Waweza Kusaidiaje Wazazi Walio Peke Yao?
WAZAZI walio peke yao, wawe wanaume ama wanawake, wastahiki ufikirio. Leo wafanyakazi wa kijamii huweka mkazo mkubwa kuhusu umuhimu wa kutegemeza kihisia-moyo familia ya mzazi mmoja.
“Vikundi vya marafiki wenye kutegemeza, watu wa ukoo wenye kujali, walimu wenye upendezi mchangamfu na wa kibinafsi, utendaji maalumu wa kijumuiya na kidini uliopangwa kwa ufikirio wa familia kama hizo,” wakaeleza wanajamii Letha na John Scanzoni, “vyaweza kufanyiza tofauti kubwa katika hali-njema ya kihisia-moyo ya wazazi walio peke yao na watoto wao wakati kitia-moyo kihitajiwapo hasa maishani mwao.” Basi, waweza kusaidiaje?
Uwe Mwenye Kuunga Mkono
Kwanza, jaribu kuelewa jinsi wazazi walio peke yao huona mambo. Jiweke katika hali yao. Amkeni! lilimhoji Margaret, ambaye ni mwenye watoto wawili, wenye umri wa miaka 7 na 14. Alitaliki miaka mitano iliyopita, naye kufikia sasa anakabiliana na hali kwa mafanikio. Bila shaka utapata maelezo yake kuwa yenye kuweka mambo wazi.
Amkeni!: “Ukiwa mzazi aliye peke yake, ni matatizo gani ambayo imekubidi kuyakabili?”
Margaret: “Kwanza kabisa, ilikuwa vigumu sana kuukubali ule uhakika wa kwamba nilikuja kuwa mzazi aliye peke yake, jambo ambalo sikuwa nimelipangia. Iliniudhi sana kuainishwa kuwa ‘mzazi aliye peke yake’ kwa sababu wengi huona familia za mzazi mmoja kuwa zilizoshuka moyo na zionekanazo kuchoka, zikiwa na watoto ambao ni wenye sifa mbaya. Kwa sababu sikuwa nimefikiria hivyo, mwanzoni nilikataa mashauri. Lakini nimekuja kung’amua kwamba kuwa mzazi aliye peke yake si kusikofaa hivyo.”
Ili kuunga mkono wazazi walio peke yao, unahitaji kufahamu kuwa ni wepesi wa hisia. Endelea kuwaonyesha fadhili.
Amkeni!: “Hupati fedha zozote kutoka kwa mume wako wa awali. Umemuduje hali kifedha?”
Margaret: “Ilinibidi kujidhabihu sana. Nilikuwa nimezoea kununua mavazi mapya ya vikusanyiko vya kijamii. Hata hivyo, bado sisi hununua vitu vipya, lakini hatuwezi kutumia fedha nyingi kadiri tulivyokuwa tukitumia. Bila shaka, nataka watoto wangu waonekane vizuri, hivyo ni lazima nipange matumizi vizuri. Nilianza kuweka akiba kidogo kidogo kila juma, nikimpa rafiki mwenye kuaminika ili anihifadhie, kwani nilijua nikiziweka huenda nizitumie.”
Je, utakuwa rafiki mwenye kutumainiwa kama huyo anayesaidia wazazi walio peke yao kupanga matumizi ya rasilimali zao?
Amkeni!: “Umekabilije upweke?”
Margaret: “Sikuzote mchana mimi huwa na shughuli nyingi. Jioni nyingi, wakati watoto wameenda kulala, huhisi upweke sana. Mimi hupigia simu mtu wa ukoo ama rafiki. Nyakati nyingine huwa na mazungumzo yenye kutiririsha machozi. Huzungumza kuhusu yaliyotokea wakati wa mchana. Kuwa tu na mtu atakayesikiliza ni msaada mkubwa.”
Labda unaweza kuchukua hatua ya kwanza na kumpigia simu mmoja mwenye upweke. Uhakika wa kwamba unasikiliza unaweza kuandaa faraja nyingi.
Amkeni!: “Ni jambo lipi ambalo wewe hulipata kuwa gumu sasa ukiwa mzazi aliye peke yake?”
Margaret: “Kulea watoto kwa njia iliyo safi kimaadili. Viwango vyenye kudhoofika vya kijamii na kimaadili hufanya watu washuku tamaa yangu ya kuweka maadili mazuri katika watoto wangu.”
Kuweka kwako kielelezo katika kufuata viwango vya kimungu kwa hakika kutatia wengine moyo kufanya vivyo hivyo.
Amkeni!: “Kulea vijana wawili huchukua wakati wako mwingi. Unapataje wakati wa kufanya utakalo kufanya?”
Margaret: “Hujaribu kuokoa wakati kwa ajili yangu. Kwa kielelezo, wakati rafiki anapowafunza somo la muziki, hilo hunipa muda wa saa moja. Hukaa kitako na kufunga televisheni. Nitakuwa kimya tu, nikifikiri kuhusu mambo niliyofanya wakati wa mchana. Sikuzote mimi huwa macho sana kuhusu lile lililo sawa na lile lisilo sawa, na hivyo mimi hutafakari kuhusu niliyofanya ili kuona kama ningeliweza kulifanya vizuri zaidi.”
Ukijitolea kutunza watoto mara kwa mara, mzazi aliye peke yake atakuwa na vipindi vyenye thamani vya kutafakari hivyo.
Toa Msaada Wenye Kutumika
Amkeni!: “Ni msaada gani ambao umepata kuwa wenye kutumika zaidi?”
Margaret: “Mimi hufurahia kualikwa na familia nyingine nyumbani kwao. Unapofahamu wengine wanakuhangaikia, hilo husaidia sana. Nyakati nyingine unafikiri ni wewe tu mwenye matatizo. Pia mwingine anaponisifu kuhusu njia ninavyolea watoto wangu, jambo hilo humaanisha mengi sana! Kisha kuna ile sehemu yenye kutumika ya mambo, kama vile kusaidia kupamba, kutunza bustani, kwenda dukani. . . . Ala, ningeweza kuendelea tu bila kuacha!”
Kunapokuwa na mzazi mmoja tu, mambo huonekana kuchukua muda mrefu zaidi na magumu zaidi. Kwa hivyo usichukue vivi hivi thamani ya ile zawadi ya wakati wako. Kwa wazazi walio peke yao ni moja ya zawadi zenye thamani kuliko zote.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Ili uwe mwenye kusaidia kikweli kwa wazazi walio peke yao, tumia wakati pamoja nao