Magazeti Yatoayo Faraja Inayotumika
“NINGEPENDA kuwashukuru sana kwa zile makala nzuri sana zenye kutumika ambazo mmetupatia tuzitumie, hasa katika miaka miwili iliyopita. Nilipopokea baadhi yazo, nimelia kihalisi na kumshukuru Yehova kwa sababu wengi wa rafiki zetu katika ile kweli wamehitaji sana habari hizo. Narejezea matoleo kama yale yanayoshughulika na kutenda watoto vibaya, kulelewa katika familia zenye uraibu wa alkoholi, kulalwa kinguvu, na jeuri ya nyumbani.”—Linda W. S., Indiana, Marekani.
Maneno hayo yalikuwa utangulizi wa barua nyingi za kutia moyo ambazo tumepokea miaka ya majuzi kuhusiana na yaliyomo katika magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, yachapishwayo na Watchtower Society na kugawanywa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote.
Tufikiriapo kwamba lile la kwanza lina mwenezo wa zaidi ya nakala 16,000,000 za kila toleo na hutolewa katika lugha 120 na kwamba mwenezo wa lile la mwisho ni karibu 13,000,000 katika lugha 75, basi twaweza kuthamini kishindo cha duniani pote cha magazeti haya. Mashahidi wa Yehova hutolea umma magazeti hayo wanapokuwa katika huduma yao ya nyumba kwa nyumba na wanapotoa ushahidi wa vivi hivi, ambao hurejezea kutoa ushahidi katika pindi zisizo rasmi, kama vile wawapo nje wakinunua vitu, wakinunua petroli kwenye kituo cha petroli, wanaposafiri katika basi, gari-moshi, na ndege, au kwenye wasaa mwingine wowote ufaao katika maisha ya kila siku. Hata hivyo, Mashahidi fulani wamepata vipengele vingine vyenye mafanikio vya kutoa magazeti hayo ambavyo wewe pia ungeweza kuvijaribu.
Kuzuru Mashirika ya Utaalamu wa Kikazi
Mhudumu anayesafiri aliandika juu ya utendaji mbalimbali wenye matokeo wa Shahidi mwingine kama ifuatavyo: “Yeye [dada] amekuwa akihakikisha kukusanya nakala za zamani zaidi za magazeti fulani ya Amkeni! ambazo Mashahidi wengine wamerundika nyumbani. Halafu yeye huzuru mashirika ambayo ahisi yangeweza kupendezwa kipekee na baadhi ya vichwa vilivyomo.” Amezuru mashirika ya aina gani?
“Amekaza fikira juu ya mashirika ya huduma za kijamii, vituo vya ushauri dhidi ya utoaji-mimba, shirika la Uzazi Uliopangwa, madaktari wa akili, wanasaikolojia, idara za polisi, ofisi za kukagua walio chini ya ulinzi wa mamlaka, vitovu vya kushughulikia matumizi mabaya ya dawa za kulevya na alkoholi, vitovu vya kutibu na kuzuia kutendwa vibaya kwa watoto, idara za kuangalia hali njema ya watu (kuuliza juu ya wafanyakazi washughulikiao visa maalumu), idara za afya katika kaunti, vitovu vya kutunza watoto mchana, shule, vitovu vya hospitali kuhusiana na mikazo, na meya wa jiji katika kisa kimoja.” Yeye amepata mafanikio gani?
“Tangu aanze kukaza fikira juu ya shamba hili lisilo na kifani miezi sita iliyopita, ameangusha matoleo 1,784 ya zamani zaidi yenye habari hususa!”
Shahidi huyu hufanyaje ziara hizi kwa wataalamu wa kikazi? Asema hivi: “Nafikiri sababu moja ya ziara hizi kufanikiwa sana, mbali na uhakika wa kwamba hayo magazeti yalizungumzia masuala ambayo watu hawa hushughulika nayo kila siku, ni kwamba sisi tulivalia na kujitokeza kwa namna ya kitaalamu.” Kwa hakika watu wa kitaalamu watatustahi tukiwa na mfikio hakika wa kikazi na tukiwa tumevalia na kujipamba ifaavyo.
Yeye aendeleza usimulizi wake hivi: “Tulikuwa tukitoa Amkeni! juu ya utoaji-mimba (Mei 22, 1993), kwa hiyo nikaamua kutembelea kitovu kilicho dhidi ya utoaji-mimba. Nilianzisha maongezi kwa kutumia kihabari kuhusu mimba iliyoharibiwa ovyo kisha nikaongoza ndani ya lile gazeti, pamoja na Mnara wa Mlinzi. Tulikuwa na mazungumzo mazuri sana hivi kwamba nikatoa pia ile broshua Je! Kweli Mungu Anatujali?, ambayo waliikubali kwa hamu.” Ziara yake iliyofuata ilikuwa ya kwenda kwenye kitovu cha shirika la Uzazi Uliopangwa ambako alifanikiwa hivyohivyo.a
Aina hii ya kuchukua hatua ya kwanza yaweza kuongoza kwenye idadi inayoongezeka daima ya watu wenye mtazamo chanya. Kutokana na barua zilizopokewa twajua kwamba wataalamu wa kikazi huvutiwa mara nyingi na utafiti na mtindo bora wa uandikaji ulio katika magazeti yetu. Hii ni kweli sana hivi kwamba katika nchi fulani, kama vile Suriname, katika Amerika Kusini, Amkeni! hutumiwa na wanafunzi na walimu kama gazeti kuu la kielimu. Mashahidi huko wana kadiri kubwa ya maangusho ya magazeti, na wenye kupendezwa hungoja kila toleo kwa hamu.
Ripoti moja iliyopokewa kutoka Nigeria ilieleza juu ya kituo kimoja cha redio kilichokuwa kikinukuu neno kwa neno lile toleo la Amkeni! juu ya “Wanawake—Wanastahili Staha.” (Desemba 8, 1992) Hiyo yadokeza nini? Kwamba twaweza kuwatolea magazeti hayo wakurugenzi wa redio na vituo vya televisheni kwa mafanikio. Kile tu kinachohitajiwa ni kujifunza kila toleo na kupambanua ni nani walio wataalamu wa kienyeji katika habari zizungumziwazo, wawe ni wanasheria, walimu, washauri, polisi, wauguzi, madaktari, au washirika wa kazi yoyote ya kitaalamu.
Mfikio tofauti umetumiwa na Shahidi ambaye amefungua utoaji wake kwa kuuliza, “Je, wewe wapenda kufanya mafumbo? Watu walio wengi hupenda. Moja ni hili hapa katika toleo la Amkeni! (Januari 8, 1994, au Septemba 8, 1994) lenye kichwa ‘Je! Umepata Kujiuliza?’ Kwa nini usiandike majibu yako kwa maswali hayo, nami nitarudi siku nyingine ili tuweze kuyalinganisha na majibu ya Biblia.” Dada huyo amekuwa na maongezi mengi ya kupendeza kwa msingi wa njia hii na ameanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia.
Dokezo jingine lenye kutumika ni kuonyesha matoleo ya majuzi yenye habari ambazo zingeweza kuvutia mtaalamu wa kikazi unayeongea naye hususa. Linda, aliyenukuliwa hapo kwanza, aliona jambo linalofuata kuhusiana na msimamizi/mshauri katika shule moja yenye programu ya masomo-badala. “Nilipokuwa nikipitia magazeti hayo pamoja na mwanamke huyo, aliona ‘Watoto Walio na Mkazo wa Akili’ akasema, ‘Mungu amekutuma leo!’ Siku hiyohiyo alikuwa na kipindi juu ya jinsi watoto wawezavyo kuepuka mkazo. Alipoona lile jambo lililoonwa katika ukurasa wa nyuma wa gazeti hilo likitangaza Kupata Faida Zote za Ujana Wako, aliomba nakala. Hapo nikamwonyesha nukuu moja kutoka kile kitabu juu ya kujiua, naye akapaaza sauti, ‘Sasa najua kwamba ni Mungu amekutuma hapa!’ Alikuwa ametoka tu kushauri mvulana asiyetaka kuishi. Sasa angekuwa na mengi zaidi ya kumtolea.”
Mambo haya yaliyoonwa yatoa kielezi cha kwamba kwa kuchukua hatua ya kwanza na kujitayarisha pamoja na kuwa na mtazamo chanya, twaweza kufikia watu wengi zaidi na Neno la Mungu la faraja. Kama vile mtume Paulo alivyoandika: “Na ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa rehema, Mungu wa faraja yote; atufarijiye katika dhiki zetu zote ili nasi tupate kuwafariji wale walio katika dhiki za namna zote, kwa faraja hizo, tunazofarijiwa na Mungu.”—2 Wakorintho 1:3, 4.
[Maelezo ya Chini]
a Katika utoaji wake mbalimbali Linda alikuwa mwangalifu kubaki bila kuwamo katika pande za kisiasa za suala la utoaji-mimba. Mashahidi wa Yehova hawavutwi fikira kando kutoka kwenye kazi yao kuu ya kutangaza Ufalme wa Mungu.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Magazeti haya yana habari zenye kutumika kwa mashirika ya huduma za kijamii
[Picha katika ukurasa wa 24]
Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yaweza kutolewa katika hali nyingi