Kanisa la Mormon—Je, Ni Urejesho wa Mambo Yote?
HEKALU la Mormon katika Salt Lake City, huko Utah, linaonwa na LDS (Watakatifu wa Siku-za-Baadaye), kuwa mfano wenye fahari wa imani yao. Bidii, thamani za familia, kujitegemea kifedha ni wito wa shime wa Wamormon. Wamishonari Wamormon, wakiwa na beji zao zenye majina, huonekana kwa kawaida ulimwenguni pote. Lakini mambo mengine ya kindani yaliyo matakatifu kwa Wamormon yamefichwa watu wa nje. Kwa hivyo hiyo dini hubaki ikiwa shabaha ya uvumi wenye kutokeza udadisi. Hata hivyo, upambanuzi ufaao, unapaswa kutegemea, si masimulizi yenye matusi, bali mambo ya hakika. Tunaweza kujifunza nini kuhusu dini hii inayosemwa vibaya?
Kanisa la Joseph Smith Leo
Wamormon wanaamini kwamba dini yao ndio urejesho wa kanisa la kweli likiwa na ukasisi na sheria zalo. Ndiyo sababu lilipata jina lalo rasmi, Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku-za-Baadaye. Katika Kanisa la Mormon, hakuna tofauti kati ya makasisi na watu wa kawaida. Badala ya hivyo, kuanzia umri wa miaka 12, kila mshiriki wa kiume anayestahili anaweza kuhusishwa katika majukumu tofauti-tofauti ya kanisa, akifikia ukasisi anapokuwa na umri wa miaka 16.
Vyeo vingi vya kanisa havina mshahara, na familia za LDS hujiunga na programu zinazotegemezwa na kutaniko la mahali pao lililo na mashirika ya ziada. Katika kiwango cha kikundi, wazee, maaskofu, na wasimamizi (wa wilaya) huangalia mambo yaliyopangwa vizuri ya kanisa. Baraza la mitume 12 katika Salt Lake City linasimamia kazi ya ulimwenguni pote. Hatimaye kuna, msimamizi wa kanisa—anaheshimiwa kama nabii, mwaguzi, mwenye kutoa mafunuo—pamoja na washauri wawili hufanyiza mamlaka ya kusimamia kanisa, iitwayo Jamii ya Usimamizi, au Usimamizi wa Kwanza.
Sheria kadhaa huathiri maisha za Wamormon waliojitolea kwa moyo wote. Ubatizo, unaofananisha toba na utii, waweza kufanywa baada ya kufika umri wa miaka minane. Kuosha na kutia mafuta hutakasa na kumweka wakfu mwamini. Sherehe ya kukubaliwa hekaluni huhusisha mfululizo wa maagano, au ahadi, na vazi la ndani la pekee la hekaluni ambalo litavaliwa muda wote baada ya hapo, likiwa ulinzi kutokana na uovu na kuwa kikumbusha cha nadhiri za usiri zilizofanywa. Pia, mume na mke Wamormon wanaweza kufunga ndoa yao katika hekalu “kwa umilele wote,” ili familia yao idumu ikiwa imeungana mbinguni, ambapo mume na mke wanaweza kuendelea kuzaa watoto.
Kanisa la Mormon limepata sifa kwa programu yalo ya kazi za kusaidia jamii, iliyoanzishwa ili “laana ya kukaa bure iondolewe.” Programu hiyo inagharimiwa na washiriki wa mahali pao ambao hujinyima milo miwili kwa mwezi ili kuchanga thamani ya hiyo milo kanisani. Kwa kuongezea, kuweka sehemu ya kumi ya mapato yao ambako ni kwa lazima kwahitajika. Familia na marafiki hutoa michango ya kutegemeza wamishonari Wamormon. Kwa kawaida hawa huwa vijana wanaume na wanawake, ambao huwa katika utumishi wa umishonari kwa miaka miwili hivi.
Kujidhabihu, familia zenye ukaribu, na madaraka ya kijamii ni mambo makuu ya maisha ya Wamormon. Lakini namna gani kuhusu itikadi za Wamormon?
Wamormon na Biblia
“Twaamini Biblia kuwa neno la Mungu mradi imetafsiriwa kwa usahihi,” chataarifu kifungu cha nane cha Articles of Faith za Wamormon. Lakini chaongeza hivi: “Pia twaamini kwamba Kitabu cha Mormon ni neno la Mungu.” Ingawa hivyo, wengi wanajiuliza ni ya nini maandiko mengine?
Mzee Bruce R. McConkie alitaarifu hivi: “Hakuna watu duniani ambao wanaiona Biblia kwa heshima kubwa kama [Wamormon] wanavyofanya. . . . Lakini hatuamini kwamba . . . Biblia ina mambo yote ya lazima kwa ajili ya wokovu.” Msimamizi Gordon B. Hinckley aliandika katika kijitabu What of the Mormons? kwamba mafarakano na makanisa mengi tofauti “yanatoa uthibitisho kwamba Biblia haitoshi.”
Waandikaji wa LDS wanaeleza tashwishi kubwa kuhusu kutegemeka kwa Biblia kwa sababu ya kufutwa na makosa ya kutafsiriwa yanayodaiwa. Mtume Mmormon James E. Talmage, katika kitabu chake A Study of the Articles of Faith, asihi hivi: “Basi acheni Biblia isomwe kwa staha na kwa uangalifu wa sala, msomaji sikuzote akitafuta nuru ya Roho ili kwamba atambue kati ya kweli na makosa ya wanadamu.” Orson Pratt mtume wa mapema Mmormon, aliongeza hivi: “Ni nani ajuaye hata kama kuna mstari mmoja wa Biblia ulioepuka uchafuzi?”
Ingawa hivyo, kuhusiana na suala hilo, Wamormon hawaelekei kutambua mambo yote ya hakika. Ni kweli, maandiko ya Biblia yamenakiliwa na kutafsiriwa tena na tena kwa miaka mingi iliyopita. Hata hivyo, uthibitisho wa usahihi wayo wa asili ni wenye kushangaza. Maelfu ya hati za awali za Kiebrania na Kigiriki yamechunguzwa kwa kina yakilinganishwa na nakala za hivi majuzi za Biblia. Kwa kielelezo, Hati-Kunjo ya Isaya ya Baharifu ya karne ya pili K.W.K., ililinganishwa na hati iliyowekewa tarehe zaidi ya miaka elfu baadaye. Je, kulikuwa na uchafuzi wowote mbaya ulioingia? Kinyume na hilo, uchanganuzi wa msomi mmoja ulitaarifu kwamba tofauti chache zilizopatikana “zilikuwa hasa za makosa madogo ya kutokaza fikira na tofauti katika mwendelezo wa herufi.”a
Baada ya kutumia maisha yote katika uchunguzi wa kindani, aliyekuwa mkurugenzi wa British Museum Sir Frederic Kenyon alitoa ushahidi hivi: “Mkristo anaweza kuchukua Biblia nzima mikononi mwake na kusema bila hofu au kusitasita kwamba anashika Neno la Mungu la kweli, lililopitishwa bila upotezo mkubwa kutoka kizazi hadi kizazi wakati wa karne nyingi.” Hivyo, maneno ya mtunga-zaburi bado ni ya kweli leo: “Maneno ya Bwana ni maneno yaliyo safi kabisa: kama fedha iliyojaribiwa katika tanuri ya dunia, iliyosafishwa mara saba.” (Zaburi 12:6, King James Version) Je, twahitaji chochote zaidi?
“Ni mpumbavu,” chakemea The Book of Mormon kwenye 2 Nephi 29:6, “atakayesema: Biblia, tuna Biblia, na hatuhitaji Biblia nyingine.” Hata hivyo, Wamormon wengi wametafakari maneno yenye uzito ya mtume Paulo katika Biblia kwenye Wagalatia 1:8 (KJ): “Iwe ni sisi au malaika kutoka mbinguni, atakayewahubiria gospeli nyingineyo yote zaidi ya ile ambayo tumewahubiria, na alaaniwe.”
Wasomi wa LDS wanaeleza kwamba andiko jipya si zaidi ya kile ambacho kimetangazwa katika Biblia bali ni usahihisho na ukamilisho wayo tu. “Hakuna mapingano kati ya hivyo viwili,” aandika Rex E. Lee, msimamizi wa Chuo Kikuu cha Brigham Young. “Vyote viwili Biblia na Kitabu cha Mormon hufundisha mpango uleule wa wokovu.” Je, kuna upatano kati ya vitabu hivi viwili? Fikiria mpango wa wokovu wa Wamormon.
“Kama Mungu Alivyo Sasa, Mwanadamu Aweza Kuwa Hivyo”
“Ingawa hatukumbuki,” aeleza Lee, “tuliishi tukiwa viumbe-roho kabla ya maisha haya.” Kulingana na itikadi hii ya LDS ya kuendelea kusikokoma, kwa utii mwingi mwanadamu anaweza kuwa mungu—muumba kama vile Mungu. “Wakati mmoja Mungu mwenyewe alikuwa kama tulivyo sasa, naye ni Mwanadamu aliyekwezwa, anayeketi enzini katika mbingu za mbali,” akataarifu Joseph Smith. “Mtahitaji kujifunza jinsi ya kuwa Miungu wenyewe, . . . sawa na vile Miungu wote wamefanya kabla yenu.” Nabii Mmormon Lorenzo Snow alisema hivi: “Kama mwanadamu alivyo sasa, wakati mmoja Mungu alikuwa hivyo; kama Mungu alivyo sasa, mwanadamu aweza kuwa hivyo.”
Je, wakati ujao kama huo unatolewa katika kurasa za Biblia? Toleo pekee la uungu lililopata kurekodiwa wakati wowote hapo lilikuwa ahadi isiyokuwa na uhalisi iliyotolewa na Shetani Ibilisi katika shamba la Edeni. (Mwanzo 3:5) Biblia huonyesha kwamba Mungu aliwaumba Adamu na Hawa waishi duniani na kuwaagiza watokeze familia kamilifu ya kibinadamu ambayo ingeishi hapa katika furaha kwa umilele. (Mwanzo 1:28; 3:22; Zaburi 37:29; Isaya 65:21-25) Kutotii kimakusudi kwa Adamu kulileta dhambi na kifo duniani.—Warumi 5:12.
The Book of Mormon chasema kwamba kama viumbe-roho wa awali Adamu na Hawa wangalibaki bila kutenda dhambi, wangalikuwa bila watoto na bila shangwe, peke yao katika Paradiso. Kwa hiyo fasili yacho ya dhambi ya mume na mke wa kwanza ilihusisha ngono na kuzaa watoto. “Adamu alikosea ili wanadamu waweze kuwapo; na wanadamu wapo, ili wawe na shangwe.” (2 Nephi 2:22, 23, 25) Kwa hiyo viumbe-roho mbinguni wanasemekana kuwa wanangojea fursa ya kuishi kwenye dunia yenye dhambi—hatua ya lazima ili kufikia ukamilifu na uungu. Lasema gazeti la LDS Ensign: “Tunakiona kile walichofanya Adamu na Hawa kwa uthamini mwingi badala ya kukiona kwa dharau.”
“Itikadi hii [kwamba mwanadamu aliishi katika uumbaji wa roho],” asema Joseph Fielding Smith, binamu wa mbali wa Joseph Smith, “haufahamiwi vizuri katika Biblia . . . kwa sababu mambo mengi yaliyo wazi na yenye thamani yameondolewa katika Biblia.” Kwa kuongezea yeye ataarifu hivi: “Itikadi hii inategemea ufunuo uliopewa Kanisa, katika Mei 6, 1833.” Kwa hiyo, ingawa inakubali mamlaka ya Biblia, kunapokuwa na kutoafikiana itikadi ya LDS sanasana huweka umaana mkubwa zaidi kwa maneno ya manabii wao.
Kitabu The Book of Mormon —Jiwe la Msingi la Dini
Joseph Smith alisifu The Book of Mormon kuwa “kitabu kilicho sahihi kuliko kitabu chochote duniani, na jiwe la msingi la dini yetu.” Seti moja ya mabamba ya dhahabu ilisemekana kwamba ilikuwa chanzo cha maandishi yake. Wamormon 11 walishuhudia kwamba waliona mabamba hayo. Ingawa hivyo, baada ya kumalizika kwa hati hiyo, Smith alisema kwamba mabamba hayo yalichukuliwa hadi mbinguni. Hivyo, hayapatikani kwa ajili ya machanganuo ya kimaandishi.
Kitabu The Pearl of Great Price (ona sanduku, ukurasa 20) chaeleza kuhusu Profesa Charles Anthon aliyeonyeshwa nakala ya baadhi ya maandishi na kuyatangaza kuwa asilia na tafsiri yayo kuwa sahihi. Lakini alipoambiwa juu ya chanzo cha mabamba hayo, usimulizi unasema kwamba yeye alibadili uamuzi wake. Hata hivyo, simulizi hilo laonekana kuwa lisilopatana, kwa dai la Smith kwamba ni yeye pekee aliyekuwa na kipawa cha kutafsiri lugha ya mabamba hayo, “ujuzi ambao ulikosekana kwa ulimwengu.” Je, Profesa Anthon angeweza kuhakikisha kuwa sahihi maandiko ambayo hangeweza kusoma na hivyo hangeweza kutafsiri?
Kitabu The Book of Mormon kinanukuu sana kutoka Tafsiri ya Biblia ya King James, ikiwa na Kiingereza chayo cha wakati wa Shakespeare ambacho tayari katika siku za Joseph Smith kilionwa kuwa cha kikale. Wasomaji fulani wamevurugika kwamba The Book of Mormon kitabu hiki kilicho “sahihi kuliko vyote”, hunakili angalau maneno 27,000 moja kwa moja kutoka tafsiri ya Biblia inayodaiwa kuwa imejaa makosa na kwamba baadaye Smith aliamua kuirekebisha.—Ona sanduku, ukurasa 24.
Ulinganisho wa toleo la kwanza la The Book of Mormon pamoja na matoleo ya wakati huu hufunua kwa Wamormon wengi uhakika wenye kushangaza—kwamba kitabu hicho kinachosemwa kuwa “kilitafsiriwa . . . kwa kipawa na nguvu za Mungu” chenyewe kimepitia mabadiliko kadhaa katika sarufi, mwendelezo wa herufi, na yaliyomo. Kwa mfano, yaonekana kuna mvurugo juu ya utambulisho wa “Baba wa Milele.” Kulingana na toleo la kwanza kwenye 1 Nephi 13:40, “Mwana-kondoo wa Mungu ndiye Baba wa Milele.” Lakini matoleo ya baadaye yanasema kwamba “Mwana-Kondoo wa Mungu ndiye Mwana wa Baba wa Milele.” (Italiki ni zetu.) Hati mbili za awali za 1830 za The Book of Mormon ziko bado. Moja ya hati hizo za awali, ambazo ni mali ya Kanisa la Yesu Kristo Lililopangwa Upya la Watakatifu wa Siku-za-Baadaye, ina maneno “Mwana” yakiwa yameongezwa katikati ya mistari.
Kwa habari ya maandiko ya Wamormon Doctrine and Covenants, kitabu The Revelations of the Prophet Joseph Smith, kilichoandikwa na msomi wa LDS Lyndon W. Cook, chaeleza hivi katika utangulizi: “Kwa sababu ya uhakika kwamba baadhi ya mafunuo yamerekebishwa na halmashauri zilizoteuliwa kuyapanga kwa ajili ya uchapishaji, kuongezwa na kufutwa kwingi kwa maandiko kumeonekana.” Badiliko moja lapatikana kwenye Book of Commandments 4:2, ambacho kilisema hivi juu ya Smith: “Ana kipawa cha kutafsiri kitabu . . . Sitampa kipawa kingine.” Lakini ufunuo huo ulipochapwa tena katika 1835 katika Doctrine and Covenants, ulisomeka hivi: “Kwa kuwa sitakupa kipawa kinginecho hadi kimalizike.”—5:4.
Mafumbo ya Kihistoria
Wengine wanaona likiwa jambo gumu kukubali kwamba Wayahudi 20 hivi walisemekana kuwa waliondoka Yerusalemu wakielekea Marekani katika mwaka 600 K.W.K. lakini kwamba kwa miaka isiyopita 30, walikuwa wameongezeka na kujigawanya kuwa mataifa mawili! (2 Nephi 5:28) Katika muda wa miaka 19 ya kufika kwao, kikundi hiki kidogo eti kilijenga hekalu “sawa na lile hekalu la Sulemani . . . na ujenzi walo ulikuwa mzuri mno”—kazi yenye kushangaza, kikweli! Ujenzi wa miaka saba wa hekalu la Sulemani katika Yerusalemu ulihitaji wafanyakazi, wahunzi, na wasimamizi wapatao 200,000.—2 Nephi 5:16; linganisha 1 Wafalme 5, 6.
Wasomaji wenye umakini wa The Book of Mormon wametatanishwa juu ya matukio fulani ambayo yanaonekana kuwa hayapatani na mfuatano wa kikronolojia ufaao. Kwa kielelezo, Matendo 11:26 lasema: “Wanafunzi waliitwa Wakristo kwa mara ya kwanza katika Antiokia.” (KJ) Lakini Alma 46:15, eti likifafanua matukio katika mwaka 73 K.W.K., lina Wakristo katika Marekani kabla hata Kristo hajaja duniani.
The Book of Mormon kinajieleza kuwa hadithi ya kihistoria zaidi ya kuwa usimulizi wa kimafundisho. Maneno “na ikawa” yanatokea mara 1,200 hivi katika toleo la sasa—mara 2,000 hivi katika toleo la 1830. Mahali pengi panapotajwa katika Biblia bado panaonekana, hata hivyo, sehemu za mahali pote panapotajwa katika The Book of Mormon kama vile Gimgimno na Zeezrom, hapajulikani.
Hadithi ya Mormon yaeleza juu ya makao yaliyoenea sana kotekote katika bara la Amerika Kaskazini. Helaman 3:8 lasomeka hivi: “Na ikawa kwamba waliongezeka na kuenea . . . ili kufunika uso wa dunia nzima.” Kulingana na Mormon 1:7, bara “likafunikwa na majengo.” Watu wengi hushangaa mahali yaliko mabaki ya ustaarabu huo ulioenea. Viko wapi vitu vya kutengenezwa vya Wanefiti, kama vile sarafu za dhahabu, panga, ngao, au mabamba ya chuma ya kifuani?—Alma 11:4; 43:18-20.
Wakifikiria maswali kama hayo, washiriki wa dini ya Mormon watafanya vyema wakifikiria kwa uzito maneno ya Mmormon Rex E. Lee: “Uasilia wa Dini ya Mormon unathibitishwa kuwa kweli au uwongo kwa kutegemea kitabu ambacho kwacho Kanisa latoa lakabu yalo.” Dini ambayo inategemea ujuzi halisi wa Kimaandiko, badala ya kipindi cha sala yenye hisia tu, hutokeza mwito wa ushindani kwa Wamormon wanyofu—na vilevile kwa wote wanaodai kuwa Wakristo.
Msingi wa Urejesho
Ni mchafuko wa kiroho uliomzunguka ambao ulimsababisha Joseph Smith akatae mafarakano yenye kupingana ya wakati wake. Wanaume wengine wenye staha kabla ya wakati wake, wakati wake, na tangu wakati wake wametafuta kurudia dini ya kweli.
Ni nini kigezo cha Ukristo wa kweli? Je, si Kristo ambaye aliweka “kielelezo, ili ninyi mfuate hatua zake”? (1 Petro 2:21, KJ) Maisha ya Yesu Kristo yako katika utofautiano mkubwa mno na mawazo ya kidini ya LDS. Ingawa Yesu hakuwa mjinyima-raha, maisha yake sahili hayakuwa na tamaa yoyote ya kukusanya utajiri, utukufu, au mamlaka ya kisiasa. Yeye alinyanyaswa kwa sababu “hakuwa wa ulimwengu.” (Yohana17:16, KJ) Lengo kuu kabisa la huduma ya Kristo lilikuwa kumtukuza Baba yake, Yehova, na kutakasa jina Lake. Jambo hilo hilo ni kweli kuhusu wanafunzi wa kweli wa Yesu. Wanaona wokovu wao kuwa na umaana wa pili.
Yesu alifundisha Neno la Mungu, akanukuu sana kutoka kwalo, na kuishi kupatana nalo. Brigham Young alisema hivi kuhusu Biblia: “Twachukua kitabu hiki kuwa kiongozi chetu, kutuongoza katika kutenda; twakichukua kuwa msingi wa imani yetu. Hicho huelekeza kwenye njia ya wokovu.” (Journal of Discourses, Buku 13, ukurasa 236) Kwa hiyo akasihi hivi: “Ichukue Biblia, linganisha dini ya Watakatifu wa Siku-za-Baadaye nayo, na uone ikiwa itastahimili huo mtihani.” (Discourses of Brigham Young) Si dini ya Mormon tu bali dini zote zinazodai kuwa za Kikristo lazima zikubali mtihani huu, kwa kuwa Yesu alisema hivi: “Waabudu wa kweli watamwabudu Baba katika roho na katika kweli.”—Yohana 4:23, KJ.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi ona Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc
[Sanduku katika ukurasa wa 20]
Maandishi Matakatifu ya Wamormon
ZAIDI ya Biblia na The Book of Mormon, Watakatifu wa Siku-za-Baadaye wanatambua maandishi mengine kadhaa.
Kitabu Doctrine and Covenants: Huu kwa msingi ni mkusanyo wa kile Joseph Smith alikiita mafunuo kutoka kwa Mungu. Haya yamefanyiwa marekebisho nyakati fulani ikitegemea maendeleo ya kimafundisho na kihistoria.
Kitabu The Pearl of Great Price: Kitabu hiki kina marekebisho ya Joseph Smith ya kitabu cha Biblia cha Mwanzo, sura ya 24 ya Mathayo, na historia ya kibinafsi ya Smith. Pia kina tafsiri ya Smith ya mafunjo aliyonunua katika 1835. Aliitangaza kuwa uandishi wa Abrahamu mwenyewe ulioeleza jinsi malaika alivyomwokoa wakati ambapo kasisi mmoja alijaribu kumtoa dhabihu kwenye madhabahu. Hayo mafunjo yalipatikana tena katika 1967 na kuchunguzwa na wastadi kadhaa wa vitu vya kale vya Misri. Ripoti moja yasema kuwa walipata kwamba “hakuna hata neno moja la tafsiri inayodaiwa kuwa ya Joseph Smith lililofanana na yaliyomo katika hati hii.” Hiyo ilikuwa Book of Breathings, hati ya Kimisri ya maziko inayozikwa na mfu. Hati ya awali ya Smith inaonyesha kwamba alitumia maneno 136 ya Kiingereza kutafsiri mwandiko wa Kimisri unaomaanisha “ziwa.”
Tafsiri ya Biblia ya Joseph Smith: Katika 1830, Smith alianza marekebisho ya Tafsiri ya Biblia ya King James, ambayo hakuyamaliza. Yeye alirekebisha mistari 3,400 na kuongeza habari nyingi, kutia ndani unabii mwishoni mwa Mwanzo kuhusu kuja kwake mwenyewe akiwa “mwaguzi bora kabisa.” Kwa kuwa hati hiyo ilibaki na mjane wa Smith, ambaye hakumfuata Brigham Young, kanisa la Salt Lake hunukuu mara chache sana kutokana nayo, ingawa yakubaliwa kuwa sahihi.
Mafundisho mengine “yaliyopuliziwa”: Haya yanaweza kutolewa na nabii wa kanisa anayeishi wakati wowote na yako sawa kimamlaka na Biblia Takatifu. Mhadhara wa King Follett uliotolewa katika 1844 ni kielelezo kimoja. Smith alitoa mhadhara huu wa maziko kwa ajili ya Mzee King Follett ambao katika huo alieleza fundisho la mwanadamu aliyefanywa kuwa mungu na Mungu aliyefanywa kuwa binadamu. Mhadhara huo unapatikana katika Journal of Discourses, mkusanyo wa mihadhara iliyotolewa na Smith, Young, na wataalamu wengine Wamormon wa karne ya 19.
[Sanduku katika ukurasa wa 21]
Familia ya Miungu ya Wamormon
Mungu: Baba wa Miungu yote, ana mwili wa mnofu na damu.—Doctrine and Covenants 130:22.
Elohim: Nyakati fulani hurejezewa kuwa mtu mmoja. Pia hufafanuliwa kuwa baraza la Miungu ambao walipanga dunia.—Doctrine and Covenants 121:32; The Pearl of Great Price, Abraham 4:1; Journal of Discourses, Buku 1, ukurasa 51.
Yesu: Mungu na Muumba wa dunia nzima, Mwokozi.—3 Nephi 9:15; 11:14.
Yehova: Jina la Yesu la Agano la Kale.—Linganisha Mormon 3:22; Moroni 10:34; na fahirisi ya Book of Mormon.
Utatu: Uungu wa watu watatu wa kiroho walio tofauti, Baba na Mwana, wa mnofu na damu, na Roho Mtakatifu.—Alma 11:44; 3 Nephi 11:27.
Adamu: Msaidizi wa Yesu katika uumbaji. Brigham Young alitaarifu hivi: “Baba yetu Adamu alikuja katika shamba la Edeni . . . na akamleta Hawa, mmoja wa wake zake. . . . Yeye ni Baba yetu na Mungu wetu.” (Journal of Discourses, Buku 1, ukurasa 50, Toleo la 1854) Baada ya dhambi yake, Adamu akawa Mkristo wa kwanza duniani. (The Pearl of Great Price, Moses 6:64-66; Ensign, Januari 1994, ukurasa 11) Yeye ndiye “Mkale wa siku” (Doctrine and Covenants 116) na ndiye Baba halisi wa kimwili wa Yesu.—Journal of Discourses, Buku 1, ukurasa 51.
Mikaeli: Jina jingine la Adamu, yule malaika mkuu.—Doctrine and Covenants 107:54.
[Sanduku katika ukurasa wa 23]
Wamormon, Utukuzo wa Taifa, na Siasa
JOSEPH SMITH—nabii, mwaguzi, mwenye kutoa mafunuo, kulingana na itikadi ya Mormon—alikuwa pia meya, mweka-hazina, jenerali-luteni, na mgombea urais wa Marekani. Wakifuata uongozi wake, Wamormon wengi ni wanasiasa wenye bidii. Hilo kanisa linaonea fahari urithi walo wa Marekani na hutaarifu kwamba Mungu aliongoza kuandikwa kwa Katiba ya Marekani. Brigham Young alisema hivi: “Wakati . . . Ufalme wa Mungu utakapoanza kutawala, bendera ya Marekani itapepea kwa fahari bila kutiwa waa kwenye mlingoti wa bendera wa Liberty na usawa wa haki, bila doa.”
Kifungu cha 12 cha Articles of Faith hutaarifu hivi: “Tunaamini katika kujitiisha chini ya wafalme, marais, watawala, mahakimu, katika kutii, kuheshimu, na kutegemeza sheria.” Ujitiisho wao ni wa kadiri gani? Marekani ilipoingia katika Vita ya Ulimwengu 1, Mzee Stephen L. Richards alisema kwa uhakika hivi: “Hakuna watu walio waaminifu zaidi kwa serikali ya Marekani kuliko Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku-za-Baadaye.” “Tunapopigana tutashinda kwa uwezo wa Mungu,” akasema mzee mwingine.
Kifungu cha 12 kilitumika katika upande ule mwingine wa uwanja wa vita vilevile. Profesa Christine E. King wa Chuo Kikuu cha Staffordshire aliandika hivi: “Wamormon Wajerumani walitiwa moyo kupigania nchi yao na kusali kwa ajili ya ushindi wayo.” Kanisa lilisema kwamba lilikuwa likipigana, si na ndugu Wamormon wa Uingereza na Marekani, bali na wawakilishi wa serikali. “Tofauti hiyo, ingawa iko wazi, ilitumika kutuliza mashaka ya maadili na kidini ya Wamormon Wajerumani.”
Wakati Hilter alinyakua mamlaka, sera ya Mormon ya uungaji-mkono wa moyo wote iliendelea. “Wanazi hawakupata ukinzani au uthibitisho wa lawama kutoka kwa kanisa la Mormon,” akaandika Dakt. King. Mkazo wa Wamormon kuhusu usafi wa jamii na uzalendo ulifaa hilo kanisa, na kwa Wamormon wengi, “mahusiano baina ya dini yao na siasa za Serikali ya Hitler yalikuwa wazi.” Wakati Wamormon kadhaa walipodhubutu kumpinga Hitler, hawakuungwa mkono na wakuu wa Mormon. “Kanisa lilikuwa lenye uzalendo na lenye uaminifu-mshikamanifu na lilikataa kwa nguvu shambulio lolote kuelekea serikali ya Nazi.” Hilo kanisa hata lilitenga na ushirika mpingaji mmoja baada ya kifo chake alipouawa na Wanazi.b
Jinsi walivyo tofauti na wale wanaosifiwa katika The Book of Mormon kwenye Alma 26:32: “Afadhali wadhabihu maisha zao kuliko hata kuua adui zao; na wamezika silaha zao za vita chini sana ardhini, kwa sababu ya upendo wao kuelekea ndugu zao.”
Yesu alisababu na Pilato hivi: “Ikiwa ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, ndipo watumishi wangu wangepigana, ili nisipelekwe kwa Wayahudi.” (Yohana 18:36, KJ) Wanafunzi wake hawakupaswa kuchukua silaha katika kumlinda Mwana wa Mungu mwenyewe, mbali na vita baina ya serikali. Hata walipaswa kupenda adui zao.—Mathayo 5:44; 2 Wakorintho 10:3, 4.
Kuna Wakristo wa kweli leo ambao wamedumisha kutokuwamo dhabiti wakiwa mmoja-mmoja na wakiwa kikundi. Kitabu Mothers in the Fatherland kilisema hivi: “Mashahidi wa Yehova tangu awali wamesimama kwa azimio mbali na serikali yoyote.” Kwa hivyo, wakati wa utawala wenye ukatili wa Hitler, “kila mmoja wao, walikataa katakata kuonyesha utii wa aina yoyote kwa serikali ya Nazi.”
Ingawa maelfu yao waliuawa kwa sababu ya itikadi zao za kidini, Mashahidi wa Yehova walichukua kwa uzito maneno ya Yesu: “Kwa hili watu wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, ikiwa mtakuwa na upendo kwa mmoja na mwenzake.”—Yohana 13:35, KJ.
[Maelezo ya Chini]
b Helmut Hübener alirudishwa katika 1948.
[Sanduku katika ukurasa wa 24]
Biblia na Maandishi ya Wamormon—Uchunguzi wa Tofauti Iliyoko
Biblia: Ingawa mahali hususa hapajulikani, shamba la Edeni yaelekea lilikuwa katika eneo la Mesopotamia kwenye Mto Frati.—Mwanzo 2:11-14.
Doctrine and Covenants: Shamba la Edeni lilikuwa katika Jackson County, Missouri, Marekani.—Doctrine and Covenants 57, kama ilivyoelezwa na Msimamizi J. F. Smith.
Biblia: Nafsi hufa.—Ezekieli 18:4, Zaire Swahili Bible; Matendo 3:23.
The Book of Mormon: “Nafsi haiwezi kufa kamwe.”—Alma 42:9.
Biblia: Yesu alizaliwa Bethlehemu.—Mathayo 2:1-6.
The Book of Mormon: Yesu alikuwa azaliwe Yerusalemu.—Alma 7:10.
Biblia: Yesu alizaliwa kupitia roho takatifu.—Mathayo 1:20.
Journal of Discourses: Yesu hakuzaliwa kupitia roho takatifu. Alizaliwa katika mnofu kupitia kwa Adamu kufanya ngono na Mariamu.—Journal of Discourses, Buku 1, kurasa 50-51.
Biblia: Yerusalemu Jipya litakuwa mbinguni.—Ufunuo 21:2.
The Book of Mormon: Yerusalemu Jipya, ni la kidunia, litajengwa na wanadamu katika Missouri, Marekani.—3 Nephi 21:23, 24; Doctrine and Covenants 84:3, 4.
Biblia: Waandikaji wa Biblia walipuliziwa kuandika mawazo ya Mungu.—2 Petro 1:20, 21.
The Book of Mormon: Manabii wacho wanasemekana kuwa waliandika kulingana na ujuzi wao wenyewe.—1 Nephi 1:2, 3; Jacob 7:26.
Biblia: Sheria ya Kimusa, kutia ndani kutoa sehemu ya kumi, ilimalizwa na kifo cha Yesu. Michango yapaswa kuwa ya hiari, si kwa kulazimishwa.—2 Wakorintho 9:7; Wagalatia 3:10-13, 24, 25; Waefeso 2:15.
Doctrine and Covenants: “Kwa kweli . . . siku ya watu wangu ya kutoa sehemu ya kumi; kwa kuwa yeye ambaye ametoa sehemu ya kumi hatachomwa (wakati wa kuja kwa [Bwana]).”—Doctrine and Covenants 64:23..
[Picha katika ukurasa wa 25]
Sanamu ya Moroni juu ya Hekalu la Mormon katika Salt Lake City, Utah