Vijana Huuliza . . .
Je, Utoaji-Mimba—Ndio Suluhisho?
“Matokeo yangu ya kupimwa mimba yalipoonyesha kuwa nilikuwa mja-mzito,” akumbuka Judy, “rafiki yangu mvulana alidai mara moja kwamba nitoe mimba. Hata alinipa fedha kwa ajili ya tendo hilo.” Judy alikuwa mwenye umri wa miaka 17.a
WAKATI Marta mwenye umri wa miaka 15 aligundua kuwa alikuwa mja-mzito, alizungumza na mshauri katika kliniki ya utoaji-mimba. “Alinielezea yote kabisa,” asema Marta. “Alinieleza kuwa ningeweza kutoa mimba, au angenisaidia kupata shirika la kulea watoto au mahali pa kulea watoto haramu, ikiwa hilo ndilo nililotaka.”
Zaidi ya wasichana wabaleghe milioni moja huwa waja-wazito kila mwaka katika Marekani pekee. Watiwao miongoni mwao ni baadhi ya vijana ambao, japo kuzoezwa Kikristo, wamekosa kutii amri ya Mungu ya ‘kuepukana na uasherati,’ au ngono kabla ya ndoa. (1 Wathesalonike 4:3) Ukosefu huu wa adili hutokeza mteseko mwingi usiohitajika. Hata hivyo, wengi wa hawa vijana, huja kughairi mwenendo wao na hutaka kunyoosha maisha yao. Lakini wakikabiliwa na tarajio lenye kuogofya la kupata mtoto nje ya ndoa, wengine huenda wakajiuliza kama utoaji-mimba waweza kuwa suluhisho sahili kwa matatizo yao. Vyovyote iwavyo, kila mwaka wasichana waja-wazito wapatao nusu milioni katika Marekani huchagua kutoa mimba. Je, hili laweza kuwa suluhisho bora kabisa kwa mimba isiyotakwa?
Sababu Inayofanya Wengine Watoe Mimba
Kwa kueleweka, huenda hisia-moyo zenye nguvu, hata zenye kuhitilafiana zikatokeza athari. Mwanamke mchanga huelekea sana kuwa na hisia za kiasili kwa mtoto anayekua ndani yake, lakini huenda pia akawa na hofu na mahangaiko halali.
Kwa kielelezo, Vicky mwenye miaka 18 “alitaka kwenda koleji, pengine hata kupata digrii ya Master’s.” Akilini mwake, mtoto angekatiza mipango yake. (Gazeti ’Teen, Machi 1992) Marta vivyo hivyo alimalizia hivi: “Ikiwa wewe ni mama, wakaa nyumbani na mtoto wako na huwezi kuhudhuria shule tena. Sikuwa tayari kwa ajili ya hilo.” Kulingana na chunguo moja, asilimia 87 ya matineja ambao hutoa mimba huhofu kwamba kupata mtoto kungebadili maisha zao kwa njia ya kutazamisha ambayo hawakujitayarishia.
Hofu ya magumu ya kifedha na hangaiko la kwamba mtu huenda asiweze kushughulikia madaraka ya uzazi bila mwenzi pia ni sababu za kawaida ambazo hufanya wengi wachague utoaji-mimba. Vicky alitaarifu hivi: “Nilitoka katika familia ambayo wazazi walitalikiana, na mama yangu alilea watoto wake watatu akiwa peke yake. Niliona akijikakamua . . . Ningeweza kujiona mwenyewe hatimaye nikiwa mzazi mmoja kama mama yangu.”
Msongo kutoka kwa wengine, hasa kutoka kwa rafiki mvulana, waweza pia kumlazimisha mtu kuelekea kukomesha mimba. Rafiki mvulana wa Judy alimpa mkataa huu: “Ikiwa hutatoa mimba, sitaki kukuona tena kamwe.” Kwa Nancy msongo wa kutoa mimba ulitoka kwa mama yake na vilevile watu wengine wa ukoo.Maoni ya wengi kawaida kwamba utoaji-mimba hautii ndani kuua kitoto hutokeza athari yenye nguvu. Vicky asema: “Singejiacha mwenyewe nikifikirie kuwa mtoto. . . . Nilisoma kwamba katika juma la tano la mimba, kijusu ni kidogo zaidi ya kucha ya kidole chako cha mwisho. Nilishikilia kwa nguvu sana wazo hilo. Nilijiambia kuwa ikiwa kilikuwa ukubwa wa kucha ya kidole cha mwisho, hakikuwa mtoto kwa kweli. Nilijaribu kufanya isiwe halisi akilini mwangu ili niweze kutoa mimba.”
Wengine pia hudai kuwa, angalau katika mataifa yaliyoendelea kiufundi, utoaji-mimba ni salama—eti salama zaidi ya uzaaji-mtoto kwa wabaleghe waja-wazito. Baada ya kufikiria sababu zote zenye kufaa, basi, utoaji-mimba waweza kuonekana wenye kutamanika. Hata hivyo, uhakika wa mambo waonyesha kwamba wengi wachaguao utoaji-mimba hughairi baadaye. Asema mwanamke mmoja: “Nilitoa mimba nilipokuwa na miaka 20. Sasa nina 34, na ni vigumu kwangu kushughulika na matatizo ya nililofanya. Nilitaka mtoto wangu, lakini rafiki yangu mvulana hakutaka. Bado ninapata mkazo mwingi wa kihisia-moyo; maumivu yako pamoja nawe kwa maisha yako yaliyobaki.”
Majeraha ya Kihisia-Moyo
Badala ya kuwa njia rahisi ya kutokea, utoaji-mimba waweza kukuza magumu ya mtu. Kwanza kabisa hupingana na hisi ya ndani ya lililo sawa na lisilo sawa—dhamiri ambayo Mungu aliiweka katika jamii ya kibinadamu. (Warumi 2:15) Zaidi ya hilo, utoaji-mimba huhitaji mwanamke mchanga ajizuie mwenyewe kutokana na hisi ya huruma nyororo juu ya uhai duni unaokua ndani yake. (Linganisha 1 Yohana 3:17.) Yasikitisha kama nini!
Marta asema: “Haikuwa hadi majuma kadhaa yalipopita [baada ya kutoa mimba] ndipo nilipoanza kuhisi hatia na aibu fulani kwa nililokuwa nimetenda.” Mambo yalikuwa magumu hata zaidi wakati Februari ilipokuja—mwezi ambao mtoto angelizaliwa. Eliasa aeleza: “Miaka 15 iliyopita nilitoa mimba. Kufuatia hilo, nilipata mshuko wa moyo mbaya sana na nililazimika kutibiwa katika kliniki mara kadhaa. Hata nilitaka kujiua.”
Ni kweli, si wanawake wachanga wote waitikiao hivyo. Wengi kwa moyo mweupe huamini kwamba kijusu si uhai wa kibinadamu. Lakini je, Muumba—“chanzo cha uhai”—asema nini kuhusu hili? (Zaburi 36:9, NW) Biblia husema wazi kwamba kwa Yehova Mungu mtoto ambaye hajazaliwa bado aliye ndani ya tumbo la uzazi ni zaidi ya mnofu wa kijusu tu. Alimpulizia Mfalme Daudi kuandika hivi: “Macho yako yaliniona kabla sijakamilika, chuoni mwako ziliandikwa zote pia.” (Zaburi 139:16) Hivyo Muumba huona hata kiinitete kuwa mtu aliye pekee, binadamu anayeishi. Kwa sababu hii, alitaarifu kuwa mtu angetozwa kwa sababu ya kuumiza mtoto asiyezaliwa bado. (Kutoka 21:22, 23) Ndiyo, kwa maoni ya Mungu, kuua mtoto asiyezaliwa bado ni kutoa uhai wa kibinadamu. Kwa hivyo, msichana anayetaka kumpendeza Mungu, hawezi kufikiria utoaji-mimba kuwa chaguo linalokubalika—licha ya msongo unaowekwa juu yake.b
Kupata Utegemezo
Judy, aliyetangulia kutajwa, alichagua kutotoa mimba ya mtoto wake. Yeye asema hivi: “Dada yangu mkubwa alitambua, na toka mwanzoni, alikuwa mwenye kutegemeza, hasa kihisia-moyo. Hata alisema angeendelea kunitegemeza baada ya mimi kupata mtoto. Hilo tu ndilo nililohitaji kusikia ili nifanye jambo nililohisi kuwa sawa ndani kabisa ya moyo wangu. Niliendelea na mipango yangu na kupata mtoto.” Hiyo ilikuwa miaka tisa iliyopita. Akimtazama mwana wake mwenye umri wa miaka minane, Judy asema: “Kutoa mimba kungelikuwa kosa kubwa zaidi ya yote katika maisha yangu.”
Mwanamke mmoja mchanga aitwaye Natisa vilevile aeleza hivi: “Miaka mitano iliyopita nilikuwa nimeketi katika kliniki ya utoaji-mimba, nikingoja zamu yangu. Badala ya kuchukua zamu yangu, nilifikiri tena na kutoka katika kliniki hiyo. Sasa nina mwana mwenye kupendeza aliye na miaka minne, mtoto mwingine atazaliwa karibuni, na nimeolewa na baba mwenye upendo.”
Yeyote anayekabiliwa na mimba nje ya ndoa, hapaswi kufanya uamuzi bila kufikiri. Hata hali ionekane kuwa mbaya jinsi gani, hali hiyo haijakosa tumaini kabisa. Lakini kwa hakika watu kama hao wanahitaji utegemezo na mwongozo mkomavu. Mtu kutoa moyo kwa wazazi ni mwanzo mzuri, hasa ikiwa wao ni Wakristo. (Mithali 23:26) Ni kweli, bila shaka wataumia kihisia-moyo na kukasirika mwanzoni. Lakini, hatimaye yaelekea watasukumwa kusaidia. Kwa kielelezo, huenda wakapanga kwa ajili ya utunzaji wa kabla ya kuzaa. Wanaweza kusaidia pia kutumia mipango yoyote ya kiserikali inayopatikana kwa wale wanaostahili kupata. La maana zaidi, wanaweza kutia moyo mkosaji ili apokee msaada wa kiroho unaohitajika kutoka kwa wazee wa kutaniko.—Yakobo 5:14, 15.Akina mama wasioolewa wamechagua kuwapa walezi watoto wao, wakihisi kwamba hawangeweza kumtolea mtoto utunzi ufaao. Ingawa kulelewa watoto kwa hakika ni bora kuliko kumaliza uhai wa mtoto, Mungu humwia mzazi daraka la ‘kutunza walio wake.’ (1 Timotheo 5:8) Mzazi asiye na mwenzi huenda asiweze kumpa mtoto wake mema kabisa kimwili, lakini aweza kutoa kitu cha maana hata zaidi—upendo. (Mithali 15:17) Kwa hiyo katika hali nyingi ingekuwa vema kwa mama asiyeolewa kumlea mtoto huyo mwenyewe.
Namna gani ile kazi ya kulea kitoto—na mabadiliko makubwa katika mtindo-maisha ambayo bila shaka yatalazimika kufanywa? Yote haya huenda yakaonekana kuwa yenye kushinda. Hata hivyo, Biblia huandaa shauri lenye kutumika ambalo laweza kusaidia watu washughulike na magumu haya. Akina mama wasioolewa ambao ni wenye kutubu waweza kunufaika pia kutokana na msaada wa kiroho unaotegemezwa kwa uthabiti na Neno la Mungu. Ndiyo, kwa utegemezo wenye upendo na mwongozo ufaao, hawa waweza kushughulikia hali vizuri iwezekanavyo.c Utoaji-mimba katu sio suluhisho!
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
b Yeyote aliyekosea wakati uliopita na kutoa uhai usiozaliwa bado, hahitaji kuamua kwamba hakuna tumaini la kupata ukubali wa Yehova. Watu kama hao waweza kuwa na uhakika kwamba Yehova hutegemeza watenda-makosa wenye kutubu na ‘husamehe kabisa.’ (Isaya 55:7) Ingawa huenda majeraha ya kihisia-moyo yakaendelea kudumu, mtunga-zaburi atoa hakikisho hili: “Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi.”—Zaburi 103:12.
c Ona Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1981, “Wazazi Wasio na Wenzi Wanashindana na Matatizo ya Ulimwengu wa Leo.” Pia, ona “Vijana Huuliza . . . Akina Mama Wasioolewa Waweza Kushughulikiaje Hali Yao Vizuri Iwezekanavyo?” katika toleo la Amkeni! la Oktoba 8, 1994.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Rafiki-wavulana mara nyingi hujaribu kusonga wasichana watoe mimbay