Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 1/1 kur. 28-31
  • Nilipata Hazina Yenye Thamani Bora Zaidi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nilipata Hazina Yenye Thamani Bora Zaidi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Historia ya Familia Yangu
  • Kupata Hazina ya Kweli
  • Safari za Kuhubiri Pamoja na Baba
  • Kukabili Majaribu Mbalimbali
  • Huduma Katika Adelaide
  • Elimu Ambayo Imeendelea Katika Maisha Yangu Yote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Kutoka Kuwa Ofisa wa Polisi Hadi Kuwa Mhudumu Mkristo
    Amkeni!—1993
  • “Kutafuta Kwanza Ufalme”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Tulipewa Mradi Maishani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 1/1 kur. 28-31

Nilipata Hazina Yenye Thamani Bora Zaidi

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA FLORENCE WIDDOWSON

Usiku ulipokaribia, tuliamua kupiga kambi karibu na wangwa mmoja. Hapo hapakuwa mahali bora pa kupigia kambi kwa wanawake wawili, lakini tufikiri pangekuwa salama kwa usiku mmoja. Nilipokuwa na shughuli nikipiga hema, Marjorie alitayarisha mlo wetu wa jioni.

NILIKUWA nimemaliza tu kupigilia kigingi cha mwisho cha hema wakati nilipoona kitu kikisongea-songea karibu na kisiki cheusi cha mti. “Je! uliona kisiki hicho kikisongea?” nikapaaza sauti kuelekea Marjorie.

“La,” akajibu, akifadhaika kidogo.

“Bila shaka kilisongea,” nikapaaza sauti. “Nipe birika!”

Nikiichukua, pamoja na shoka lililokuwa begani pangu, nilitembea kuelekea wangwa. Nilipokuwa karibu sambamba na kisiki hicho, mtu alitokea nyuma yacho!

“Je! maji ya wangwa yafaa kwa kunywa?” nilisema kwa kutatarika.

“La, hayafai,” yeye akajibu kwa sauti ya ukali, “lakini ikiwa wataka maji ya kunywa, nitakuletea.”

Nilikataa toleo lake upesi, na kwa kitulizo changu kikubwa, aligeuka kwa ghafula na kwenda zake. Nikitetemeka, nilirudi na kumwambia Marjorie kilichokuwa kimetukia. Tuling’oa hema upesi, tukafunga mizigo, na kuondoka. Baadaye tuliambiwa kwamba mtu huyo alikuwa tu amefunguliwa kutoka jela.

Ingawa mara nyingi wenye kutafuta-tafuta dhahabu walipiga kambi katika nyanja zenye dhahabu za Australia huko nyuma katika 1937, sisi tulikuwa watafutaji wa kitu tofauti. Tulikuwa tukiwatafuta watu waliokuwa wenye thamani kwa Mungu.

Historia ya Familia Yangu

Miaka mia moja iliyopita, baba yangu alikuwa mhunzi katika kijiji kidogo cha Porepunkah katika jimbo la Viktoria. Nilizaliwa huko katika 1895, na kukua pamoja na ndugu wanne karibu na Mto Ovens, chini ya Mlima Buffalo. Wazazi wangu walikuwa wahudhuriaji wa kawaida kwenye Union Church, nami nilienda shule ya Jumapili, ambako baba yangu alikuwa msimamizi.

Katika 1909, mama alipatwa na ugonjwa wa moyo wa ghafula wakati wa dhoruba yenye nguvu akafa mikononi mwa babangu. Kisha, katika 1914, mmoja wa ndugu zangu aliondoka nyumbani, na muda wa saa chache baadaye, alirudishwa kwetu—akiwa amekufa. Alikuwa amejiua. Majonzi yetu yaliongezewa na lile fundisho la kanisa kwamba helo ilimngojea, kwa kuwa kujiua kulisemwa kuwa dhambi isiyosameheka.

Baadaye mwaka huo Vita ya Ulimwengu 1 ilianza, na wawili kati ya ndugu zangu walijiandikisha katika utumishi wa ng’ambo. Zile habari mbaya sana za umwagaji wa damu na kuteseka zilichochea sisi wanawake wachanga sita, pamoja na baba yangu, kuanza funzo la Biblia la kitabu cha Yohana.

Kupata Hazina ya Kweli

Ellen Hudson alikuwa na nakala ya kitabu The Time Is at Hand, cha Charles Taze Russell. Idili yake kwa ajili yacho ilivutia sisi wengine katika kikundi hicho. Alipoona kwamba kitabu hicho kilikuwa kimojapo tu cha mfululizo wa mabuku sita yenye kichwa Studies in the Scriptures, yeye alipeleka barua kwa International Bible Students Association katika Melbourne na kuomba mabuku yale mengine ya mfululizo huo. Kikundi chetu kilikubali kutumia buku la kwanza, The Divine Plan of the Ages, katika mafunzo yetu ya kila juma.

Ebu wazia shangwe ya baba yangu na yangu mwenyewe ya kuvumbua kwamba hakukuwako helo yenye moto. Hofu ya kwamba ndugu yangu alikuwa amefungwa katika moto wa helo iliondolewa. Tulijifunza kweli kwamba wafu hawana ufahamu, kana kwamba wamo usingizini, na kwamba hawaishi kwingineko wakipatwa na mateso. (Mhubiri 9:5, 10; Yohana 11:11-14) Wengine katika kikundi chetu cha funzo la Biblia waliamua kuwaendea majirani wetu ili kuhubiri zile kweli tulizokuwa tukijifunza. Tulitembea hadi nyumba za karibu, lakini tulitumia baiskeli na gari lenye magurudumu mawili yenye kuburutwa na farasi kuwafikia wale walio mashambani.

Nilionja ushahidi wa nyumba kwa nyumba kwa mara ya kwanza katika Sikukuu ya Kuadhimisha Mwisho wa Vita, Novemba 11, 1918. Sisi watatu kutoka kikundi chetu cha funzo tulisafiri kilometa 80 hadi mji wa Wangaratta ili kugawa ile trakti Peoples Pulpit. Miaka kadhaa baadaye, tukiwa katika mgawo wa kuhubiri katika mojayapo sehemu za barani, nilikuwa na ono lililotajwa mwanzoni.

Katika 1919, nilihudhuria mkusanyiko wa Wanafunzi wa Biblia katika Melbourne. Huko, mnamo Aprili 22, 1919, nilifananisha wakfu wangu kwa Yehova kwa uzamisho wa maji. Karamu hiyo ya kiroho iliongezea uthamini wangu kwa ajili ya hazina ya kiroho ya Ufalme wa mbinguni na kwa ajili ya tengenezo la Yehova la kidunia—Mathayo 13:44.

Sikurudi nyumbani baada ya mkusanyiko lakini nilikubali mwaliko wa kujiunga na Jane Nicholson, mhubiri wa wakati wote, kwa mwezi mmoja wa kutoa ushahidi. Mgawo wetu ulikuwa zile jumuiya za ukulima na za kufugia ng’ombe zilizo karibu na Mto King. Miaka michache tu iliyopita, eneo hilo lenye milima ilikuwa mahali ambapo sinema The Man From Snowy River ilifanyiwa.

Katika 1921 tulipokea ule msaada mzuri kwa ajili ya funzo la Biblia The Harp of God. Baba alipoanza kukitumia kikiwa kitabu cha mafundisho kwa ajili ya darasa lake la shule ya Jumapili, wazazi wengi walipinga wakamwomba ajiuzulu. Alifanya hivyo upesi. Baadaye tulipokea kile kijitabu Hell, pamoja na maswali yacho ya jalada yenye kuvutia, “Hiyo Ni Nini? Ni Nani Walio Humo? Je! Wanaweza Kutoka?” Baba alisisimuliwa sana na ule uthibitisho wa Biblia wa wazi uliotolewa juu ya habari hiyo hivi kwamba alianza mara iyo hiyo kugawa nakala hizo nyumba kwa nyumba. Aliangusha mamia yazo katika kijiji chetu na katika maeneo ya mashambani ya karibu.

Safari za Kuhubiri Pamoja na Baba

Hatimaye, baba alinunua gari ili kufikia watu katika maeneo mengine na ujumbe wa Ufalme. Akiwa mhunzi, alizoelea farasi zaidi, kwa hiyo nilikuwa dereva wa gari. Mwanzoni, tulilala kwenye hoteli usiku. Upesi hilo lilithibitika kuwa ghali sana, tukaanza kupiga kambi nje.

Baba alitengeneza kiti cha mbele cha gari hivi kwamba kililazwa na ningeweza kulala ndani ya gari. Tulipiga hema dogo ili baba alale humo. Baada ya kupiga kambi majuma kadhaa, tulikuwa tukirudi Porepunkah, ambako baba alikuwa akifungua duka lake la uhunzi tena. Hatukuacha kamwe kustaajabu kwamba sikuzote kulikuwa na wateja wengi waliolipia gharama zao kuweza kulipia safari yetu nyingine ya kuhubiri.

Watu wengi wenye nia ifaayo waliitikia ziara zetu vizuri na hatimaye wakakubali mafunzo ya Biblia nyumbani. Sasa kuna makutaniko saba yaliyo na Majumba ya Ufalme yayo yenyewe katika lile eneo ambalo mwanzoni lilitumikiwa na kikundi chetu kidogo kutoka Porepunkah. Kwa kweli, ni nani awezaye kudharau “siku ya mambo madogo”?—Zekaria 4:10.

Katika 1931, baba nami tuliendesha gari karibu kilometa 300 kwenye barabara mbaya mno ili kuhudhuria mkutano wa pekee, tulikokubali jina letu jipya, “Mashahidi wa Yehova.” Sote wawili tulifurahia jina hilo la pekee, la Kimaandiko. (Isaya 43:10-12) Hilo lilitutambulisha kwa wazi zaidi kuliko lile jina lisilo dhahiri sana “Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa,” ambalo tulikuwa tumejulikana kwalo hadi wakati huo.

Siku moja tulipokuwa tukitoa ushahidi katika mji wa Bethanga, nilikutana na kasisi kutoka Church of England. Alikasirika na kuanza kufuatisha maangusho yetu mengi ya vitabu, akiamuru watu wampe vitabu vyao. Baadaye aliongoza hatua ya kuchoma vitabu katikati ya mji. Lakini tendo lake lenye kuchukiza lilikuwa kwa hasara yake.

Baada ya mimi kuarifu ofisi ya tawi ya Sosaiti juu ya lile lililotukia, barua ya kupinga hilo ilichapwa ambayo ilishutumu lile ambalo kasisi alikuwa amefanya. Pia, mipango ilifanywa ili magari yenye vikundi vya Mashahidi vigawe barua hiyo kotekote katika wilaya hiyo. Baba nami tulipozuru mji huo tena baadaye, tuliangusha vitabu vingi zaidi ya wakati ule mwingine. Watu wa mji walikuwa na udadisi juu ya yale yaliyokuwa katika fasihi hiyo “iliyokatazwa”!

Mtu wa kwanza kukubali kweli ya Biblia katika kaskazini-mashariki mwa Viktoria kwa sababu ya kuhubiri kwetu alikuwa Milton Gibb. Kati ya ziara zetu, alijifunza kikamili vichapo vyote vya Sosaiti tulivyomwachia. Katika mojayapo ziara zetu za kurudia, alitushangaza kwa kusema: “Mimi sasa ni mmoja wa wanafunzi wenu sasa.”

Ingawa nilifurahia uamuzi wake, nilieleza hivi: “La, Milton. Usingeweza kuwa mmoja wa wanafunzi wangu.”

“Haya basi, mimi ni mmoja wa wanafunzi wa Rutherford [aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo].”

Nilimweleza tena: “La, [huwezi kuwa] mmoja wa wanafunzi wa Rutherford, lakini natumaini [wewe ni] mmoja wa wanafunzi wa Kristo.”

Milton Gibb alithibitika kuwa mmoja tu wa zile hazina nyingi zenye thamani ambazo kwa ajili yazo nimetumia miaka mingi sana nikitafuta-tafuta. Yeye na wawili wa wana wake ni wazee Wakristo, na washiriki wengine wa familia yake ni wenye bidii kutanikoni.

Kukabili Majaribu Mbalimbali

Ijapokuwa kupigwa marufuku kwa kazi ya Mashahidi wa Yehova katika Australia katika Januari 1941, tuliendelea kuhubiri, tukiitumia Biblia pekee. Kisha upainia wangu, au utumishi wangu wa wakati wote, ulikatizwa nilipoitwa nyumbani kumtunza baba yangu aliyekuwa mgonjwa mahututi. Baadaye, mimi pia nilikuwa mgonjwa nikahitaji upasuaji mkubwa. Kurudia kwangu afya kulichukua muda fulani, lakini nilijionea ukweli wa ahadi ya Mungu: “Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.” (Waebrania 13:5) Dada mmoja Mkristo alinihakikishia, akisema hivi: “Kumbuka, Flo, huko pekee yako kamwe. Na wewe na Yehova hufanyiza watu wengi sikuzote.”

Kisha kukaja ugonjwa wa mwisho wa baba yangu mpendwa wa muda wa majuma 13. Mnamo Julai 26, 1946, aliyafumba macho yake katika kifo. Alikuwa amefurahia maisha kamili, na alikuwa na tumaini la kimbingu. (Wafilipi 3:14) Kwa hiyo nikiwa na umri wa miaka 51, nilikuwa pekee yangu, nikiwa nimekuwa pamoja na baba kwa sehemu kubwa ya miaka yangu ya mapema. Kisha nikakutana na yule ambaye angekuwa mume wangu wa wakati ujao. Tulioana katika 1947 tukaanza kupainia pamoja. Lakini kipindi hicho chenye furaha hakikudumu muda mrefu, kwa kuwa alipatwa na ugonjwa wa ghafula wa moyo katika 1953 akawa hajiwezi.

Usemi wa mume wangu uliathiriwa vibaya, na ikawa vigumu kuzungumza naye. Hilo lilikuwa ndilo jambo gumu zaidi katika kumtunza. Mkazo wa akilini wa kujaribu kuelewa alichokuwa aking’ang’ana kusema ulikuwa mwingi kwelikweli. Ingawa tulikuwa tukiishi katika eneo la mbali ambako hakukuwa kutaniko karibu, Yehova hakutuacha katika miaka hiyo yenye majaribu. Niliendelea kwenda sambamba na habari zote za karibuni za kitengenezo, pamoja na ugavi wenye kuendelea wa chakula cha kiroho katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Mnamo Desemba 29, 1957, mume wangu mpendwa alikufa.

Huduma Katika Adelaide

Nilikuwa pekee yangu mara nyingine tena. Ningefanya nini? Je! ningekubaliwa tena kuwa mhudumu wa wakati wote baada ya kipindi cha kuacha cha karibu miaka mitano? Nilikubaliwa, kwa hiyo niliuza nyumba yangu nikaanza upya kazi ya painia katika Adelaide, jiji kuu la Australia Kusini. Mapainia walihitajiwa huko wakati huo, nami niligawiwa Kutaniko la Prospect.

Kwa kuwa nilikuwa na hofu kidogo juu ya kuendesha gari kati ya magari mengi ya jiji, niliuza gari langu nikaanza kutumia baiskeli tena. Niliitumia hadi nilipofikia umri wa miaka 86, nikija kujulikana katika eneo hilo kuwa “yule mama mdogo kwenye baiskeli ya buluu.” Hatimaye nilizidi kuwa na wasiwasi nikiwa kati ya magari mengi; gurudumu la mbele la baiskeli yangu lilionekana likitetemeka daima. Tukio lililonifanya niache kabisa lilitokea alasiri moja nilipoanguka ndani ya ua. ‘Huu ndio mwisho,’ nikajiambia, na kwa hiyo, nilianza kutembea tena.

Miaka michache iliyopita, nilipokuwa nikihudhuria mkusanyiko wa wilaya, miguu yangu ilianza kushindwa, na baadaye nilikuwa na upasuaji mara mbili kwenye viungo vya nyonga yangu. Nilikuwa nafuu baada ya upasuaji mpaka mbwa mkubwa aliponigonga nikaanguka. Hilo lilifanya iwe lazima nipate matibabu zaidi, na tangu wakati huo nimehitaji kifaa cha kunisaidia kutembea. Akili yangu ingali chonjo sana. Ni kama vile rafiki mmoja alivyosema: “Yaonekana mwili wake wenye kuzeeka hauwezi kuifikia akili yako yenye ujana.”

Kwa muda wa miaka iliyopita, nimeona makutaniko katika Adelaide yakikua, kupanuka, na kugawanyika. Kisha, katika 1983, nilipokuwa na miaka 88, niliondoka Adelaide ili kuishi pamoja na familia moja Kyabram katika jimbo la Viktoria, ambako nimetumia miaka kumi yenye furaha. Ningali naweza kwenda katika huduma ya shambani; marafiki kutanikoni hunipeleka huko na huko kwa gari ili kuzuru wale ambao hupata magazeti kwangu kwa kawaida. Watu hao huja kwenye gari kwa fadhili ili niweze kuongea nao.

Nikifikiria ile miaka yangu zaidi ya 98 ya kuishi, nakumbuka kwa shauku nyingi wale waaminifu-washikamanifu na waaminifu wengi ambao wamemsifu Yehova pamoja na mimi, hasa baba yangu mzuri ajabu. Yaonekana nimeishi muda mrefu zaidi ya wale waaminifu walioshiriki na mimi katika huduma ya painia. Lakini ni shangwe iliyoje iningojeayo niunganapo tena na wale wanaoshiriki tumaini la zawadi ya uhai katika Ufalme wa Mungu wa kimbingu, kwa kweli ni hazina yenye thamani bora zaidi!

[Picha katika ukurasa wa 28]

Nilibatizwa katika Aprili 22, 1919

[Picha katika ukurasa wa 31]

Mwenye furaha bado nikimtumikia Yehova nikaribiapo miaka 100

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki