hilo. Lakini litakuwa jambo zuri kama nini ikiwa wazazi watatambua kwamba kuanzia wakati wa kuzaliwa kwa mtoto wao, wanaunda mawazo yake na ya ulimwengu. Mambo ya kimwili na kihisia-moyo ya mtoto yanadhibitiwa sana na wazazi wake.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Maneno yanaweza kuumiza kuliko ngumi