Vijana Huuliza..
Mbona Nakua Upesi Hivi?
“Nilipokuwa katika darasa la sita, nilikuwa mrefu kuliko kila mtu. Niliona haya. Nilikuwa na rafiki mwenye umbo dogo sana na nilimwonea wivu.”—Annie.
“Kwa kuwa naonekana kana kwamba nina miaka kumi na sita au kumi na saba, watu wengi, kutia na wazazi wangu, hunitazamia nitende kikomavu zaidi.”—Tanya, mwenye miaka 12.
KUBALEHE—labda wengi wetu ambao tumepitia kipindi hicho tungependelea kusahau yote tuliyopatwa nayo. Ni kizuri ajabu na pia chenye kuhofisha. Wakati wa kubalehe, mwili wako hupata mabadiliko ya haraka, yenye kutazamisha, na, nyakati nyingine, yenye kuaibisha. Hisia mpya, mielekeo, na tamaa zakushambulia. Vijana wengi hufarijiwa na uhakika wa kwamba marika wao wapatwa na mambo ayo hayo. Hata hivyo, kwa vijana fulani, hali ya kubalehe huonekana ikija mapema mno. Wanajipata wenyewe wakikua na kuwa wakubwa zaidi, warefu zaidi, waliokua zaidi, wenye kuonekana kuwa watu wazima kuliko rafiki zao na wanadarasa wenzao.
Ikiwa hilo limekupata, huenda ukafarijika kujua kwamba hakuna kasoro yoyote katika kubalehe mapema. Saa ya kila mtu ya kupata mabadiliko ya mwili huenda kwa mwendo wayo yenyewe, na inaonekana kwamba yako inaenda kwa mwendo wa haraka kidogo kuliko ile ya marika wako. Kwani, mabadiliko ya kubalehe ya mvulana yaweza kuanza mapema kama umri wa miaka kumi, na ya msichana, mapema kama miaka minane. Labda hivi karibuni sana rafiki zako wataanza kupata mabadiliko ayo hayo. Kwa wakati huu, huenda una matatizo fulani ya kukabili.
Raha na Maumivu ya Kuwa Mrefu
Msichana mmoja tineja aliambia Amkeni! hivi: “Ninapendelea kuwa kijana mrefu zaidi darasani. Watu hukuheshimu.” Uchunguzi waonyesha kwamba wavulana wenye kupevuka mapema hasa hufurahia manufaa kadhaa hususa zaidi ya marika wao ambao hawajapevuka sana. Kitabu Adolescent Development cha Barbara na Philip Newman chasema: “Wavulana wenye kupevuka mapema huwa warefu na wenye nguvu zaidi ya marika wao. . . . Inaelekea zaidi kwamba wavulana warefu, wenye nguvu watapewa madaraka, wakionwa kuwa viongozi wa marika, na kutendewa kana kwamba walikuwa wamepevuka zaidi kiakili na kimwili.”
Hata hivyo, pia kuna hasara katika kuwa mrefu sana upesi sana. Kwanza, huenda ukafanyiwa mzaha mwingi usiopendeza ambao hauna mwisho kutoka kwa wanadarasa wenzako. Msichana mmoja mchanga aliliambia Amkeni! hivi: “Nilikuwa msichana mrefu zaidi darasani. Waliniita ‘Miguu Mirefu.’” Kijana aitwaye Dwayne akumbuka hivi: “Vijana walikuwa wakiniita majina kama vile ‘Korongo.’ Nyakati nyingine walikuwa wakiuliza, ‘Hali ya hewa ikoje huko juu?’”a
Hasa inakuwa vigumu miguu yako mirefu inaposhindwa kufanya kazi pamoja kwa upatano. (Linganisha Waefeso 4:16.) “Nilikuwa mrefu, mwembamba, na asiyevutia,” akumbuka Christine juu ya miaka yake ya utineja. “Nilikuwa bure katika michezo,” aongeza Dwayne. “Ilionekana kana kwamba ubongo wangu ulipeleka amri, nayo miguu yangu ingeipokea juma moja baadaye! Nilikosa usawaziko kama twiga aliye juu ya viatu vyenye magurudumu.” Uwe na uhakika kwamba kipindi hiki kisichopendeza ni cha kawaida. Kitapita baada ya muda. Huenda pia ukapata kwamba kiasi fulani cha ‘mazoezi ya mwili chafaa.’ (1 Timotheo 4:8) Kadiri utumiavyo mwili wako zaidi, ndivyo utakavyoweza kuuendesha vizuri.
Vipi juu ya kuitwa majina na kutusiwa? Huenda ukashawishwa kulipiza kwa maneno yako mwenyewe yenye kuchoma, lakini Biblia yasema hivi: “Usimjibu mpumbavu sawasawa na upumbavu wake; usije ukafanana naye.” (Mithali 26:4) Isitoshe, mwishowe, ‘kulipa ovu kwa ovu’ hufanya hali mbaya iwe mbaya zaidi. (Warumi 12:17) Biblia husema kwamba kuna “wakati wa kucheka.” (Mhubiri 3:4) Hali ya ucheshi yaweza kukusaidia ukabili pindi zenye kuaibisha.b
‘Wao Hufikiri Mimi ni Mkubwa Zaidi’
Nyakati nyingine, tatizo si marika, bali ni watu wazima wanaofikiri kwamba wewe ni mkubwa kuliko vile ulivyo hasa. Dwayne akumbuka: “Nilikuwa nikiteuliwa miongoni mwa kikundi kuwa mwenye mamlaka, kiongozi. Wakati mmoja nilikuwa karibu na kikundi cha vijana, na wakaanza kurusha vitu wakiwa juu ya daraja. Polisi walikuja na wakaanza kunilaumu kwa sababu nilikuwa mrefu zaidi kati yao. Lakini hata sikujua ni nini kilichokuwa kikiendelea.”
Hata hivyo, nyakati nyingine huenda ukafurahi kutendewa kama mtu mzima. Tatizo ni kwamba, ukuzi wa kimwili waweza kupita ukuzi wa kiakili na wa kihisiamoyo. Hata uwe waonekanaje, bado huenda ukafikiri na kusababu kama mtu wa umri wako, na si kama mtu mzima. (Linganisha 1 Wakorintho 13:11.) Kwa hiyo watu wanapokutaka utende kama mtu mzima, huenda ukawa na wakati mgumu kuwatosheleza.
Huenda mara kwa mara ukahitaji kupatia rafiki na washiriki wa familia yako vikumbusha vya upole kwamba wewe si mkubwa kama vile unavyoonekana. “Pasipo mashauri makusudi hubatilika,” yasema Mithali 15:22. Kwa hiyo ukihisi kwamba wazazi wako wanakutaka ufanye mengi zaidi ya kawaida, waambie hivyo kwa heshima. Gazeti moja la matineja lilidokeza kwamba huenda ukasema hivi: “Ninajua kwamba kwa sababu ninaonekana kuwa nimepevuka sana, ni rahisi kunitazamia nitende kama mtu mzima. Lakini ndani, ningali mwenye umri wangu halisi, na nyakati nyingine ni vigumu kwangu kufanya yote mnayonitazamia nifanye na kuwa.”
Usikosee kwa kuendeleza dhana ya kuwa mtu mzima kwa kujifanya mkomavu zaidi, au mwenye sura ya mtu mzima, au kwa kuvalia na kujipamba katika njia isiyofaa umri wako. Vijana fulani wenye kupevuka mapema hata huwatoroka marafiki zao wa utotoni wenye kuonekana wachanga na kujaribu kufaa katika kikundi chenye umri mkubwa zaidi! Lakini mtu anayejaribu kuficha vile alivyo hasa kwa habari hii aweza kuaibishwa. (Linganisha Zaburi 26:4.) Baada ya muda wengine wataona unafiki wako. Kwa hiyo Biblia husema kwa hekima, kwamba “hekima hukaa na wanyenyekevu [wenye kiasi, NW].” (Mithali 11:2; Mika 6:8) Mtu mwenye kiasi ajua mipaka yake.
Udhia wa Kingono
Kutenda kwa njia ya kiasi kwaweza pia kukulinda na tatizo ambalo mara nyingi hukabili wa-sichana wenye kupevuka mapema hasa: udhia wa kingono. Katika muda mfupi ajabu, mwili wa msichana mdogo waweza kubadilika kuwa mwanamke mwenye kuvutia. (Linganisha Wimbo Ulio Bora 8:8, 10.) Hata hivyo, kwa wasichana fulani wachanga, kuwa na matiti na nyonga kama za mwanamke kwaweza kuwa—yaani—kwenye kuaibisha.
Mwandikaji Ruth Bell aonelea hivi: “Wasichana wanaokua huwa hasa watazamwa sana na wanaume.” Msichana mwenye miaka 12 aitwaye Denise aeleza hivi: “Tangu nilipopevuka zaidi kimwili, watu hunikodolea macho sana ninapotembea.” (Changing Bodies, Changing Lives) Wanadarasa wenzako wa jinsia zote mbili waweza hata kujaribu kukugusa isivyofaa. Haishangazi kwamba kitabu Adolescent Development chasema hivi: “Wanawake wanaopevuka mapema waweza kulegeza mabega, kuvaa sweta kubwa-kubwa, au kuona haya na kujitenga ili kuepuka marika wasitambue mabadiliko ya mwili wao.”
Ingawa hushurutishwi ujifiche mwenyewe kwa nguo nyingi, ni busara kuepuka nguo na mitindo ya mavazi inayoamsha nyege au kuvuta uangalifu kwako isivyofaa. Hilo lapatana na shauri la Biblia kuvaa “kwa kiasi na utimamu wa akili.”—1 Timotheo 2:9, NW.
Labda kuna mambo mengine yenye kufanya kazi ambayo unaweza kufanya. Huko nyuma katika nyakati za Biblia, Ruthu alikabili uwezekano wa udhia wa kingono alipoenda kufanya kazi katika shamba la Boazi. Kwa fadhili Boazi ‘aliamuru vijana wasimguse.’ Hata hivyo, yeye alimwonya hivi: “Usiende kuokota masazo katika shamba lingine, . . . lakini ukae papa hapa karibu na wasichana wangu.” (Ruthu 2:8, 9) Kwa njia iyo hiyo, wasichana fulani wachanga wameweza kukaa karibu na wasichana wengine Wakristo wanaohudhuria shule ileile. Wao huepuka kutembea bila mtu mwingine katika maeneo yanayojulikana kuwa hatari.
Hata iweje, hakuna mtu aliye na haki ya kukusumbua—ama kimwili ama kwa maneno. Ikiwa unapatwa na matatizo fulani kuhusiana na hilo, zungumzia hayo na wazazi wako au mtu mzima unayemtumaini. Huenda wakawa na madokezo fulani au wakajitolea kuingilia katika njia fulani.
Hata chini ya hali bora kabisa, kubalehe ni wakati mgumu wa maisha. Kuwa mkubwa zaidi—au mdogo zaidi—kuliko marika wako kwaweza kukufanya kuwe kugumu hata zaidi. Hata ufanye nini, huwezi kufanya chochote kuhusu ukuzi wako wa kimwili. Lakini unaweza kufanyia bidii ukuzi wako wa kiroho. Na ukifanya hivyo, kama vile kijana Samweli wa nyakati za Biblia, utakua uwe ‘mkubwa zaidi na mwenye kibali kwa Yehova, na kwa watu pia.’—1 Samweli 2:26.
[Maelezo ya Chini]
a Majina fulani yamebadilishwa.
b Ili upate madokezo zaidi juu ya kushughulika na matusi, ona Sura ya 19 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 25]
Mara nyingi vijana warefu hufanyiwa mizaha inayokeray