Jinsi Watu Wawezavyo Kuishi Pamoja kwa Amani
ULIKUWA mwezi wa Septemba 1944, na ulimwengu ulikuwa umejaa chuki. Vita ya Ulimwengu 2 ilikuwa ikiendelea, na mamilioni ya watu walikuwa wanateseka vibaya sana. Nilikuwa Mjerumani aliyekuwa mfungwa wa vita nchini Ufaransa.
Pindi moja niliwekwa mbele ya kikosi cha kufyatua risasi. Lakini baada ya muda fulani wale ambao wangeniua wakaanza kwenda zao. Kumbe walikuwa wakinitisha tu. Nilishtuka sana, lakini nilishukuru sana kwamba nilikuwa ningali hai. Majuma machache baadaye, nilifanyiwa vivyo hivyo. Ingawa niliokoka, idadi kadhaa wa wafungwa wenzangu waliuawa au walikufa kutokana na maradhi na njaa. Nilikujaje katika hali hizo?
Nashikwa
Miezi michache iliyopita, katika Juni 1944, majeshi ya Muungano yalikuwa yamevuka Mlango-Bahari wa Uingereza na kufanikiwa kuweka kituo katika ufuo wa pwani wa Ufaransa. Mashambulizi yao na uvamizi wao wa kaskazini mwa Ufaransa uliofuata ulilazimisha Jeshi la Ujerumani kurudi nyuma. Nilikuwa sajini-meja katika Jeshi la Wanahewa la Ujerumani. Mnamo Agosti, sehemu ya kikosi chetu, nikiwa pamoja na wengine 16, ilikamatwa na jeshi la kisiri la Ufaransa lililoitwa Maquis.[1] Baada ya kukaa miezi michache katika kambi ya wafungwa wa vita, tulihamishwa kwenda kambi nyingine iliyokuwa karibu na Montluçon katika kusini mwa Ufaransa.
Wafungwa walilazimishwa kufanya kazi ngumu, lakini kwa sababu nilikuwa ofisa wa jeshi sikulazimishwa kufanya kazi. Hata hivyo, nilijitolea kufanya kazi nami nikawekwa kuwa msimamizi wa jikoni. Siku moja kikundi kipya cha wafungwa kilifika, na katika kikundi hicho kulikuwa na kijana aliyeitwa Willy Huppertz aliyetoka mji wa kwetu. Nilimwomba ofisa msimamizi kama Willy angenisaidia katika kazi ya jikoni, na mpango huo ukafanywa.
Baadaye, Willy nami tukawa na aina ya urafiki unaoweza kuunganisha watu wote pamoja kwa amani. Kabla ya kueleza jinsi nilivyokuja kujifunza njia hiyo ya kupata amani, acheni niwasimulie mambo mengi maishani yasiyopatana yaliyonisumbua.
Kwa Nini Hakuna Muungano na kwa Nini Kuna Chuki Sana Hivyo?
Nikiwa kijana anayekua katika Aachen, Ujerumani, nilikerwa na ukosefu wa muungano wa kidini, uliokuwapo hata katika nyumba yetu. Baba alikuwa Mlutheri, lakini mama alikuwa Mkatoliki wa Roma. Kwa hiyo mama alihakikisha kwamba dada yangu na mimi tulifundishwa imani ya Kikatoliki. Kutoka miaka yangu ya mapema, nilihudhuria Kanisa la Katoliki kwa ukawaida, ingawa sikuelewa sababu iliyofanya baba afuate dini tofauti. Wakati ulipoendelea, mara nyingi nilikuwa nikijiuliza, ‘Ikiwa kuna Mungu mmoja tu, kwa nini kuna dini nyingi sana hivi?’
Vita ya Ulimwengu 2 ilipoanza katika 1939, nilisajiliwa katika Jeshi la Wanahewa la Ujerumani. Baada ya mazoezi ya kwanza katika Ujerumani, nilipelekwa Vienna, Austria, ambako nilijiunga na kikosi cha kuzoeza wasajiliwa wapya. Kisha, katika Desemba 1941, nilipelekwa kaskazini mwa Uholanzi. Huko nilikutana na Jantina, mwanamke mchanga kutoka Den Helder. Tukapendana hata ingawa nchi zetu zilikuwa maadui katika vita.
Muda mfupi baadaye, katika Aprili 1942, kwa ghafula nilihamishwa kwenda La Rochelle, kusini mwa Ufaransa. Kufikia wakati huo nilikuwa sajini-meja, na kikosi chetu kilikuwa na mgawo wa kufunza wasajiliwa wapya na kulinda kiwanja-ndege kidogo kilichokuwa huko. Kwa sababu hiyo sikupata kupigana kihalisi wakati wowote katika vita. Na ninashukuru kwa sababu sikutaka kuua mtu yeyote.
Lakini kitu kilichoniudhi katika miaka hiyo ya vita ilikuwa ni kuona makasisi wa karibu dini zote—Katoliki, Lutheri, Episkopali, na kadhalika—wakibariki ndege na majeshi yazo kabla ziende kuangusha mabomu yazo hatari. Mara nyingi nilikuwa nikijiuliza, ‘Mungu anaunga mkono upande gani?’ Lakini, sikupata hasa kuwauliza makasisi wa jeshi kwa sababu nilikuwa na hakika kwamba hawakujua jambo lolote.
Wanajeshi wa Ujerumani walivaa mishipi iliyokuwa na vifungo (ona juu kushoto katika ukurasa 12) vilivyoandikwa Gott mit uns (Mungu yu pamoja nasi), lakini nilikuwa nikijiuliza, ‘Mbona Mungu asiunge mkono wanajeshi wa upande mwingine waliokuwa wa dini ileile na waliokuwa wakimwomba Mungu yuleyule?’
Miaka ilipita, na vita iliendelea kwa muda mrefu. Mara moja-moja niliweza kuenda Uholanzi kumwona Jantina, mara ya mwisho ikiwa ni Desemba 1943, tulipoanza uchumba wetu. Kufikia 1944 hali ya vita ilianza kubadilika, na majeshi ya Muungano yalipoingia Ufaransa, tulianza kung’amua kwa mara ya kwanza kwamba Ujerumani ingeweza kushindwa katika vita hiyo. Mawazo hayo yalishtua sana! Kisha ukaja ule mwezi wa Agosti wakati sisi watu 17 tulipokamatwa.
Maisha ya Gerezani
Hatimaye sisi wafungwa katika kambi iliyokuwa karibu na Montluçon tulikubaliwa kuwasiliana na wapendwa wetu. Hivyo nikaanza kuwasiliana na Jantina. Baadaye, nikiwa pamoja na mateka wengine kadhaa, nilijitolea kufanya kazi katika shamba la jumuiya ambako bado tulionwa kuwa wafungwa wa vita. Hata nikagundua kwamba nilianza kupenda maisha ya shambani. Hilo lilikuwa badiliko kubwa la mtindo wa maisha wa kijana aliyelelewa jijini.
Vita katika Ulaya iliisha mnamo Mei 1945, lakini serikali ya Ufaransa haikutuachilia tukiwa wafungwa wa vita mpaka Desemba 1947. Kisha tuliambiwa tuchague kati ya kujiunga na Kikosi cha Kigeni cha Ufaransa au kubaki katika Ufaransa tukiwa wafanyakazi wa kujitolea mpaka mwisho wa 1948. Nilichagua kuwa mfanyakazi wa kujitolea, nikiwa mfanyakazi katika shamba la jumuiya pamoja na wafungwa wengine kadhaa. Tulifurahia uhuru zaidi chini ya mpango huo kuliko kufanya kazi katika shamba tukiwa wafungwa wa vita. Hata hivyo, bado tulikuwa na vizuizi fulani. Kwa hiyo, shangwe yetu kuu ilikuwa kupokea barua kutoka kwa wapendwa wetu.
Kuungana Tena na Jantina
Siku moja katika 1947, nilipokea barua kutoka kwa Jantina ambamo alikuwa ameweka kimakosa kikaratasi kidogo chenye nambari za nyumba kadhaa na rekodi ya vitabu na magazeti. ‘Naam,’ nikawaza, ‘Jantina anapata fedha kwa kuuza vitabu.’ Kumbe sikujua kwamba alikuwa amekutana na Mashahidi wa Yehova na sasa alikuwa akihubiri kwa bidii nyumba kwa nyumba na kugawanya fasihi ya Biblia, wala si ‘kuuza vitabu.’
Muda mfupi baadaye, mnamo Desemba 1947, sisi wafungwa tulipata jambo la kutufurahisha—tulipewa likizo ya huruma ya majuma manne tuzuru nyumbani. Bila shaka, likizo ilitolewa ikiwa tungerudi Ufaransa kutimiza kazi zetu. Jantina alisafiri kutoka Uholanzi hadi Ujerumani ili akae na wazazi wangu pamoja nami kwa majuma hayo. Kama ujuavyo, hiyo ilikuwa ni pindi ya kuungana tena iliyojaa hisia-moyo sana baada ya kutengana kwa zaidi ya miaka minne. Ndipo nilipojifunza maana ya kile kikaratasi chenye maandishi nilichopata katika barua yake. Jantina aliniambia kwamba alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova naye akanieleza kwa shauku mambo ya ajabu aliyokuwa amejifunza.
Ingawa niliweza kuona ukweli fulani kwa mambo aliyokuwa akisema, nilimwambia kwamba nilifurahi kubaki Mkatoliki. Niliona kwamba hangeweza kujua mengi kuliko makasisi ambao walikuwa wamejifunza dini kwa miaka mingi. Na mambo yakawa hata magumu zaidi kwa sababu familia yetu haikufurahia itikadi mpya za Jantina. Hata wakawa wapinzani sana, na ubaguzi wao ukanishawishi pia.
Badiliko Katika Maisha Yangu
Likizo yangu ya majuma manne ilipokwisha, nilirudi Ufaransa. Nilipokuwa nikitoa mavazi yangu, nilipata kitabu kilichoitwa Deliverance miongoni mwayo. Jantina alikiweka humo alipokuwa akipakia sanduku langu. Ili nimfurahishe tu niliketi usiku huo na kuanza kukisoma. Nilishangaa sana kuona kabla ya muda mrefu kwamba maswali mengi niliyokuwa nikifikiria wakati nilikuwa nimefungwa yalikuwa yakijibiwa. Nikawa na tamaa ya kusoma kitabu hicho chote.
Nilikumbuka andiko moja ambalo Jantina alikuwa amenukuu: “Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” (Yohana 8:32) Kwa kweli, nilihisi ninaanza kujifunza kweli juu ya mambo mengi. Watu wote ni sawa, hata wawe wa jamii gani. (Matendo 17:26-28) Wakristo wa kweli wanapendana na hawapigani na kuua mtu yeyote kama nilivyokuwa nimeona wengi wanaojidai kuwa Wakristo wakifanya. (Yohana 13:34, 35; 1 Yohana 3:10-12) Kwa wazi basi, utukuzo wa taifa ni chombo cha Ibilisi cha kugawanya watu na kuzuia udugu wa kweli.
Nikaanza kuona kwamba amani ya kweli ingekuja maadamu tu watu wote wangetumia maishani mafundisho ya Yesu Kristo. Kwa sababu mataifa hayataweza kutimiza jambo hilo, tumaini la pekee la amani ni kupitia serikali ya Mungu, ambayo Yesu alifundisha wafuasi wake wasali juu yayo. (Mathayo 6:9, 10) Tayari nikaanza kuhisi uhuru wa kweli na uradhi kwa kujifunza mambo hayo. Nilishukuru mpenzi wangu Jantina kama nini kwa kuweka kitabu hicho katika sanduku langu! Lakini sasa ningefanya nini?
Nafanya Maendeleo ya Kiroho
Naam, kumbe sikupaswa kuwa na wasiwasi. Siku chache baadaye, mtu mmoja aliyeitwa Lucien alikuja katika shamba nililokuwa nikifanya kazi naye akajitambulisha kuwa mhudumu wa Mashahidi wa Yehova. Alieleza kwamba alikuwa ameagizwa na ofisi ya tawi ya Mashahidi katika Paris awasiliane nami kwa maombi ya mchumba wangu. Lucien alikuwa mtu mwenye fadhili, mnyoofu, nami nikazoeleana naye mara moja. Kwa uzuri, kufikia sasa nilikuwa nikisema Kifaransa kwa ufasaha, na hilo likafanya mambo yawe rahisi sana kwangu.
Nilikubali kujifunza naye Biblia, na kila Jumapili Lucien na mke wake, Simone, walikuwa wakinichukua kutoka shamba niliyofanya kazi na kunipeleka nyumbani kwao kwa ajili ya funzo. Baadaye tulikuwa tukitembea huku tukizungumzia uumbaji wa ajabu wa Yehova. Wote walikuwa walimu wazuri, nao pia walinipa kitu kingine nilichokuwa nimekosa kwa muda mrefu sana—upendo halisi. Na upendo huo ulikuwa ukionyeshwa na mume na mke Wafaransa—watu ambao nilikuwa nimezoeza watu wawalipue mabomu na kuwaua!
Nilifanya maendeleo mazuri katika mafunzo yangu, na Lucien akanialika nihudhurie sherehe ya kila mwaka ya Ukumbusho wa kifo cha Kristo siku ya Machi 25, 1948. Nilivutiwa sana na mkutano huo sahili lakini wenye uzito na tangu siku hiyo sijapata kukosa Ukumbusho wowote.
Jantina alifurahia maendeleo yangu ya kiroho, na kwa hiyo akajiunga nami katika Ufaransa. Tulioana huko katika Novemba 1948. Lucien na Simone wakatuandalia mlo murua kwa arusi yetu, na mapainia wawili (wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova) walikuwa nasi kwenye pindi hii yenye furaha. Jioni hiyo ambayo siwezi kusahau iliimarisha mkataa wangu kwamba Mashahidi kwa kweli wana ile aina ya upendo ambao Yesu alisema ungetambulisha wafuasi wake wa kweli.—Yohana 13:35.
Kwenda Ujerumani, Kisha Kuhamia Nchi Mpya
Tulirudi Ujerumani mnamo Desemba 1948, na huduma ya Kikristo ikawa njia yetu ya maisha. Ingawa familia yetu iliendelea kupinga utendaji wetu, hatukuacha utumishi wetu. Tuliendelea kusaidia wapole na wanyenyekevu wajifunze ile njia ya pekee ambayo jamii ya kibinadamu yaweza kufurahia amani na usalama wa kweli.
Katika 1955, Jantina nami tukahamia Australia. Kwanza tulikaa katika kisiwa maridadi ambacho ni jimbo la Tasmania, ng’ambo ya Mlango-Bahari wa Bass kutoka rasi ya kusini ya bara hilo kubwa. Kwa msaada wenye upendo na saburi ya ndugu na dada zetu wa kiroho, hatimaye tuliweza kuongeza Kiingereza kwa lugha tulizojua.
Katika 1969, baada ya kukaa Tasmania kwa miaka 13, tulihamia jimbo la kaskazini la Queensland, ambako tumeishi tangu wakati huo. Wakati huu ninatumika nikiwa mzee wa Kikristo katika kutaniko letu na nathamini sana ushirika wa Jantina tunapomtumikia Yehova pamoja. Wakati wowote tuliporudi Ujerumani wakati wa likizo, tulikuwa tukimtafuta Willy Huppertz na kujifunza naye Biblia. Hatimaye yeye vilevile aliweka maisha yake wakfu amtumikie Yehova, na tunafurahia aina ya urafiki uwezao kuunganisha watu wote pamoja kwa amani.
Ninapokumbuka matukio ya maisha yangu tangu miaka ile nilipokuwa mfungwa wa vita nchini Ufaransa, kwa kweli nashukuru kwamba niliweza kumjua Muumbaji wetu mwenye upendo, Yehova Mungu. Nafurahi kama nini sasa kwamba Jantina alichukua hatua ya kwanza kuweka kile kitabu Deliverance katika sanduku langu kisha akawaandikia Mashahidi katika Ufaransa wapange kunitafuta! Matokeo ni kwamba maisha yangu binafsi na maisha yetu pamoja tukiwa mume na mke yamekuwa bora sana na yenye kuthawabisha kwa njia nyingi.—Kama ilivyosimuliwa na Hans Lang.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Nikiwa na Jantina leo