Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g95 5/22 kur. 19-23
  • Utafutaji Wangu Wenye Mafanikio wa Maana ya Uhai

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Utafutaji Wangu Wenye Mafanikio wa Maana ya Uhai
  • Amkeni!—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ushirika Wangu na Theodore Dreiser
  • Naanza Utafutaji Wangu wa Maana
  • Nilisadiki Nilikuwa Nimepata Maana ya Uhai
  • Dreiser na Mashahidi wa Yehova
  • Kumkumbuka Muumba Wetu Kutoka Ujanani Kuendelea
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Kazi Nyingi za Akina Mama
    Amkeni!—2002
  • Kwa Sababu tu ya Tabasamu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Upendo Unawatambulisha Wakristo wa Kweli​—Linda Umoja Wetu Wenye Thamani
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2018
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1995
g95 5/22 kur. 19-23

Utafutaji Wangu Wenye Mafanikio wa Maana ya Uhai

ULIKUWA mwaka wa 1951. Umati wa watu uliojipanga barabarani ili upate kuona wacheza sinema wengi mashuhuri wa jukwaani na wa kiwamboni huku gari moja baada ya jingine likipita kuelekea Jumba la Maonyesho ya Sanaa katika Beverly Hills, California. Pindi muhimu ilikuwa wonyesho mkuu wa A Place in the Sun, uliotegemea riwaya maarufu ya binamu yangu Theodore Dreiser iliyoitwa An American Tragedy. Ilikuwa mshindanaji mwenye nguvu kwa ajili ya tuzo itunukiwayo filamu bora zaidi iliyotolewa na Paramount Pictures kwa mwaka huo na ilielekezwa na George Stevens, mmoja wa wakurugenzi wayo bora zaidi. Ilionyesha watatu wa wacheza sinema mashuhuri wa wakati huo, Elizabeth Taylor, Montgomery Clift, na Shelley Winters. Kwa nini nilikuwa pale katika moja ya magari hayo makubwa, yakipita kati ya umati wa watu wenye kupiga mayowe? Na kwa nini nilihisi kutofaa kabisa katika mazingira hayo? Acheni turudi nyuma hadi mwanzoni ili tuone ni nini kilichoongoza kwenye pindi hii.

Nilizaliwa katika moja ya vipindi vyenye maana sana katika historia yote—Oktoba 1914. Katika siku ya 20 ya mwezi huo saa kumi na nusu alasiri, nyumbani mwetu katika Seattle, Washington, nilizaliwa kwa msaada wa daktari.

Katika siku hizo familia yetu iliishi kwenye Alki Beach katika sehemu iliyoitwa Bonair. Baada ya muda mfupi familia yetu ikakua na kufikia washiriki watano, ikiwa na wazazi wangu, ndugu yangu mkubwa na mdogo, na mimi. Tuliishi katika nyumba kubwa yenye kupendeza iliyokuwa ikiangaliana na bichi, ambayo iliandaa mandhari yenye kuvutia mno ambapo mtu angeweza kutazama meli na feri zikipita kwenye maji ya Puget Sound kati ya Seattle mjini na majiji mengine njiani.

Kufuatia kudidimia kwa soko la hisa katika 1929, hali ya kiuchumi ilikuja kuwa mbaya sana hivi kwamba tulibadilishana nyumba yetu kwenye Alki Beach na duka la chakula katika sehemu ya Seatle iitwayo Highland Park, ambalo lilitupatia mapato machache wakati wa ile miaka ya Mshuko mkubwa wa kiuchumi.

Katika 1938 mama yangu alikufa, akimwacha baba yangu akiwa peke yake kabisa kuendesha duka hilo. Nilijiunga naye katika biashara hiyo, na tukalibadili kuwa soko la kisasa la chakula. Mara tukawa na biashara iliyoendelea vyema.

Halafu likaja shambulio la Pearl Harbor katika Desemba 7, 1941, na muda mfupi baadaye nilijikuta nikikabili uandikishaji wa wanajeshi wapya na Vita ya Ulimwengu 2. Ilitubidi kuiuza biashara hiyo, ambayo ilimpa baba yangu fedha chache za kujipatia mahitaji ya lazima, na nikajitolea kwenda jeshini siku chache tu kabla ya kuchaguliwa. Kwa kweli, kwenda jeshini kulisumbua dhamiri yangu, na nakumbuka jinsi nilivyosali kwa Mungu anisaidie niepuke kuua mtu yeyote. Baada ya mazoezi ya msingi, nilipewa mgawo kwenda kwenye Jeshi la Usafirishaji. Hatimaye nilipandishwa cheo kuwa luteni wa pili.

Ushirika Wangu na Theodore Dreiser

Kufikia sasa ilikuwa 1945, na nilipewa mgawo kwenda kwenye Bandari ya Kupakia Vitu Chomboni katika Los Angeles, ambapo nilitumika kuwa ofisa wa usalama wa mizigo kwenye meli zilizokodiwa na jeshi ili kusafirisha ugavi na wanajeshi wachache hadi maeneo yaliyokuwa katika Pasifiki. Kati ya migawo nyakati fulani ningetembelea binamu yangu Theodore Dreiser na mke wake, Helen. Walikuwa na nyumba kubwa katika West Hollywood na walikuwa wakarimu mno kunielekea katika pindi hizo. Dreiser alikuwa na akili yenye kutafuta sana na alipenda kujaribu kujua maoni yangu juu ya nililowazia kuhusu sehemu nilizozuru.

Bila shaka, Dreiser alijua kwamba nilikuwa pia binamu ya Mbunge Martin Dies wa Texas, mwenyekiti wa Kamati ya Dies, mtangulizi wa Un-American Activities Committee. Wengi wa Waandikaji na wataalamu wengine katika biashara ya sinema walitendewa kikatili kwa ajili ya maelekeo ya Kikomunisti, na Dreiser hakuponea, kwa kuwa alijulikana kuwa mwenye kupendelea Warusi. Kwa hiyo wakati wa ziara zangu za kwanza, aliniuliza: “Je, wewe hushiriki maoni sawa na huyo binamu yako, Martin Dies?” Nilimhakikishia kwamba sikuwa na uhusiano wowote na Martin wala na malengo yake yoyote ya kisiasa, jambo ambalo lilifanya uhusiano wangu na Dreiser uwe wa kirafiki zaidi.

Baada ya Japani kusalimu amri, Septemba 2, 1945, niliamua kubaki kwa kitambo kidogo jeshini, kwa sababu nilikuwa nikiendelea kuona sehemu zenye kupendeza za ulimwengu. Mara nikapandishwa cheo na kuwa luteni wa kwanza na kupewa mgawo wa kuwa ofisa mwenye kusimamia mahali pa kuweka ugavi kwenye moja ya meli kubwa za wanajeshi. Nilipokuwa bado Japani, nilichukua likizo na kusafiri kupita katikati ya Japani kutoka Yokohama hadi Hiroshima, ambapo ile bomu ya atomi iliharibu jiji hilo.

Asubuhi niliyofika katika Hiroshima, niliona watu bado wakilala katika mabustani ya kupumzikia kwa ukosefu wa nyumba. Bila shaka, nilihisi kusumbuka mno kutembea sehemu hiyo, kwa kuwa ilikuwa wazi kwamba kihalisi kila mtu niliyekutana naye alikuwa amepoteza watu wa ukoo na marafiki katika teketezo hilo la umati lenye kuogofya. Umivu kali nililoona katika nyuso zao, na vilevile chuki halisi au niliyowazia kuwa niliona katika macho yao kuelekea wengine wetu tuliokuwa wenye yunifomu, lilikuwa jambo lenye kuumiza moyo.

Naanza Utafutaji Wangu wa Maana

Kwa sababu ya Hiroshima na visa vingine vingi vya ugonjwa na umaskini nilivyoona, nilianza kusababu kuhusu maana ya uhai. Kuwa melini katika bahari kuliandaa wakati mwingi sana wa kufikiria kuhusu mambo hayo. Katika pindi fulani, ningeweza kuongea na kasisi aliyekuwa melini ili kuona kama angeweza kujibu baadhi ya maswali yangu kuhusu ukosefu wa haki maishani. Hakuna hata mmoja wa makasisi hao aliyekuwa na majibu yenye kuridhisha.

Theodore Dreiser alikufa katika Desemba 1945, baada ya kutumia muda wote wa maisha akitafuta maana ya uhai. Katika insha yake iliyokuwa na kichwa “Muumba Wangu,” yeye alikiri hatimaye kwamba hakuwa karibu na suluhisho wakati huo kuliko wakati wa mwanzoni. Helen Dreiser, mjane wake, pia binamu yangu, alikuwa akifanyia kazi historia yake ya maisha, ambayo ingekuwa na kichwa My Life With Dreiser. Alikuwa amenisihi kwa muda nije Hollywood kumsaidia kutayarisha hati yake kwa ajili ya uchapishaji na kushughulikia baadhi ya shughuli za kibiashara pamoja na maajenti tofauti-tofauti kuhusiana na kichapo cha uandishi wa Theodore, ambacho kilikuwa kikitokezwa katika nchi nyingi. Kwa hiyo katika Desemba 1947, niliondoka jeshini na kuanza kuishi kwenye makao ya Dreiser katika West Hollywood.

Lakini sikuacha utafutaji wangu wa maana ya uhai. Helen Dreiser pia alikuwa akitafuta uelewevu wa kiroho wa uhai, na hivyo tulianza kuzuru vikundi tofauti-tofauti, tukitafuta jambo lililokuwa na maana. Hakuna kimoja cha vikundi hivyo kilichokuwa na majibu yenye kuridhisha.

Baadaye, tulipokuwa katika Gresham, Oregon, tukimtembelea mama ya Helen, nilijulishwa kwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova ambaye aliimba kwa kinanda cha nguvu za umeme katika baadhi ya hoteli kubwa katika Portland. Tuliingia katika mazungumzo kuhusu dini, na mengi ya mambo aliyosema yalionekana yakiwa na maana. Alipodokeza kwamba mmoja wa wahudumu wao atutembelee tuliporudi Los Angeles, nilikubali kwa utayari.

Tuliporudi Los Angeles, mara tulitembelewa na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alitupangia tuwe na funzo la Biblia la kila juma pamoja na Shahidi mwingine na mke wake, ambao wote wawili walikuwa mapainia (wahudumu wa wakati wote). Mwanzoni funzo halikuendelea vizuri sana kwa sababu ya baadhi ya mawazo yangu ya mwanzoni, lakini haya yaliondoshwa mara kwa kusababu kiakili juu ya Biblia.

Sasa ilikuwa mapema 1950, na kulikuwa na upendezi mwingi katika uandishi wa Dreiser wakati huo. Paramount Pictures ilikuwa katika taratibu ya kutokeza sinema mbili za riwaya za Dreiser zenye kupendwa zaidi ya zote: An American Tragedy, ambayo ingeitwa A Place in the Sun, kwa ajili ya kutolewa katika 1951, na Sister Carrie, kwa ajili ya kufuatia kutolewa chini ya kichwa Carrie katika namna ya filamu. Sinema hizi zilikuwa washindanaji wa tuzo ya kutunukiwa filamu bora zaidi kwa miaka miwili mfululizo. Kwa hiyo ulikuwa mwaka wenye maana kwa Helen, na akiwa amamemaliza hati yake iliyokuwa na kichwa My Life With Dreiser, aliondoka kuelekea New York City, ambapo alikuwa akutane na maafisa wa World Publishing Company, ambayo ilikuwa ichapishe hati yake.

Nilisadiki Nilikuwa Nimepata Maana ya Uhai

Wakati hakuwepo, niliendelea na funzo langu la Biblia, kwa wakati nilijifunza jinsi ilivyokuwa kwenda mlango kwa mlango ukizungumza kuhusu Biblia. Kufikia wakati Helen Dreiser aliporudi kutoka New York, nilikuwa na uhakika kwamba hatimaye nilikuwa nimepata maana ya uhai, ambayo nilikuwa nikitafuta. Lakini ilishangaza kama nini Helen alipotangaza kwamba hakutaka lolote lililohusiana na funzo la Biblia! Kwa wazi mashirika yake katika New York yalimsadikisha kwamba lile alilokuwa akijifunza katika Biblia halikupendwa sana na ulimwengu. Yeye alisema hivi waziwazi: “Funzo la Biblia huondoa kila sehemu ya maisha.” Kwa hiyo akakataa kuendelea kujifunza Biblia nasi.

Kufikia sasa ilikuwa wazi kwamba ingekuwa kinyume cha kweli mimi kubaki katika kambi ya kijeshi. Nilikuwa nimeazimia kubatizwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ubatizo wa kipekee ulipangwa kwa ajili yangu kwenye nyumba ya Shahidi fulani ambaye alikuwa na kidimbwi cha kuogelea. Nikiwa nimejiweka wakfu kwa Yehova, nilibatizwa Agosti 19, 1950. Halafu nikaandikia jeshi kuwaeleza kwamba kwa kuwa nilikuwa mhudumu rasmi, singeweza tena kutumikia katika kambi ya kijeshi. Ingawa kuacha kwangu kazi kulikataliwa mwanzoni, miezi michache baadaye, nilikubaliwa kuondolewa kiheshima.

Wakati huohuo, Paramount Pictures ilikuwa karibu kutoa A Place in the Sun, na Helen nami tulialikwa kwenye mlo wa faragha ulioandaliwa na mkurugenzi George Stevens. Tulielezwa kwamba wonyesho wa kwanza ulimwenguni ungefanywa kwenye Jumba la Maonyesho ya Sanaa katika Beverly Hills, na mipango ilikuwa ikifanywa kwamba tufikapo kwenye jumba la maonyesho, Helen, akiwa mke wa mwandishi, angeongea katika redio ya kitaifa. Huu ulikuwa uwe usiku mkubwa zaidi ya wote kwa binamu yangu, na nilitarajiwa kuandamana naye. Kwa hiyo katika saa iliyowekwa, tulikodi gari, na katika upambo wetu wote, tukaelekea hadi jumba la maonyesho. Tulipita polepole katikati ya umati wa watu waliojipanga barabarani, wakitumaini kuona baadhi ya wacheza sinema mashuhuri waliotarajiwa kufika kwa ajili ya wonyesho huo.

Nilihisije juu ya sehemu yangu katika wonyesho huo wenye ushaufu? Katika nyakati zilizopita, nilikuwa nimeona matukio ya aina hiyo katika sinema na nilikuwa nimejiuliza ingekuwaje kuwa katika mwangaza wa aina ile. Lakini sasa, nikiwa nimepata ujuzi wa kweli, nilijihisi kutofaa mahali hapo. Labda nilihisi ukosefu wa kibali cha Yehova kwa mambo hayo kulingana na yale ambayo Biblia husema kwenye 1 Yohana 2:16, NW: “Wonyesho wa mtu kujivunia njia yake ya kutegemeza uhai . . . hautokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.” Ilikuwa rahisi kuona kwamba mmeremeto na uzuri huo wenye kudanganya ulikuwa kinyume cha njia yangu mpya ya maisha ya Kikristo. Ijapokuwa nilifurahia sinema hiyo bora mno, nilihisi pumziko tukio hilo lote lilipoisha.

Muda mfupi baada ya hapo, Helen Dreiser alipata mshtuko wa akili uliomfanya apooze nusu. Mshtuko wa akili wa pili ulifanya iwe vigumu kwake kuendelea na shughuli za kibiashara zaidi. Dada yake Myrtle Butcher alitoa ombi ili apate ruhusa ya kuwa mtunzi wake na alitaka kumchukua hadi nyumbani kwake mwenyewe katika Gresham, Oregon. Sikubishania ombi hilo, kwa kuwa nilihisi ingekuwa bora zaidi kwa Helen, ambaye angekuwa na uhitaji wa utunzi mwingi, ambao dada yake angeweza kuandaa. Kwa hiyo sasa nilikosa kazi. Nilikuwa nifanye nini? Nilikuwa na uhakika katika maneno ya Yesu kwenye Mathayo 6:33, NW: “Basi, fulizeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote mtaongezewa.”

Kwa kuwa nilikuwa mimi peke yangu kujitunza, baba yangu akiwa amekufa miezi michache iliyokuwa imepita, nilitaka kumtumikia Yehova kwa wakati wote. Karibu mara hiyo tu, nilithawabishwa kwa toleo la kazi isiyo ya wakati wote, ambayo ilinipa kile nilichohitaji tu ili kuanza kumtumikia Yehova nikiwa mhubiri wa wakati wote wa habari njema ya Ufalme wa Mungu. Kama alivyosema Yesu ingekuwa hivyo, Yehova amenitunza miaka hii yote zaidi ya 42 ambayo nimekuwa katika utumishi wake wa wakati wote.

Katika kiangazi cha 1953, nilihudhuria mkusanyiko wangu wa kwanza wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova, katika Yankee Stadium katika New York City, na jinsi hilo lilivyokuwa ono zuri! Kufikia wakati huo nilikuwa nimemaliza mwaka wangu wa kwanza nikiwa painia, na huku nikiwa na furaha mno katika kazi hiyo ya kueneza evanjeli, nilikuwa na tamaa ya kufikia ushiriki mkubwa hata zaidi katika utumishi wa Ufalme. Mapema nilikuwa nimetoa ombi kwa ajili ya utumishi wa wakati wote kwenye makao makubwa ya Sosaiti, na sasa katika mkusanyiko huu nilitoa ombi kwa ajili ya mazoezi ya umishonari kwenye Watchtower Bible School of Gilead. Muda mfupi baada ya kurudi Los Angeles, jinsi nilivyoshangaa kupata mwaliko wa kutumikia kwenye makao makubwa ya Sosaiti, yaitwayo Betheli!

Nikiwa na hisia zilizochanganyika niliingia Betheli Oktoba 20, 1953, nikijiuliza vile ingekuwa na kama ningekuwa mwenye furaha kama nilivyokuwa nilipokuwa painia. Lakini miaka yote iliyopita 41 ya utumishi wangu wa Betheli, sijapata kusikitika kwa kufanya uamuzi huo. Mapendeleo mengi ambayo nimefurahia nikiwa Betheli yameniletea shangwe kubwa mno na furaha kuliko ile ambayo ningepata katika aina nyingine yoyote ya utumishi wa Ufalme.

Katika 1955, Helen Dreiser alikufa, nami nikawekwa rasmi kuwa msimamizi na hatimaye nikawa mdhamini wa mali zake. Katika kuandika wosia wake, Theodore Dreiser alikuwa ameachia kila kitu mke wake, na kushughulikiwa kwa mali zake kulihusisha haki za uandishi wake wote ulionukuliwa. Helen alikuwa ameniambia kwamba Dreiser alikuwa msomaji wa kawaida wa Biblia, na katika kupitia maktaba yake, niliona kwamba nyakati fulani yeye angenakili pambizoni mwa Biblia yake kuhusu fasiri ya badala katika tafsiri nyingine za Biblia.

Dreiser na Mashahidi wa Yehova

Bila shaka, sikujua lolote kuhusu Mashahidi wa Yehova nilipokuwa na mazungumzo pamoja na Dreiser, lakini niligundua baadaye kwamba alijua kuhusu msimamo wa kutokuwamo wa Mashahidi wa Yehova. Katika kitabu chake chenye kichwa America Is Worth Saving, aliwasifu kwa msimamo wao juu ya suala la kusalimu bendera. Dreiser hakuwa mwoga wa kuchukua msimamo thabiti juu ya jambo aliloamini, na ikiwa ningalikuwa nimejua Biblia kama niijuavyo sasa, yamkini tungalikuwa na mazungumzo yenye kupendeza sana.

Nikitazama nyuma miaka 45 tangu nianze kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, naweza kusema kwa weupe wa moyo kwamba kwa kweli nimepata maana ya uhai ambayo nilikuwa nikitafuta. Maswali yangu kuhusu ukosefu wa haki katika maisha yalijibiwa kwa kujua kwamba mungu na mtawala wa ulimwengu huu ni Shetani Ibilisi, wala si Mungu mwenye upendo na mweza yote, Yehova. (Yohana 14:30; 2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 4:8) Na ni kisababishi cha shangwe kama nini kujua kwamba Ufalme wa Mungu ulisimamishwa mbinguni katika Oktoba 1914 na kujua kwamba karibuni utachukua utawala wa dunia na kuondosha kazi za Ibilisi!—1 Yohana 3:8; Ufunuo 20:10.

Kwa wakati uliopo, kumjua Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja naye, na kuwa na maisha yenye umaana katika utumishi wake wa Ufalme kwaweza kufananishwa na lulu ambayo mfanya biashara aliipata katika safari zake. Hiyo lulu ilikuwa na thamani ya juu mno hivi kwamba aliuza vyote alivyokuwa navyo ili tu aipate.—Mathayo 13:45, 46.

Nikiwa nimepata hazina kama hiyo, nathamini maneno ya mtunga zaburi Daudi: “Nikae nyumbani mwa BWANA siku zote za maisha yangu. Niutazame uzuri wa BWANA, na kutafakari hekaluni mwake.” (Zaburi 27:4)—Kama ilivyosimuliwa na Harold Dies.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kwa kweli, kwenda jeshini kulisumbua dhamiri yangu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kutumikia katika Betheli tangu 1953

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki