Maoni ya Biblia
Je, Wakristo wa Kweli Wanaweza Kutazamia Ulinzi wa Kimungu?
ILI kupeleka vitu vya kutuliza kwa waabudu wenzi, Wakristo, baada ya sala, walisafiri katika msafara kupita eneo lenye vita ambapo wangeweza kuuawa. Walifika salama, kwa mshangao mkuu wa majeshi yenye kupigana. Je, malaika wa Mungu aliwalinda?
Mume na mke Wakristo ambao walikuwa wametumikia wakiwa wahudumu kwa miaka mingi waliuawa wakati ndege ilipoanguka mahali ambapo walikuwa wakieneza evanjeli nyumba kwa nyumba. Kwa nini malaika wa Mungu hakuwaongoza au kuongoza hiyo ndege kwingineko katika pindi hiyo hususa?—Linganisha Matendo 8:26.
Tukilinganisha matukio haya, twaweza kuuliza: “Kwa nini Wakristo fulani hufa wakiwa wanafanya mapenzi ya Mungu, ilhali wengine, mara nyingi katika hali hatari mno, huishi? Je, Wakristo waweza kutazamia ulinzi wa kimungu, hasa katika hizi “siku za mwisho” zilizo hatari?—2 Timotheo 3:1.
Kusudi la Ulinzi wa Kimungu
Yehova Mungu ameahidi kubariki na kulinda watu wake. (Kutoka 19:3-6; Isaya 54:17) Alifanya hivyo kwa njia yenye kutokeza katika karne ya kwanza, wakati ambapo kutaniko la Kikristo lilikuwa changa. Kulikuwa na miujiza ya kila aina. Yesu alizidisha chakula kulisha maelfu; yeye na wafuasi wake walitibu kila aina ya maradhi na kasoro, kutoa viumbe-roho wenye kupita uwezo wa kibinadamu kutoka kwa wale waliopagawa na roho waovu, na hata kufufua wafu. Chini ya mwelekezo wa kimungu kutaniko hilo lisilokomaa lilikua na kuimarishwa kabisa. Hata hivyo, licha ya utegemezo ulio wazi wa Mungu, Wakristo wengi waaminifu walipatwa na kile kiwezacho kuitwa kifo cha kabla ya wakati.—Linganisha Zaburi 90:10.
Fikiria visa vya Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo. Wakiwa wamechaguliwa kuwa mitume, wao, pamoja na Petro, walikuwa miongoni mwa marafiki wa Kristo wa karibu zaidi.a Lakini Yakobo aliuawa kwa sababu ya imani yake katika mwaka wa 44 W.K., ilhali ndugu yake Yohana aliishi hadi kwenye mwisho wa karne ya kwanza. Kwa wazi wote walikuwa wakifanya mapenzi ya Mungu. Kwa nini Yakobo aliruhusiwa kufa, ilhali Yohana aliishi?
Mungu Mweza Yote kwa hakika alikuwa na uwezo wa kuokoa uhai wa Yakobo. Kwa kweli, muda mfupi baada ya kuuawa kwa Yakobo kwa sababu ya imani, Petro aliokolewa kutoka kifo na malaika wa Yehova. Kwa nini malaika hakumwokoa Yakobo?—Matendo 12:1-11.
Kutumiwa Katika Kutimiza Kusudi la Mungu
Ili kuelewa kwa nini ulinzi wa kimungu hutolewa, lazima tuelewe kwamba huo hutolewa si tu ili kuwezesha watu mmoja-mmoja waishi muda mrefu bali ili kulinda jambo la maana zaidi, kutimizwa kwa kusudi la Mungu. Kwa kielelezo, kuokoka kwa kutaniko la Kikristo kwa ujumla kumehakikishwa kwa sababu kunapatana kwa ukaribu na kutimizwa kwa kusudi hilo. Hata hivyo, Kristo aliwaambia waziwazi wanafunzi wake kwamba wao wakiwa watu mmoja-mmoja wangeweza kukabili kifo kwa sababu ya imani yao. Baada ya kutaarifu hilo, Yesu alikazia, si wokovu wa kimuujiza, bali ‘uvumilivu hadi mwisho.’ (Mathayo 24:9, 13) Uhakika wa kwamba watu fulani mmoja-mmoja walilindwa, ilhali wengine hawakulindwa, hauonyeshi kwamba Mungu ni mwenye upendeleo. Mungu alitumia tu mtu aliyekuwa katika hali bora zaidi ili kutimiza kusudi lake, ambalo hatimaye litanufaisha wanadamu wote.
Kwa kuwa kifo cha kabla ya wakati katika utumishi wa Mungu ni jambo liwezalo kutokea kihalisi, Wakristo wanapaswa kuwa na mtazamo wenye usawaziko kama wale Waebrania watatu waaminifu ambao walihukumiwa kifo kwa sababu ya kumwabudu Mungu. Wao walimwambia mfalme wa Babiloni hivi: “Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa na tanuru ile iwakayo moto; naye atatuokoa na mkono wako, Ee mfalme. Bali kama si hivyo, ujue, Ee mfalme, ya kuwa sisi hatukubali kuitumikia miungu yako, wala kuisujudia hiyo sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha.”—Danieli 3:17, 18.
Yehova alihifadhi uhai wa Petro na Yohana kwa sababu ya fungu lao kuu katika kutimizwa kwa kusudi lake. Petro alitumiwa ‘kuimarisha’ kutaniko kwa kufanya kazi ya uchungaji, ambayo ilihusisha kuandika vitabu viwili vya Biblia vilivyopuliziwa. (Luka 22:32) Yohana aliandika vitabu vitano vya Biblia naye alikuwa “nguzo” katika kutaniko la mapema.—Wagalatia 2:9; Yohana 21:15-23.
Jinsi Yehova aamuavyo kihususa ni wakati gani na kwa njia gani ataingilia katika maisha za watumishi wake ni vigumu kusema kimbele. Yote yawezayo kusemwa kwa uhakika ni kwamba Kristo aliahidi kuwa na wafuasi wake “siku zote, hata ukamilifu wa dahari.” (Mathayo 28:20) Kihususa, yeye ‘atakuwa pamoja nasi’ kupitia mwelekezo wa kimalaika wa kazi ya kuhubiri. (Mathayo 13:36-43; Ufunuo 14:6) Zaidi ya maonyesho hayo ya ujumla, hatuwezi kutarajia kihususa jinsi msaada wa kimungu utakavyoonyeshwa au ni nani ambao huenda watapokea ulinzi wa kimungu. Namna gani ikiwa Mkristo ahisi kwamba amekuwa akipata ulinzi na mwongozo wa Mungu? Kwa kuwa hili haliwezi kuthibitishwa au kutothibitishwa kwa uhakika, hakuna yeyote apaswaye kuhukumu madai yenye unyoofu ya mtu huyo.
Je, Mungu Hana Hisia?
Je, uhakika wa kwamba Mungu huruhusu kifo cha Wakristo huonyesha kwamba kwa njia fulani yeye hana hisia? Sivyo hata kidogo. (Mhubiri 9:11) Yehova anafanya kazi ili kuhifadhi uhai wetu si kwa miaka michache tu au hata miongo michache bali kwa umilele. Kutoka kwenye mahali pake pakuu pa kutazama, yeye huongoza matukio kwa ajili ya hali-njema idumuyo milele ya kila mtu ampendaye au amkaribiaye. (Linganisha Mathayo 18:14.) Utimizo wa kusudi lake utamaanisha kuondolewa kabisa kwa kitu chochote ambacho kimetutesa katika mfumo huu wa mambo—hata kifo. Shughuli za Mungu ni tata sana na kamilifu hivi kwamba mtume Paulo alisukumwa kupaaza sauti hivi: “Jinsi zilivyo kuu utajiri na hekima na maarifa ya Mungu! hukumu zake hazichunguziki, wala njia zake hazitafutikani!”—Warumi 11:33.
Kwa kuwa hakuna kitu kiwezacho kututenganisha na upendo wa Mungu, swali ambalo kila Mkristo apaswa kuuliza si ‘Je, nitapata ulinzi wa kimungu?’ bali ‘Je, nina baraka ya Yehova?’ Ikiwa tunazo, yeye atatupatia uhai wa milele—hata tupatwe na nini katika mfumo huu wa mambo. Kukilinganishwa na umilele wa uhai mkamilifu, kuteseka kokote—hata kifo—katika mfumo huu wa mambo kutaonekana kuwa hali “nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu.”—2 Wakorintho 4:17.
[Maelezo ya Chini]
a Petro, Yakobo, na Yohana walishuhudia mgeuko-sura wa Yesu (Marko 9:2) na ufufuo wa binti ya Yairo (Marko 5:22-24, 35-42); walikuwa karibu na Bustani la Gethsemane wakati wa jaribio la kibinafsi la Yesu (Marko 14:32-42); na wao, pamoja na Andrea, walimwuliza Yesu kuhusu uharibifu wa Yerusalemu, kuwapo kwake kwa wakati ujao, na umalizio wa mfumo wa mambo.—Mathayo 24:3; Marko 13:1-3.