Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g96 10/22 kur. 8-11
  • Kutoka Maneno Yaumizayo Hadi Maneno Yaponyayo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutoka Maneno Yaumizayo Hadi Maneno Yaponyayo
  • Amkeni!—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kulifunua Hilo Tatizo
  • Kupata Msaada
  • Wewe Waweza Kubadilika
  • Maoni Yafaayo Kuhusu Mafungu ya Kupewa na Mungu
  • Mikazo Inapozuka
  • Maneno Yaponyayo
  • Kufunua Visababishi vya Usemi Wenye Kuudhi
    Amkeni!—1996
  • Onyesha Upendo na Heshima kwa Kuzuia Ulimi Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Usitenganishe Kile Ambacho Mungu Ameunganisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Waume, Waheshimuni Wake Zenu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1996
g96 10/22 kur. 8-11

Kutoka Maneno Yaumizayo Hadi Maneno Yaponyayo

“Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi.”—MITHALI 18:21.

UTUKANAJI—zoea la kimakusudi la kutumia usemi wenye kutusi na kuudhi—hushutumiwa waziwazi katika Biblia. Chini ya Sheria ya Kimusa, mtu ambaye angewatukana wazazi wake angepata adhabu ya kifo. (Kutoka 21:17) Hivyo, Yehova Mungu hachukui jambo hilo kwa wepesi. Neno lake, Biblia, haliungi mkono wazo la kwamba chochote kitendekacho ‘katika usiri wa nyumba ya mtu’ hakina maana mradi mtu adai kumtumikia Mungu. Biblia hutaarifu hivi: “Mtu akidhani ya kuwa anayo dini, wala hauzuii ulimi wake kwa hatamu, hali akijidanganya moyo wake, dini yake mtu huyo haifai.” (Yakobo 1:26; Zaburi 15:1, 3) Kwa hiyo ikiwa mwanamume amuudhi mke wake kwa maneno, kazi zake nyinginezo zote za Kikristo zaweza kuonwa kuwa bure machoni pa Mungu.a—1 Wakorintho 13:1-3.

Isitoshe, Mkristo ambaye ni mtukanaji aweza kuondoshwa kutanikoni. Aweza hata kupoteza baraka za Ufalme wa Mungu. (1 Wakorintho 5:11; 6:9, 10) Kwa wazi, mtu ambaye ni mwenye kuumiza kwa maneno yake ahitaji kufanya badiliko kubwa. Lakini hilo laweza kutimizwaje?

Kulifunua Hilo Tatizo

Kwa wazi, mkosaji hatabadilika isipokuwa afahamu waziwazi kwamba ana tatizo zito. Kwa kuhuzunisha, kama mshauri mmoja alivyoonelea, wanaume wengi ambao hutumia usemi wenye kuudhi “hawaoni mwenendo wao kuwa wenye kuudhi hata kidogo. Kwa wanaume hawa, vitendo kama hivyo ni vya kawaida kabisa navyo ni njia ‘asilia’ ambayo waume na wake huchangamana.” Hivyo, wengi hawataona uhitaji wa kubadilika hadi waonyeshwe hali hiyo moja kwa moja.

Mara nyingi, baada ya kuchanganua hali yake kwa mwelekeo wa sala, mke atasukumwa kusema kwa ujasiri—kwa ajili ya hali-bora yake mwenyewe na ile ya watoto wake na kwa sababu ya kuhangaikia msimamo wa mume wake pamoja na Mungu. Ni kweli, sikuzote kuna uwezekano kwamba kusema kwa ujasiri kwaweza kufanya mambo yawe mabaya zaidi na kwamba maneno yake huenda yakakabili mlipuko wa kujitetea. Labda mke aweza kuiweza hali hiyo kwa kufikiri kwa uangalifu kimbele jinsi atakavyotokeza habari hiyo. “Neno linenwalo wakati wa kufaa. Ni kama machungwa katika vyano vya fedha,” yasema Biblia. (Mithali 25:11) Mfikio wenye fadhili lakini wa waziwazi katika wakati mtulivu huenda ukaufikia moyo wake.—Mithali 15:1.

Badala ya kutokeza mashtaka, mke apaswa kujaribu kujieleza kulingana na jinsi usemi wenye kuumiza unavyomwathiri. Taarifa za “Mimi” mara nyingi hufanya kazi vyema. Kwa kielelezo, ‘Mimi nahisi kuumizwa kwa sababu . . .’ au ‘Mimi nahisi kupondeka unaponiambia . . .’ Taarifa kama hizo zitaelekea zaidi kuufikia moyo, kwa kuwa hushambulia tatizo badala ya mtu.—Linganisha Mwanzo 27:46–28:1.

Mwingilio wa mke ulio imara lakini wenye busara waweza kuwa na matokeo mazuri. (Linganisha Zaburi 141:5.) Mwanamume tutakayemwita Steven aliona ndivyo ilivyo. “Mke wangu alitambua mtazamo wa kuudhi ndani yangu ambao sikuutambua, naye alikuwa na ujasiri wa kunieleza kuuhusu,” yeye asema.

Kupata Msaada

Lakini mke aweza kufanya nini ikiwa mume wake akataa kukubali tatizo hilo? Kufikia hatua hii wake fulani hutafuta msaada wa nje. Katika nyakati za taabu hizo, Mashahidi wa Yehova waweza kuwaendea wazee wao wa kutaniko. Biblia huwahimiza wanaume hawa wawe wenye kuonyesha upendo na fadhili wakati wanapochunga kundi la kiroho la Mungu na, kwa wakati huohuo, ‘kuwaonya watu wenye kupinga’ mafundisho yenye mafaa ya Neno la Mungu. (Tito 1:9; 1 Petro 5:1-3) Ingawa hawapaswi kuingilia mambo ya kibinafsi ya waume na wake, wazee wana haki ya kuhangaika wakati mwenzi mmoja anateswa kwa usemi mkali wa yule mwingine. (Mithali 21:13) Wakitii kwa ukaribu viwango vya Biblia, wanaume hawa hawaachilii au kupunguza uzito wa usemi wenye kuudhi.b

Huenda wazee wakaweza kurahisisha mawasiliano kati ya mume na mke. Kwa kielelezo, mzee mmoja alifikiwa na mwanamke aliyemweleza juu ya miaka mingi ya kupigwa kwa maneno na mume wake, mwabudu mwenzake. Mzee huyo alipanga kukutana nao wawili. Kila mmoja alipokuwa akisema, yeye alimwomba yule mwingine asikilize bila kukatiza. Ilipokuwa zamu ya mke, yeye alisema kwamba hangeweza tena kustahimili hasira yenye kulipuka ya mume wake. Kwa miaka mingi, yeye akaeleza, alikuwa na hofu sana mwishoni mwa kila siku, akiwa hajui kamwe ikiwa mume wake angekuwa amekasirika alipokuja nyumbani. Alipolipuka, alikuwa akisema mambo yenye kushushia heshima familia ya mke, marafiki wake, na mke mwenyewe.

Mzee huyo alimuuliza mke huyo aeleze jinsi maneno ya mume wake yalivyomfanya ahisi. “Nilihisi kama kwamba nilikuwa mtu mbaya ambaye hakuna mtu angeweza kumpenda,” yeye akajibu. “Nyakati nyingine nilikuwa nikimuuliza mama yangu, ‘Mama, je, mimi ni mtu mgumu sana kuishi naye? Je, mimi ni mtu asiyeweza kupendeka?’” Alipokuwa akifafanua jinsi maneno ya mume wake yalivyomfanya ahisi, mume wake alianza kulia. Kwa mara ya kwanza, aliweza kuona jinsi alivyokuwa akimuumiza sana mke wake kwa maneno yake.

Wewe Waweza Kubadilika

Wakristo fulani katika karne ya pili walikuwa na tatizo na usemi wenye kuudhi. Mtume Mkristo Paulo aliwaonya waweke mbali “hasira, na ghadhabu, na uovu, na matukano, na matusi.” (Wakolosai 3:8) Hata hivyo, usemi mkali ni tatizo la moyo hasa kuliko la ulimi. (Luka 6:45) Hiyo ndiyo sababu Paulo aliongeza: ‘Uvueni kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake, na mvae utu mpya.’ (Wakolosai 3:9, 10) Kwa hiyo badiliko huhusisha si tu kuzungumza kwa njia tofauti bali pia kuhisi tofauti.

Mume atumiaye usemi wenye kuumiza huenda akahitaji msaada ili kupambanua ni nini hasa kichocheacho mwenendo wake.c Yeye atataka kuwa na mtazamo wa mtunga-zaburi: “Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu, unijaribu, uyajue mawazo yangu. Uone kama iko njia iletayo majuto ndani yangu.” (Zaburi 139:23, 24) Kwa kielelezo: Kwa nini yeye ahisi uhitaji wa kumtawala, au kumdhibiti, mwenzi wake? Ni nini kianzishacho udhia wa maneno? Je, mashambulizi yake ni dalili za chuki yenye kina? (Mithali 15:18) Je, ana hisia za kwamba yeye hafai kitu, labda zikitokana na kulelewa kwake ambako kulikuwa na usemi wa kuchambuliwa? Maswali kama hayo yaweza kumsaidia mwanamume agundue chanzo cha mwenendo wake.

Ingawa hivyo, usemi wenye kuudhi ni mgumu kung’oa, hasa ikiwa umekazwa kikiki na wazazi ambao wenyewe walikuwa wenye kukejeli kwa maneno au kwa utamaduni ambao huchochea mwenendo wa kutawala. Lakini chochote ajifunzacho mtu—kwa wakati na jitihada—chaweza kutanguliwa. Biblia ndio msaada mkubwa zaidi kuhusu jambo hili. Yaweza kumsaidia mtu kutangua hata mwenendo uliotia mzizi sana. (Linganisha 2 Wakorintho 10:4, 5.) Jinsi gani?

Maoni Yafaayo Kuhusu Mafungu ya Kupewa na Mungu

Mara nyingi, wanaume ambao ni wenye kuumiza kwa maneno wana maoni yaliyopotoka kuhusu mafungu ya kupewa na Mungu kwa waume na wake. Kwa kielelezo, mwandikaji wa Biblia Paulo ataarifu kwamba wake wapaswa ‘kutii waume zao’ na kwamba “mume ni kichwa cha mkewe.” (Waefeso 5:22, 23) Huenda mume akahisi kwamba ukichwa humpatia mamlaka ya kuwa na udhibiti kamili. Lakini sivyo ilivyo. Mke wake, ingawa yuko chini ya ujitiisho, si mtumwa wake. Yeye ni ‘msaidiaji’ na ‘kikamilisho.’ (Mwanzo 2:18, NW) Hivyo, Paulo aongeza: “Imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye anavyolitendea kanisa.”—Waefeso 5:28, 29.

Akiwa kichwa cha kutaniko la Kikristo, Yesu hakuwakemea-kemea wanafunzi wake, akiwafanya wawe na wasiwasi ni wakati gani tena mlipuko ufuatao wa uchambuzi utakapotokea. Badala ya hivyo, yeye alikuwa mwororo, hivyo akidumisha hadhi yao. “Nitawapumzisha,” akawaahidi. “Mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo.” (Mathayo 11:28, 29) Kutafakari kwa mwelekeo wa sala juu ya jinsi Yesu alidhihirisha ukichwa wake kwaweza kumsaidia mume aone ukichwa wake kwa maoni yaliyosawazika zaidi.

Mikazo Inapozuka

Ni rahisi kujua kanuni za Biblia; kuzitumia ukiwa chini ya mkazo ndilo jambo gumu zaidi. Mikazo inapozuka, mume anaweza kuepukaje kurudia kitabia cha usemi wenye kudhulumu?

Si ishara ya uanamume kwa mume kuwa mkali kwa maneno anapokasirika. Biblia hutaarifu: “Asiye mwepesi wa hasira ni mwema kuliko shujaa; na mtu aitawalaye roho yake kuliko mtu atekaye mji.” (Mithali 16:32) Mwanamume halisi hudhibiti roho yake. Yeye huonyesha hisia-mwenzi kwa kufikiria: ‘Maneno yangu yanamwathirije mke wangu? Mimi ningehisije kama ningekuwa mahali pake?’—Linganisha Mathayo 7:12.

Ingawa hivyo, Biblia hukubali kwamba hali fulani zaweza kuchochea hasira. Kuhusu hali kama hizo mtunga-zaburi aliandika hivi: “Kasirikani, lakini msitende dhambi: Semezanani kila mtu na moyo wakwe, vile alivyo mwakwe kitandani, mnganyamaa kimya.” (Zaburi 4:4, The Old Testament In Swahili [Mombasa]) Pia imesemwa hivi: “Hakuna kosa lolote kukasirika, lakini ni kosa kushambulia kwa maneno kwa kuwa mwenye kukejeli, mwenye kuaibisha au mwenye kushusha heshima.”

Ikiwa mume ahisi kwamba anapoteza udhibiti wa usemi wake, yeye aweza kujifunza kujiondokea. Labda lingekuwa jambo la hekima kuondoka chumbani, kwenda kutembea, au kutafuta mahali pa faragha ili apoe. Mithali 17:14 (NW) yasema: “Kabla magombano hayajalipuka, jiondokee.” Rudieni mazungumzo baada ya hasira kupoa.

Bila shaka, hakuna aliye mkamilifu. Mume ambaye amekuwa na tatizo la usemi mkali aweza kuangukia tena hali hiyo. Hili linapotukia, apaswa kuomba radhi. Kuvaa “utu mpya” ni utaratibu wenye kuendelea, lakini ule ambao huvuna thawabu kubwa.—Wakolosai 3:10.

Maneno Yaponyayo

Ndiyo, “Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi.” (Mithali 18:21) Usemi wenye kuumiza lazima ubadilishwe na maneno yajengayo na yenye kuimarisha ndoa. Methali ya Biblia hutaarifu: “Maneno yapendezayo ni kama sega la asali; ni tamu nafsini, na afya mifupani.”—Mithali 16:24.

Miaka fulani iliyopita, uchunguzi ulifanywa ili kujua ni mambo gani yaliyosababisha familia zenye nguvu kufanya kazi kwa matokeo. “Uchunguzi huo ulipata kwamba washiriki wa familia walipendana, na waliendelea kuambiana kwamba wanapendana,” aripoti mtaalamu wa ndoa David R. Mace. “Kila mmoja alihakikishiwa kwamba anakubaliwa, wakaonyeshana kwamba kila mmoja astahili, na kuchukua kila fursa ifaayo kuzungumza na kutenda kwa upendo. Tokeo, kiasili, lilikuwa kwamba walifurahi kuwa pamoja na kuimarishana kwa njia ambazo zilifanya mahusiano yao yaridhishe.”

Hakuna mume mwenye kumhofu Mungu awezaye kusema kwa kweli kwamba ampenda mke wake ikiwa amuumiza kimakusudi kwa maneno yake. (Wakolosai 3:19) Bila shaka, ndivyo ilivyo kwa mke ambaye humpiga mume wake kwa maneno. Kwa kweli, ni wajibu wa wenzi wote kufuata onyo la Paulo kwa Waefeso: “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji, ili liwape neema wanaosikia.”—Waefeso 4:29.

[Maelezo ya Chini]

a Ingawa twamrejezea mkosaji kuwa mwanamume, kanuni zilizopo hapa zatumika sawasawa kwa wanawake.

b Ili kustahili kutumikia au kuendelea kutumikia akiwa mzee, mwanamume hapaswi kuwa mpiganaji. Hawezi kuwa yule ambaye apiga watu kimwili au kuwadhulumu kwa maneno yenye kuumiza. Wazee na watumishi wa huduma wanapaswa kusimamia nyumba zao kwa njia nzuri. Haidhuru hata atende kwa fadhili namna gani katika hali nyinginezo, mwanamume hastahili ikiwa yeye ni mtawala mkatili nyumbani.—1 Timotheo 3:2-4, 12.

c Iwe Mkristo atatafuta tiba ya mwenendo wenye kuudhi au la ni uamuzi wa kibinafsi. Hata hivyo, apaswa kuhakikisha kwamba tiba yoyote apokeayo haipingani na kanuni za Biblia.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mzee Mkristo aweza kusaidia mume na mke wawasiliane

[Picha katika ukurasa wa 10]

Waume na wake wapaswa kufanya jitihada ya kweli ya kuelewana

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki