Ni Zaidi ya Adui Mkatili
MAUMIVU yasiyoisha yaweza kuvuruga sana maisha za watu. Huondoa amani yao, shangwe, na riziki, yakifanya maisha yawe ya kusikitisha sana hivi kwamba watu fulani hutafuta kitulizo kwa kujiua. Mishonari wa kitiba Albert Schweitzer alikata shauri hivi: “Maumivu ni bwana mwenye kutawala wanadamu kwa kuogofya kuliko hata kifo chenyewe.”
Kwa kweli, mamia ya mamilioni huteseka vibaya sana. ‘Kama sisi tungeweza kuning’inizwa katika lile anga la juu lisilo na mipaka tukiwa juu ya shimo kubwa mno ambamo milio ya dunia yenye kuzungukazunguka ingeinuka juu iyafikie masikio yetu,’ akasema mpasuaji mmoja Mfaransa, ‘tungesikia mngurumo wa maumivu ukitolewa humo kama kwamba na sauti moja ya wanadamu wenye kuteseka.’[2]
Kwa kweli, yale ambayo mtume Mkristo Paulo aliandika zaidi ya miaka 1,900 iliyopita yana nguvu hata zaidi leo: “Viumbe vyote vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa.”—Warumi 8:22.
Tatizo Kubwa la Afya
Mmoja kati ya Waamerika 8 hupatwa na maumivu makali ajabu ya yabisi-kavu inayozorotesha mifupa ya maungo, ipatikanayo kwa wingi kuliko namna nyingine za yabisi-kavu.[3] Watu wengi hata zaidi wana maumivu ya mgongo yenye kuwamenya kwelikweli.[4] Wengine hulazimika kuvumilia athari zenye kuumiza za kansa na ugonjwa wa moyo.
Mamilioni zaidi huteswa na maumivu makali ya kichwa, maumivu ya meno, maumivu ya masikio, bawasiri, na magonjwa na majeraha mengine mengi. Si ajabu kwamba katika mwaka fulani wa majuzi, Waamerika walitumia dola bilioni 2.1 kuhusiana na dawa za kutuliza maumivu tu ambazo hawakuandikiwa na matabibu, wala si ajabu kwamba maumivu huitwa “kishindo kilichofichika cha Marekani.”[5][6]
John J. Bonica, ambaye labda ndiye mashuhuri zaidi kuhusiana na habari za maumivu, alisema hivi: “Kwa habari ya fedha, na kwa habari ya mateso ya kibinadamu, maumivu ya daima ndiyo hutaabisha kuliko karibu matatizo mengine yote kwa ujumla ya utunzaji wa afya.”[7]
Je! Kuwe na Maisha Bila Maumivu?
Kwa kukabiliana na maumivu makali hayo, huenda kudokeza kwamba kuna uwezekano wa maisha yasiyo na maumivu kukaonekana ni kubobokwa na maneno tu. Kwa hiyo, yale isemayo Biblia huenda yakaonekana kuwa ya kuwazia tu, yaani: “[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao . . . wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:4.
Hata hivyo, uwezekano wa maisha yasiyo na maumivu si jambo la kuwazia tu. Lakini fikiri kidogo. Andiko hilo lamaanisha nini kweli? Leo kuna watu wasio na hisi ya maumivu. Wao huzaliwa bila kuwa nayo. Je! waonewe kijicho? Mtaalamu wa mwili wa binadamu Allan Basbaum alisema hivi: “Kutokuwa na maumivu hata kidogo ni msiba.”[8]
Kama ungekuwa huwezi kuhisi maumivu, labda hungejua kwamba umepatwa na lengelenge mpaka liwe kidonda kibaya. Kulingana na ripoti moja ya habari, wazazi wa kisichana kimoja ambacho hakikuhisi maumivu yoyote “walikuwa nyakati fulani wakihisi harufu ya mnofu wenye kuchomeka na kukikuta kikiwa kimeegemea jiko bila kujali kitu.”[9] Hivyo, maumivu ni zaidi ya adui mkatili. Yaweza kuwa baraka pia.
Namna gani, basi, juu ya ile ahadi ya Biblia: “Wala maumivu hayatakuwapo tena”? Je! hii ni ahadi ambayo kweli twapaswa kutaka itimizwe?
Je! Kuwe na Maisha Bila Machozi?
Angalia kwamba muktadha wa mstari huu wasema hivi pia: “[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao.” (Ufunuo 21:4) Hili lafaa kufikiriwa, kwa kuwa machozi ni muhimu. Hayo husaidia kutulinda, kama vile hisi ya maumivu itulindavyo.
Machozi huweka macho yetu yakiwa na unyevunyevu na kuzuia jicho na ukope visikwaruzane. Hayo huosha vitu vya kigeni vitoke machoni mwetu. Kwa kuongezea, yana kemikali iitwayo lisozaimu ya kuzuia ukuzi wa viini vibaya, inayoondoa na kuzuia viini vya ambukizo ndani ya macho.[10] Hivyo uwezo wa kutoa machozi ni sehemu ya maana sana ya miili yetu iliyoundwa vizuri ajabu, kama vile hisi yetu ya maumivu ilivyo.—Zaburi 139:14.
Hata hivyo, machozi huhusianishwa sana na huzuni, kihoro, na udhia. “Kila usiku ninanyeshea kitanda changu maji,” akaomboleza Mfalme Daudi wa nyakati za Biblia. “Ninatia malalo yangu maji kwa machozi yangu.” (Zaburi 6:6, Zaire Swahili Bible) Hata Yesu ‘alilia machozi’ kwa kifo cha rafiki. (Yohana 11:35) Mungu hapo awali hakukusudia watu watoe machozi ya huzuni. Dhambi ya mtu wa kwanza, Adamu, ndiyo ya kulaumiwa kwa hali isiyokamilika ya kufa kwa familia ya kibinadamu. (Warumi 5:12) Hivyo, machozi yatokanayo na hali yetu isiyokamilika ya kufa ndiyo ambayo haitakuwapo tena.
Kwa kuwa Biblia hurejezea aina fulani ya machozi yatakayokomeshwa, ile ahadi ya kwamba maumivu hayatakuwapo tena itatimizwaje? Je! watu, angalau pindi kwa pindi, hawatateswa na maumivu yasababishayo huzuni na kulia?