Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 11/22 kur. 20-23
  • Si Mwamba Wala Kisiwa Tena

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Si Mwamba Wala Kisiwa Tena
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mashahidi wa Yehova Waja Wakitembelea Watu
  • Yule Shahidi Arudi
  • Tuliumbwa Tupende na Kupendwa
  • Biblia Inabadili Maisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Familia Iliyonipenda Kikweli
    Amkeni!—1995
  • Niliacha Kupiga Watu Barabarani Nikawa Mhudumu Mkristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Kumkaribia Mungu Kulinisaidia Niwezane na Hali
    Amkeni!—1993
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 11/22 kur. 20-23

Si Mwamba Wala Kisiwa Tena

UBETI kutoka wimbo mmoja wa miaka ya 1960 ulienda hivi: ‘Mimi ni mwamba/Mimi ni kisiwa/Na mwamba hauumii/Na kisiwa hakilii.’ Wimbo huu ulikuwa kipenzi changu maana hivyo ndivyo nilivyoishi. Singeweza kamwe kukumbuka nikipata kuhisi mambo ambayo wengine walisema waliyahisi, kama vile upendo, huruma, na usikitikivu. Nilikuwa nikijihisisha hisia hizo kwa ubandia na kuamini kwamba ndivyo wengine pia walivyofanya. Singeweza kukumbuka nikipata kamwe kulia nikiwa mtu mzima. Na sasa nilikuwa mimi huyu— nimefika miaka 50 nikitumikia kama mzee katika kutaniko la Kikristo, nikiwa peke yangu nyumbani mwangu, nikisongwa koo na vilio vya kwikwi kwa sababu ya kitabu nilichokuwa nikisoma. Hili lingewezaje kuwa likipata “mwamba” huu, “kisiwa” hiki?

Nilizaliwa katika 1936 katika kitongoji cha jiji la Boston, nikiwa wa nne kwa watoto wanane. Baba na mama yangu walikuwa waraibu wa alkoholi. Sisi hatukuzungumza hisia, hatukukumbatiana, wala kuonyeshana upendo kwa njia yoyote niwezayo kukumbuka. Nilipokuwa na miezi sita, mtu fulani alinitia katika hodhi, akaweka kizibo humo, akafungulia maji, akaondoka. Mtunza-nyumba alinipata akaokoa uhai wangu. Mambo pekee niliyohisi nikiwa mtoto yalikuwa hofu, ogofyo kubwa, hasira kali, na maumivu ya kimwili.

Hayo nilifunzwa na baba yangu aliyekuwa akipasuka kwa hasira kali na karibu nyakati zote akaionyesha juu ya mwili wangu mdogo kwa ngumi zake na miguu. Mtazamo wa uso wake nyakati hizo bado hunitisha nusu-karne baadaye. Muda mwingi wa maisha yangu niliamini kwamba nilipata mipigo hiyo kwa sababu nilikuwa mvulana mbaya sana, lakini sasa najua kwamba hasira yake kali iliyoonyeshwa dhidi yangu haikuhusiana katu na kuwa kwangu mwema au mbaya.

Katika mwaka wangu wa tano na wa sita, nilitendwa vibaya kingono na daktari wa familia. Nilipoanza shule, tuliishi katika jiji lenye Waprotestanti Waingereza-Wasaksoni weupe (washiriki 250,000 wa WASP), na wanashule wenzangu walinitesa-tesa na kunifukuza mimi, yule kivulana Myahudi. Wakati ambao magenge haya ya vitoto 10 au 12 yangeweza kunishika, walikuwa wakinivua nguo, kunipiga, na kurusha nguo zangu juu katika vilele vya miti. Nililazimika kuipanda miti nikiwa uchiuchi ili nizipate tena nguo zangu.

Mwezi mmoja kabla ya siku ya kuzaliwa kwangu ya mwaka wa 18, nilijiunga na jeshi ili niondoke nyumbani. Hadi wakati huo sikuwa kamwe nimeonja alkoholi, lakini karibu papo hapo nilianza kunywa na nikaingiwa na uraibu karibu papo hapo. Nilikaa miaka 20 jeshini nikalewa wakati wowote ule ambao ningeweza kuomba, kukopa, au kuiba kiasi cha kununua pombe. Nilioa nikiwa na miaka 24 nikapata mwana, lakini mke wangu na mwanangu waliishi katika nyumba iliyotawalwa na kudhibitiwa na mraibu wa alkoholi—mimi—aliyewaona wao kuwa mzigo na gharama isiyo ya lazima.

Nilistaafu jeshini katika 1974 nikajaribu biashara kwa muda mfupi, lakini upesi nikaacha. Sikuwa tena nikinywa, kwa kuwa mwili wangu haungeweza tena kustahimili alkoholi zaidi. Nilikuwa nikitokwa-tokwa na miwasho na mikuno mikali baada ya pombe moja au mbili tu. Sasa nilikuwa na uraibu wa dawa za kulevya—sana-sana kasumba, lakini pia zile nyingine zilipopatikana. Hii ilifanya isiwezekane mimi kushikilia kazi, kwa hiyo nilikaa kwangu nikatunza nyumba huku mke wangu, Donna, akifanya kazi.

Mashahidi wa Yehova Waja Wakitembelea Watu

Asubuhi moja mke wangu alikuwa akiondoka kwenda kazini. Ilikuwa saa 1:30, nami nilikuwa tayari nimelewa chakari. Hii ilimkasirisha mke wangu. Alipokuwa akienda nje mlango wa mbele alinitupia ishara fulani akapiga kelele hivi: “Afadhali wakuhangaishe mpaka ufe.” Ilikuwa ni ishara aliyokuwa ameiweka dirishani sikuzote na iliyosomeka kwa herufi kubwa, “MWY HAWATAKIWI.” Niliitia katika takataka. Asubuhi iliyofuata wanawake wawili walikuja mlangoni pangu. Walikuwa Mashahidi wa Yehova.

Kufikia wakati huu nilikuwa nimechagua kufuata Dini ya Buddha. Hapo zamani nilikuwa nimeikataa Biblia kwa sababu ya unafiki wa mzazi wangu Myahudi na mwingine Mkatoliki. Nilikuwa nimetafuta Mungu kwa muda fulani lakini nikawa nimechoka kutafuta, nikichukua kwamba hakukuwa na Mungu. Niliamini mageuzi na nikahisi nilikuwa nimethibitisha hakukuwa na Mungu kwa kusimama nje peupe wakati wa radi ya msimu na kutazama juu na kuita Mungu kila jina chafu ambalo ningeweza kufikiria na kusema: “Ikiwa wewe uko, nifyatue nife.” Kama mimi ningalikuwa Mungu, ningalifanya hivyo. Kwa kuwa hakufanya hivyo, nilikata shauri kwamba ni lazima iwe hakuna Mungu. Nilifikiri ulimwengu haungeweza kuepuka maangamizi kwa sababu ya kutoweza kwa mwanadamu kuacha kuuharibu, nami nilikuwa nikitumaini ningeweza kutazama katika televisheni kutendeka kwa yote hayo kwa kubaki nikiwa nimelewa chakari.

Ikawa kwamba, asubuhi iliyofuata wale wanawake wawili walikuja. Nilikuwa nimelewa chakari nikitafuta ufurahisho. Tulifanya maongezi yasiyo na maana kwa karibu dakika 20, yakaisha kwa toleo lao la kitabu kidogo cha samawati kwa senti 25 (za Marekani). Nilikadiria kwamba dakika 20 za ufurahisho zilistahiki kutoa senti 25 na kwa hiyo nikachukua kitabu hicho na kukirusha juu ya meza bila upendezi.

Asubuhi iliyofuata nilikuwa nikitafuta kitu cha kusoma ili niweze kuacha kidogo kuvuta kasumba. Nilikiona kile kitabu kidogo cha samawati nikakiinua, nikitumaini kingeweza kunitumbuiza kwa saa moja hivi. Muda wa saa nne baadaye nilikuwa nimemaliza kitabu hicho na nilisadiki kabisa kwamba kilikuwa sawasawa na vile kichwa chacho kilivyosema: Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Nilikuwa na dawa za kulevya nyumbani humo na nilijua kwamba mara tu niwekapo chini kitabu hicho ningelemewa na dawa za kulevya na kuachilia mbali kila jambo nililokuwa nimesoma. Ukurasa wa mwisho ulitolea watu Biblia kwa dola moja tu, kwa hiyo nikaingiza dola katika bahasha nikaipeleka kwa njia ya posta, nikimwambia Mungu—nilikuwa sijapata kamwe kusali maishani mwangu—“Mungu, hilo tu ndilo niwezalo kufanya, wewe utapaswa kufanya yale mengine.” Niliipeleka kwa njia ya posta, nikalewa chakari, nikaachilia mbali kila jambo lililokuwa limetoka kunivutia sana sasa hivi.

Biblia ilikuja kwa njia ya posta, lakini nikaiweka kando tu. Upesi baada ya hapo, Mashahidi wawili walikuja wakajitolea kujifunza Biblia nami, nikakubali. Mafunzo hayo yalifurahika lakini hayakuwa na maendeleo kwa sababu kwa sehemu kubwa nilijaribu kuwavutia kwa ujuzi wangu wa falsafa. Kwa kuongezea, nilikuwa nikitumia dawa za kulevya mara tu walipoondoka, na hii ilikuwa ikifuta maendeleo yoyote niliyokuwa nimefanya siku hiyo.

Mwishowe, baada ya mwaka mmoja, mmoja wa wale Mashahidi, Jim, alikuja akaniomba nisome Ezekieli 33:9. Nilifanya hivyo, nikisoma hivi: “Walakini ukimwonya mtu mbaya kwa sababu ya njia yake, kusudi aiache; wala yeye asiiache; atakufa huyo katika uovu wake, lakini wewe umejiokoa roho [“nafsi,” NW] yako.” Kisha akaniuliza niliwaza hilo lamaanisha nini. Nikajibu: “Lamaanisha wewe huji tena na mimi nitakufa.” Akasema, “Ndivyo ilivyo,” na kuondoka.

Yule Shahidi Arudi

Naterema kusema niligundua nilikuwa bado na dhamiri—nilikuwa nimeamini nilikuwa nimekwisha kuiua yangu zamani. Kwa kuwa nilihisi tamanio fulani kwa wakati ujao niliokuwa nimeuona katika Biblia, niliamua kujaribu kuacha dawa za kulevya. Nilijaribu nikiwa peke yangu kwa muda wa majuma kadhaa lakini wapi. Jioni moja mke wangu alidokeza nipigie simu “rafiki yule,” akirejezea yule Shahidi, Jim. Nilimwambia mke wangu kwamba mwanamume huyo alikuwa amesema hangerudi, nami sikujua nambari yake ya simu. Nilijihisi hoi.

Siku ileile iliyofuata, tulikuta Mnara wa Mlinzi limepachikwa katika mlango wetu wa mbele huku nambari ya simu ya Jim ikiwa imepachikwa juu yalo. Mke wake alikuwa ameliacha “bila sababu hususa.” Nilimpigia mume wake simu nikaungama tatizo langu la alkoholi na dawa za kulevya na kumuuliza kama angeweza kunisaidia. Aliniambia kwamba ikiwa ningefuliza kuacha dawa za kulevya, angekuja na kujifunza nami kila siku.

Hii ilianzisha kipindi cha funzo lenye bidii lililokula michana na masiku yangu yote. Si kwamba alijifunza nami kila siku tu bali alinigawia pia vitabu vya funzo la Biblia na makala za Mnara wa Mlinzi. Nililala muda wa saa nne tu kila usiku—tatizo la kawaida kwa waraibu wa alkoholi—nami niliutoa wakati wangu mwingine wote uwe wa funzo la Biblia. Dawa za kulevya zilipokwisha kutokomea, yote niliyokuwa nimejifunza mwaka uliopita, kuongezea yote niliyokuwa nikijua kwa kujifunza kwa muda wa saa 18 hadi 20 kila siku, yalipenya mara moja kwenye kina changu.

Kwa kuongezea, nilianza kuhudhuria mikutano yote ya Mashahidi. Mnamo majuma machache tu, nilikuwa nimefanya maendeleo kufikia hatua ya kutoa sala halisi iliyo ya kwanza maishani mwangu, iliyokuwa pia sala yangu ya wakfu. Nilianza kwenda mlango kwa mlango na kuhubiria kila mtu niliyemjua. Mafunzo saba yalianzishwa, na matano kati ya haya yakafanya maendeleo hadi ubatizo, kutia ndani mke wangu na mwanangu. Nilibatizwa kwenye kusanyiko la mzunguko Mei 23, 1976, miezi mitatu tu baada ya mimi kupigia simu “rafiki yule.” Nilianza kupainia (kuhubiri wakati wote) na kuendelea kwa miaka 13.

Hii yanirudisha mahali nilipoanzia hadithi hii—mwenye miaka 50, nikiketi nyumbani peke yangu, nikilia juu ya kitabu fulani. Vitabu vya kujisaidia binafsi vilipendwa sana katika miaka ya 1980, nami nilisoma kimojapo. Kusema wazi, ile sehemu ya kujisaidia binafsi haikunisaidia. Sikuhisi nikiwa na mbetuko wa kufuata kufikiri kwa kilimwengu ambako ilinitolea. Lakini kitabu hicho kilinionyesha kwa mara ya kwanza jinsi nilivyokuwa nimeachiwa ulemavu wa kihisia-moyo na ile miaka iliyotiwa makovu ya utoto wangu na yale mahitaji ya hisia-moyo yaliyonyimwa upendo. Machozi yaliyokuja yalikuwa machozi ya shangwe kwa sababu sasa ningeweza kuelewa ni kwa nini sikuzote sikuwa na uwezo wa kupatwa na hisia-moyo, na pia yalikuwa machozi ya kihoro juu ya hasara kubwa sana niliyokuwa nimepata kwa miaka 50 nikiwa mwanadamu wa kihisia-moyo asiyeweza kuitikia kihisia-moyo. Hiyo ilieleza ni kwa nini nilikuwa nimepatwa na pindi za kushuka moyo muda wote wa maisha yangu.Pole kwa pole, hisia-moyo zilinikumba niliposoma katika Biblia juu ya Yehova na upendo wake, ulio hata kwa ajili yangu, niliokuwa sijapata kamwe kuuhisi. Upendo kwa mke wangu na mwanangu, kwa ndugu na dada zangu katika makutaniko ya Mungu, na pia watu niwahubiriao habari njema ya Ufalme wa Mungu, ili wao pia waipate fursa ya kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Yehova wenye uadilifu ulioahidiwa hapa duniani.

Tuliumbwa Tupende na Kupendwa

Tuliumbwa tupende na kupendwa. Mtoto azaliwapo, yeye huhitaji upendo huu, naye huhitaji kukubaliwa. Mtoto asipopokea upendo na ukubali kutoka kwa wazazi wake, yeye huhisi hapendeki na hana hisia za ustahiki wa kibinafsi. Nilipokuwa mdogo sana, nilikuwa na uchu wa kuinuliwa, kupakatwa, kushikwa-shikwa kwa upenzi. Naweza kukumbuka hata sasa kwamba wageni walipoingia nyumbani, walikuwa wakinitazama nikiwa katika kijizimba changu cha kuchezea, nami nilikuwa nikitumaini wangeniinua. Hawakufanya hivyo kamwe, nami nilikuwa nikianza kulia kwa sababu hakuna mtu aliyeniinua kamwe.

Makovu hayo ya utotoni yalikuwa yameniacha mlemavu katika fungu langu la kimume na nikiwa kichwa cha familia na yalikuwa yameniacha nikiwa siwezi kuamini kwamba Yehova, yule Baba wa kimbingu, angeweza kunipenda. Ile kweli juu ya Yehova ilinibadili pole kwa pole, ikahamisha wazo langu juu yake kutoka kichwani mwangu hadi moyoni mwangu, na sasa mimi najua Yehova anipenda bila mipaka. Pia najua kwamba hakuna njia ambayo sisi twaweza kulipwa upendo huo. Hiyo ni fadhili isiyostahiliwa kutoka kwa Yehova Mungu, yule Mungu wa upendo.

Wazo kuu la kisa chote hiki ni kwamba kwa sababu ya baraka za Yehova, mke wangu na mimi sasa tuna maisha mema. Sasa tunatumikia kwenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme, pamoja na kikutaniko chenye upendo katika ule mji mdogo wenye mandhari ya kupendeza katika milima ya Arizona. Mimi hutumikia nikiwa mwangalizi-msimamizi wa kutaniko, huongoza funzo la kitabu la kutaniko, na pia ni shangwe yangu kubwa kuongoza Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Nina biashara ndogo ya kuosha madirisha iliyo nyongeza kwa malipo yangu ya uzeeni hivi kwamba sisi hupata mahitaji yetu yote ya kimwili na wakati wa kutosha kwa huduma yetu na sehemu ile nyingine ya utumishi wetu kwa Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo.

Ninapotazama nyuma nilikokuwa asubuhi ile mke wangu aliponirushia ile ishara ya “MWY HAWATAKIWI,” ninajawa na shukrani kwa Baba yangu wa kimbingu kwa yale ambayo amenifanyia. Kutoka kuwa mraibu asiyeweza kushikilia kazi na mwenye tumaini moja tu la kuona kila mtu mwingineye akiuawa pamoja nami, sasa mimi ni mshiriki wa tengenezo la Yehova lionekanalo duniani na aliyejifunga wajibu wa kujulisha wengi iwezekanavyo ile habari njema ya Ufalme wa Mungu, tumaini pekee kwa ulimwengu. Pia Yehova amejaza maisha yangu na watu wanipao mambo yale ambayo nimetaka sikuzote: upendo, itibari, na ukubali.

Nami sijaribu tena kuwa “mwamba” usioumia wala “kisiwa” kisicholia.—Kama ilivyosimuliwa na Larry Rubin.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Larry Rubin na mke wake, Donna

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki