Utegemezo Ufaao
“NILILAZIMIKA kupigana na hali ya kuhofu kifo na vipindi vya kushuka moyo,” aeleza Virginia, mmoja wa Mashahidi wa Yehova nchini Argentina. Alipasuliwa na kuondolewa matiti na vilevile kuondolewa vifuko vyote viwili vya mayai katika vita yake dhidi ya kansa ya matiti.a
Kwa kweli, hofu ya kifo kwa sababu ya kupatwa na kansa ya matiti yaenea ulimwenguni pote. Hofu hiyo, ikiandamana na ogofyo la kulemaa na la kupoteza viungo vinavyohusika sana na hali ya kike na uwezo wa malezi ya watoto, yaweza kuharibu kabisa kihisia-moyo maisha ya mwanamke. Hisia zenye nguvu sana za upweke zaweza kumfanya atamauke sana. Anaweza kusaidiwaje asipate mapigo ya kihisia-moyo kama hayo?
Uhitaji wa Utegemezo
“Ahitaji utegemezo!” ajibu Joan, kutoka United States. Mama yake mwenyewe na nyanya yake walipatwa na kansa ya matiti, na sasa yeye mwenyewe anakabili pigano ilo hilo waliokuwa nalo. Huu ni wakati ambao watu wa ukoo na marafiki walio waaminifu-washikamanifu waweza kuandaa utegemezo na msaada wenye kufariji. Mume wa Joan, Terry, akawa mteteaji wake mkubwa zaidi. Terry aeleza hivi: “Hali yangu, kama nilivyoiona, ilikuwa ni kuwa na uvutano wenye kumwimarisha. Nilihitaji kumsaidia Joan afikie maamuzi kuhusu aina ya matibabu ambayo ingempa uhakika na nguvu ya kuendelea kupigana bila kushindwa. Ilitulazimisha tukabiliane na hofu yake ya upasuaji wa matiti, na nilijaribu kuhakikisha kwamba maswali yake na hofu zake zilishughulikiwa katika mazungumzo yetu na madaktari.” Terry aongezea hivi: “Hili ni jambo tuwezalo kufanyia familia zetu na Wakristo wenzetu ambao hawana utegemezo wa familia. Twaweza kuwa kama macho yao, masikio yao, na sauti zao kwa madaktari.”
Waseja au wajane wahitaji uangalifu wa pekee. Diana, kutoka Australia, atuambia hivi: “Mume wangu alikufa miaka mitano iliyopita baada ya kupasuliwa kwa sababu ya kansa, lakini watoto wangu walijazia nafasi yake. Walikuwa wenye fadhili lakini si wenye kusisimka kihisia. Jambo hilo lilinipa nguvu. Kila kitu kilishughulikiwa haraka na kwa utulivu.”
Kansa ya matiti huathiri sana familia nzima kihisia-moyo.[10] Kwa hiyo wote wahitaji hangaikio lenye upendo kutoka kwa watu wengine (hasa kutoka kwa ndugu na dada zao wa kiroho, kama wao ni Mashahidi wa Yehova).
Rebecca, kutoka United States, ambaye mama yake alipigana na kansa ya matiti, aeleza hivi: “Kutaniko ni familia-tanzu yako, na matendo yao yana uvutano sana kwa hisia zako. Ingawa wengi hawakupenda binafsi aina ya matibabu yasiyo ya kawaida ambayo mama yangu alichagua, walitutegemeza kihisia-moyo kwa kutupigia simu na kutuzuru. Baadhi yao hata wangekuja kutusaidia kazi ya kumtayarishia mama mlo wa kipekee. Wazee walipanga tuunganishwe kwa simu ili tusikose mikutano. Kutaniko hata lilituletea zawadi ya kadi iliyokuwa na fedha.”[11]
Joan akiri hivi: “Hata sasa, nifikiripo juu ya upendo ambao ndugu na dada zangu wa kiroho walinionyesha, hisia zangu huchochewa sana! Kwa majuma saba, siku tano kwa juma, dada zangu wenye upendo wangechukua zamu ya kunipeleka hospitalini kwa matibabu na kunirudisha nyumbani. Na huo ulikuwa mwendo wa jumla ya kilometa 150! Namshukuru Yehova kama nini kwa baraka zake nyingi za udugu huu wa Kikristo!”[12]
Njia nyingine ambayo sisi sote twaweza kuwa wenye kutia moyo na wenye kutegemeza ni kwa maneno yetu ya kujenga. Twapaswa kuwa waangalifu ili tusije tukasababisha msononeko kwa kukazia mno mambo yasiyofaa. June kutoka Afrika Kusini aeleza hivi: “Huwezi kutarajia mtu ambaye hajapata kuwa na kansa kusema jambo lifaalo tu. Katika hali yangu niliona kuwa haifai kwa wengine kutaja visa vya kansa kama visa hivyo havikuwa na matokeo mazuri.”[13] Noriko kutoka Japani akubaliana na hayo: “Watu wakiniambia juu ya mtu mwingine aliyepona na hakurudiwa na kansa, basi mimi pia hupata tumaini kwamba labda hata mimi nitakuwa kama wao.”[14]
Kumbuka kwamba wanawake fulani hawapendelei kusema juu ya afya zao nyakati zote.[15] Lakini, wengine nao, kwa ajili ya hali njema yao wenyewe, huhitaji kusema juu ya kansa ya matiti, hasa na wale walio karibu sana nao. Mtu aweza kujuaje jambo la kufanya lenye msaada zaidi? Helen, kutoka United States, apendekeza hivi: “Muulize mgonjwa mwenyewe kama anataka kuongea juu ya ugonjwa wake, na umwache aseme.”[18] Naam, “uwe tayari kusikiliza,” asema Ingelise kutoka Denmark. “Wewe mtegemeze tu kihisia-moyo ili asiachwe pekee na mawazo yake yenye huzuni.”[19]
Kujitahidi Kuwa na Mwelekeo Ufaao
Tiba ya kansa ya matiti yaweza kufanya mgonjwa achoke sana na kuwa mwenye uchovu sana kwa majuma, miezi, au miaka. Mojapo majaribu makuu zaidi kwa mwanamke mwenye kansa ya matiti yaweza kuwa ni kutoweza kufanya mambo kwa kadiri alivyokuwa akifanya zamani. Kukubali mapungufu ya mwili wake kwamaanisha kujiwekea utendaji wa kiasi na kupumzika wakati wa mchana.[20]
Anaposhuka moyo, hatua za haraka zahitajiwa ili kuendeleza mtazamo ufaao. Noriko aeleza ono lake: “Matokeo ya matibabu ya hormoni yalinifanya nishuke moyo. Nilishindwa kufanya mambo ambayo ningependa kufanya niliposhuka moyo, nami nikaanza kuhisi kuwa sifai kitu mbele za Yehova na katika kutaniko la Kikristo. Fikira zangu zilipoendelea kuwa zisizofaa, ningeanza kuyakumbuka mateseko ya mwisho ya watu wa familia yetu waliokufa kwa kansa. Ningejawa na hofu sana nilipojiuliza hivi, ‘Je! ningeyavumilia kama wao?’”
Noriko aendelea kusema: “Ni wakati huo nilipojaribu kurekebisha njia yangu ya kufikiri kwa kutumia vichapo vya Mashahidi wa Yehova ili nifikirie jinsi Yehova aonavyo kuwapo kwetu. Nilijifunza kwamba ujitoaji wa kimungu huonyeshwa na madhumuni yetu bali si kwa kiasi ambacho kinafanywa. Na kwa sababu nilitaka Yehova afurahie hali ya moyo wangu na fikira zangu, Niliamua nimtumikie kwa nafsi yote hata kama ningeweza kufanya machache sana katika huduma ya Kikristo.”[21]
Hali ya muda mrefu ya kutokuwa na hakika kwa wanawake wengi wanaopigana na kansa ya matiti yaweza kuharibu mtazamo ufaao. Diana aeleza kwamba kitu kilichomsaidia sana ni kujaza moyo wake na akili zake vitu vyote vizuri ambavyo Yehova Mungu amempa: “Familia yangu, rafiki, muziki mtamu, kutazama bahari yenye nguvu na machweo ya jua yaliyo maridadi.” Yeye hasa atia moyo hivi: “Eleza wengine juu ya Ufalme wa Mungu. Na usitawishe tamaa halisi kwa hali zitakazokuwa duniani chini ya Ufalme, ambamo hamtakuwa na ugonjwa!”[22]—Mathayo 6:9, 10.
Virginia vilevile apata nguvu ya kupigana na hali yake ya kushuka moyo kwa kutafakari juu ya kusudi lake maishani: “Kwa kweli ninataka kuishi kwa sababu nina kazi bora sana ya kufanya.” Na kwa habari ya nyakati ambazo pindi zilizo ngumu zamjia na hofu kumjaa, yeye asema hivi: “Naweka itibari yangu yote kwa Yehova, nikijua kwamba hataniacha kamwe. Na nafikiria juu ya mstari wa Biblia kwenye Zaburi 116:9, unaonihakikishia kwamba ‘nitaenenda mbele za BWANA katika nchi za walio hai.’”[23]
Wanawake hao wote wameweka tumaini lao kwa Mungu wa Biblia, Yehova. Kitabu cha Biblia cha 2 Wakorintho, kwenye sura ya 1, mistari ya 3 na 4, chamwita Yehova “Mungu wa faraja yote, atufarijiye katika dhiki zetu zote.” Je! Yehova hunyoosha mkono wake na kutegemeza wale wanaohitaji faraja?
Mieko kutoka Japani ajibu hivi: “Nina hakika kwamba kwa kudumu katika utumishi wake, ninapokea faraja na msaada wenye nguvu wa Yehova.”[24] Yoshiko atuambia hivi pia: “Ingawa huenda watu wasielewe mateseko yangu, Yehova ajua kila kitu, na nina hakika kwamba amenisaidia kulingana na mahitaji yangu.”[25]
Joan asema hivi: “Sala ina nguvu ya kukusaidia kuacha kutamauka na kukurudisha kwenye hali ya kawaida. Ninapofikiria yale maponyo matukufu ambayo Yesu alifanya alipokuwa duniani na yale maponyo kamili atakayofanya katika ulimwengu mpya, maneno hayo hunifariji kama nini!”—Mathayo 4:23, 24; 11:5; 15:30, 31.[26]
Je! waweza kuwazia ulimwengu bila kansa ya matiti, kwa kweli, ulimwengu bila ugonjwa wowote? Hii ndiyo ahadi inayotolewa na Mungu wa faraja zote, Yehova. Isaya 33:24 lasema juu ya wakati ambapo hakuna mtu duniani atakayesema kwamba yeye ni mgonjwa. Tumaini hilo litatimizwa hivi karibuni wakati Ufalme wa Mungu ukiwa mikononi mwa Mwana wake, Kristo Yesu, uletapo utawala wao kamili duniani, ukiondoa kabisa visababishi vyote vya magonjwa, huzuni, na vifo! Mbona usisome juu ya tumaini hilo kwenye Ufunuo 21:3 hadi 5? Jipe moyo mkuu ukabili wakati ujao ukiwa na utegemezo unaofariji kwelikweli.
[Maelezo ya Chini]
a Vifuko vya mayai huwa chanzo kikuu cha estrojeni katika wanawake ambao hawajakoma hedhi.