Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 5/1 kur. 3-7
  • Maonyo Yanayopaswa Kufuatwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maonyo Yanayopaswa Kufuatwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MAONI YA VIONGOZI WA MJI
  • MAONYO LEO
  • HAR-MAGEDONI—WAKATI GANI?
  • JE! YANAPASWA KUFUATWA?
  • MAHALI AMBAPO USALAMA UNAPATIKANA
  • Je, Mwisho wa Ulimwengu Uliotabiriwa Uko Karibu?
    Amkeni!—1995
  • Je! Tunakaribia Har–Magedoni?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Wakati wa Taabu Duniani Pote—Sababu Gani, na Wakati Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Uko Macho Kuelekea Nyakati Zetu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 5/1 kur. 3-7

Maonyo Yanayopaswa Kufuatwa

YALIKUWA masika ya mwaka 1902. Mambo yote yalikuwa yakiendelea kama kawaida katika kisiwa chenye kuvutia cha Caribbean kiitwacho Martinique. Mavuno ya miwa yalikuwa yakionekana kuwa yatakuwa mazuri sana, na, katika mji wa kisiwa hicho wenye watu wengi zaidi wa St. Pierre, wanasiasa walikuwa wakifanya Kampeni ya uchaguzi.

Walakini wakati huo, mwishoni-mwishoni mwa Machi, kulikuwako tukio lililoelekea kuharibu tamasha hiyo yenye furaha sana. Mlima Pelée, uliokuwa kama maili tano (kilometres 8) kutoka St. Pierre, ulianza kutoa moto. Hapo kwanza watu hawakukaza fikira sana. Katika Aprili, hata hivyo, moshi, majivu na vipande vya mawe vilipoanza kutupwa, pamoja na hewa kali, watu wa miji huo walianza kuogopa. Mwishoni mwa Aprili mwanamke mmoja aliandikia hivi dadaye katika United States:

“Mji umefunikwa na majivu. Harufu ya kiberiti ni kali sana hata farasi barabarani wanasimama na kupiga chafya. Watu wengi wanalazimika kujifunika vitambaa vyenye maji ili wajikinge na hiyo hewa kali.”

Mapema katika Mei moto huo wa volkeno uliongezeka kukiwa na milipuko yenye sauti kubwa mara kwa mara. Les Colones, gazeti la St. Pierre, lilisema kwamba “mvua ya majivu haikomi kamwe . . . magari yanayokokotwa na farasi hayasikiki yakipita barabarani. Magurudumu yananyamazishwa.” Mkaaji mmoja wa St. Pierre aliandikia hivi nduguye katika Marseilles, Ufaransa:

“Naandika nikiwa na maoni yenye kukosa tumaini kabisa, ijapokuwa natumaini hali si mbaya kama ninavyosema. Mume wangu hucheka; walakini naona anahangaika sana. . . . Joto linafanya kupumua kuwe kugumu. Hatuwezi kuacha cho chote bila kufunikwa, kwa kuwa vumbi linaingia kila mahali, likichoma nyuso na macho yetu. Mazao yote yameharibiwa.”

Ilikuwa wazi kwamba hatari ya kweli ilikuwa inakaribia. Walakini maonyo yaliyokuwa yakitolewa na Mlima Pelée yalifuatwa?

MAONI YA VIONGOZI WA MJI

Kwa sababu mavuno ya miwa yalikuwa yanakaribia, wafanya biashara wa St. Pierre walihakikishia watu kwamba hakukuwako hatari yo yote. Wanasiasa, wakihangaikia uchaguzi uliokuwa ukija, wao pia hawakutaka watu watoroke, kwa hiyo wakasema kama hivyo. Kwa kweli, meya (mkuu wa mji) alitoka mji mmoja akaja St. Pierre kusadikisha watu kwamba hakukuwako sababu ya kuwa na wasiwasi. Viongozi wa kidini, mapadri wa Katoliki, walishirikiana na wafanya biashara na vikundi vya kisiasa katika kujaribu kushawishi washiriki wao kwamba mambo yote yalikuwa sawa.

Kisha ikatokea. Muda mfupi kabla ya saa 2 asubuhi, Mei 8, Mlima Pelée ulilipuka kwa mshindo mkuu. Mawingu makubwa meusi yenye joto jingi sana yakaja kwa mwendo wa kasi sana kuelekea St. Pierre. Mwandikaji mmoja aliandika hivi:

“Maelfu mengi ya maiti zilizokuwa ndani ya magofu zilionyesha jambo lile lile, juu ya kifo cha mara moja wakati tufani hiyo yenye kuchoma kutoka Mlima Pelée ilipowafikia. Hakukuwako wakati wa kujaribu kutoroka, au hata kufanya machachari; mamia walikufa tu walipokuwapo. Mvuke huo ulifanya kazi kwa haraka sana, ukaua maelfu kwa muda wa dakika mbili au tatu.”

Karibu kila mtu katika St. Pierre alikufa—watu 30,000 au zaidi. Ni watu watatu tu waliookoka, na wawili kati yao wakafa muda si muda kwa ajili ya majeraha yao. Mtu pekee aliyepona majeraha aliyokuwa nayo na akaishi alikuwa mfungwa kijana. Alikuwa ametiwa ndani ya gereza la chini, ambapo alipatikana siku kadha baada ya mlipuko huo.

Kufikia wakati huu kuna magofu mengi, katika St. Pierre yakishuhudia mauaji hayo makubwa. Vilevile, ishara moja ya ukumbusho inaeleza juu ya mamia mengi waliopoteza maisha yao katika kanisa la Katoliki wakihudhuria Misa.

Kufikiri kidogo tu kungepaswa kuwaamuru waondoke St. Pierre wakati hewa ilipokuwa mbaya sana ikawa vigumu kupumua. Na kama wafanya biashara, wanasiasa na viongozi wa kidini wangehangaikia zaidi maisha za watu wao kuliko faida yao ya wakati huo, basi, mahali pa kujaribu kuwashawishi watu wasiondoka wangejiunga pamoja nao wautoroke mji huo. Jambo hilo lingeokoa maisha zao.

MAONYO LEO

Hivi karibuni maonyo ya uharibifu mkubwa zaidi yametangazwa sana. Tunazungumza juu ya maonyo gani? Si yale yaliyotolewa na Mlima St. Helens, wa Washington State, U.S.A., mwanzoni mwaka uliopita. Mkaaji mmoja huko aliandika hivi: “Mlima huo uliendelea ‘kulipuka’ kwa nguvu zaidi, kana kwamba ulikuwa ukituonya tujitayarishe kwa ajili ya mlipuko wenyewe.” Wakuu wa serikali na wa mahali hapo walisema hivyo, vilevile wakionya juu ya hatari kubwa kwa wale walioko katika eneo la volkeno hiyo.

Walakini sisi hatufikirii juu ya uharibifu wa mahali fulani unaotazamiwa. Mahali pake, ni maonyo, ambayo sasa yanatangazwa duniani pote, juu ya uharibifu wa ulimwengu unaokaribia—Har–Magedoni ndio tunasema juu yake. Akitabiri uharibifu huo, Yesu Kristo alisema hivi: “Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.” (Mt. 24:21) Kulingana na maelezo ya Yesu, hiyo “dhiki kubwa” itakuwa yenye kuharibu uhai wa kibinadamu zaidi ya misiba yote isiyofanywa na wanadamu ambayo imewapata ikiwekwa pamoja.

“Haiwezekani!” pengine wasema? Hata hivyo nabii wa Mungu, Yesu Kristo, hajapata kukosea wakati uliotangulia. “Vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi,” ambayo kwa kawaida inaitwa Har–Magedoni, lazima itakuja. (Ufu. 16:14-16) Itakuwa sehemu ya mwisho ya “dhiki kubwa.” Basi je! si jambo la akili, kufikiria maonyo ya kwamba Har–Magedoni imekaribia, watu wengi wanaoishi sasa wakiwa wangali hai?

HAR-MAGEDONI—WAKATI GANI?

Kuhusiana na “dhiki kubwa,” kutia ndani Har–Magedoni, Yesu aliendelea kusema hivi katika unabii huu wa maana: “Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku ya [Noa], ndivyo kutakavyokuwa [kuwapo] kwake Mwana wa Adamu. Kwa kuwa kama vile siku zile zilizokuwa kabla ya Gharika watu walivyokuwa wakila, na kunywa, wakioa na kuolewa, hata siku ile aliyoingia [Noa] katika safina, wasitambue, hata Gharika ikaja, ikawachukua wote, ndivyo kutakavyokuwa [kuwapo] kwake Mwana wa Adamu.” Kwa kuwa kama vile siku zile zilizokuwa kabla ya Gharika watu walivyokuwa wakila, na kunywa,wakioa na kuolewa, hata siku ile aliyoingia [Noa] katika safina, wasitambue, hata Gharika ikaja,ikawachukua wote, ndivyo kutakavyokuwa [kuwapo] kwake Mwana wa Adamu.”​—Mt. 24:37-39.

Hivyo Yesu alionyesha wazi kwamba uharibifu wa ulimwengu unaokuja—ambao ukubwa wake utashinda Gharika ile—unahusiana na kuwapo kwake. Huo ni wakati ‘ajapo katika utukufu wake na kuketi katika kiti cha utukufu wake’ atawale kama mfalme. (Mt. 25:31) Je! kuna njia yo yote ya kuweza kujua wakati wa Har–Magedoni?

Ndiyo, kunayo. Wanafunzi wa Yesu walipendezwa na mambo hayo. Kwa hiyo walimwuliza juu yake. Ulizo ambalo lilianzisha mazungumzo ya Yesu ambayo katika hayo alizungumza juu ya “dhiki kubwa” lilikuwa hili: “Mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya mwisho wa taratibu ya mambo?” (Mt. 24:3, NW) Hakika twapaswa kupendezwa sana na kujua “ishara” ambayo Yesu alitoa.

Unaweza kujichunguzia “ishara” hiyo. Imeandikwa katika Biblia katika Mathayo sura za 24 na 25, Marko sura ya 13 na Luka sura ya 21. Hapo utaona kwamba Yesu alisema kuwapo kwake na kukaribia kwa “dhiki kubwa” kungeonyeshwa na taabu kubwa za dunia. Kungekuwako vita, kutia ndani kuinuka kwa taifa moja juu ya jingine, matetemeko makubwa, upungufu wa chakula, magonjwa ya kuenea, pamoja na ongezeko la uvunjaji wa sheria upendo wa wengi utapoa. Vilevile, Yesu alitabiri kwamba wafuasi wake wangeteswa, hata hivyo “habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu . . . na ndipo ule mwisho [kutia Har–Magedoni] utakapokuja.”

Katika unabii mwingine, mtume Paulo aliongozwa na Mungu aandike hivi: “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini Wakikana nguvu zake.”​—2 Tim. 3:1-5.

Je! waweza kusema kwamba unabii wa Yesu Kristo na mtume Paulo juu ya “siku za mwisho” unatimizwa sasa? Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni mbili wanaamini unatimizwa, na hiyo ndiyo sababu Mashahidi wa Yehova kila mahali wanatoa onyo kwamba Har–Magedoni inakaribia. Wanaalika watu wachunguze ushuhuda ili wajiamulie kama maonyo hayo yana msingi wa kweli.

JE! YANAPASWA KUFUATWA?

Bila shaka, maonyo fulani yanakuwa bila msingi, nao ungekuwa upumbavu kuyafuata. Walakini uhakika wa kwamba wengi—kutia ndani washiriki maarufu wa ujamii—wanadhihaki au kupunguza uzito wa maonyo, huo si msingi wa kuyapuza. Kumbuka hali ile ya Mlima Pelée. Katika Mei 5, siku tatu kabla ya mlipuko wake mkubwa, volkeno hiyo ilitupa vitu vyenye kuchoma ambavyo viliua chungu nzima ya watu waliokuwapo mahali vilipotupwa. Watu wengi waliona jambo hilo kuwa onyo la kufaa wapate kutoroka, kama ambavyo Peter Francis anavyoandika katika kitabu chake cha karibuni kiitwacho Volcanoes:

“Wengi walijaribu kuondoka St. Pierre, waende Fort-de-France, mji mkuu wa pili wa Martinique. Hata hivyo, wakuu wa huko, hawakuvutiwa na taraja la kuhamisha watu wengi. Licha ya tatizo la kushughulika na hesabu kubwa ya wakimbizi wenye hofu, kulikuwako pia uchaguzi uliokuwa unakuja Mei, 10, navyo vyama vya kisiasa katika mji huo havikutaka jambo lo lote liukatize, kwa hiyo kulikuwako jitihada ya kushirikiana ya kuonyesha hapakuwa hatari kubwa. ‘Tume ya kisayansi’ ambayo washiriki wake walikuwa watu wenye elimu zaidi katika kisiwa hicho ilianzishwa, nayo ikatoa ripoti ambayo kusudi lake lilikuwa kutuliza hofu.”

Kwa kadiri fulani walifaulu kufanya hivyo. Watu waliendelea kukaa​—nao wote wakaangamia, isipokuwa mmoja!

Leo unabii wa Biblia juu ya “siku za mwisho” unatimizwa. Sehemu zote za “ishara” yenye mambo mengi aliyotoa Yesu zinatimizwa. Ndiyo, yale ambayo Kristo na mitume wake walitabiri yangetokea muda mfupi tu kabla ya “dhiki kubwa” yanatokea sasa. Ushuhuda ni mwingi sana. Kama alivyotabiri Yesu, kuna “huzuni kuu ya mataifa, wasijuwe njia ya kutokea.” Vilevile, “wanadamu wakizimia moyo kwa sababu ya hofu na kutazamiwa kwa mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu.”​—Lu 21:25, 26, NW.

Maelezo ya mhariri wa gazeti la Miami Herald, Jim Hampton, yanaonyesha kutimizwa kwa mambo hayo. Ingawa haioni Har–Magedoni kulingana na maoni ya Biblia kabisa, yeye aliandika hivi katika Mei 4, 1980:

“Je! wewe, kwa maoni yako, unaliona tatizo likikua, kama lile ninaloona likikua ndani yangu? Tatizo kubwa linalokufanya usilale usingizi usiku, likikuambia kwamba kuna kasoro kubwa katika nchi yako, katika ulimwengu wote? Tatizo linaloogopesha mara nyingine kwa sababu umepata kufahamu kwamba Har—Magedoni si fumbo tu la maneno unalosoma katika Biblia, [bali] ni kweli? Na kwamba kwa mara ya kwanza maishani mwako kuna hali inayoelekea sana kuchochea ugomvi na kutokeza Har–Magedoni?

“Mimi ninalo tatizo hilo. Sioni haya kusema hivyo, kwa sababu nimeuliza rafiki wengi kama wanaona hivyo, wote wanaona hivyo.”

Kuna wale wanaofanya mzaha juu ya Mungu kukomesha uovu. Wengine wanapunguza uzito wa ushuhuda wa kwamba unabii wa Biblia unaendelea kutimizwa. Walakini Biblia ilitabiri hali iyo hiyo, ikisema hivi: “Katika siku za mwisho watakuja wadhihaki pamoja na dhihaka yao, wakiendelea kulingana na tamaa zao wenyewe na kusema: ‘Ku wapi huku kuwapo kwake kulikoahidiwa? Kwani, tangu ile siku mababu zetu walipolala usingizi wa mauti, mambo yote yaendelea sawa-sawa kama yalivyokuwa tangu mwanzo wa kuumba.’”​—2 Pet. 3:3, 4, NW.

Walakini wadhihaki hao wamekosea. Ukweli ni kwamba mambo yamebadilika. Unabii wa Biblia unatimizwa. Ushuhuda u wazi kwamba Har–Magedoni inakaribia kama ilivyokuwa wazi mwanzoni mwaka uliopita kwamba Mlima St. Helens ulikuwa karibu kulipuka. Hata hivyo wengi huko walikataa kufuata maonyo ya kuondoka katika eneo hilo la hatari. Walipoteza maisha yao. Mwanamke mmoja aliyehojiwa katika televisheni alisema yeye hakubaliani na vizuizi vya kusafiri ambavyo viliwekwa vizuie watu wasije kwenye eneo hilo. Baada ya mlipuko huo alionekana tena kwenye televisheni akishukuru kwa unyofu kwa ajili ya vizuizi hivyo, ambavyo, alisema, viliokoa maisha yake.

MAHALI AMBAPO USALAMA UNAPATIKANA

Tukielekeana na mlipuko wa volkeno, ni wazi kabisa mahali ambapo usalama unapatikana—mbali kabisa na volkeno hiyo. Kwa kushangaza eneo ambalo watu walikufa kutokana na mlipuko wa St. Helens liliripotiwa kuwa la maili za mraba 150 (kilometres za mraba 380). Miti iliangushwa ikiwa umbali wa maili 14 (kilometres 23) kuelekea pande tatu, na kila kitu kiliteketezwa maili kadha wa kadha kutoka hapo! Walakini usalama unaweza kupatikana wapi wakati wa “dhiki kubwa” inayokaribia?

Si mahali fulani pa nchi. Kama ilivyokuwa wakati wa Gharika, Yehova Mungu atakuwa na uwezo wa kuharibu waovu po pote watakapojificha. Kwa njia iyo hiyo, ataweza kuhifadhi wo wote atakaochagua, po pote watakapokuwapo. Njia ya usalama inatolewa na mtume Yohana, anaposema hivi: “Ulimwengu [wa wanadamu wasiotii] unapita na tamaa yake pia, walakini yeye afanyaye mapenzi ya Mungu abaki milele.”​—1 Yohana 2:17, NW.

Mahali pa pekee pa usalama ni katika uhusiano unaofaa pamoja na Yehova, unaoweza kufurahiwa na wote wanaofanya mapenzi yake. Walakini kabla ya kuweza kufanya mapenzi ya Yehova, lazima tujifunze anayotaka kwetu. Hiyo inatia ndani kujifunza Neno lake, Biblia, na kisha kuitumia maishani mwetu. Je! una nia ya kufanya hivyo? Mashahidi wa Yehova watapendezwa kukusaidia. Kwa vyo vyote, usipuze maonyo yenye msingi wa Biblia wanayotoa juu ya kukaribia kwa Har–Magedoni. Hayo ni maonyo yanayostahili kuchunguzwa kwa uangalifu—nayo yapaswa kufuatwa.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Mamia, waliokataa kufuata maonyo hayo, walitorokea ndani ya kanisa nao wakapoteza maisha yao

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki