Yule Atakayelinda Wanyama Wetu wa Pori
KUANZIA mwanzo wa historia ya kibinadamu, mwanadamu amefurahia kujifunza juu ya wanyama wa pori. Ingawa hivyo, inasikitisha kwamba baada ya Mungu kumpa mwanadamu ruhusa ya kuongeza nyama katika ulaji wake, kule kuthamini wanyama wa pori kulipotea kukawa jambo la kuwachinja ovyoovyo na kuwinda kikatili sehemu zao za mwili.—Mwanzo 2:19, 20; 9:2; 10:9; 25:27.
Lakini watu fulani waliendelea kustaajabia wanyama wa pori wa dunia. Miaka yapata 3,000 iliyopita, maneno ya Zaburi 104 yaliandikwa na mpendaji wa wanyama wa pori. Yeye ataja kwa majina wanyama kadhaa wa pori, kama vile pundamilia, simba, mbuzi-milima, wibari, na korongo. Kutokana na uchunguzi wake wa ndege, nyimbo za ndege, na wanyama wa mwitu, mtunga-zaburi alisukumwa aangue sifa hii: “[Yehova amevifanya] vyote kwa hekima.”—Zaburi 104:10-12, 17-21, 24, New World Translation.
Kwa kweli, Yehova Mungu aweza kwa haki kufurahia kazi zake za ajabu za uumbaji. (Mwanzo 1:31) Kwa hiyo, twaweza kuwa na hakika kwamba hataruhusu wanyama wa pori wa dunia wanaobaki waangamizwe kabisa. Kwa kupatana na jambo hilo, Mungu alitia roho yake kwa mtunga-zaburi ili aandike habari zenye kufurahisha watu wote wapendao wanyama wa pori. Twaelezwa kwamba ‘nchi . . . haitatikisika milele.’ (Zaburi 104:5) Mahangaiko kama hayo kwa ajili ya hali njema ya milele ya dunia-sayari kwa kweli yatia ndani viumbe viishivyo ndani yayo. (Isaya 45:18) Yesu Kristo alithibitisha hangaiko la Mungu kwa ajili ya wanyama wa pori aliposema hivi: “Je! mashomoro watano hawauzwi kwa senti mbili? Wala hasahauliwi hata mmojawapo mbele za Mungu.” (Luka 12:6) Hangaiko la Mungu kwa ajili ya viumbe vyake lakaziwa pia katika Zaburi 104, mstari wa 14, isemayo hivi: “Huyameesha majani kwa makundi, na maboga kwa matumizi ya mwanadamu; ili atoe chakula katika nchi.”
Kwa kupatana na mambo hayo ya hakika, Yehova Mungu hatawavumilia milele wanadamu wanaomkataa na wanaotisha wakati ujao wa dunia na wanyama wayo wa pori. Ikisisitiza jambo hilo, Zaburi 104 yamalizia kwa maneno haya yenye kufariji: ‘Wenye dhambi wataangamizwa katika nchi, watendao ubaya wasiwepo tena.’—Zaburi 104:35.
Inafariji kama nini kujua kwamba Mungu ameonyesha kauli yake ya “kuwaharibu hao waiharibuo nchi.” (Ufunuo 11:18) Katika kipindi hicho unabii mwingine mwingi unaotimizwa sasa kwa njia ya kimfano utapata utimizo kwa njia ya kihalisi. Kwa kielelezo, kupitia nabii wake Hosea, Yehova Mungu atangaza hivi: “Nami siku hiyo nitafanya agano na wanyama wa mashamba kwa ajili yao, tena na ndege wa angani, tena na wadudu wa nchi; nami nitavivunja upinde na upanga na silaha vitoke katika nchi, nami nitawalalisha salama salimini.”—Hosea 2:18; Isaya 11:6-9.
Ebu ujione mwenyewe ukiwa katika Paradiso hiyo ya kidunia inayokuja. Utakuwa wakati wenye kufurahisha kama nini! ‘Lakini,’ huenda ukajiuliza, ‘ni nini kinachohitajiwa ili urithi baraka kama hizo?’ Kwanza kabisa, ni lazima ujifunze Neno la Mungu. Kisha, kwa wale wanaotii mwelekezo wa Biblia, Yehova Mungu atoa ahadi hii nzuri ajabu: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:29.