Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g95 6/22 kur. 4-6
  • Sababu ya Wengi Kuamini Ulimwengu Utakwisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sababu ya Wengi Kuamini Ulimwengu Utakwisha
  • Amkeni!—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Vyanzo vya Kibiblia
  • Biblia na Mwisho wa Ulimwengu
  • Uelewevu wa Kimakosa wa Karne ya Kwanza
  • Wengine pia Wahitaji Sahihisho
  • Ufunuo—Wakati Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Je, Ulimwengu Utakwisha Karibuni? Apokalipsi Ni Nini?
    Habari Zaidi
  • Ufunuo Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Ufunuo—Upeo Wao Wenye Furaha!
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1995
g95 6/22 kur. 4-6

Sababu ya Wengi Kuamini Ulimwengu Utakwisha

KWA kweli ulimwengu uko katika hali ya kukata tamaa, kama wengi leo wakubalivyo haraka. “Nimeuliza watu kutoka sehemu tofauti-tofauti za ulimwengu wanachofikiri kuhusu uwezekano wetu wa kuwa na matokeo mazuri kwa wakati ujao,” mwevanjelisti Billy Graham aliandika. “Wengi wao wana maoni hasi kuhusu wakati ujao. . . . Kwa kawaida maneno ‘Har–Magedoni’ na ‘Apokalipsi’ yanatumiwa kufafanua matukio kwenye mandhari ya ulimwengu.”

Kwa nini maneno “Har–Magedoni” na “apokalipsi” yanatumiwa mara nyingi kufafanua hali ya leo ya ulimwengu? Yana umaana gani?

Vyanzo vya Kibiblia

Biblia husema juu ya “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” na huhusianisha vita hii na mahali “paitwapo kwa Kiebrania, Har–Magedoni.” (Ufunuo 16:14-16) Webster’s New Collegiate Dictionary hufafanua Har–Magedoni kuwa: “pigano la mwisho na la kukata maneno kati ya mamlaka za wema na za uovu.”

Ingawa “Apokalipsi” latoka kwenye neno la Kigiriki linalomaanisha “ufunuo,” au “kufunuliwa,” limechukua maana nyingine. Kitabu cha Biblia cha Ufunuo, au Apokalipsi, hukazia uharibifu wa Mungu juu ya waovu na Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Mwana wake, Yesu Kristo. (Ufunuo 19:11-16; 20:6) Hivyo, Webster’s New Collegiate Dictionary hufafanua “apokalipsi” kuwa “msiba wa mwisho wa ulimwengu mzima ulio karibu kutokea ambao katika huo Mungu aharibu mamlaka za uovu zinazotawala na kuinua waadilifu kwenye uhai katika ufalme wa kimesiya.”

Watu wazungumzapo leo juu ya ulimwengu na hali yao, kwa wazi wanaathiriwa na kile kinachosemwa katika Biblia. Biblia hasa husema nini kuhusu mwisho wa ulimwengu?

Biblia na Mwisho wa Ulimwengu

Biblia kwa wazi hutabiri mwisho wa ulimwengu. Yesu Kristo na wanafunzi wake walisema juu ya wakati wa mwisho. (Mathayo 13:39, 40, 49; 24:3; 2 Timotheo 3:1; 2 Petro 3:3; King James Version) Hata hivyo, hawakumaanisha kwamba dunia yenyewe itaharibiwa. Kuhusu dunia halisi, Biblia yasema hivi: “Haitafanywa itikisike hata wakati usio dhahiri, au milele.” (Zaburi 104:5, New World Translation) Maneno “mwisho wa ulimwengu” kwa usahili humaanisha “umalizio wa mfumo wa mambo.”—NW.

Mtume Petro alisema juu ya ulimwengu wa kabla ya Furiko katika siku ya Noa na kusema: “Ulimwengu wa wakati huo ulipatwa na uangamizo ulipogharikishwa kwa maji.” Halafu Petro aliendelea kusema kwamba ulimwengu wetu wa wakati huu ‘umewekwa akiba mpaka siku ya hukumu na ya uangamizo wa watu wasiomwogopa Mungu.’ (2 Petro 3:5-7, NW) Mtume Yohana pia aliandika hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye afanyaye mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:17, NW.

Wakati wa mwisho wa ulimwengu huu, mtawala wao asiyeonekana na asiyemwogopa Mungu atafungwa pia. (Ufunuo 20:1-3) Mtume Paulo aliandika kuhusu huyo mtawala mwovu hivi: “Mungu wa ulimwengu huu amepofusha akili zao ambao hawaamini.” Yesu alisema hivi kumhusu: “Sasa ndio mwana-mfalme wa ulimwengu huu [Shetani Ibilisi] atatupwa nje.”—2 Wakorintho 4:4; Yohana 12:31; KJ.

Je, haitakuwa baraka kuondolewa kwa ulimwengu huu pamoja na mtawala wao mwovu? Wakristo wamesali kwa muda mrefu hili litukie, wakiomba Ufalme wa Mungu uje na mapenzi yake yatimizwe duniani. Wanasali kwamba Yesu Kristo atende kwa kutii amri ya Baba yake ya kuondoa uovu wote duniani!—Zaburi 110:1, 2; Mithali 2:21, 22; Danieli 2:44; Mathayo 6:9, 10.

Hata hivyo, hili lazusha swali: Yawezekana kwamba matabiri ya uwongo, au yenye makosa, yametokea kwa sababu watu walitabiri tarehe ya tukio hili wakitegemea kuelewa kimakosa au kupotosha unabii wa kweli wa Biblia? Acheni tuone.

Uelewevu wa Kimakosa wa Karne ya Kwanza

Fikiria kilichotokea katika karne ya kwanza. Yesu alipokuwa karibu kupaa mbinguni, mitume wake waliuliza kwa hamu hivi: “Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?” Walitaka kufurahia baraka zote za Ufalme mara hiyo, lakini Yesu alisema: “Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe.”—Matendo 1:6, 7.

Siku tatu tu kabla ya kifo chake, Yesu alikuwa amesema vivyo hivyo: “Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu.” Yeye aliongeza hivi: “Habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba. Angalieni, kesheni, [ombeni], kwa kuwa hamjui wakati ule utakapokuwapo.” (Mathayo 24:42, 44; Marko 13:32, 33) Miezi michache mapema, Yesu alikuwa ametia moyo hivi: “Nanyi jiwekeni tayari, kwa kuwa saa msiyodhani ndipo ajapo Mwana wa Adamu.”—Luka 12:40.

Licha ya maonyo hayo yaliyotolewa na Yesu, Wakristo wa mapema, wakiwa na hamu ya kuwapo kwa Kristo na zile baraka kutakazoleta, walianza kukisia-kisia kuhusu wakati ambapo ahadi za Ufalme zingetimizwa. Hivyo, mtume Paulo aliandikia Wathesalonike hivi: “Kwa habari ya kuwapo kwa Bwana wetu Yesu Kristo na kukusanywa kwetu pamoja kwake, twawaomba nyinyi msiwe wenye kutikiswa upesi kutoka kwenye kufikiri kwenu wala msiwe wenye kusisimuliwa kupitia usemi uliopuliziwa au kupitia ujumbe wa maneno au kupitia barua kama kwamba ni kutoka kwetu, ya kuwa siku ya Yehova ipo hapa.”—2 Wathesalonike 2:1, 2, NW.

Maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba Wakristo fulani wa mapema walikuwa wamesitawisha matazamio yenye makosa. Ingawa Wakristo katika Thesalonike huenda ikawa hawakutabiri tarehe hususa ya ‘kukusanywa kwao pamoja kwa Kristo katika mbingu,’ kwa wazi walifikiri kwamba tukio hilo lilikuwa karibu sana. Walihitaji kurekebishwa maoni yao, na barua ya Paulo ilifanya hilo.

Wengine pia Wahitaji Sahihisho

Kama tulivyoona katika makala ya kwanza, baada ya karne ya kwanza, wengine pia walitazamia utimizo wa ahadi za Mungu katika wakati hususa. Wengine walifanya matabiri kwamba mwisho wa miaka elfu, kwa kuhesabu ama kuanzia kuzaliwa kwa Yesu ama kuanzia kifo chake, ungeona mwisho wa ulimwengu. Lakini matabiri yao vilevile yalithibitika kuwa ya uwongo, au yenye makosa.

Hili latokeza maswali: Je, makosa kuhusu utimizo wa ahadi za Biblia yamemaanisha kwamba hizo ahadi zenyewe zilikuwa na makosa? Je, ahadi za Mungu ni zenye kutegemeka? Na ni jinsi gani Wakristo wa kisasa wamekubali sahihisho juu ya jambo hili?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki