Vijana Huuliza . . .
Kwa Nini Mungu Huruhusu Maovu Yatokee?
LIDIJA alikuwa tineja tu vita ilipofyatuka katika nchi yao—nchi ambayo zamani ilijulikana kuwa Yugoslavia. “Nilikaa katika maficho yenye giza kwa siku nyingi mchana na usiku,” akakumbuka. “Mara nyingi nilishawishwa kukimbilia nje ingawa ingeweza kumaanisha kuuawa! Kabla ya vita, ulikuwa na kila kitu, lakini sasa unafurahi unapokuwa hai tu.”
Baada ya muda mfupi mikazo na magumu ya vita yalimwathiri sana Lidija kiroho. Yeye asema: “Kwa majuma kadhaa hatukuweza kwenda kuhubiri au kwenye mikutano. Nilifikiria kihalisi kwamba Yehova alikuwa ametuacha. Ningejiuliza mwenyewe, ‘Kwa nini hatusaidii sasa?’”
Vita, uhalifu, ujeuri, maradhi, misiba, aksidenti—maovu kama haya yaweza kuwapata hata vijana. Msiba umfikiapo mtu kibinafsi, kiasili unaweza kujiuliza, ‘Kwa nini Mungu huruhusu maovu haya yatokee?’
Watu wa Mungu wa nyakati zilizopita waliuliza swali kama hilo. Kwa mfano nabii Habakuki, alipoona hali mbaya ya mambo iliyokuwapo miongoni mwa watu wa Mungu, alilalamika: “Ee BWANA, nilie hata lini, wewe usitake kusikia? Nakulilia kwa sababu ya udhalimu, ila hutaki kuokoa. Mbona wanionyesha uovu, na kunitazamisha ukaidi?” (Habakuki 1:2, 3) Leo, baadhi ya vijana wa Kikristo hukabili mkazo wa kihisia-moyo kama huo.
Fikiria namna kijana mmoja Mkristo alivyohisi baada ya kifo cha ghafula cha baba yake. Yeye asema: “Nilirukwa akili na kulia kwa nguvu, nikimpigia kelele Yehova Mungu. . . . Nilimlaumu kwa kila kitu. Hili lingetokeaje? Baba alikuwa mzuri sana na mume mwenye upendo na sasa hili latokea—kwani, Yehova hajali?” Katika hali kama hii, ni kawaida tu kuhisi kuchanganyikiwa, umizo, au hata hasira. Kumbuka, nabii mwaminifu Habakuki pia alisumbuliwa kwamba uovu uliruhusiwa kuwapo. Walakini, ikiwa mtu aendelea kukuza hisia za uchungu, kuna hatari. Angeweza “kughadhabika dhidi ya Yehova.”—Mithali 19:3, NW.
Hivyo basi, unawezaje kuepuka hisia za ghadhabu na uchungu? Kwanza, wapaswa kuelewa uovu watoka wapi?
Maovu Hayatokani na Mungu
Biblia yaonyesha wazi kwamba kamwe Mungu hakukusudia tuteseke namna hii. Aliwaweka wenzi wa kwanza katika makao ya paradiso ambayo hayakuwa na maumivu na kuteseka. (Mwanzo 1:28) Bila shaka unaelewa vizuri jinsi mambo yalivyoharibika: Kiumbe-roho asiyeonekana, ambaye baadaye alikuja kujulikana kuwa Ibilisi na Shetani, aliwashawishi Adamu na Hawa wasimtii Mungu. (Mwanzo, sura ya 3; Ufunuo 12:9) Kwa kufanya hivyo, Adamu aliwaletea wazao wake wote dhambi na matokeo yayo yenye kuharibu.—Warumi 5:12.
Kwa wazi, si Mungu aliyeleta uovu kwa wanadamu, bali ni mwanadamu mwenyewe aliyejiletea. (Kumbukumbu la Torati 32:5; Mhubiri 7:29) Kwa kweli, maovu yote ambayo watu huteseka leo—ugonjwa, kifo, vita, na ukosefu wa haki—yalitokana na kitendo cha hiari cha Adamu cha kutokutii. Zaidi ya hayo, sisi sote tupo chini ya kile Biblia ikiitacho “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11, NW) Waovu na wenye haki wote hupatwa na aksidenti na misiba isiyotazamiwa.
Hali ya Mungu Kuruhusu Uovu
Ingawa inafariji kujua kwamba Mungu si chanzo cha uovu, bado waweza kujiuliza, ‘Kwa nini yeye huruhusu uovu uendelee?’ Tena, hili lahusiana na masuala yaliyotokea katika Edeni. Mungu alimwambia Adamu kwamba ikiwa angekosa kutii, angekufa. (Mwanzo 2:17) Hata hivyo, Ibilisi alimwambia Hawa kwamba ikiwa angekula kutokana na mti uliokatazwa, asingekufa! (Mwanzo 3:1-5) Kama tokeo, Shetani alimwita Mungu mwongo. Zaidi ya hayo, Shetani alidokeza kwamba mwanadamu angekuwa na hali bora zaidi ikiwa angejifanyia maamuzi yake mwenyewe na asingekuwa na haja ya Mungu kumwambia jambo la kufanya!
Mungu asingeweza kuyapuuza mashtaka haya. Umeshawahi kumwona mwanadarasa mwenzako akisai mamlaka ya mwalimu? Mwalimu huyo akikosa kumwadhibu, wanafunzi wengine wangekaidi pia. Katika njia hiyo pia, kungeweza kutokea machafuko ulimwenguni kote ikiwa Yehova asingekabiliana na Shetani moja kwa moja. Yehova alifanya hivyo kwa kumruhusu mwanadamu kufuata njia ya Shetani ya kufanya mambo. Je, mwanadamu amefurahia uhuru wa kimungu ambao Shetani aliahidi? Hapana. Utawala wa Shetani umeleta madhara makubwa sana, ukithibitisha kuwa yeye ni mwongo mbaya sana!
Je, Mungu ataruhusu uovu uendelee milele? Hapana. Ili kusuluhisha masuala aliyozusha Shetani, karibuni Mungu atamaliza uovu wote. (Zaburi 37:10) Lakini twawezaje kukabiliana na hali hiyo sasa?
Suala Lenye Kukuhusisha Wewe
Zaidi ya yote, elewa kwamba suala hili kati ya Mungu na Shetani hukuhusisha wewe! Namna gani hivyo? Fikiria kitabu cha Biblia kilichoitwa kwa jina la mtu mwadilifu Ayubu. Mungu alipoelekeza kwa Ayubu kuwa mfano wa mwabudu mwaminifu, Shetani alijibu: “Je! huyo Ayubu yuamcha BWANA bure?” (Ayubu 1:9) Kwa kweli Shetani alidai kwamba ikiwa angeruhusiwa kuweka mkazo, angeweza kukengeusha mtu yeyote asimtumikie Mungu!—Ayubu 2:4, 5.
Hivyo, Shetani amewachongea wote wenye kumhofu Mungu. Amekuchongea wewe. Lakini, Mithali 27:11 husema: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” Naam, umtumikiapo Mungu ingawa katika magumu yenye kuumiza, kwa kweli unasaidia kuthibitisha Shetani kuwa mwongo!
Inaeleweka, upatwapo na maovu, si rahisi kufikiria masuala yenye kuhusika. Diane, ambaye alikuwa na umri wa miaka kumi tu mama yake alipokufa, asema: “Niliogopa kwamba ningekuwa mgumu au mwenye uchungu kwa sababu ya majaribio katika maisha yangu.” Lakini, kujua kwa nini Mungu ameruhusu uovu kumemsaidia kupata maoni yanayofaa ya maisha yake. Sasa asema: “Ijapokuwa yapo mambo magumu kushughulika nayo katika maisha yangu, mkono wa Yehova nyakati zote umekuwa pamoja nami.”
Diane atukumbusha jambo muhimu sana: Yehova hatutarajii tukabiliane na mikazo hii wenyewe. Zaburi 55:22 yatuhakikishia: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” Kijana Kotoyo alipata jambo hili kuwa ni kweli. Alikabili msiba wazazi wake walipouawa na tetemeko la dunia lililoikumba Kobe, Japani katika 1995. Akiongea kwa niaba yake na wadogo wake wachanga, asema: “Kwa sababu mama yangu alitufundisha kumtegemea Yehova, twaweza kuvumilia.”
Vipi kuhusu Lidija, msichana mchanga aliyetajwa mwanzoni? Baadaye, alitambua kwamba Yehova hakuwa amemwacha hata kidogo. Sasa asema: “Wakati wote Yehova alikuwapo kwa ajili yetu. Alituongoza na kuelekeza hatua zetu.”
Yehova—Mungu Mwenye Upendo Ambaye Hujali
Wewe pia waweza kujionea mwenyewe msaada kutoka kwa Mungu maovu yakupatapo. Kwa nini? Kwa sababu Yehova akujali wewe! Ingawa yeye huruhusu mambo maovu yawapate watu wazuri, pia yeye huandaa faraja yenye upendo. (2 Wakorintho 1:3, 4) Njia moja aitumiayo ni kupitia kutaniko la Kikristo. Hapo waweza kupata ‘rafiki waambatanao na mtu kuliko ndugu,’ ambao waweza kukutia nguvu magumu ya kihisia-moyo yatokeapo. (Mithali 18:24) Kotoyo akumbuka: “Tokea siku ya kwanza baada ya tetemeko, tulikwenda mahali ambapo ndugu walikutana, na tulipata kitia-moyo na mambo yaliyohitajika. Hii ilinifanya nijisikie salama. Kadiri tuendeleavyo kuwa na Yehova na akina ndugu, mimi hujisikia kwamba twaweza kuvumilia chochote.”
Kwa sababu Yehova akujua wewe kibinafsi, aweza pia kushughulikia mahitaji yako maovu yatokeapo. Daniel akumbuka jinsi ambavyo ameshughulika na kifo cha baba yake, akisema: “Yehova awa baba kwako, na tengenezo lake huandaa wanaume wa kiroho wakiwa watu wa kuigwa. Sikuzote, Yehova huandaa majibu ya maswali ambayo ninayo na ambayo kiasili ningezungumza na baba yangu.” Diane pia amejionea mwenyewe upendo wenye kujali wa Yehova tangu kifo cha mama yake. Asema: “Kupitia wazee wakomavu kiroho ambao wameandaa kitia-moyo, mwongozo na shauri, ameniongoza na kunisaidia kukabiliana na kivunja-moyo chochote.”
Bila shaka, kupatwa na maovu si jambo zuri. Lakini jifariji katika kujua ni kwa nini Mungu aruhusu mambo haya. Jikumbushe daima kwamba karibuni sana Mungu atamaliza tatizo hilo. Ahaa, alama zote za maovu ambayo tumepatwa nayo hatimaye zitafutwa! (Isaya 65:17; 1 Yohana 3:8) Kwa kujifaidi na maandalizi yote ambayo Mungu huandaa kutusaidia kupambana, waweza kufanya sehemu yako katika kuthibitisha Shetani kuwa mwongo. Karibuni, ‘Mungu atafuta kila chozi katika macho yako.’—Ufunuo 21:3, 4.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Karibuni Yehova atakomesha maovu yote