Uasilishaji—Napaswa Kuuonaje?
NI DHAHIRI kwamba matatizo yanaweza kuzuka ikiwa wazazi-walezi wanatalikiana au mwenzi mmoja anakufa. Lakini huenda ni mtoto aliyeasilishwa ambaye mara nyingi huhisi mkazo mwingi zaidi. Kwa nini?
Wengi wetu tunawajua wazazi wetu wa kiasili. Hata kama walikufa tulipokuwa wachanga, tuna kumbukumbu, au labda picha, za kukamilisha muunganisho. Ingawa hivyo, namna gani juu ya mtoto ambaye alipelekwa akaasilishwe mara tu baada ya kuzaliwa? Shirika la uasilishaji huweka habari kumhusu mama, lakini habari hiyo mara nyingi haitolewi hadi mtoto anapokuwa na umri wa kutosha. Katika visa vingine, mama husajili jina lake mwenyewe kwenye cheti cha kuzaliwa lakini huacha lile la baba. Vitoto fulani ni vipatikanwaji—vilivyopatwa baada ya wazazi wavyo wasiojulikana kuviacha. Watoto katika hali hizi zote hukosa misingi ya kiasili—huenda wakahisi kuwa wameondoshwa kutoka vyanzo au asili yao.
Ni Imara Kadiri Gani?
Miti huhitaji mfumo mzuri wa mizizi ili usimame imara. Chipukizi jipya lililopandikizwa kwenye shina lililokomaa huenda likasitawi vyema, lakini huenda likanyauka pia na kukosa kutokeza matunda. Vivyohivyo, ingawa huenda wazazi-walezi wakaandaa utunzi wote na ujitoaji wenye upendo iwezekanavyo, watoto fulani hawaponi kamwe mshtuko wa kuondoshwa kutoka vyanzo vyao.
Fikiria kisa cha Kate.a Akizaliwa na wazazi kutoka West Indies, akiwa kitoto Kate aliasilishwa na mume na mke weupe wenye upendo, lakini hakuweza kujipatanisha na mazingira yake mapya. Alipokuwa na umri wa miaka 16, aliondoka nyumbani na kutorudi tena kamwe. Kufikia wakati huo uchungu ulikuwa umegeuka kuwa chuki isiyosababu. “Kwa nini mama yangu alinipa kwenu?” akataka kujua. Kwa kuhuzunisha, familia hii ilishindwa kuweza tatizo hilo.
Mervyn aliwekwa katika utunzi wa mamlaka ya mahali alipoishi baada ya kuzaliwa tu na kisha kwa wazazi-walezi. Alipokuwa na umri wa miezi tisa, aliasilishwa. Malezi yake ya mwanzoni yasiyo salama, pamoja na chuki yenye kuwaka kwa kuwa wa jamii iliyochanganyika, ilisitawi na kuwa mtazamo wa uasi ukimletea taabu nyingi na huzuni yenye kina kwa wazazi-walezi wake, ambao walimfanyia mengi sana. “Ikiwa mtu yeyote angeniuliza shauri kuhusu uasilishaji,” mama yake akasema, “sasa ningesema, ‘Lifikirie jambo hilo kwa uangalifu.’”
Kinyume na hilo, fikiria ono la Robert na Sylvia. Walikuwa na mwana mmoja na hawakuweza kupata watoto zaidi. “Je, mmepata kufikiria juu ya kuasilisha mtoto wa taifa jingine?” waliulizwa. Upesi walichukua Mak-Chai, kitoto kisichana chenye umri wa miezi tisa kutoka Hong Kong ili kukiasilisha. “Mara nyingi mimi hujiuliza ni kwa nini niliachwa,” asema Mak-Chai, “na ikiwa nina ndugu au dada wowote. Lakini nafikiri niko karibu zaidi na mama na baba-mlezi wangu kuliko watoto wengi wa kiasili kwa wazazi wao. Ikiwa ningewajua wazazi wangu wa kiasili, hilo halingetokeza tofauti yoyote, isipokuwa kwamba labda, ningeweza kufahamu tabia zangu chache vyema zaidi.” Je, wazazi wake walezi wanapendekeza uasilishaji? “Ndiyo,” wao wasema, “kwa sababu kwetu limekuwa ono zuri ajabu!”
Sababu za Kutahadhari
Graham na Ruth waliasilisha watoto wawili walipokuwa vitoto, mvulana na msichana, ili kuwachangamanisha pamoja na mwana na binti yao. Watoto wote wanne walilelewa wakiwa familia moja iliyoungana katika mazingira yenye furaha. “Watoto wetu wote waliondoka nyumbani miaka mingi iliyopita na kuishi maisha ya kujitegemea. Sisi hudumisha mawasiliano ya kawaida na twawapenda wote,” asema Ruth. Lakini kwa kuhuzunisha, watoto wote wawili wa kuasilishwa walikuwa na matatizo mazito. Kwa nini?
“Daktari wetu alituambia kwamba mazingira ya mtoto ni jambo la maana sana,” asema Graham, ambaye sasa ahisi kwamba vitabia vilivyorithiwa ni kisababishi kikuu. Yeye aongeza: “Pia, namna gani afya ya mama alipokuwa mja-mzito? Sasa twajua kwamba dawa za kulevya, vileo, na tumbaku, zaweza kuathiri mtoto asiyezaliwa bado. Napendekeza uchunguzi mkali ufanywe kwa wazazi wote, na hata wazazi-wakuu ikiwezekana, kabla ya kuasilisha.”
Mama ya Peter aliolewa tena, na Peter akatendwa vibaya na baba yake wa kambo kimwili na kiakili. Alipokuwa na umri wa miaka mitatu, akapelekwa akaasilishwe. “Niliwakataa wazazi-walezi wangu mara tu nilipotoka nje ya mahakama,” akasema Peter. Yeye akaongeza: “Niliharibu kila kitu kilichokuwa karibu nami. Nilipolala, nilipata ndoto zenye kutisha. Nikitazama nyuma sasa, naweza kuona jinsi nilivyosumbuka. Baada ya wazazi-walezi wangu kutalikiana pia, mambo yakawa mabaya hata zaidi kwangu—dawa za kulevya, kuiba, kuharibu vitu, karamu za ukosefu wa adili za kila siku.
“Nilipokuwa na umri wa miaka 27, sikuweza kuona sababu ya kuendelea kuishi nikafikiria kujiua kimakusudi. Kisha siku moja mtu nisiyemjua akanipa trakti ya Biblia ambayo ilitaarifu kwamba karibuni dunia hii itakuwa paradiso. Ujumbe huo ulinifurahisha. Ulisikika kuwa na kweli. Nilianza kusoma na kujifunza Biblia na kuanza kufanya mabadiliko katika maisha na tabia yangu, lakini mara kwa mara niliangukia njia zangu za kale. Baada ya kitia-moyo kingi na ushirika wa Kikristo wenye msaada, sasa nahisi nikiwa na furaha zaidi na usalama katika kumtumikia Mungu zaidi kuliko vile nilivyoweza kuwazia miaka michache iliyopita. Nimeweza pia kuamsha tena uhusiano wenye shauku pamoja na mama yangu, jambo ambalo ni lenye kufurahisha.”
Kukabili Uhalisi
Inapohusu kuasilisha mtoto asiye wako, hisia-moyo huwa nyingi mno. Upendo mwingi mno na shukrani zinaonyeshwa na vilevile uchungu na ukosefu wa shukrani. Kwa kielelezo, Edgar Wallace, hakumsamehe kamwe mama yake kwa kumwacha, njia ambayo yeye alipima matendo yake. Mama yake alienda kumwona katika mwaka wake wa mwisho wa uhai, akiomba kwa kusita-sita msaada wa kifedha, lakini Edgar, ingawa alikuwa tajiri sana wakati huo, alikataa waziwazi kumsaidia mamake. Muda mfupi baadaye, alipopata habari kwamba mama yake angalizikwa katika kaburi la watu maskini ikiwa si kwa fadhili za marafiki ambao walilipia maziko yake, Edgar alighairi sana ukosefu wake wa huruma.
Ni lazima watu wanaofikiria uasilishaji watoto wasio wao wajitayarishe kukabili kihalisi matatizo na magumu ambayo huenda yakazuka. Watoto hawawi wenye shukrani kila wakati kwa kile wazazi wao—walezi au wa kiasili—wanachowafanyia, hata katika hali bora kabisa. Kwa hakika, Biblia husema juu ya watu mmoja-mmoja katika siku yetu kuwa “wasio na shauku ya asili” na “wasio na shukrani” na “wasio waaminifu-washikamanifu.”—2 Timotheo 3:1-5, New World Translation.
Kwa upande ule mwingine, kufungua nyumba yako—na moyo wako—kwa mtoto anayehitaji wazazi kwaweza kuwa jambo bora na lenye kuthawabisha. Kwa mfano, Cathy, anashukuru sana wazazi-walezi wake kwa kumwandalia nyumba ya Kikristo na kutunza mahitaji yake ya kimwili na ya kiroho.—Ona sanduku “Tulifanikiwa,” ukurasa 8.
Wanapofafanua jinsi wanavyohisi kuhusu wana na mabinti wao wa kuasilisha, wazazi wa watoto kama hao huenda wakakumbuka maneno ya mtunga-zaburi: “Watoto ni zawadi kutoka kwa Bwana; wao ni baraka kwelikweli.”—Zaburi 127:3, Today’s English Version.
[Maelezo ya Chini]
a Baadhi ya majina yamebadilishwa ili kulinda hali ya kutojulikana.