Risasi Ilibadili Maisha Yangu
JAMBO lililo bora zaidi wazazi wawezalo kufanyia watoto wao ni kuwafundisha ujuzi kuhusu Muumba wao na tamaa ya kumtumikia. Msiba ulionipata nilipokuwa tineja umenisaidia kuthamini ukweli huu.
Kabla ya kueleza kile kilichotukia wakati huo—zaidi ya miaka 20 iliyopita—acha nieleze kidogo kuhusu maisha yangu nilipokuwa nikikua katika eneo la kusini mwa Marekani. Hayo yaathiri moja kwa moja jinsi nimeweza kukabiliana na hali zenye kupita kiasi.
Kilichofanyiza Maisha Yangu
Nilizaliwa katika Birmingham, Alabama—eneo la Ndani lenye ubaguzi wa kijamii la Kusini—katika Januari 1955. Nilipokuwa na umri wa miaka minane tu, mlipuko wa bomu si mbali kutoka nyumbani kwetu ulilipua kanisa wakati wa mawaidha ya kidini ya Jumapili kwa ajili ya watoto. Watoto weusi wenye hofu, wengi wakiwa karibu umri wangu, walikimbia nje wakipiga mayowe; wengine walitokwa damu na kulia. Wanne walikuwa wamekufa—wakiwa wameuawa kimakusudi na weupe.
Maafa kama hayo yalikuwa ya kawaida katika Kusini. Kiangazi kilichofuata wafanyakazi watatu wa kutetea haki za raia waliuawa kimakusudi katika Mississippi. Hizo zilikuwa siku zenye kuogofya za mvurugo wa kijamii uliotuathiri sisi sote.
Mama alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, naye Baba akawa mmoja katika 1966. Muda si muda familia nzima ilishiriki na majirani wetu tumaini letu lenye kutegemea Biblia la ulimwengu mpya wa amani. (Zaburi 37:29; Mithali 2:21, 22; Ufunuo 21:3, 4) Kila Jumamosi wakati wa viangazi vya mwishoni-mwishoni mwa miaka ya 1960, tulisafiri hadi maeneo ambayo bado kuhubiriwa nje ya Birmingham ili kuhubiri. Huko, watu walikuwa hawajasikia kamwe kuhusu Mashahidi wa Yehova au kuhusu ujumbe wa Ufalme tuliohubiri. Hata hawakujua jina la Mungu, Yehova. (Zaburi 83:18) Wakati wa nyakati hizo zenye mvurugo, kwa kweli nilifurahia kuzungumza na watu kuhusu kusudi la Yehova la kuubadilisha ulimwengu huu wa kale wenye ufisadi kwa kuleta paradiso ya kidunia.—Luka 23:43.
Kuweka Mradi Maishani
Katika Desemba 1969, nilifananisha wakfu wangu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji. Nilisali kwa Yehova na kuonyesha tamaa yangu ya moyo mweupe ya kufuatia huduma ya wakati wote ikiwa kazi-maisha. Majuma machache baadaye, Baba alipewa mgawo wa kusaidia kutaniko dogo lililoko Adamsville, kilometa chache kutoka Birmingham. Badiliko hili la eneo lilizidisha tamaa yangu ya kuwa painia, au mhudumu wa wakati wote. Kwenye kila fursa katika miaka yangu ya sekondari, nilikuwa nikifanya upainia wa muda, ambao ulitia ndani kutumia angalau saa 75 katika huduma kila mwezi.
Niliamua kujifunza ufundi fulani ili kujitayarishia huduma ya wakati wote baada ya kuhitimu. Lakini katika mwaka wangu wa mwisho katika sekondari, nilikabili tatizo fulani. Nilikuwa miongoni mwa kikundi cha wahitimu wa gredi ya juu, hivyo basi siku moja nilipelekwa kwenye koleji iliyoko karibu ili kufanya mitihani fulani ya kielimu. Baadaye niliitwa kwenye ofisi ya mkuu wa koleji. Mwanamke huyo alivutiwa na kufurahishwa nami. “Umefaulu!” akasema kwa shauku. “Unaweza kuingia koleji yoyote uichaguayo!” Alinitaka nijaze fomu za kuomba msaada wa fedha wa masomo kutoka kwa serikali mara moja.
Niliudhika kwa sababu sikuwa nimejitayarishia hilo. Mara moja nilimweleza mipango yangu ya kuwa mhudumu wa wakati wote na kufanya kazi isiyo ya wakati wote ili kujitegemeza katika huduma. Hata nilimweleza kwamba, baadaye kama vile Mashahidi wengineo wamefanya, huenda nikaweza kutumikia nikiwa mishonari katika nchi ya nje. Lakini alikuwa kana kwamba hakunisikia. Alidokeza kwamba nijifunze somo la sayansi na kwamba ikiwa ningehudhuria koleji ya hapo, angehakikisha kwamba nimepata kazi katika kitovu cha sayansi.
“Gloria, dini yako ishugulikie wakati wa miisho-juma,” akasema, “wazazi wako bado watakuonea fahari.” Nilihisi kuudhiwa kwamba alidhania mradi wangu wa huduma ya wakati wote ulikuwa tokeo la kusukumwa na wazazi wangu. Alinifanya nijihisi kusongwa, kana kwamba nilikuwa nikiipa kisogo jamii zima ya weusi kwa kukataa nafasi hii kuu. Hata hivyo, nilishikamana na uamuzi wangu. Baada ya kuhitimu, badala ya kufuatia elimu ya koleji, nilianza kufanya kazi isiyo ya wakati wote nikiwa karani.
Nilitafuta painia mwenzi lakini sikumpata. Mwangalizi asafiriye alipozuru kutaniko letu, nilimweleza tatizo langu. “Huhitaji mwenzi,” akasema. Kisha akanipangia ratiba ambayo ningeweza kutimiza madaraka yangu ya kazi ya kimwili na pia kuwa na wakati wa kutosha wa kupainia. Nilihisi hiyo ratiba ilikuwa kamili. Nilipatwa na msisimuko hivi kwamba niliweka Februari 1, 1975, kuwa siku yangu ya kuanza upainia.
Hata hivyo, siku chache baadaye, Desemba 20, 1974, nilipokuwa naenda nyumbani kutoka dukani, nilipigwa na risasi iliyofyatuliwa kiholela tu.
Nachungulia Kaburi
Nikiwa nimelala chini, kihalisi ningeweza kuona damu yangu ikimwagika. Nakumbuka nikifikiria kwamba nilielekea kufa. Nilimwomba Yehova aniruhusu kuishi kwa muda wa kutosha kumwelewesha Mama kwamba aksidenti zenye kudhuru kama hizo zingeweza hata kutukia kwa familia yenye kujitoa kumtumikia Yehova kabisa. Ingawa tulifahamu lile andiko la Biblia “wakati na tukio lisiloonwa kimbele huwapata wote,” sidhani kama tulikuwa tayari kushughulikia msiba mbaya kama huo.—Mhubiri 9:11, NW.
Hiyo risasi ilinipiga upande wa kushoto wa shingo, ikitenganisha mishipa katika uti wangu wa mgongo. Kuzungumza na kupumua kwangu kuliathiriwa. Sikutarajiwa kuishi kwa zaidi ya siku mbili. Kisha walisema “majuma mawili.” Lakini niliendelea kuishi. Mchochota wa mapafu uliponipata, nilihamishwa kwa mashine ya kusaidia kupumua ambayo ni tata zaidi. Hatimaye, hali yangu ikawa afadhali, na mipango ilifanywa kwa ajili ya urekebishaji.
Majaribio ya Urekebishaji
Sikuhisi kuvunjika moyo kwa majuma kadhaa ya mwanzo. Nilihisi kufa ganzi tu. Kila mtu kwenye Kitovu cha Urekebishaji cha Hispania cha Birmingham alikuwa mwenye fadhili na walifanya wawezavyo kwa niaba yangu. Nilianza kujua kutokana na wafanyakazi wa hospitali kwamba madaktari walinitazamia kulemaa kabisa, nikilala chali, muda wote usalio wa maisha yangu. Niliainishwa kwenye kiwango cha C2, yaani kupooza kwa miguu na mikono, ambacho kilimaanisha walihisi ningetumia mashine ya kusaidia kupumua kwa muda wote wa maisha yangu, nikiwa siwezi kusema kuzidi mnong’ono.
Madaktari walikuwa wameweka mrija wa kikoromeo ambao nilitumia kupumulia. Baadaye mtaalamu wa mapafu aliweka mrija mdogo kuona kama ningeweza kusema. Hata hivyo, hiyo saizi haikufanyiza tofauti yoyote. Hivyo wakafikia mkataa kwamba kutoweza kwangu kuzungumza kulisababishwa na kudhuriwa kwa mishipa. Yaelekea wakati huohuo nilianza kushuka moyo, na hakuna chochote mtu yeyote angeweza kusema kingenifanya nihisi afadhali. Hata neno la fadhili nililiona kama udhia. Hivyo nililia sana.
Niling’amua kwamba ikiwa jambo fulani lakinza hali yako ya kiroho, mambo mawili yanaweza kusaidia—kudumu katika sala kwa Yehova na kuwa mtendaji katika huduma, ukieleza wengine kuhusu kweli za Biblia. (Mithali 3:5) Naam, kusali kulikuwa rahisi. Ningeweza kufanya hivyo. Lakini ningewezaje, katika hali yangu, kuwa mtendaji zaidi katika huduma?
Niliomba familia yangu waniletee nakala za magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! na misaada mingine ya kujifunzia Biblia ambayo tulitumia wakati huo hudumani, kama vile Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, True Peace and Security—From What Source?, na Je, Uzima Ndio Uu Huu Tu? Hivyo viliwekwa katika sehemu mbalimbali za chumba changu. Wafanyakazi wa hospitali mara nyingi walinitazama kwa huruma na kuuliza hivi: “Kipenzi, kuna lolote naweza kukufanyia?”
Ningetazama fasihi fulani, na kwa kutamka-tamka maneno bila sauti, ningemwomba huyo mtu anisomee. Nilikuwa nikihesabu wakati ambao huyo mtu alitumia kusoma kuwa saa zangu katika huduma. Kuonyesha shukrani zangu kwa huyo mtu kwa kunisomea, mara kwa mara ningempa zawadi ya kitabu hicho au gazeti. Hivyo nilivihesabu kama maangusho yangu. Mmoja aliponisomea mara ya pili, nilihesabu ziara ya kurudia. Kushiriki kwa njia hiyo katika huduma kulinitia moyo, kama ilivyokuwa na kadi, maua, na ziara zenye kuchangamsha za wengi wa akina ndugu na dada zangu Wakristo.
Baada ya miezi ya urekebishaji, niliweza kuinua kichwa changu kidogo tu. Lakini nilikuwa nimeazimia kufikia utendaji mkubwa zaidi. Hivyo niliomba kuwa na wakati zaidi wa tiba ya maungo na kupitia utendaji. Niliomba niwekwe kwenye kiti cha magurudumu, niliambiwa kwamba hilo haliwezekani, kwamba singeweza kuweka kichwa changu kikiwa wima kiasi cha kuweza kukaa. Ingawa hivyo, niliwaomba wajaribu.
Baada ya madaktari kutoa idhini, tabibu aliyenishughulikia alinisaidia kupanda kwenye kiti cha magurudumu. Walinifunga kwa bendeji kutoka kifua hadi nyongani, kutoka paja hadi goti, na kutoka goti hadi wayo. Nilifanana na mumiani. Hii ilikuwa tahadhari kuhakikisha kwamba msongo wangu wa damu haukubadilika na kuzuia mshtuko. Ilifanya kazi! Bado, niliruhusiwa tu kuketi kwa saa moja kila wakati. Lakini niliketi—baada ya kulala chali kwa siku 57!
Nyumbani Hatimaye!
Hatimaye, baada ya miezi mitano mirefu, mrija wa kikoromeo uliondolewa, nami niliruhusiwa kwenda nyumbani. Hiyo ilikuwa Mei 1975. Baadaye, nilikuwa nikisafiri kwenda na kurudi kutibiwa kwenye kituo cha urekebishaji. Mapema kufikia kiangazi cha 1975, nilianza kwenda katika huduma ya Kikristo nikiwa katika kiti cha magurudumu changu. Singeweza kufanya mengi, lakini angalau nilikuwa huko nje na wenzangu.
Mwanzoni mwa 1976, niliombwa kwenda kwa uchanganuzi mwingine na VRS (Vocational Rehabilitation Services), shirika lililolipia urekebishaji wangu. Nilifikiri afya yangu ilikuwa ikiboreka. Nilikuwa nikijifunza kuchora kwa burashi niliyoshikilia kwa meno yangu. Nikitumia kijiti kwa njia hiyohiyo, nilikuwa nimeanza kuchapa maneno na hata kuandika mengine kwa penseli. Kwa kuwa VRS lililipia mengi ya matibabu yangu, lilitaka kunitafutia kazi ili niwe mshirika wa jamii mwenye mapato.
Mwanzoni huyo mshauri alionekana mwenye kujali, lakini alianza kuniomba niseme kwa sauti ya juu zaidi. Wakati huo ningeweza tu kusema kidogo kuzidi mnong’ono. Kisha akaniuliza hivi: “Je, huwezi kukaa wima?”
Singeweza.
“Songeza tu kidole kimoja,” akasema.
Niliposhindwa hata kufanya hivyo, alitupa kalamu yake kwenye meza na kusema kwa sauti ya kuudhika: “Wewe hufai kitu!”
Aliniambia niende nyumbani na ningojee simu kutoka kwake. Nilifahamu tatizo lake. Awali hakuna mgonjwa yeyote katika Kituo cha Urekebishaji cha Hispania aliyepata kuwa na matatizo mabaya kama yangu. Gharama ya vifaa vilivyotumiwa pale ni ya juu sana, na yule mtu mwenye madaraka ya kufanya maamuzi hakuwa na miongozo kuhusu la kufanya na mgonjwa mwenye matatizo kama yangu. Hata hivyo, iliniumiza kuitwa asiyefaa kitu, kwani tayari nilikuwa nimeanza kujihisi hivyo.
Siku chache baadaye, nilipokea simu na niliambiwa kwamba sikuwa mshirika wa hiyo programu tena. Nilijihisi kuachwa. Na hilo lilitokeza mshuko-moyo tena.
Kuushinda Mshuko-Moyo
Kisha nilifikiria lile andiko kwenye Zaburi 55:22, ambalo husema hivi: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza.” Jambo moja ambalo lilinihangaisha lilikuwa kuwalemea kifedha wazazi wangu, nami nilisali kuhusu hili.
Hali yangu ya kushuka moyo iliniathiri vibaya sana kimwili, kwa hiyo wakati wa mkusanyiko wa wilaya kiangazi hicho singeweza kuketi. Nilisikiliza programu nikiwa nimelala chini. Ile ambayo huitwa kazi ya upainia msaidizi ilianzishwa kwenye mkusanyiko huo wa 1976, nayo ilivuta uangalifu wangu. Kufanya upainia msaidizi huhitaji utumie saa 60 kwa mwezi katika huduma, wastani wa saa 2 tu kila siku. Nilihisi ningeweza kufanya hivyo. Baadaye, nilimwomba dada yangu Elizabeth anisaidie kufanya upania msaidizi. Yeye alifikiri ni mzaha, lakini nilipopeleka ombi langu la upainia katika Agosti, naye pia alipeleka.
Elizabeth angeamka mapema na kushughulikia mahitaji yangu ya kibinafsi. Kisha tungeanza kutoa ushahidi kwa kutumia simu. Ilihusisha kupigia watu simu na kuongea nao kuhusu baraka ambazo Mungu atawapa watu chini ya utawala wake wa Ufalme. Pia tuliandika barua, hasa kwa watu waliohitaji faraja. Miisho-juma familia au marafiki walinipeleka katika huduma ya nyumba kwa nyumba nikiwa katika kiti cha magurudumu changu. Yakini, kwa sababu siwezi kutumia miguu na mikono yangu, siwezi kufanya lolote ila kutangaza ujumbe wa Ufalme, kunukuu maandiko, au kuomba wengine kusoma kutoka Biblia.
Kufikia siku ya mwisho ya mwezi, bado nilihitaji muda wa saa 6 ili kutimiza takwa langu la 60. Elizabeth hakuwako kunisaidia, hivyo nilimwomba mama anirekebishie sehemu ya nyuma ya kiti cha magurudumu changu ili kikae wima. Kisha, nikitumia kijiti cha mdomo, nilichapa barua kwa muda wa saa sita. Hakuna madhara yoyote mabaya yaliyonipata! Kile nijuacho ni kwamba nilichoka kwelikweli!
Sala Yangu Yajibiwa
Juma lililofuata, nikiwa nimekaa wima katika kiti cha magurudumu changu, nilizuru Kituo cha Urekebishaji cha Hispania ili kufanyiwa ukaguzi. Daktari wangu, ambaye alikuwa hajaniona tangu nilipoondolewa kutoka kwa hiyo programu mapema mwakani, alishangaa. Hangeweza kuamini maendeleo yangu. “Umekuwa ukifanya nini?” aliuliza. Hata kabla ya kumaliza kumweleza kuhusu huduma yangu, alinipatia kazi.
Msaidizi wake alinihoji naye alipendezwa na yale niliyokuwa nikifanya katika huduma. Yeye aliniomba nishiriki katika ile iliyoitwa programu ya wagonjwa wa kiolezo. Hivyo wangenishirikisha na mgonjwa mwingine ambaye ningemsaidia. Akirejezea huduma yetu, yeye alisema hivi: “Hiyo ndiyo watu wenu hufanya, sivyo?” Nilipewa mgawo wa kusaidia mgonjwa ambaye yaelekea alikuwa na matatizo kama yangu.
Kwa njia fulani habari kuhusu yale niliyokuwa nikifanya katika huduma kwa msaada wa familia yangu zilifikia VRS. Walipendezwa sana hivi kwamba walipendekeza kwamba nirudishwe tena kwa hiyo programu. Jambo hili lilimaanisha familia yetu wangepata msaada wa kulipia vifaa maalumu na utunzi niliohitaji kutimiza utendaji wangu. Nilihisi kwamba Mungu alikuwa amejibu sala zangu.
Hali Yangu Yawa Nzuri
Kiwango changu cha kupata nafuu kimwili kimekuwa kwamba nimeweza kuinua kichwa changu, kukigeuza, na kuketi. Nashukuru kwamba uwezo wangu kamili wa kusema ulinirudia. Kwa kutumia kijiti cha mdomo, naweza kuandika, kuchapa taipureta, kupiga simu, na kuchora. Baadhi ya michoro yangu imepata kuonyeshwa katika maonyesho ya kuchora kwa mdomo. Mimi hutembea kwa kiti cha magurudumu chenye injini ambacho mimi huendesha hukiendesha kwa uelekezi wa kidevu. Lifti ya umeme hupandisha kiti cha magurudumu changu kuingia ndani ya gari, na kwa hiyo naweza kupelekwa mahali popote pale nitakapo kwenda.
Nimekuwa na matatizo mengi ya kupumua—mchochota wa mapafu ni kitisho cha daima. Nyakati nyingine mimi huhitaji oksijeni usiku. Katika 1984, nilikuwa karibu kufa kama tokeo la utatanishi uliotokana na ambukizo fulani. Nilienda hospitalini mara kadhaa. Lakini tangu wakati huo afya yangu imekuwa nzuri. Kuanzia 1976, niliweza kufanya upainia msaidizi mara moja au mara mbili kwa mwaka. Lakini sikujisikia kama nimetimiza mradi wangu. Niliendelea kufikiri kuhusu ile mipango niliyokuwa nayo nikiwa tineja ambayo ilikatizwa na risasi.
Naufikia Mradi Wangu
Hatimaye, Septemba 1, 1990, nilijiunga na mapainia wa wakati wote, hivyo nikitimiza tamaa yangu ya utotoni. Wakati wa miezi ya kipupwe kunapokuwa baridi, mimi hutoa ushahidi kwa kuandika barua na kutumia simu. Lakini hali ya hewa ikiwa na ujoto kidogo, mimi hushiriki pia katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Mwaka mzima, mimi huongoza mafunzo ya Biblia kutoka nyumbani kwa kutumia simu.
Kwa hamu kubwa natazamia wakati ujao wa ajabu katika dunia iliyo Paradiso wakati Kristo Yesu na Yehova Mungu watanikomboa kutoka kwa kiti cha magurudumu hiki. Kila siku mimi humshukuru Yehova kwa ahadi zake za afya nzuri na uwezo wa ‘kuruka-kuruka kama kulungu.’ (Isaya 35:6) Nitakimbia kadiri niwezavyo kulipia wakati niliopoteza, kisha nitajifunza jinsi ya kuendesha farasi.
Nikingojea wakati huo, nina shangwe isiyoelezeka hata sasa ya kuwa mmoja wa watu wa Yehova wenye furaha na kuwa na ushirika kamili katika huduma.—Kama ilivyosimuliwa na Gloria Williams.
[Picha katika ukurasa wa 15]
Huduma yangu ya Kikristo—kwenda nyumba kwa nyumba, kutoa ushahidi kwa kupiga simu, kuandika barua
[Picha katika ukurasa wa 16]
Michoro yangu imepata kuonyeshwa katika maonyesho ya kuchora kwa mdomo