Saidieni Watoto Wenu Wakabiliane na Mkazo wa Akili
“Watoto wengi hawapati mtu yeyote nyumbani —kimwili au kihisia-moyo—wanapohitaji kuongea.” —Depression—What Families Should Know.
FAMILIA imeitwa kwa kufaa maabara ya hisia-moyo. Ni kitovu cha utafiti ambamo mtoto hujaribu imani zake, huchunguza matokeo, na kufikia mkataa fulani kuhusu maisha. Wazazi wanaweza kuhakikishaje kwamba watoto wao wanafanya jaribio hilo katika mazingira mazuri badala ya yenye kujawa na mkazo wa akili?
Sikiliza
Kitabu The Child in Crisis husihi wazazi: “Endeleeni kuwasiliana na mtoto wenu.” Kati ya mzazi na mtoto, mawasiliano ni ya muhimu hasa wakati kumekuwa na tukio fulani baya katika familia. Usifikirie kamwe kwamba kwa sababu mtoto ni mnyamavu, yeye hahisi uchungu wa tukio hilo au anapatana na hali hiyo. Huenda ikawa anakandamiza hisia za hangaiko hilo na kukimya, kama alivyofanya msichana mmoja mwenye umri wa miaka saba aliyeongeza kilogramu 15 kwa miezi sita baada ya wazazi wake kutengana.
Neno “kuwasiliana” lamaanisha kwamba wasemaji wawili au zaidi wanahusika. Hivyo, mzazi hapaswi kuongea tu peke yake. Rick na Sue walitafuta shauri wakati mtoto wao wa miaka sita alipoanza kuwa na tabia ya kiburi isiyodhibitiwa nyumbani. Baada ya kukutana na familia nzima, mshauri aliona jambo fulani. “Wazazi walichanganua kila kitu kiakili, wakiwa na maelezo marefu yenye kupita kiasi,” akasema. “Wazazi walijaribu kuongea zaidi katika mazungumzo hayo, na ningeweza kuona watoto wakianza kukosa subira.” Ni jambo linalofaa kumwacha mtoto ajieleze mwenyewe. (Linganisha Ayubu 32:20.) Ikiwa hawezi kuzungumzia matatizo yake yanapotokea, huenda akayaonyesha kupitia mwenendo baadaye.—Linganisha Mithali 18:1.
Mawasiliano ni ya maana wakati nidhamu inahitajika. Mtoto anahisije juu ya marekebisho? Je! anaelewa kwa nini nidhamu hiyo inatolewa? Badala ya kumwambia tu mtoto jinsi anavyopaswa kuhisi, tafuta kilichoko moyoni mwake. Sababu naye ili kwamba aongozwe kwenye uamuzi unaofaa. “Toa shauri analoweza kufikiria kwa uangalifu,” aandika Elaine Fantle Shimberg, “lakini umwache mtoto wako alifikirie.”
Kubali Hisia
Wazazi wengine huzuia mawasiliano na misemo kama vile: “Acha kulia.” “Hupaswi kuhisi hivyo.” “Jambo hilo si baya kama ulifikirivyo.” Ni jambo linalofaa kukubali hisia za mtoto wako. “Naona kama kuna kitu kimekuhuzunisha.” “Unaonekana umekasirika kweli.” “Najua umeudhika sana.” Hayo yatafanya mawasiliano yaendelee.
Kitabu How to Talk so Kids Will Listen & Listen so Kids Will Talk chataja jambo moja la kweli kuhusiana na hili: “Kadiri unavyozidi kukandamiza hisia za mtoto za kukosa furaha, ndivyo anavyokosa kuziondolea mbali hisia mabaya. Unapokubali hisia mbaya kwa ustarehe, watoto watazisahau. Nafikiri ungesema kwamba ikiwa unataka kuwa na familia yenye furaha, ingekuwa vizuri kujitayarisha kuruhusu maelezo mengi ya ukosefu wa furaha.”—Linganisha Mhubiri 7:3.
Hurumia
“Kwa kuwa watu wazima huona ulimwengu wa watoto kutokana na maoni yao,” aandika Mary Susan Miller, “ni vigumu kwao kuwazia maisha mengine yoyote ila yao wenyewe kuwa yamejawa na mkazo wa akili.”
Ndiyo, wazazi husahau haraka maumivu waliyopata wenyewe wakiwa wanakua. Kwa hiyo, huwa wanapunguza mikazo ya akili ambayo watoto wao wanayo. Wazazi wanapaswa kukumbuka jinsi ilivyokuwa vigumu kukabiliana na kifo cha mnyama kipenzi, kifo cha rafiki na kuhamia katika ujirani mpya. Wanapaswa kukumbuka woga wao wa utotoni, hata ule usiokuwa wa kiakili. Kukumbuka ni ufunguo wa kuonyesha huruma.
Weka Mfano Mzuri
Jinsi mtoto wako anavyoshughulika na mkazo wa akili hutegemea kwa kadiri kubwa jinsi wewe ukiwa mzazi unavyoshughulika nao. Je! unajaribu kupunguza mkazo wa akili kwa kugeukia jeuri? Basi usishangae mtoto wako anaposhughulika na hangaiko lake kwa njia hiyohiyo. Je! unanyamaza ukisumbuliwa zaidi? Basi unawezaje kudai kwamba mtoto wako aseme wazi na kuwa mwenye kutumainika? Je! hisia zenye kujaa mikazo zimejificha katika watu wa nyumba yako hivi kwamba zinakataliwa badala ya kukubaliwa na kusuluhishwa? Basi usishangazwe na matokeo mabaya ambayo huenda zikatoa kwa mtoto wako, kwa sababu jaribio lolote la kukandamiza hangaiko kwa kawaida litaongeza tu ubaya wa tokeo layo.
Kulea watoto katika ulimwengu uliojaa mkazo wa akili huleta magumu ya pekee kwa wazazi. Funzo la Biblia limesaidia wengi wakabiliane na magumu haya. Hilo ni jambo ambalo tungetazamia, kwa sababu Mwandikaji wa Biblia pia ni Mwanzilishi wa maisha ya familia. “Hekima ya Mungu inathibitishwa kuwa na haki kwa matokeo yayo,” akasema Yesu Kristo. (Mathayo 11:19, The New English Bible) Kwa kutumia kanuni za Biblia, wazazi wataona kwamba Maandiko ‘yafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki.’—2 Timotheo 3:16.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Kuwasiliana kunakojenga huondoa mkazo wa akili
[Sanduku katika ukurasa wa 11]
Mvulana anamwaga maziwa, ndugu yake anamdhihaki, lakini baba anamfariji kwa kuelewa