Mwongozo Ulio Mkamilifu wa Kiadili
NAHODHA wa meli anahitaji ramani na vifaa vinavyotegemeka ili aendelee katika mwendo bila kukengeuka. Wanadamu vilevile wanahitaji mwongozo unaotegemeka ili wafanye maamuzi ya kiadili wanayokabili kila siku. Mwongozo wa kiadili ambao unabadilika-badilika au kugeuka-geuka hautafaa, wala mwongozo ambao unatumika tu kwa tamaduni au jamii fulani pekee hautafaa. Mwongozo ulio mkamilifu wa kiadili ni lazima uvuke mipaka ya kabila na utamaduni.
Inashangaza kwamba Biblia—kile kitabu ambacho kimekataliwa na mamilioni ya watu, kitabu ambacho kimeitwa na watu fulani kuwa hadithi inayopendeza iliyotungwa tu, kitabu ambacho kimechambuliwa kuliko kitabu kingine chochote katika historia—ndicho mwongozo ulio mkamilifu zaidi wa kiadili. Biblia inajieleza yenyewe kuwa mwongozo wa kiadili uliotolewa na Muumba kwa binadamu, ile “taa” inayoweza kutuangazia ‘njia zetu za haki.’—Zaburi 23:3; 119:105.
Je! kuna uthibitisho wowote wa kutegemeza dai kubwa kama hilo? Je! kuna uthibitisho kwamba kuishi kulingana na viwango vya Biblia ni bora kuliko kuishi kulingana na adili zilizofanyizwa na binadamu?
Biblia na Maadili ya Ngono
Ebu fikiria jambo hili la maadili ya ngono. Biblia inaamuru kuepuka mahusiano ya kingono nje ya ndoa, ikisema: “Ukimbie ukosefu wa adili kingono.” (1 Wakorintho 6:18, New International Version; Waefeso 5:5) Inashauri waume na wake hivi: “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.” (Waebrania 13:4) Biblia huonyesha zaidi kwamba mtu yeyote anayepuuza agizo hilo anajiharibu na anavunja haki za mwingine.—Mithali 6:28-35; 1 Wathesalonike 4:3-6.
Yale matatizo makubwa ya vijana kushika mimba, tisho la UKIMWI, ugonjwa wa vilengelenge, kaswende, na magonjwa mengine yanayoambukiza kingono, na kule kuongezeka kwa talaka, zote ni uthibitisho kwamba shauri hilo bado linafaa kwa maisha katika miaka ya 1990. Mtu anayeshikamana na maadili ya Biblia huepuka maumivu mengi na uchungu mwingi. Na jambo la maana zaidi, anadumisha dhamiri safi. (1 Petro 3:16) “Ninajistahi na nina uradhi wa kufanya yaliyo sawa mbele ya Mungu,” asema Jonathan mwenye umri wa miaka 24. Yeye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. “Kukiwa na vijana wengi wanaokufa kwa sababu ya UKIMWI, kuendelea kuwa safi kiadili kunaweza kuokoa maisha yangu kihalisi.”
Waume na wake wanaomwogopa Mungu wameona kwamba kufuata maadili ya Biblia kumekuwa na matokeo mema katika ndoa yao. Mke mmoja mwenye umri wa miaka 23 asema hivi: “Mume wangu nami tulikuwa mabikira tulipooana. Ninahisi tulikuwa na kitu cha pekee cha kushiriki pamoja, kitu ambacho ni vijana wachache wanaweza kushiriki na wenzi wao siku hizi. Ninajua kwamba hilo limeimarisha kile kifungo cha upendo kati yetu.”
Biblia na Biashara
Biblia pia ina kanuni zayo za adili ya kibiashara. Ingawa inakubali kwamba watu wasiofuata haki wanaweza kuonekana wakifanikiwa, bado inatuhimiza tuwe wenye kufuatia haki. (Zaburi 73:1-28) “Vipimo mbalimbali [kipimo sahihi kwa ununuzi na kisicho sahihi, kisicho cha haki kwa uuzaji], na pishi mbalimbali, vyote viwili ni chukizo kwa BWANA [Yehova, New World Translation].” (Mithali 20:10) Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova huepuka mbinu za kibiashara zinazotiliwa shaka.
Ni kweli kwamba Mkristo anaweza kupata mambo yasiyofaa akifanya hivyo. Inaweza kuwa vigumu kwake kushindana na wafanya biashara wasiofuatia haki sana. Wengine wanaweza kufikiri kwamba uhaki wake ni wa kiajabu, labda hata wa kipumbavu, lakini yeye adumisha dhamiri njema—kitu ambacho kina thamani kuliko fedha. Ana amani ya akili na anaweza kufurahia usingizi mzuri usiku. Hataabishwi na woga wa kukamatwa na kuadhibiwa kwa sababu ya kutofuata haki.—Linganisha Mithali 3:21-26.
Na zaidi, Mashahidi wengi wameona kwamba mtu anaweza kushikamana na maadili ya Biblia na kufanikiwa kifedha. Mara nyingi mtu afuataye haki hutumainiwa na wafanya kazi, wateja, waleta bidhaa za kuuzwa, na hata watu wanaowadai deni. Jambo hilo laweza kumsaidia.
Je! Ukiokota Kitu Kinakuwa Chako?
Kama tulivyoona mapema, lile wazo la ukiokota kitu kinakuwa chako limefanya watu wenye mwelekeo wa kuwa wafuataji haki wawe wezi. Hata hivyo, Biblia iliwaambia watu wa Mungu wa nyakati za kale hivi: “Umwonapo ng’ombe wa nduguyo au kondoo wake akipotea, usijifiche kama usiyemwona; sharti utamrudisha kwa nduguyo. Na kwamba yule nduguyo hayupo karibu nawe, na ukiwa humjui, umchukue kwenu nyumbani kwako, uwe naye hata aje nduguyo kumtafuta, nawe mrudishie. Tena fanya vivyo kwa punda wake; tena fanya vivyo kwa mavazi yake; tena fanya vivyo kwa kila kitu kilichopotea cha nduguyo, kilichompotea ukakiona wewe.”—Kumbukumbu la Torati 22:1-3.
Mashahidi wa Yehova waendelea kufuata kanuni hiyo leo. Shahidi mmoja katika Brooklyn, New York, aliokota mfuko uliokuwa na dola za U.S. 25,000 barabarani. Ulikuwa umeanguka kutoka kwenye gari la ulinzi wakati wa aksidenti ndogo. Ingawaje fedha hizo zilikuwa noti zenye thamani ndogo-ndogo ambazo zilikuwa zimetumiwa—na hivyo haingewezekana kufuatwa—alipeleka fedha hizo kwa polisi. Wafanyakazi wenzake walimkemea kwa sababu ya uamuzi wake. Na kwa kushangaza, polisi nao walimdhihaki kwa sababu ya ufuatiaji haki wake. Lakini Mkristo huyo aeleza hivi: “Najaribu kushikamana na mafundisho ya Biblia katika maisha yangu ya kila siku.” Biblia inasema hivi katika Waebrania 13:18: “Tuombeeni; maana tunaamini kwamba tuna dhamiri njema, tukitaka kuwa na mwenendo mwema katika mambo yote.”
Uvutio wa Ulimwenguni Pote!
Biblia huandaa pia miongozo inayofaa katika masuala mengine ya kiadili. Inatia moyo kutumia fadhili, wema, haki, kweli, heshima, staha, hisia ya kuwa na daraka, na kuhangaikia wanadamu wengine. Shauri layo la kiadili hutajwa kifupi katika ile Kanuni ya Kidhahabu: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.
Ikipatana na Chanzo chayo, miongozo ya kiadili ya Biblia inatumiwa kwa mafanikio katika nchi au utamaduni wowote ule. Katika kitabu Christianity’s Contributions to Civilization, Charles D. Eldridge asema hivi: “Mara nyingi vitabu vinavyoandikwa katika nchi moja havipendwi katika nchi nyinginezo; hivyo ni kama miti ambayo haiwezi kustahimili kupandikizwa . . . Lakini sivyo na Biblia: imepandikizwa katika kila udongo chini ya jua bila kuathiriwa vibaya kwa kukosa nguvu na uvutio.”
Basi, kwa njia ya pekee, Biblia ina uvutio wa ulimwenguni pote, ikipita lugha, utamaduni, na rangi. Mwandikaji mmoja wa Biblia alisema hivi: “Kila andiko lina pumzi ya Mungu na linafaa katika kufundisha imani na katika kurekebisha kosa, kwa kuongoza upya mwelekeo wa maisha ya mtu na kumzoeza katika maisha mema.” (2 Timotheo 3:16, Phillips) Ni kweli kwamba nyakati fulani inakuwa vigumu kuelewa Biblia. Katika nyakati za kale msomaji mmoja wa Biblia mwenye bidii aliulizwa kama alielewa aliyokuwa akisoma. Yeye alijibu hivi: “Nitawezaje kuelewa, mtu asiponiongoza?”—Matendo 8:29-35.
Mtu huyo alipata msaada wa kibinafsi katika kuelewa Biblia. Leo, msaada huo wa kibinafsi unapatikana kupitia kazi ya kufundisha Biblia ya Mashahidi wa Yehova. Tayari wamesaidia mamilioni ya watu katika nchi zaidi ya 200 wapate kuwa na ujuzi wa Neno la Mungu. Na wanakualika wewe pia upate kuelewa vema zaidi Kitabu hicho Kitakatifu kwa kuzuru Jumba la Ufalme lililo karibu nawe.
Kwa kupendeza, imesemwa kwamba mwenendo wa kiadili “waweza kusitawishwa kupitia mfano mwema, . . . au ‘kuwa tu na’ watu wenye adili.” Hilo pia ni sababu nyingine kubwa ya kukufanya ufahamiane na wale wanaohudhuria Jumba la Ufalme la kwenu. Si kwamba kiasili Mashahidi wa Yehova wanashinda watu wengine, lakini mafanikio yao katika maadili ni uthibitisho wa nguvu ya Neno la Mungu.—2 Wakorintho 4:7.
Maadili ya ulimwengu yataendelea kupotea. Biblia inatabiri hivi: “Watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu.” (2 Timotheo 3:13) Hata hivyo, usichukuliwe na wimbi hilo lenye kuleta uharibifu. Mungu ameandaa mwongozo unaotegemeka, kiongozi kisichoweza kukosea. Je! utakifuata?
[Blabu katika ukurasa wa 8]
Biblia inajieleza yenyewe kuwa mwongozo wa kiadili uliotolewa na Muumba kwa binadamu, ile “taa” inayoweza kutuangazia njia yetu
[Blabu katika ukurasa wa 9]
Miongozo ya kiadili ya Biblia inatumiwa kwa mafanikio katika nchi au utamaduni wowote ule
[Blabu katika ukurasa wa 10]
“Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.”—Mathayo 7:12.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Waume na wake wanaomwogopa Mungu wameona kwamba kufuata maadili ya Biblia kumekuwa na matokeo mema katika ndoa yao.