Mungu Aliacha Tumpate
WAKATI Mfalme Daudi alipokuwa tayari kumpa mwanaye Sulemani ufalme, yeye alimshauri hivi: “Mjue Mungu wa baba yako, ukamtumikie kwa moyo mkamilifu, na kwa nia ya kumkubali; kwa kuwa BWANA hutafuta-tafuta mioyo yote, na kuyatambua mawazo yote ya fikira; ukimtafuta, ataonekana nawe; ukimwacha, atakutupa milele.”—1 Mambo ya Nyakati 28:9.
Tumeliona hili kuwa kweli katika kisa chetu. Tulimtafuta Mungu, nasi kwa hakika tulimpata—lakini baada tu ya kupitishwa katika njia nyingi zisizofaa. Twaamini kwamba Yehova alitambua jinsi mawazo yetu yalivyokuwa yenye nguvu kumwelekea yeye na utumishi wake, naye akajiacha apatikane nasi. Hivi ndivyo ilivyokuwa.
Tulikuwa ndugu wanne, tuliolelewa Florida, Marekani. Baba yetu alifanya kazi kwa muda mrefu akiwa mpishi ili airuzuku familia, mama alikuwa ndiye mtunza nyumba, nasi vijana wanne tulifyeka nyasi, kuuza magazeti—chochote ambacho kingeongezea mapato ya familia. Mama alikuwa Mkatoliki, naye baba alikuwa Mbaptisti. Sote tulimwamini Mungu na Biblia lakini hatukufanya zaidi ya hilo, nasi tulienda kanisani mara chache sana. Ilikuwa mapema miaka ya 1970 na kitu, wakati ambapo amani, dangarizi zilizo kubwa sehemu za chini, nywele ndefu, na muziki wa roki yalikuwa mambo yaliyoenea sana. Yote hayo yaliathiri maisha zetu.
Ni kufikia 1982 tu ndipo wawili kati yetu, Scott na Steve—kila mmoja tukiwa wenye umri wa miaka 24 na 17—tulipoanza kuwa na upendezi wenye uzito katika Biblia na hangaiko lenye kuongezeka la hali za ulimwengu zenye kuharibika. Scott alikuwa na biashara yake mwenyewe ya ujenzi. Ilikuwa ikiendelea vizuri, hivyo tukahamia nyumba moja. Tulikuwa tumechoshwa na kutumia wakati mwingi katika mabaa na aina hiyo ya maisha na tulijua kwamba lazima kuwe na maisha mengine yenye kupendeza zaidi kwingineko. Tulianza kuhisi njaa ya mambo ya kiroho. Kuisoma Biblia yetu kwa ukawaida kulitusaidia kutamani ujuzi zaidi na ufahamu wenye kina wa Neno la Mungu.
Tulianza kwenda kwenye makanisa tofauti tofauti kila Jumapili. Katika yale tuliyoendea karibu na nyumbani kwetu katika Lake Worth, Florida, dakika 25 za hotuba ya Jumapili zilitumiwa kuzungumzia utoaji fedha. “Toa kwa ukarimu, tieni mikono yenu chini zaidi kwenye mifuko yenu,” ndivyo mhudumu angesema akiwa ameegemea kinara cha msemaji. Mara nyingi wangepitisha kisahani cha kukusanyia fedha mara tatu katika mkutano mmoja, jambo ambalo lilifanya wengine waondoke wakiwa bila fedha zozote mifukoni mwao. Tulienda kwenye makanisa mengi, lakini tulilokuta ni visahani zaidi vya kukusanyia fedha vikipitishwa na vikusanyiko vya kirafiki.
Twaonywa Juu ya Mashahidi wa Yehova
Tulikuwa tumefundishwa tuliyofikiri kuwa mafundisho ya msingi ya Biblia, nasi tuliyakubali kwa kuwa walimu walikuwa wataalamu wa kitheolojia. Somo moja lilikuwa juu ya vidhehebu vya Amerika, na cha kwanza katika hiyo orodha kilikuwa Mashahidi wa Yehova. Tulionywa kuwa wao hawakumwamini Yesu, kwamba walikuwa na Biblia yao wenyewe, kwamba hawakuwa wanaenda mbinguni, na kwamba waliamini hakukuwa na moto wa mateso. Bila shaka yote haya yalifanya tufikie mkataa wa kwamba Mashahidi walikuwa dini ya uwongo.
Kufikia sasa tulikuwa na bidii sana lakini si kupatana na ujuzi sahihi. (Warumi 10:2) Tulijua aliyosema Yesu kwenye Mathayo 28:19, 20—lazima tuhubiri habari njema za ufalme na kufanya wanafunzi. Kwa wakati huo tulikuwa tunahudhuria kanisa lenye washiriki 2,000 linaloitwa Bible Town, ambako tulikuwa sehemu ya kikundi cha vijana karibu 100 wenye umri wa kati ya miaka 17 na 30. Scott alijaribu kuwafanya washiriki kuhubiri angalau kwa njia moja au nyingine—lakini hakufanikiwa.
Hivyo tukaanza kampeni yetu wenyewe ya kuhubiri. Scott alipata wazo la kusimamisha kibanda katika soko la huko la kuuza vitu vilivyokwisha kutumiwa ili kugawanya trakti na Biblia. Kwa hivyo hilo ndilo tulilofanya. Tulienda kwenye duka la vitabu la “Kikristo” tukanunua trakti na Biblia nyingi, kisha tukaenda kwenye soko, tukasimamisha meza mbili, tukaweka mbao juu yazo, tukaweka trakti na Biblia zetu juu yazo, na kujaribu kuwa “watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu.”—Yakobo 1:22.
Kadiri majuma yalivyopita, huduma katika lile soko ilizidi kukua, tukiangusha fasihi za Kiingereza na hata zile za Kihispania. Pia, tulikuwa na Biblia kadhaa, aina mbalimbali 30 za trakti, na hata vibandiko kwenye kofia vilivyosema “Mungu akupenda.” Muda mfupi baadaye, Scott alinunua mashine ya kuchapishia jumbe ndogondogo za Biblia kwenye T-shati—ziliandikwa mambo kama vile: “Je, umeisoma Biblia yako leo?,” “Je, unajiuliza ni kwa nini ninatabasamu? Yesu yuko moyoni mwangu,” na mengine mengi. Moja iliandikwa “Ufunuo” pamoja na picha ya wale wapanda farasi wanne.
Tulidhani kwamba kwa kuvaa hizo T-shati kila mahali, tulikuwa tukitoa ushahidi wa kimya-kimya. Kila Jumamosi na Jumapili, kuanzia saa 2 asubuhi hadi saa 7 mchana, mtu angeweza kuona huduma zetu mbalimbali katika lile soko la kuuzia vitu vilivyokwisha kutumika. Ikiwa ungekuwa ukitembea kwenye sehemu ya kuegesha magari na ukaona trakti kwenye magari—hiyo ilikuwa kazi yetu. Fasihi zote zilitolewa kwa upaji wa hiari, ingawa tulipata fedha chache sana. Mwaka mmoja tulihesabu gharama za matumizi ya mwaka huo, nazo zilifikia zaidi ya dola 10,000.
Twakutana na Mmoja wa Mashahidi wa Yehova
Wakati mmoja, tulipokuwa tukiogelea kwenye mojapo fuo katika Bonita Springs, mtu mwenye umri zaidi alitufikia na kusema kwamba aliona vile vibandiko kwenye gari letu na T-shati zetu. Alianza kuzungumza juu ya Biblia na kusababu kutoka kwenye Maandiko. Alitokeza ile hoja kwenye Matendo 2:31, akiuliza: “Ikiwa kungekuwa na helo yenye moto na ikiwa ni watu wabaya tu ndio walioenda huko, basi ni kwa nini Biblia iseme kwamba Yesu alikuwa huko?” Naye akaendelea, akizungumzia maandiko mengine mengi. Hatimaye, Scott akasema: “Lazima uwe mmoja wa Mashahidi wa Yehova.” Akajibu: “Ndiyo, mimi ni mmoja wao.” Kisha Scott akasema: “Ninyi watu hammwamini Yesu.” Kwa dakika 20 zilizofuata, huyo Shahidi alizungumza juu ya Yesu, lakini kwa njia fulani mazungumzo yake hayakuwa na matokeo yoyote kwetu.
Tuliendelea na huduma zetu kwenye lile soko la kuuzia vitu vilivyokwisha kutumika wakati wa miisho-juma. Tulikuwa tumefanya hivyo kwa miaka mitatu—nyakati zote tukiamini kwamba tulikuwa na ile kweli nasi tulikuwa tukifanya jambo lifaalo. Bado tulikuwa tukitembelea makanisa, kanisa moja kila jioni ya Jumapili, nasi hatukuridhishwa na lolote la yale tulitembelea. Tulikuwa karibu kumaliza makanisa ya kutembelea, hivyo jioni moja tuliamua kwenda kwenye mojapo “makanisa ya Mashahidi wa Yehova,” kama tulivyoyaita. Tulikuwa tunaenda kuwahubiria juu ya Yesu. Tulipata anwani yao kwenye kitabu cha simu nasi tukaenda huko jioni moja ya Jumapili. Tulipogundua kwamba hawakuwa wakikutana jioni ya Jumapili kama yalivyofanya makanisa mengine yote, tukaamua kwamba kwa kweli hawakumwamini Yesu. Tuliona funzo la kitabu la jioni ya Jumatatu kwenye maandishi yanayoonyesha nyakati za mikutano. Basi tukarudi huko tukiwa tumebeba Biblia zetu na tukiwa tumevaa T-shati zetu. Twakumbuka tukitumia dakika kadhaa ili kuamua ni T-shati zipi ambazo tungevaa—ni zipi zingetoa ushahidi mzuri. Tulifika huko mapema kidogo, ndugu kadhaa walitufikia. Walikuwa wenye shauku na urafiki. Mara moja tukaanza mazungumzo mazito juu ya Ufunuo. Wakatuomba tuhudhurie ule mkutano. Wakatupa kile kitabu Wenye Umoja Katika Ibada, hivyo tukakaa kitako.a Ndugu mmoja alifungua funzo hilo kwa sala.
Tulisikiliza kwa makini. Katika kumalizia, alisema: “Katika jina la Yesu. Ameni.” Tulitazamana kwa mshangao. “Je, tulimsikia vizuri? Yeye alisali katika jina la Yesu!” Wakati huo ni kana kwamba macho yetu yalifumbuka na magamba yakaanguka. Ikiwa mioyo yetu ilikuwa sawa, huu ulikuwa ndio wakati wa kusikia. Yule ndugu akawaomba wote kufungua sura ya 21 ya kitabu Wenye Umoja Katika Ibada, ambayo ilikuwa juu ya Yesu na kutokuwa sehemu ya ulimwengu. Hakukuwa na funzo jingine bora kuliko hilo ambalo tungepata kuhudhuria. Lilikuwa juu ya maisha ya Yesu na huduma yake, siku za mwisho, na kutokuwamo. Tuliwasikia walio wachanga wakitoa maelezo juu ya mambo mengi ambayo hatukuyajua kamwe. Halafu tena, katika kumalizia mkutano, yule ndugu akaomba katika jina la Yesu!
Twalishwa Kiroho
Tulikuwa tumeingia ndani ya hilo jumba tukiwa wenye kiu kwa ajili ya kweli, nayo kweli ilikuwa humo, haikuwa mbali kamwe. Tuliondoka tukijua kwamba tulikuwa tumelishwa kiroho, nasi hatukutembelea makanisa tena. Jioni iliyofuata, tulipokuwa tukifua nguo zetu katika mahali pa kufulia nguo, tuliona rundo kubwa la magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! karibu na mashine ya kuuzia soda—angalau magazeti 150. Mbeleni hatungeweza kuyasoma, lakini sasa tuliyafunga mafungu-mafungu, na kwenda nayo kwa sababu tulipendezwa na habari zayo mbalimbali.
Makala moja iliuliza, “Je, wewe waamini Utatu?” Nyingine, “Je, kweli kuna helo?” Katika Amkeni! moja kulikuwa na makala juu ya mifano. Usiku huo Steve alisoma ile makala juu ya Utatu, akafanya utafiti mwingi, akasoma maandiko yote, na kumwamsha Scott saa 6:30 usiku kwa sababu ya yale aliyokuwa amejifunza. Siku iliyofuata, Jumatano, baada ya kazi, Steve akasoma ile makala juu ya helo. Makala hiyo ilisababu kwa kutumia Yohana 11:11, ambapo Yesu alisema kwamba Lazaro alikuwa amelala. Steve alipomwona Scott, yeye alisema: “Biblia yangu haifundishi kwamba kuna moto wa helo.” Baada ya kusoma Amkeni! juu ya mifano na aina mbalimbali za misalaba, tulitupa vyetu kwenye gari la kuchukua takataka nasi tukaangalia vikipelekwa. Sote wawili tukatazamana, tukatikisa vichwa vyetu, na kutabasamu. Tulijua tulikuwa tumepata kitu cha pekee sana—ile kweli.
Siku moja baadaye masanduku mawili yalifika. Ndani yamo mlikuwa na trakti 5,000 zilizosema kwamba ikiwa hungetubu, ungeenda kwenye moto wa mateso. Tulijua nyingi za trakti hizo hazikuwa sahihi kulingana na mafundisho ya Biblia. Tukiwa tumetatanika kidogo, tukahudhuria tena funzo la kitabu Jumatatu jioni na tukabeba nyingi za trakti zetu. Tuliuliza, “Je, trakti hii ni sawa?” Usiku mmoja tulizichunguza zote. Upesi kukawa na rundo la trakti kwenye sakafu; hakuna hata moja iliyopatana na mafundisho ya Biblia. Tukaziondoa zote. Tulijua kwamba imani yetu mpya ilimaanisha uhai wetu na wa wale tuliohubiria. Tukataka kuondoka ili tujifunze Biblia bila masumbufu.
Tulihamia Alaska. Kwenye mkutano wetu wa kwanza huko, tulimuuliza mzee ikiwa angeweza kujifunza nasi kila siku. Nafikiri kwamba wote waliokuwapo walitusikia. Tulifanya maendeleo mazuri, tukamaliza kitabu Kuishi Milele, na kutaka kubatizwa kwenye mojapo makusanyiko ya siku mbili.b Lakini tulilazimika kungoja kwa muda kidogo. Mradi wetu ulikuwa kupainia. Bila kutazamia, baba yetu akawa mgonjwa, ikawa lazima turudi Florida ili kusaidia.
Twafanya Maendeleo Kufikia Ukomavu wa Kiroho
Katika Florida tulifanya maendeleo mazuri, tukamaliza kitabu Wenye Umoja Katika Ibada, na kisha tukabatizwa 1987. Ilikuwa miezi 11 tangu tulipoanza kwa mara ya kwanza. Mara tu baada ya hapo tukawa mapainia-wasaidizi kwa miezi sita halafu mapainia wa kawaida. Mwaka mmoja na nusu tu baadaye, sote wawili tukawekwa kuwa watumishi wa huduma. Miaka miwili baada ya ubatizo, tukajikuta tukitumikia kwenye Betheli ya Brooklyn, ambako Scott angali anatumikia leo naye amekuwa akijifunza Kichina kwa miaka miwili. Steve sasa anatumikia katika Moscow, Urusi, akiwa painia wa kawaida. Sote wawili tuliiona kweli na kule kuitafuta kuwa tu kama vile Mithali 2:1-5 ielezavyo: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; naam, ukiita busara, na kupaza sauti yako upate ufahamu; ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; ndipo utakapofahamu kumcha BWANA, na kupata kumjua Mungu.”
Jinsi Steve Alivyofika Moscow
Nikiishi katika New York, ambako kujua lugha ya ziada kungefanya kazi ya kuhubiri iwe yenye kupendeza zaidi—nami nikifikiria kwamba Yehova angefungua mlango wa kuingia Urusi karibuni—niliamua kujifunza Kirusi. Wakati huo, nikitumika katika Betheli ya Brooklyn, nikaanza kuhudhuria funzo la kitabu la Kirusi. Kulikuwa na kikundi kimoja tu cha funzo la kitabu la Kirusi ambacho kilikutana kila Ijumaa. Kadiri muda ulivyopita, nikaanza kujihusisha zaidi na zaidi katika kikundi cha Kirusi. Nilijiunga nao katika utendaji wa kuhubiri, ambao ulikuwa wenye kupendeza sana kwa sababu ya uchangamfu wa Warusi. Niliandikia Idara ya Utumishi nikiomba kuhamia kikundi cha Kirusi. Nilifurahi walikubaliana na hili.
Siku moja kwenye ibada ya asubuhi ya Betheli, msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society, Milton G. Henschel, aliiambia familia kwamba kungekuwa na ripoti ya pekee. Kisha akatangaza kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wametambuliwa kisheria katika Urusi na kwamba ndugu zetu wangeweza sasa kufurahia uhuru wa ibada. Sidhani kwamba yeyote katika Betheli asubuhi hiyo atasahau furaha tuliyohisi baada ya kusikia habari hizo za ajabu. Katika pindi hiyo nilifikiri kwamba lingekuwa pendeleo kubwa kuweza kuwa katika sehemu ya eneo hilo kubwa jipya.
Nilianza kuandikiana na ndugu wa Kirusi aitwaye Volodeya, anayeishi Krasnodar, Urusi. Alinialika nitembelee Urusi. Hivyo katika Juni 1992, nilifunga mizigo yangu na kuelekea Moscow. Nilipofika, nilifurahi sana kumwona Ndugu Volodeya akiningoja kwenye uwanja wa ndege. Nilikaa na Ndugu Stephan Levinski—mwenye miaka 45 katika kweli. Yeye alikuwa Shahidi wa kwanza niliyekutana naye Moscow, naye alikuwa amefungwa miaka mingi katika gereza kwa sababu ya msimamo wake kwa ajili ya kweli. Ukarimu wa kina ndugu ulikuwa wenye kupendeza kwelikweli.
Hivyo nilikuwa Moscow, bila kuijua lugha hiyo. Wakati huo, kulikuwa na makutaniko manne tu, na ilionekana kuwa tuliwajua ndugu wote. Tangu wakati huo, kwa kufanya hili na lile, nimefaulu kurefusha muda wangu wa kukaa. Ninaweza kufanya kazi mara kwa mara ili kulipia matumizi yangu. Tatizo kubwa zaidi nililokuwa nalo lilikuwa kujifunza Kirusi cha kutosha ili kuwasiliana na kulishwa kiroho kwenye mikutano. Hilo lilikuwa polepole, na bila shaka, ningali nashughulika nalo.
Nimekuwa na pendeleo la kuhudhuria mikusanyiko mingi sana na kujionea ukuzi wenye kushangaza na watu wengi sana wakibatizwa. Kuona bidii ya ndugu zetu huku kumekuwa kitia-nguvu cha imani sana. Singeweza kubadili hilo kwa ajili ya kingine chochote. Wengi wa ndugu na dada niliokutana nao ambao walikuwa wakijifunza tu au walikuwa wamebatizwa tu wakati nilipokuja sasa wanatumikia wakiwa mapainia wa wakati wote au watumishi wa huduma au Wanabetheli katika Solnechnoye, karibu na St. Petersburg, Urusi.
Katika kutaniko ninalohudhuria watu 530 hujaa pomoni kila Jumapili, na kila mwezi tuna wastani wa wahubiri wapya 12 wasiobatizwa. Hesabu ya mwisho iliyofanywa ilionyesha wahubiri 380, wazee 3, na watumishi wa huduma 7. Kutaniko letu laripoti zaidi ya mafunzo ya Biblia nyumbani 486. Katika mwezi wa Februari 1995, nilikuwa na pendeleo la kutembelea mafunzo yetu ya kitabu 29 ili kutoa hotuba ya utumishi. Nilitembelea vikundi vinne kila juma. Pia tuna shughuli nyingi ya kurudia yale maswali pamoja na wataka-kubatizwa kabla ya kila mkusanyiko. Katika mwezi wa Mei 1995, tulikuwa na siku ya kusanyiko la pekee ambapo 30 walibatizwa kutoka kwenye kutaniko letu. Kwa ujumla, 607 walibatizwa na karibu 10,000 wakahudhuria. Katika mkusanyiko wa wilaya uliofanywa wakati wa kiangazi, 24 kutoka kwenye kutaniko letu walikuwa miongoni mwa 877 waliobatizwa! Tuna mapainia 13 katika kutaniko letu na mapainia 3 wa pekee. Wote pamoja wanaripoti mafunzo 110! Kwa sasa, tuna wahubiri wasiobatizwa 132.
Kwenye ukumbusho wetu katika 1995, hudhurio lilikuwa 1,012! Sosaiti imemtuma ndugu Mpolandi, Mateysh, kwenye kutaniko letu. Alifuzu Shule ya Mazoezi ya Kihuduma naye atakuwa msaada mkubwa. Sasa tuna wazee watatu. Hivyo kutaniko jingine litaanzishwa, na eneo letu—linalokaribia watu milioni moja—litagawanywa mara mbili. Kila kutaniko litakuwa na karibu wahubiri 200. Kutaniko moja litakuwa na wazee wawili na lile jingine mzee mmoja. Kuna kusanyiko jingine linalokaribia, hivyo sasa tunarudia maswali na wale 44 ambao watakuwa tayari kwa ajili ya ubatizo wakati huo. Lasikika kuwa jambo lisilosadikika! Paradiso ya kiroho kwelikweli! Inastaajabisha! Kwelikweli ni mkono wa Yehova unaofanya kazi hiyo. Gari lake laonekana kuwa lasonga mbio kupitia Urusi wakati huu. Kuanzia Oktoba 1995, kuna makutaniko 40 Moscow. Yangeweza kuongezeka maradufu kwa urahisi ikiwa kungekuwa na wazee wa kutosha.
Zile siku za huduma zetu kwenye soko la kuuzia vitu vilivyokwisha kutumiwa zimepitilia mbali. Scott yuko katika Betheli ya Brooklyn, Steve anatumikia akiwa mzee katika mojawapo makutaniko ya Moscow—sote wawili tukiwa wenye furaha sana kwamba Mungu alijiacha apatikane nasi. Twasali kwamba mamilioni bado yatapata kumtafuta na kwamba Mungu atajiacha apatikane nao.—Kama ilivyoelezwa na Scott na Steve Davis.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 12]
Scott
[Picha katika ukurasa wa 13]
Steve
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kutaniko moja la Moscow lina wahudhuriaji zaidi ya 530 kila Jumapili