Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g93 11/22 kur. 20-23
  • Kutoka Kuwa Ofisa wa Polisi Hadi Kuwa Mhudumu Mkristo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutoka Kuwa Ofisa wa Polisi Hadi Kuwa Mhudumu Mkristo
  • Amkeni!—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Malezi ya Mapema
  • Kujifunza Kweli za Biblia
  • Maendeleo Katika Kweli ya Biblia
  • Jinsi Nilivyopoteza Kazi Yangu ya Polisi
  • Kutumikia Chini ya Marufuku
  • Kutovumiliana kwa Kidini
  • Elimu Ambayo Imeendelea Katika Maisha Yangu Yote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Mambo Yaliyotarajiwa na Kuhofiwa Kuhusu Polisi
    Amkeni!—2002
  • Nilipata Hazina Yenye Thamani Bora Zaidi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Nilipata Utajiri wa Kweli Katika Australia
    Amkeni!—1994
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1993
g93 11/22 kur. 20-23

Kutoka Kuwa Ofisa wa Polisi Hadi Kuwa Mhudumu Mkristo

KATIKA Februari 1942, nilikuwa gerezani katika Adelaide, Australia Kusini, kwa sababu ya kukataa kuchukua silaha wakati wa Vita ya Ulimwengu 2. Kinyozi, aliyekuwa karibu kuninyoa, alinitambua kuanzia wakati nilipotokea katika vyumba vya mahakama kuwa ofisa wa kikosi cha polisi cha Australia Kusini. “Unafanya nini hapa?” yeye akauliza kwa mshangao. Yeye alijua kwamba hapo mwanzoni nilikuwa nimetumikia mara kwa mara nikiwa shahidi dhidi ya wahalifu. Kwa hiyo nilimweleza itikadi zangu za Kikristo.

Yule hakimu aliyekuwa ameisikiliza kesi yangu siku kadhaa mapema, alinijua vema pia. Yeye pia alisikiliza kwa uangalifu nilipoeleza kwa nini dhamiri yangu ya Kikristo haingeniruhusu kuchukua silaha. Baada ya kunishukuru kwa yale aliyoyaona kuwa maelezo dhahiri, alinipa kifungo cha mwezi mmoja gerezani.

Sasa, wafungwa wenzangu walikuwa watu ambao muda mfupi uliopita nilikuwa nimewapiga picha na kuchukua alama za vidole vyao. Hata hivyo, niliweza kutoa ushahidi juu ya itikadi zangu kwa askari-walinzi na wafungwa wengi waliouliza juu ya kutokuwamo kwa Kikristo.

Mwaka uliofuata nililetwa mbele ya mahakama tena, na wakati huu nilipewa kifungo cha miezi sita ya kazi ngumu. Nilipelekwa Yatala, ambamo wafungwa walikuwa wakitumikia vifungo vya maisha kwa ajili ya kuua kimakusudi. Lakini kwa mara nyingine tena nilikuwa na fursa nyingi ya kuzungumza na wengine juu ya tumaini la Ufalme wa Mungu na amani ya kudumu ambayo utaleta kwenye ulimwengu huu uliojaa vita.

Kabla ya kuja mbele ya mahakama kwenye kila pindi, nilipelekwa kwenye makao ya wanajeshi. Mara ya kwanza nilipokuwa huko, nilidhihakiwa na kudhulumiwa na Luteni Laphorn kwa sababu ya kukataa kwangu kula kiapo cha uaminifu jeshini. Lakini nilipokuja mbele yake kwa mara ya tatu, yeye alisema hivi: “Wajua, nilifikiri kwamba wewe ni mwoga. Lakini nimetazama namna unavyostahimili adhabu yako. Uliacha kazi-maisha nzuri na umethibitisha imani yako kwa kuja kupata adhabu zaidi.”

Ilipokuwa kwamba nihukumiwe kifungo cha gereza kwa mara ya tatu, maombi yalitolewa kwa niaba yangu ili nihukumiwe nikiwa mtu anayekataa kwa ajili ya dhamiri. Hakimu alilazimika kukubali ombi langu, kwa kuwa nilikuwa nimestaafu kutoka kikosi cha polisi katika 1940 kwa ajili ya suala la dhamiri. Hata hivyo, akionyesha ubaguzi wake, yeye alisema: “Nataka iwe katika rekodi kwamba naamini ni hatari mtu mshupavu kama wewe awe bila vizuizi katika jumuiya.”

Malezi ya Mapema

Nilizaliwa katika 1908 katika Gawler, si mbali kutoka Adelaide, Australia Kusini. Nilipokuwa na umri wa karibu miaka sita, Sarah Marchant, rafiki mpendwa wa mama yangu, alinifundisha kwamba helo ni kaburi la kawaida la mwanada-mu na si mahali pa moto wa mateso. Yeye alikuwa mmoja wa Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo.

Baadaye, nilipokuwa nikikua, nilimuuliza mhubiri wetu Mbaptisti jinsi Yesu Kristo hutofautiana na Mungu, na hangeweza kunipa jibu lenye kuridhisha. Kwa hiyo nilipoteza upendezi katika makanisa, ingawa nilifurahia kusikiliza Sarah Marchant tulipokutana mara kwa mara.

Katika 1924, nilianza kufanya kazi katika Adelaide nikiwa karani wa kamishna wa Polisi wa Australia Kusini, Brigedia Jenerali Bwana Raymond Leane. Halafu, katika 1927, Bw. Leane alitoa maombi katika bunge ili niteuliwe kuwa mstadi mdogo wa kuchukua alama za vidole na mpiga-picha za uhalifu kwa ajili ya kikosi cha polisi cha jimbo.

Kujifunza Kweli za Biblia

Miaka mitatu baada ya kuoa katika 1928, nilipokuwa kwenye likizo na wakwe wangu katika Gawler, nilipata kitabu kiitwacho Creation, kilichotangazwa katika 1927 na Watch Tower Bible and Tract Society. Kilikuwa kimeachwa na Sarah Marchant kwa wakwe wangu. Kitabu hicho kilieleza kwamba mwanadamu ni nafsi na hana nafsi nyingine iliyo kando, isiyoonekana. Hilo lilikuwa jambo la akili. Lakini nilitaka kujionea mwenyewe katika Biblia. Kwa hiyo nilitafuta King James Version ya familia na kusoma Mwanzo 2:7: “BWANA Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.”

Hilo lilinisisimua sana, kwa hiyo niliendelea kusoma. Singeweza kuweka chini kitabu hicho Creation. ‘Hii kwa hakika ndiyo kweli,’ nikajisemeza. Sasa nilitaka vitabu zaidi vya Watch Tower Society ili kusoma. Kile cha pekee ambacho familia hiyo ilikuwa nacho kilikuwa na kichwa Life. Kwa hiyo nilikisoma chote pia.

Siku chache baadaye, tulirudi Adelaide na tukahamia nyumba nyingine. Siku iyo hiyo tulitembelewa kwa ghafula na Sarah Marchant. Mama-mkwe wangu alikuwa amemwambia juu ya kupendezwa kwangu, naye akazuru ili kuona jinsi tulivyokuwa tukizoelea nyumba yetu mpya na kuona ni msaada gani wa kiroho niliohitaji. Asubuhi iliyofuata jirani yetu mpya alipaza sauti kupitia ua akisema: “Naamini wapendezwa na maandishi ya Judge Rutherford [wakati huo akiwa msimamizi wa Watch Tower Society].”

“Wajuaje hilo?” nikauliza.

“Oh, mtu fulani aliniambia,” yeye akajibu.

Bila shaka, Sarah alikuwa amemwambia. Mtu huyo, James Irvine, ndiye aliyekuwa Shahidi pekee wakati huo akiishi katika viunga vya kaskazini vya Adelaide. Yeye alikuwa painia, au mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, naye alianza funzo la Biblia nyumbani la kawaida pamoja nami.

Maendeleo Katika Kweli ya Biblia

Niliporudi kazini katika idara ya polisi, nilisisimka kwa mambo mazuri niliyokuwa nimejifunza. Kwa hiyo wakati wowote nilipopata fursa, nilianza kuwaambia wafanyakazi wenzangu juu ya imani yangu mpya. Hata hivyo, nilikatishwa tamaa wakati idili yangu ilipodhihakiwa.

Bila kutazamiwa kabisa mke wangu mwenyewe alianza kunipinga kwa kuwa na upendezi huo katika Biblia. Lakini kwa msaada wa Yehova, niliweza kushinda upinzani wake. Katika 1935, niliweka maisha yangu wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Katika siku hizo kulikuwa na kutaniko moja tu katika Adelaide, na ni karibu 60 tu waliohudhuria funzo la Biblia la kila juma wakitumia Mnara wa Mlinzi.

Siku moja, Harold Jones, mwangalizi msimamizi wa kutaniko hilo aliniambia hivi: “Tuna kazi kwa ajili yako. Tunahitaji mtu fulani atunze rekodi zetu za maeneo.” Kazi hiyo ilinifaa kabisa, kwa kuwa katika kazi yangu ya polisi, nilikuwa nikiendesha gari kotekote katika Adelaide. Nilijua jiji hilo kabisa na hivyo niliweza kutayarisha vyema ramani za maeneo tulizotumia katika kuhubiri kwetu.

Katika Aprili 1938, Joseph Rutherford, msimamizi wa Watch Tower Society, alizuru Australia na akatoa hotuba katika Sydney iliyohudhuriwa na watu zaidi ya 12,000, hata ingawa wakati huo kulikuwa na Mashahidi 1,300 tu katika Australia yote. Katika Adelaide karibu 20 kati yetu tulishindwa kufunga safari ya kilometa 1,800 hadi Sydney. Kwa hiyo tulikodisha Jumba la Michezo la Tivoli lililo nzee na kuweka simu ya telegrafu ili tuweze kusikia hotuba ya Rutherford kutoka Sydney. Tulitoa matangazo ya redio, na kama tokeo, karibu watu 600 walikuja kusikia hotuba katika Adelaide!

Jinsi Nilivyopoteza Kazi Yangu ya Polisi

Katika 1939, Vita ya Ulimwengu 2 ilianza, na kutokuwemo kwa Mashahidi wa Yehova kulichunguzwa kwa ukaribu na wenye mamlaka mbalimbali. Katika pindi moja, maripota wawili wa gazeti liitwalo Truth walikuja kwenye Jumba la Ufalme na kwa uhasama wakajaribu kuingia kwa nguvu. Niliwazuia kufanya hivyo kwani walionekana kuwa hawakuwa na makusudi mazuri. Asubuhi iliyofuata kichwa kikuu katika gazeti kilisema: “Polisi wa A[ustralia] K[usini] Alinda Lango la Jumba la Ufalme la M.Y.”

Kama tokeo la kisa hicho, nilibaguliwa na wafanyakazi wenzangu. Mkubwa wangu wa karibu, Mkatoliki mshupavu, alimpatia kamishna wa polisi, Raymond Leane, habari za uwongo juu yangu. Kisha ghafula, katika Agosti 1940, nililetwa mbele za Bw. Leane, mtu yuleyule ambaye nilianza kumfanyia kazi miaka 16 iliyopita. Shtaka lenyewe? Kwamba sikutii amri zake zote.

“Je! ungeweza kumpiga mtu risasi nikikuamuru kufanya hivyo?” yeye akauliza.

“Hiyo ni hali ngumu,” nikajibu. “Lakini, la, kwa kweli nisingempiga mtu risasi.”

Kwa muda wa saa mbili alijaribu kunionyesha jinsi nilivyokuwa mpumbavu kuwa katika shirika lililoonwa kuwa lisilofaa na ambalo lingepigwa marufuku katika Australia. Yeye alimalizia hivi: “Na hayo ni baada ya yote ambayo nimekufanyia, kwa kukupa kazi-maisha nzuri hivyo.”

“Nathamini jambo hilo,” nikaitikia. “Na nimejaribu kuonyesha uthamini wangu kwa kazi ya bidii. Lakini siwezi kukutanguliza mbele ya ibada yangu kwa Yehova Mungu.”

“Napendekeza ama uache Mashahidi wa Yehova ama ujiuzulu,” kamishna akaitikia.

Kwa hiyo nilijiuzulu mara hiyo. Katika Agosti 1940 kichwa kikuu katika gazeti Truth kilisema: “Polisi wa Rutherford Ajiuzulu.” Sasa ilinibidi nimfahamishe mke wangu na kupata kazi nyingine. Kwa furaha, nilipata kazi kwenye matbaa ya kwetu ambako chapa ya Australia ya Consolation (sasa Amkeni!) ilitokezwa.

Kutumikia Chini ya Marufuku

Nilifurahi kufanya kazi katika kazi yangu mpya hadi Januari 1941, wakati ambapo Mashahidi wa Yehova walipigwa marufuku nchini kote. Uchapaji wote wa fasihi nchini ulikoma, angalau kulingana na wenye mamlaka. Kwa kweli, matbaa za kichini-chini zilianzishwa—zote katika eneo la Sydney—na hatukukosa kamwe kupokea toleo la Mnara wa Mlinzi wakati wa marufuku hiyo!

Muda mfupi baada ya kazi yetu kupigwa marufuku, nilitumikia vifungo viwili gerezani vilivyoelezwa mwanzoni. Hatimaye, katika Juni 1943, Mahakama Kuu ya Australia iliamua kwamba marufuku hiyo ilikuwa kinyume cha Katiba, kwa hiyo serikali ilirudisha mali yote iliyokuwa imenyakuliwa kutoka kwa Watch Tower Society.

Nikikumbuka, ni vigumu kuamini kwamba wakati wa miaka hiyo, nyumba nyingi (kutia na yangu) zilipekuliwa na maofisa wa polisi. Lakini, kujapokuwa upinzani, tuliendelea kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa kutumia Biblia zetu pekee. Mara nyingi polisi walitufuata. Polisi wa nguo za raia hata walihudhuria mikutano yetu iliyofanywa katika nyumba za faragha. Wakati mmoja, nilipokuwa nikimjulisha mwakilishi mmoja wa ofisi ya tawi ya Sydney, nilisema hivi: “Miongoni mwetu kuna washiriki wawili wa kikosi cha polisi wa Australia Kusini. Tafadhali wakaribisheni!” Walishtuka na wakaona aibu lakini wakaendelea kukaa na wakafurahia mkutano huo, wakisema baadaye kwamba wangeweza tu kutoa ripoti nzuri.

Kutovumiliana kwa Kidini

Katika Aprili 1945 tulipanga mkusanyiko kwenye jumba kuu la mjini katika kiunga cha Adelaide. Siku ya Jumapili, Aprili 29, hotuba ya watu wote iliyotangazwa sana “Wapole Watairithi Dunia” ilipangwa. Lakini matata yalianza kutokea mapema asubuhi. Nikiwa mwangalizi wa mkusanyiko, nilienda kwenye stesheni ya polisi ya mahali hapo ili kutoa onyo juu ya matata yaliyokaribia kutokea. Hata hivyo, ziara yangu na malalamiko yalipuuzwa.

Wakati ulipowadia wa hotuba ya watu wote kuanza, genge la watu lilikusanyika. Baadhi yao wakaingia ndani punde tu baada ya hotuba kuanza. Washiriki kadhaa walio kabambe wa genge hilo walisonga mbele, wakijaribu kuharibu vyombo vya sauti. Halafu mawe yakaanza kutupwa kupitia madirisha. Stesheni za redio zilijulishwa juu ya matata hayo, na upesi wakatangaza kwamba kulikuwa ghasia. Maelfu ya watu wadadisi walikusanyika nje.

Kwa kusikitisha, tulilazimika kukatisha mkutano. Lakini ulipofika wakati wa kuondoka kwenye jumba hilo, polisi walitufungulia kijia, na umati wote ukawa kimya. Wote wangeweza kuona upumbavu wa wale waliotupinga kwa sababu wale waliotoka nje walikuwa watu wa kawaida, kutia ndani wanaume na wanawake wa umri mkubwa zaidi pamoja na watoto wachanga. Ushupavu huo wa kidini ulishutumiwa katika “Barua kwa Mhariri” katika siku zilizofuata.

Lakini, kwa miaka mingi baadaye, Mashahidi wa Yehova hawakuruhusiwa kutumia jumba la mji katika Australia Kusini. Wakati mmoja, katika miaka ya katikati ya 1950, nilizungumza na mtunzaji wa jumba la mji wa Norwood katika kiunga cha Adelaide juu ya kutumia jumba lao kwa ajili ya mkusanyiko wetu wa wilaya.

“Mmepigwa marufuku milele kutumia majumba ya mjini,” yeye akasema.

“Unafikiri mambo ya zamani,” nikajibu.

Kisha nikatoa katika mfuko wangu broshua juu ya mkusanyiko wa kimataifa wa 1953 kwenye New York Yankee Stadium. “Angalia yale yanayoendelea juu ya Mashahidi wa Yehova katika mahali penginepo—zaidi ya 165,000 kwenye mkutano mmoja!” nikasema.

Aliichukua broshua, akaichunguza kwa uangalifu, na baada ya muda akasema: “Naam, yaonekana kana kwamba mambo yamebadilika.” Kuanzia wakati huo na kuendelea tuliweza kutumia vifaa hivyo kotekote katika Australia Kusini.

Katika 1984, baada ya ugonjwa wa muda mrefu, mke wangu alikufa. Hata hivyo, kabla ya kifo chake alianza kupenda kweli ya Biblia na Yehova Mungu. Hiyo kwa sehemu kubwa ilikuwa ni kwa sababu ya fadhili aliyoonyeshwa na Mashahidi wenye upendo kwa muda wa miaka. Kisha, katika Desemba 1985, nilimwoa Thea, ambaye amemtumikia Yehova kwa miaka mingi.

Kwa karibu miaka 60 sasa, nimekuwa nikimtumikia Yehova kwa uradhi. Kwa sababu ya kumtumaini Yehova sikuzote, kushikamana kwa ukaribu na tengenezo lake, na kutoridhiana chini ya mkazo, naweza kutazama nyuma kwenye maisha ya mapendeleo mengi na baraka. Naendelea kujitahidi kuweka macho yangu yakiwa yamekazwa kikiki kwenye zawadi ya mwito wa kutoka juu. (Wafilipi 3:14)—Kama ilivyosimuliwa na Hubert E. Clift.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kutumikia nikiwa mhudumu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki