Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 10/15 kur. 464-468
  • Wakati wa Taabu Duniani Pote—Sababu Gani, na Wakati Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wakati wa Taabu Duniani Pote—Sababu Gani, na Wakati Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NI WAKATI GANI? NI WAKATI GANI? NI WAKATI GANI?
  • Kutoa Onyo la Kimungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Karibuni Kusudi la Mungu Kutimizwa
    Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?
  • Maswali Manne Kuhusu Mwisho Yajibiwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Jinsi Sisi Tujuavyo Kwamba Tumo Katika “Siku za Mwisho”
    Je, Kweli Mungu Anatujali?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 10/15 kur. 464-468

Wakati wa Taabu Duniani Pote​—Sababu Gani, na Wakati Gani?

“Waliouawa na [Yehova] siku ile watakuwapo, toka upande mmoja wa dunia hata upande wa pili; hawataliliwa, wala kukusanywa, wala kuzikwa.”​—Yer. 25:33.

1-3. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba mara nyingi watu wanaumia kwa sababu hawasikilizi maonyo?

“HUTUKIA katika kila msiba. Kuna watu wengi sana wanaokataa kutii onyo. . . . Kwa sababu ya kutojali maonyo, watu wengi sana hufa bure.” Ndivyo mwandikaji wa kitabu kinachozungumza juu ya misiba alivyoandika. Mafuriko ya mwaka wa 1953 yaliyofurika maeneo makubwa ya Netherlands, ambayo katika hayo mamia wengi walipoteza maisha zao, yako miongoni mwa mifano mingi sana anayotaja ili athibitishe maneno yake. Anasema hivi: “Kati ya misiba hii, haikuwa lazima watu 1,835 wafe. Wangaliokoka kwa urahisi. Walikuwa wana wakati wa kutosha.” Lakini hawakutii maonyo yaliyotolewa. Wakafa bure.

2 Vilevile miongoni mwa hao waliokufa ni watu 135 na wengine zaidi waliopoteza maisha zao katika mafuriko ya Genge Kubwa la Thompson huko Colorado, Jumamosi jioni, Julai 31, 1976. Likiarifu hilo, gazeti la Denver, Colorado, Post, la Agosti 2, lilisema hivi: “Kila mtu alikuwa ameonywa na mkuu wa wilaya,” magari ya mkuu wa wilaya yakiwa na vipaza-sauti yalipita mara tatu katika genge yakitoa onyo. Watu waliotii maonyo hayo wakakimbia kutoka genge hilo ndio waliookoka peke yao.

3 Tena, gazeti The Unesco Courier, la Mei 1976, lilieleza jinsi wanasayansi Wachina walivyotabiri kwa usahihi sana kutukia kwa tetemeko la nchi katika sehemu ya Haich’eng ya Jimbo la Liaoning. Karibu watu wote wa sehemu hiyo walitii onyo hilo, wakaokoa maisha zao. Walakini, jamaa moja haikujali na watatu kati yao wakapoteza maisha zao.

4. Ni baadhi ya sababu gani ambazo labda zinafanya watu wasisikilize maonyo hayo mara nyingi?

4 Kwa nini watu hukataa mara nyingi kutii maonyo yanayotolewa wakati maisha zao zi hatarini? Kwa nini? Labda wamezaliwa na hali hiyo ya kutojali, bila kuthamini au kujali uhai wao ulio wenye thamani sana. Au labda ni kwa sababu ya kuthamini mali zaidi kuliko uhai wenyewe. Mara nyingine huwa kwa sababu maonyo ya zamani hayakuwa ya kweli.

5. Ni kwa njia gani watu wengine wametafuta msaada wasiupate?

5 Kwa upande mwingine, watu wamegeukia kitu kisichoweza kusaidia wakati wa msiba. Hivyo, mwaka wa 1944 wakati Mlima Vesuvius ulipolipuka na mawe yenye moto yaliyoyeyuka yakaporomoka katika kando za mlima, wakulima wenye ushirikina waliziweka sanamu za kidini katika njia ya mawe hayo yaliyoyeyuka kana kwamba sanamu hizo zingeweza kuzuia mporomoko huo. Ndivyo alivyofanya pia Mkalifornia mmoja aliyefanya haraka na kukamata sanamu ya mtakatifu wakati mioto ya msitu ilipokaribia nyumba yake mnamo kiangazi cha 1976, na kwa sababu sanamu hiyo haikuweza kusaidia kuzuia moto huo wa msitu, alianza kunung’unika akisema, “Ni bure tu!”

6, 7. (a) Kwa sababu gani leo tunatakiwa tutii onyo la Mungu upesi? (b) Kwa sababu ya mambo yaliyotangulia kutajwa, ni maulizo gani ambayo watu wengine wanauliza?

6 Kwa vile zamani watu wengi wamepoteza maisha zao kwa kutokutii maonyo, hiyo ni sababu yenye nguvu inayofaa sana tulitii onyo la Mungu Muumba, linalopatikana katika Neno lake Biblia Takatifu. Ndiyo, hili ni jambo la muhimu zaidi kuliko yote. Kwa nini? Kwa sababu wanadamu wote wanakabili hatari ya wokovu wao, na si wale tu wanaoishi katika eneo au katika mji fulani. Kusema hivi, hatumaanishi hatari ya vita ya kutumia silaha za atomiki kati ya mataifa makubwa ya duniani. Badala yake, tunamaanisha uharibifu mkuu uliotabiriwa katika Neno la Mungu. Ni uharibifu utakaoletwa na Muumba mkuu, Yehova Mungu, peke yake.

7 Lakini labda wengine watauliza hivi, Twawezaje kuwa na hakika kwamba Mungu ataingilia mambo ya dunia na ya wanadamu? Twawezaje kuwa na hakika kwamba zile ahadi au yale maonyo yaliyoandikwa katika Biblia yapaswa kutiwa maanani? Kwa sababu hiyo, twawezaje kuwa na hakika hata kwamba kuna Mungu na kwamba Biblia Takatifu ni ufunuo wake kwetu? Maulizo hayo yatukumbusha maneno ya mtume Paulo ya kwamba: “Si [watu] wote walio na imani.”​—2 The. 3:2.

8, 9. (a) Kwa sababu gani tunaweza kuwa na hakika kwamba unabii mbalimbali wa Biblia unaohusu taabu ya dunia yote utatimizwa? (b) Mungu alitabiri nini kuhusu taabu hiyo, kwa kutumia Yeremia, Sefania, Danieli na Yesu Kristo?

8 Kwa sababu unabii mwingi sana wa Biblia umetimizwa, twaweza kuwa na hakika kwamba unabii ule mwingine unaotabiri kuja kwa uharibifu mkubwa wa kuenea ulimwengu wote utatimizwa pia. Uharibifu huu mkubwa utaletwa na Muumba mkuu mwenyewe. Katika maana hii utakuwa kama uharibifu unaosimuliwa katika Yeremia 25:33, linalosema hivi: “Waliouawa na [Yehova] siku ile watakuwapo, toka upande mmoja wa dunia hata upande wa pili; hawataliliwa, wala kukusanywa, wala kuzikwa; watakuwa samadi juu ya uso wa nchi.”

9 Kwa habari ya msiba huo mkubwa, nabii Sefania aliongozwa na Mungu aandike hivi: “Basi ningojeni, asema [Yehova], hata siku ile nitakapoondoka kuteka mateka; maana nimeazimia kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu; kwa maana dunia yote itateketezwa kwa moto wa wivu wangu.” (Sef. 3:8) Na kwa habari ya wakati huo, nabii Danieli aliongozwa na Mungu kusema hivi: “Wakati huo Mikaeli atasimama, jemadari mkuu, asimamaye upande wa wana wa watu wako; na kutakuwa na wakati wa taabu, mfano wake haukuwapo tangu lilipoanza kuwapo taifa hata wakati uo huo.” (Dan. 12:1) Yesu Kristo aliutaja wakati huo katika unabii wake mkuu kuhusu mwisho wa taratibu hii ya mambo, akisema: “Wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe. Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote.” (Mt. 24:21, 22) Nacho kitabu cha Ufunuo kinaeleza pigano la siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi, litakalotokea katika Har–​Magedoni.​—Ufu. 16:14, 16; 19:11, 19.

10, 11. (a) Ni hali gani iliyokuwa duniani wakati siku sita za kuumba zilipomalizika? (b) Sababu moja itakayomfanya Mungu achukue hatua ya kutengeneza mambo duniani ni nini?

10 Lakini kwa sababu gani Muumba ataletea wanadamu uharibifu huo mkubwa duniani pote? Ni kwa sababu yeye kama Muumba na Mwenye dunia anapendezwa sana na sayari hii na watu wanaokaa juu yake. Wakati Mungu alipomaliza siku zake sita au vipindi vya kuumba, “akaona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.” (Mwa. 1:31) Na miaka karibu elfu tatu baadaye, Mfalme Sulemani alitaja jambo ilo hilo: “Kila kitu amekifanya kizuri kwa wakati wake.”​—Mhu. 3:11; Zab. 111:2; 104:5-27.

11 Na leo, twaona nini katika sayari hii? Vita vingi vyenye kuchukiza sana, mapinduzi, namna zote za udhalimu, uvunjaji wa sheria na ufisadi, kuonea na kugandamiza wengine, vilevile magonjwa mengi ya mwili na ya akili yanayosumbua wanadamu na kufanyiza mateso makuu. Lakini kumbuka, Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, alituambia tuombe ufalme wa Mungu uje, tuombe mapenzi ya Mungu yafanyike duniani kama mbinguni. (Mat. 6:10) Ili sala hiyo ipate kujibiwa, itakuwa lazima Mungu aondoe jeuri yote na uovu wote, pamoja na wanadamu wote na vyama vinavyopinga enzi yake kuu, na vinavyopinga mapenzi ya Mungu yasifanyike hapa duniani.​—Zab. 37:10, 11.

12-14. (a) Ni sifa gani mbili za Mungu zinazohakikisha kwamba atachukua hatua ya kuletea dunia na wanadamu hali nzuri? (b) Kwa sababu gani tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu anaweza kufanya lo lote atakalo katika habari hiyo?

12 Jambo jingine pia linalofaa kutajwa ni kwamba Yehova ni Mungu mwenye haki ya hukumu: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kum. 32:4) Si kwamba yeye mwenyewe anatenda haki nyakati zote tu, bali pia anataka kuona haki ikidumu kati ya watu walio chini ya mamlaka yake. Bila shaka anapendezwa na watu wanaotendwa udhalimu, kama vile Ayubu wa kale alivyopendezwa nao na kusema hivi juu yake mwenyewe: “Nalimwokoa maskini aliyenililia; yatima naye, na yule asiyekuwa na mtu wa kumsaidia.” (Ayubu 29:12) Mungu hatavumilia udhalimu milele.

13 Zaidi ya hilo, je! hatusomi kwa habari ya Yehova kwamba “Mungu ni upendo”? (1 Yohana 4:8) Na je! hatusomi kwamba “Mungu aliupenda ulimwengu [wa wanadamu], hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele”? (Yohana 3:16) Ingawa Yehova Mungu ni mkuu sana, anafikiria hali za viumbe vyake vinyonge duniani, na kuvihurumia. Tunaonyeshwa jambo hilo wazi na maneno ya nabii wake: “Katika mateso yao yote”​—yaani, ya watoto wa Israeli​—“yeye aliteswa.” Alijisikia vibaya kuona watu wake wakitaabika, basi akawakomboa mara nyingi, tangu wakati wa Musa na kuendelea.​—Isa. 63:9; Kut. 2:23, 24; Amu. 2:18.

14 Tuna hakika kwamba Mungu atachukua hatua ya kusaidia wanadamu wenye kuonewa kwa sababu ni mwenye haki na upendo. Lakini je! yeye ana uwezo wa kunyosha mambo katika dunia hii? Bila shaka! Uwezo wake ni mwingi sana, maana yeye ndiye Mwenye Nguvu Zote. (Mwa. 17:1; 18:14, 25) Kwa sababu ya uwezo na hekima aliyoonyesha kwa kuumba ulimwengu wote, hakuna shaka kwamba anaweza kuleta uharibifu mkuu duniani pote ukomeshe uovu na taabu katika dunia hii.​—Mit. 3:19, 20.

15, 16. Ni sababu gani yenye nguvu zaidi inayohakikisha kwamba Yehova. Mungu ataleta taabu ya dunia yote asafishe uovu duniani?

15 Kuna sababu yenye nguvu hata zaidi kwa nini Muumba, Yehova Mungu, ataleta uharibifu huu mkubwa wa dunia nzima, awaharibu waovu wote. Ni sababu gani? Kwa sababu uovu wote ni uasi juu yake kama Mwenye Enzi mweza yote. Yote hayo ni makufuru kwake, ambayo hawezi kuvumilia kwa wakati usiojulikana. Ndiyo sababu Yesu alianza Sala ya Kielelezo kwa ombi hili: “Jina lako na litakaswe.”​—Mt. 6:9, tafsiri ya Kiingereza ya New World.

16 Maelezo ya Mungu juu ya siku za Nuhu yaonyesha kwamba hali mbaya zilizokuwako wakati huo zilimkufuru sana akachukua hatua. (Mwa. 6:3, 5, 6) Kwa muda wa miaka mingi sasa, watu wenye haki wamekuwa wakiuliza ulizo ambalo nabii Habakuki aliuliza kutaka kujua kwa nini Mungu asiye na udhalimu na mwenye haki huruhusu waovu wawasimange wenye haki. (Hab. 1:13) Kwa hiyo tunaona Neno la Mungu likisimulia kwamba atakomesha uonevu na uovu wote, ili watu wapate kujua kwamba yeye ndiye Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote. Katika unabii wa Ezekieli kuna usemi unaoonekana karibu mara sitini kwamba Mungu atachukua hatua hata ‘watu watajua ya kwamba ndiye Mungu wa kweli, Yehova.’ (Eze. 6:7–39:28, tafsiri ya Kiingereza ya New World) Vilevile, mtunga zaburi Mwebrania alimwomba Mungu achukue hatua ili watu “wajue ya kuwa wewe tu unayeitwa Yehova, ni peke yako uliye juu, juu ya nchi yote.” (Zab. 83:18, tafsiri ya Kiswahili ya Zaire) Ndiyo, Yehova Mungu atauleta uharibifu mkubwa wa dunia nzima ili akomeshe uovu na mateso yote duniani, kwa sababu mbili: anahurumia wanadamu wanaoteswa, tena enzi yake kuu na jina lake vyahusika.

NI WAKATI GANI? NI WAKATI GANI? NI WAKATI GANI?

17. Yesu alisema nini juu ya kama tunaujua wakati barabara wa “siku ile”?

17 Ulizo ambalo ni la maana kupita yote wanalouliza watu wengi ni hili, “Dhiki kubwa” hii, msiba huu wa kuenea ulimwengu wote, uharibifu mkubwa huu, utatukia wakati gani? Muumba ataingilia mambo ya wanadamu wakati gani, kama alivyofanya katika nyakati za kale, akomeshe hali za ulimwengu zenye kusumbua? Maadamu watumishi wa Mungu wametamani sana kuujua wakati huo, jambo hili moja ni hakika: Hakuna mtu anayeweza kusema kwa hakika siku na saa barabara. Yesu mwenyewe alieleza jambo hili waziwazi, akisema: “Hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba.” Alisema pia kwamba itakuwa ‘katika wakati wasiodhani wafuasi wake.’​—Marko 13:32; Luka 12:40.

18. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Yehova ana nyakati za kuchukua hatua?

18 Lakini Yehova Mungu ameweka wakati wake. Tunasoma hivi katika Neno lake, Biblia: “Kwa kila jambo kuna majira. yake, na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu.” (Mhu. 3:1) Wakati hali duniani zilipozidi kiasi cha ustahimilivu wa Yehova Mungu katika siku za Nuhu, alipeleka gharika kuu. (Mwa. 6:3, 5-7) Watu wake Waisraeli walipokuwa utumwani katika Misri, aliwakomboa katika wakati wake. Habari yasema hivi: “Mungu akasikia kuugua kwao, . . . na Mungu akawaangalia,” akawatoa kwa mkono wa Musa. (Kut. 2:24, 25) Baadaye, taifa la Israeli lilipojaribu subira ya Mungu kupita kiasi kwa sababu ya ukafiri na uovu wao, “hata kusiwe na kuponya,” Mungu “akaleta juu yao mfalme wa” Babeli. (2 Nya. 36:15-17) Tena, “ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe” duniani.​—Gal. 4:4.

19. Sababu moja ya kukata maneno na kusema Mungu atachukua hatua karibuni ni nini?

19 Ni lazima ufike upesi wakati wa Mungu wa kukomesha uovu duniani, kwa maana ikiwa hali zilizopo sasa zinazozidi kuwa mbaya zisingekomeshwa na Muumba, watu wenye choyo wangemaliza wanadamu duniani, ama kwa kuichafua ama kwa vita ya kutumia silaha za atomiki. Kulingana na wataalamu wa viumbe na mazingira yavyo, kuenezwa haraka kwa uchafu katika dunia, katika hewa na hasa katika bahari kuu, kunahatirisha wokovu wa jamaa ya kibinadamu. Kupatana na maneno ya Yesu Kristo, taratibu mbaya ya sasa ni nyumba iliyojigawanya yenyewe; kwa sababu hiyo, haiwezi kusimama kwa muda mrefu zaidi. Tena kulingana na mfano mwingine wa Maandiko, mataifa ‘yamepanda upepo, nayo yatavuna tufani’ ya uharibifu.​—Mt. 12:25, 26; Hos. 8:7.

20-22. (a) Ni unabii gani wa Yesu unaoonyesha kwamba wakati wa taabu ya dunia yote unakaribia? (b) Maneno ya Paulo yanaonyeshaje kwamba tumo katika “siku za mwisho”?

20 Hasa unabii wa Biblia unaotimizwa unahakikisha kwamba tunaishi katika mwisho wa taratibu hii mbovu ya mambo. Katika kujibu ulizo la mitume wake la kutaka kujua wakati ‘mwisho wa ulimwengu’ au mwisho wa taratibu hii ya mambo ungetukia, Yesu Kristo alitabiri vita vya kuenea mahali pote, njaa, matetemeko ya ardhi na magonjwa ya kipuku kuwa ishara ya kukaribia kwa mwisho huo. Bila shaka tumeyaona mambo haya yote yakitukia kizazi chetu kwa kadiri isiyo na kifani, hasa tangu mwaka wa 1914.​—Mt. 24, 25; Marko 13; Luka 21.

21 Vilevile maneno ya unabii ya mtume Paulo yanakazia sana wakati huu wa sasa kwamba “siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake.” (2 Tim. 3:1-5) Ni nani awezaye kusema kwamba hali hizi hazipo leo, kwa kadiri isivyopata kuonwa zamani? Bila shaka hakuna mtu mnyofu na mwenye akili awezaye kukana.

22 Kama sehemu ya “ishara” yake yenye mambo mengi ya mwisho wa taratibu hii ya mambo, Yesu alitabiri kwamba “habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14) Vilevile unabii huu umetimizwa sana, hasa katika muda wa miaka 50 iliyopita. Yehova Mungu anawaonya kwa haki waovu na wema wote kabla hajawachukulia hatua, na mifano mizuri sana ya jambo hilo ni vile alivyowaagiza manabii wake watoe tangazo kabla ya kuharibiwa kwa Yerusalemu na hekalu lake mwaka wa 607 K.W.K., tena mwaka wa 70 W.K.

23. Inatupasa tufanye nini kwa sababu matukio hayo yanakaribia?

23 Hayo yote yana maana gani? Maana yake ni kwamba kuna uwezekano wa kuokoka kama zamani, nyakati Muumba, Yehova Mungu, alipoleta uharibifu mkubwa. Tena, maana yake ni kwamba tunatakiwa tuchukue haraka hatua za kuokoka, kama ilivyokuwa siku za Lutu na wakati Wakristo wa kwanza walipoyaona majeshi ya Rumi yakiuzunguka Yerusalemu. Naam, huu ni wakati wa kujipatia imani upesi na kutenda kupatana na imani hiyo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki