Je, Mwisho wa Ulimwengu Uliotabiriwa Uko Karibu?
GAZETI Detroit Free Press Magazine la Februari 6, 1994, lilionelea hivi: “Mawazo kuhusu uharibifu kamili yalikuja kuwa yenye kutaabisha wakati wa muhula wa kinyukilia. Baada ya teketezo la Hiroshima Agosti 6, 1945, ilikuwa wazi kwa kila mtu: Sasa ulimwengu kwelikweli ungeweza kwisha!”
Desemba uliopita, Charles B. Strozier, mchanganuzi wa hisia-moyo na profesa wa historia wa New York, alisema hivi: “Hatuhitaji washairi tena watuambie ungeweza kwisha kwa kishindo, au utakuwa mwisho wa ghafula wenye kutazamisha, au katika umivu la UKIMWI.” Kwa hakika, yeye aliongeza hivi: “Sasa inahitaji wazo la kiajabu kutofikiri kuhusu miisho ya binadamu.”
Kwa kuwa Yesu Kristo alifundisha kwamba ulimwengu ungeisha, je, twaweza kutambua kutokana na mafundisho yake kama mwisho uko karibu kwelikweli?
Ule Mwisho—Lini?
Wanafunzi wa Yesu walimuuliza “ishara” ya kutambulisha wakati ambapo ulimwengu huu, au mfumo huu wa mambo, ungeisha. “Ni wakati gani mambo haya yatakuwa,” wao wakauliza, “nayo itakuwa ni nini ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3, NW) Unaweza kutazama “ishara” aliyotoa Yesu katika kujibu swali hili. Imerekodiwa katika Biblia katika Mathayo sura ya 24, Marko sura ya 13, na Luka sura ya 21. Baadhi ya matukio makuu yanayofanyiza ishara hiyo ni kama yafuatavyo:
VITA KUU: “Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme.” (Mathayo 24:7) Kwa hakika tumeona sehemu hii ya ile ishara ikitimizwa. “Vita ya Ulimwengu ya Kwanza [iliyoanza katika 1914] ilikuwa vita ‘kamili’ ya kwanza,” akaonelea mwanahistoria mmoja. Hata hivyo, Vita ya Ulimwengu 2 ilikuwa mbaya mara nyingi zaidi, ikiua majeruhi milioni 50. Na vita inaendelea kuharibu dunia.
UPUNGUFU WA CHAKULA: “Kutakuwa na upungufu wa chakula.” (Mathayo 24:7, NW) Vita ya Ulimwengu 1 ilifuatiwa na njaa kali mno, na tangu wakati huo njaa imeendelea kuenea katika njia isiyoweza kudhibitiwa katika sehemu nyingi za dunia. Hata katika nchi tajiri zaidi, njaa na utapiamlo vimeenea sana.
MATETEMEKO MAKUBWA YA DUNIA: “Kutakuwa na matetemeko makubwa ya dunia.” (Luka 21:11, NW) Fikiria machache yayo yaliyo makuu: 1920, China, 200,000 waliuawa; 1923 Japani, maisha za watu 143,000 zilipotea; 1970, Peru, 66,800 waliuawa; na 1976, China, wajeruhiwa 240,000 (wengine husema 800,000). Mstadi katika uhandisi wa kuzuia matetemeko ya dunia aliliita tetemeko la China la 1976 kuwa “msiba mkubwa wa tetemeko la dunia kuliko yote katika historia ya wanadamu.”
MAGONJWA: “Tauni mahali mahali.” (Luka 21:11) Mara tu baada ya Vita ya Ulimwengu 1, watu wapatao 21 milioni walikufa kwa homa ya Kihispania. Science Digest iliripoti hivi: “Katika historia yote kifo hakikuwa kamwe kimeenea kwa haraka na bila upunguo kwa watu wengi sana hivyo.” Tangu wakati huo, maradhi ya moyo, kansa, UKIMWI, na maradhi mengine mengi yameua mamia ya mamilioni.
UHALIFU: “Kuongezeka kwa maasi.” (Mathayo 24:12) Katika nchi nyingi uhalifu hauwezi kudhibitiwa. Uuaji wa kimakusudi, unyang’anyi, ulalaji kinguvu, uharamia, ufisadi—kila siku sisi husikia kuhusu uhalifu kama huo au hujionea wenyewe.
Unabii mwingine wa Biblia ulitabiri pia hali ambazo zingekuwako katika siku za mwisho. Kwa kielelezo, katika kitabu cha Ufunuo, kuna njozi ya uendeshaji wa wapanda-farasi wanne. (Ufunuo 6:1-8) Mpanda-farasi wa kwanza anaonyesha Yesu mwenyewe akiwa Mfalme-mshindaji. Wale wapandaji wengine na farasi zao wanaonyesha matukio duniani yanayoashiria mwanzo wa utawala wa Yesu: vita, njaa, na kifo kisichotazamiwa kupitia njia mbalimbali.
Na bado unabii mwingine mbalimbali wa Biblia unafafanua mitazamo na hali ambazo zingekuwako kwa wingi wakati wa “muhula wa mwisho wa ulimwengu huu.” Fikiria kile alichoandika mtume fulani wa Yesu. Unaposoma unabii huu, jiulize: Je, hili halielezi hasa nyakati za taabu za leo?
“Muhula wa mwisho wa ulimwengu huu,” huyo mtume akaandika, “utakuwa wakati wa taabu. Watu hawatapenda chochote ila pesa na wao binafsi; watakuwa wenye kunyeta, wenye kujivuna, na wenye matukano; wasio na staha kwa wazazi, bila shukrani, bila uchaji, bila shauku ya asili; wao watakuwa wasiotulizika chuki zao, wachuuzi wa vitendo vya kashifa, wasiozuia hasira yao na wakali, watu ambao ni wageni kwa wema wote, wahaini, wenye kujihatarisha wakijitafutia faida zao, waliofura kwa kujiona mashuhuri. Watakuwa watu wanaotia raha katika mahali pa Mungu, watu ambao wanahifadhi umbo la nje-nje la dini, lakini wanadumu wakiwa wenye kukana uhalisi walo.”—2 Timotheo 3:1-5, The New English Bible.
Unabii mwingine muhimu kuhusu mwisho wa ulimwengu ni ule unaoahidi kwamba Mungu ‘ataharibu hao waiharibuo dunia.’ (Ufunuo 11:18) Binadamu katika vizazi vilivyopita hawakuwa kamwe na uwezo wa kitekinolojia wa kuharibu dunia, lakini sasa wanao. Na leo tekinolojia mpya zina sehemu kubwa katika kuchafua mazingira. Katika Novemba 1992, magazeti ya habari yalikuwa na vichwa vikuu kama hiki: “Wanasayansi wa Juu Wanaonya Kuhusu Uharibifu wa Dunia.”
Tambua Unabii wa Kweli
Hakuwezi kuwa na shaka kuhusu jambo hilo. Mambo yote ambayo Biblia ilitabiri yangetokea wakati wa “muhula wa mwisho,” au “umalizio wa mfumo wa mambo,” yanatukia wakati huuhuu. Twaona unabii wa kweli katika mkondo wa utimizo, na ni muhimu sana kwamba tuutii. Yesu alionyesha hili katika kufafanua hali katika siku za Noa, “mhubiri wa uadilifu,” muda mfupi kabla ya ulimwengu wa wakati huo kwisha.—2 Petro 2:5, NW.
Yesu alielezea hivi: “Kama walivyokuwa katika siku hizo kabla ya furiko, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiozwa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka furiko likaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” (Mathayo 24:38, 39, NW) Wakati unabii wa kweli unapuuzwa, matokeo huwa yenye kuangamiza.
Labda wewe wasema, ‘Ndiyo, naamini unabii huo mbalimbali wa Biblia; mwisho utakuja siku fulani, lakini hautatokea katika wakati ujao ulio karibu.’ Hata hivyo, una uhakika? Je, hupaswi kutii hilo onyo sasa?
Maonyo Yanayopasa Kutiiwa
Ni wazi kwamba, maonyo mengine hayana msingi, na ingekuwa upumbavu kuyatii. Lakini mengine sivyo. Kwamba tu wengi, kutia ndani washiriki wa jamii walio mashuhuri, wanapuuza onyo, si sababu ya kulipuuza. Fikiria kielelezo.
Ilikuwa Machi 1902, na kwenye kisiwa cha Karibea chenye kuvutia cha Martinique, Mlima Pelée wa kivolkeno ulianza kutenda. Kufikia Aprili, moshi, jivu, na vijipande vya miamba vilibubujishwa pamoja na mivukizo mikali. Wananchi wa jiji la St. Pierre, lililo kilometa nane hivi kutoka kwenye mlima huo, walipatwa na wasiwasi. “Jiji limefunikwa kwa jivu,” mkazi mmoja aliandika. “Wengi wa watu wanalazimika kuvaa vitambaa vya mkononi vilivyo na umaji-maji kwenye pua na midomo yao ili kujikinga kutokana na mivukizo yenye nguvu.”
Mapema katika Mei utendaji wa kivolkeno uliongezeka. Gazeti la habari la mahali hapo lilisema hivi: “Mvua ya jivu haikomi kamwe . . . Kupita kwa magari ya kukokotwa hakusikiki tena katika barabara. Magurudumu yamefunikwa.” Hilo joto lilikuwa lenye kuzuia pumzi.
Halafu, Mei 5, volkeno ilitoa kijito cha mmwagiko wenye kuchoma ambao uliua dazani za watu njiani mwacho. Lakini viongozi wa jiji walisema nini?
Mavuno ya miwa yalikuwa yakikaribia, na wafanyabiashara waliwahakikishia watu kwamba hakukuwa na hatari kubwa. Wanasiasa pia, wakihangaikia uchaguzi uliokuwa mbele katika Mei 10, hawakutaka watu wakimbilie usalama. Kwa hiyo walijaribu kuzima hofu za watu. Isitoshe, makasisi walishirikiana na wafanyabiashara na vikundi vya kisiasa na kuwashurutisha waparishi wao wasiende.
Halafu ikatokea. Mei 8, muda mfupi kabla ya saa 2:00 asubuhi, Mlima Pelée ulilipuka kwa mgurumo wenye kustaajabisha. Mawingu makubwa mno, yaliyo na joto la kiwango cha juu mno yaliteremka kwa mwendo usiowazika kuelekea St. Pierre. Ile gesi moto ilizima mara moja maelfu ya uhai. Kwa uhalisi kila mtu katika St. Pierre alikufa—yapata watu 30,000 au zaidi. Mtu pekee aliyeokoka alikuwa mfungwa mchanga katika jela ya chini ya gereza.
Hali ya Leo
Vivyo hivyo leo, kuna wengi wanaopuuza uthibitisho kwamba unabii wa Biblia uko katika mkondo wa utimizo. Wanakataa kutii uthibitisho unaopaswa kuwa wenye usadikisho kwa mtu yeyote mwenye busara kwamba mwisho wa ulimwengu huu uko karibu. Hata hivyo, Biblia ilitabiri mtazamo wao, ikisema hivi: “Katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe, na kusema, Iko wapi ahadi ile ya kuja kwake? kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.”—2 Petro 3:3-4.
Lakini wadhihaki wa leo wamekosea. Uhakika ni kwamba, mambo yamebadilika. Unabii mbalimbali wa Biblia unatimizwa. Uthibitisho kwamba mwisho wa ulimwengu uko karibu ni mwingi.
Kwa hekima, wewe hupaswi kuchelewesha tendo la kuokoa uhai. Lakini unahitaji kufanya nini?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]
Picha ya U.S National Archives
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]
WHO/E. Hooper
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 11]
Picha ya WHO na W. Cutting