Dini Isiyo ya Kweli Yaelekea Kwenye Uharibifu!
ILI kujua ikiwa dini za ulimwengu huu zimekaribia mwisho, ebu tuchunguze mmojawapo unabii wenye kutazamisha zaidi wa Biblia. Unahusu mwanamke mmoja wa mfano na wa kifumbo afafanuliwaye katika kitabu cha mwisho cha Biblia, Ufunuo.
Je, waweza kuona akilini mwanamke ambaye ametawala akiwa malkia juu ya mataifa, akiwa na uvutano juu ya maisha ya mabilioni ya watu katika historia yote—mwanamke tajiri ambaye amejivika kwa umadaha sana kwa rangi ya zambarau na nyekundu-nyangavu, akiwa amejirembesha kwa dhahabu, vito, na lulu nyingi sana? Kwenye kipaji cha uso wake kumeandikwa jina refu, fumbo: “Babiloni Mkubwa, mama wa makahaba na wa mambo yenye kuchukiza sana ya dunia.” Yeye atambulishwa bila kukosea na maisha yake ya ukaidi na ya ngono ya ovyoovyo, akiwa amefanya “uasherati” pamoja na watawala wa ulimwengu. Dhambi zake zimejaa hadi mbinguni. Yeye amepanda hayawani-mwitu mwenye kutisha sana aliye na vichwa saba, pembe kumi na rangi nyekundu-nyangavu.—Ufunuo 17:1-6, NW; 18:5.
Ikiwa unaweza kupiga picha ya huyu mwanamke akilini, unajua mhusika-mkuu katika drama ya kiunabii ambayo Yohana mtume wa Yesu aliona katika ono alilopewa kupitia malaika. Yeye afafanua kwa uwazi jambo hilo katika Ufunuo sura za 17 na 18. Soma sura hizi katika Biblia yako mwenyewe. Utaweza kufuata matukio jinsi yanavyofuatana tokea kufichuliwa kwa utambulisho wa mwanamke huyo wa kifumbo hadi kifo chake.
Kumtambulisha Yule Kahaba
Dokezo la kuweza kufahamu utambulisho wake linapatikana katika vitu viwili ambavyo malkia huyo aliye kahaba ameviketia kwa njia ya mfano. Kwenye Ufunuo 17:18, yeye afafanuliwa kuwa “mji ule mkubwa, wenye ufalme juu ya wafalme wa nchi.” Hilo humruhusu kuketi juu ya “maji mengi,” ambayo humaanisha “jamaa na makutano na mataifa na lugha,” kama ionyeshwavyo kwenye Ufunuo 17:1, 15. Kulingana na mstari wa 3 katika sura hiyo, yeye ameketi pia juu ya hayawani-mwitu mwenye vichwa saba—hayawani kwa kawaida hutumiwa katika Biblia kuwa ishara za mamlaka au mashirika ya kisiasa ya kilimwengu.
Hilo laonyesha kwamba huyo kahaba, Babiloni Mkubwa, ni mfano wa milki iliyotukuzwa, milki ambayo hudhibiti mamlaka nyinginezo na raia zazo. Hilo laweza kuwa tu milki ya dini zisizo za kweli za ulimwengu.
Uvutano wa viongozi wa kidini kwa masuala ya sera za serikali na siasa ni sehemu inayojulikana sana ya historia. Kitabu The World Book Encyclopedia chasema: “Baada ya kuanguka kwa Milki ya Kiroma ya Magharibi [karne ya 5], papa alikuwa na mamlaka kubwa zaidi kuliko mtu mwingine awaye yote katika Ulaya. . . . Papa alikuwa na mamlaka ya kisiasa na vilevile ya kiroho. Katika [mwaka wa] 800, Papa Leo 3 alimtawaza mtawala Mfranka Charlemagne [Charles Mkubwa] kuwa maliki wa Waroma. . . . Leo 3 alikuwa ameanzisha haki ya papa ya kuhalalisha mamlaka ya maliki.”
Mamlaka ambayo Kanisa Katoliki na “wakuu” walo walikuwa nayo juu ya watawala ilithibitishwa zaidi na kadinali Thomas Wolsey (1475?-1530). Yeye afafanuliwa kuwa “mtu mwenye nguvu zaidi katika Uingereza kwa miaka mingi.” Chini ya utawala wa Mfalme Henry 8, “upesi ni yeye aliyekuwa akiongoza mambo yote ya serikali. . . . Aliishi kwa anasa sana na alikuwa na mamlaka nyingi sana.” Ensaiklopedia hiyo yaendelea kusema: “Kadinali Wolsey alitumia uwezo wake mkubwa akiwa mkuu wa serikali na msimamizi hasa katika kusimamia masuala ya Uingereza ya nchi za kigeni kwa niaba ya Henry 8.”
Kielelezo kingine chenye kutokeza cha mamlaka ya Katoliki juu ya mambo ya kilimwengu ya serikali ni Kadinali Richelieu wa Ufaransa (1585-1642), ambaye “kwa zaidi ya miaka 18 . . . alikuwa hasa ndiye mtawala wa Ufaransa.” Hiyo ensaiklopedia ambayo ilinukuliwa awali yasema: “Alikuwa mwenye tamaa ya makuu sana na upesi akawa hana subira ya kupanda cheo.” Alitawazwa kuwa kadinali katika 1622 “na upesi akaja kuwa mwenye uvutano mwingi zaidi katika serikali ya Ufaransa.” Yaonekana, alikuwa mtu wa kuchukua hatua, kwa kuwa “yeye mwenyewe aliongoza jeshi la mfalme katika kuzingiwa kwa La Rochelle.” Makala hiyo yaongezea hivi: “Upendezi mkuu wa Richelieu ulikuwa masuala ya nchi za kigeni.”
Hali ya Vatikani ya kuendelea kujihusisha na mamlaka za kisiasa yaonekana wazi katika matangazo ya daima kwenye gazeti la Vatikani L’Osservatore Romano ya mabalozi wakitoa vitambulisho vyao kwa papa mwenye enzi. Kwa wazi Vatikani ina mfumo wa Wakatoliki waaminifu-washikamanifu ambao wanaweza kumwarifu papa juu ya maendeleo ya kisiasa na ya kibalozi ulimwenguni pote.
Vielelezo vingine vingi vyaweza kutolewa ili kuonyesha uvutano wenye nguvu wa viongozi wa kidini—ndani na nje ya Jumuiya ya Wakristo—katika masuala ya kisiasa ya ulimwengu huu. Uhakika wa kwamba huyo kahaba wa mfano ameketi juu ya “maji mengi” yote (yakiwakilisha “jamaa na makutano na mataifa”) na hayawani-mwitu (akiwakilisha mamlaka zote za ulimwengu za kisiasa) wadokeza pia kwamba uvutano wake juu ya vikundi vya watu, mataifa, na mamlaka ni wa aina tofauti na wa hali ya juu kuliko tu udhibiti wa kisiasa. Ebu tuone ni wa aina gani.
Sehemu ya jina refu katika kipaji cha uso wake ilikuwa “Babiloni Mkubwa.” Hiyo yarejezea Babiloni la kale, lililoanzishwa miaka yapata 4,000 iliyopita na Nimrodi, ambaye alikuwa “dhidi ya Yehova,” Mungu wa kweli. (Mwanzo 10:8-10) Kuitwa kwake kwa jina hilo kwaonyesha kwamba yeye ni mfano mkubwa zaidi wa Babiloni la kale, akionyesha hali zinazofanana. Hali zipi hizo? Babiloni la kale lilijaa dini ya kifumbo, mapokeo yenye kupotosha, ibada za sanamu, mizungu, unajimu, na ushirikina—zote ambazo hushutumiwa na Neno la Yehova.
Kitabu The New International Dictionary of New Testament Theology chasema kwamba katika karne ya 18 K.W.K., Marduki alitawazwa kuwa “mungu wa jiji la Babiloni, na hivyo akawa mkuu wa mkusanyo wa viabudiwa vipatavyo 1300 vya Wasumeria na Waakadi. Hiyo ilichanganya mapokeo yote ya kidini katika mfumo mmoja. . . . Katika Mwa. 11:1-9 ujenzi wa hekalu kubwa la Babiloni huonwa kuwa wonyesho wa kiburi cha kibinadamu kinachotaka kupindua mbingu.”
Hivyo, Babiloni la kale lilikuwa kitovu cha dini isiyo ya kweli, ambayo baadaye iliathiri ulimwengu wote. Mazoea, mafundisho, mapokeo, na ishara za kidini za Kibabiloni zimejaa katika sehemu zote za dunia nazo zinaonekana katika mchanganyiko wa maelfu mengi ya dini za ulimwengu. Falme na milki za kisiasa zimeinuka na kuanguka, lakini dini ya Kibabiloni imeokoka kuzipita zote.
Kwa Nini Uharibifu Wayo U Karibu Sana?
Kama ambavyo imeelezwa mara nyingi katika matoleo yaliyopita ya gazeti hili, unabii wa Biblia na matukio yanayopata ulimwengu tangu 1914 bila shaka yaonyesha kwamba sasa sisi twaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3, NW) Hiyo yamaanisha kwamba mwisho wa mfumo huu wa ulimwengu wa kihayawani unakaribia upesi, na vilevile mwisho wa yule “hayawani-mwitu wa rangi-nyekundu-nyangavu” aliye na pembe kumi, ambaye sasa yule kahaba amempanda. (Ufunuo 17:3, NW) Hayawani huyu bila shaka huwakilisha mkusanyo wa kisiasa wa karibu mataifa yote ya dunia—Umoja wa Mataifa. Mwisho uliotabiriwa wamaanisha kuondolewa kwa utawala wa kisiasa wenye kugawanya na usio wa kimungu juu ya wanadamu. Lakini namna gani juu ya malkia-kahaba ambaye amempanda yule hayawani?
Malaika wa Mungu aeleza: “Pembe kumi ulizoziona, na hayawani-mwitu, hawa watamchukia kahaba na watamfanya ukiwa na kuwa uchi, na watakula kabisa sehemu zake zenye nyama na watamchoma kabisa kwa moto. Kwa maana Mungu alitia hilo ndani ya mioyo yao ili kutekeleza fikira yake, hata kutekeleza fikira yao moja kwa kumpa hayawani-mwitu ufalme wao, mpaka maneno ya Mungu yawe yamekwisha kutimizwa.”—Ufunuo 17:16, 17.
Hivyo unabii waonyesha kwamba punde tu kabla ya hayawani-mwitu kuharibiwa, huyo ataanza kumchukia yule ambaye amempanda na kumgeukia. Kwa nini? Yaonekana watawala na serikali watahisi kwamba uwezo wao na mamlaka yao inatishwa na dini mashuhuri inayotenda katika eneo lao. Kwa ghafula, wakihimizwa na kani yenye kushurutisha, wao watatimiza “fikira” ya Mungu, uamuzi wake, kwa kutekeleza hukumu yake juu ya milki ya dini isiyo ya kweli yenye uzinzi na madoa ya damu.a—Linganisha Yeremia 7:8-11, 34.
Mwisho wa dini zisizo za kweli za ulimwengu huu utakuja wakati zingali zinaonekana kuwa zenye nguvu na zenye uvutano. Ndiyo, unabii waonyesha kwamba kabla tu ya kahaba huyo kuharibiwa, angali atakuwa akisema moyoni mwake: “Nimeketi malkia, wala si mjane, wala sitaona huzuni kamwe.” (Ufunuo 18:7) Hata hivyo, uharibifu wake utashangaza mabilioni ya raia zake. Utakuwa mojawapo matukio yasiyotazamiwa kabisa na yenye msiba zaidi kupata kutukia katika historia ya wanadamu.
Tangu kuinuka kwa Babiloni la kale, dini zisizo za kweli zimedhihirisha uvutano mwingi sana juu ya wanadamu kupitia viongozi wazo na waungaji-mkono wazo; mafundisho, mapokeo, mazoea yazo; majengo yazo mengi ya kustaajabisha ya ibada; na utajiri wazo mwingi sana. Bila shaka hazitatokomea bila kuonekana. Kwa hiyo, malaika aliyekabidhiwa kupitisha ujumbe wa hukumu kwa huyo kahaba asema waziwazi hivi atangazapo: “Mapigo yake yatakuja katika siku moja, mauti, na huzuni, na njaa, naye atateketezwa kabisa kwa moto. Kwa maana Bwana Mungu aliyemhukumu ni mwenye nguvu.” Hivyo, mwisho wa Babiloni Mkubwa utakuja kwa ghafula kabisa na kupita haraka sana, kana kwamba kwa “siku moja.”—Ufunuo 18:8; Isaya 47:8, 9, 11.
Maneno yenye nguvu ya malaika yatokeza swali, Je, kuna dini yoyote itakayobaki, na ikiwa ndiyo, ni dini ipi na kwa nini? Unabii waonyesha nini? Hili litashughulikiwa katika makala ifuatayo.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi juu ya unabii huo mbalimbali, ona Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, sura 33, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Hatia ya Damu ya Jumuiya ya Wakristo Katika Afrika
Kwenye Ufunuo 18:24, Biblia husema kwamba katika Babiloni Mkubwa mna damu ya “wale wote waliouawa katika nchi.” Ebu fikiria vile vita ambavyo vimepiganwa kwa sababu ya tofauti za kidini na kwa sababu ya kushindwa kwa viongozi wa kidini kuvizuia. Kielelezo cha majuzi cha jambo hili kilionekana wazi katika maangamizi ya jamii nzima-nzima katika Rwanda, ambamo watu wapatao 500,000 waliuawa kimakusudi—thuluthi moja kati yao wakiwa watoto.
Mtungaji wa vitabu Mkanada Hugh McCullum aripoti hivi kutoka Rwanda: “Padri mmoja Mhutu katika Kigali [Rwanda] asema kwamba kushindwa kwa kanisa kuandaa uongozi wa kiadili hakuwezi kuelezeka. Madaraka ya maaskofu katika jamii ya Warwanda yalipaswa kuwa muhimu kabisa. Walijua juu ya msiba uliokuwa ukikaribia muda mrefu kabla ya mauaji hayo kuanza. Madhabahu ya makanisa yalipasa kuandaa fursa kwa karibu watu wote kusikiliza ujumbe wenye nguvu ambao ungezuia maangamizi ya jamii nzima-nzima. Badala ya kufanya hivyo viongozi hao walinyamaza.”
Baada ya machinjo mabaya zaidi katika 1994, Justin Hakizimana, mzee mmoja wa kanisa, alisema hivi kwenye mkutano mdogo uliofanywa katika kanisa moja la Presbiteri katika Kigali: “Kanisa lilihusika karibu sana na siasa za Habyarimana [rais wa Rwanda]. Hatukushutumu yale yaliyokuwa yakiendelea kwa sababu tulikuwa wafisadi. Hakuna hata moja la makanisa yetu, hasa Wakatoliki, ambalo limeshutumu machinjo hayo.”
Aaron Mugemera, pasta wa kanisa, alisema hivi katika mkutano mwingine katika Rwanda baada ya maangamizi hayo: “Kanisa lina aibu. . . . Mauaji yameendelea hapa tangu 1959. Hakuna mtu yeyote aliyeshutumu mauaji hayo. . . . Hatukusema kwa ujasiri kwa sababu tuliogopa, na kwa sababu sisi tulikuwa tumestarehe.”
[Picha katika ukurasa wa 7]
Huyu “kahaba” huathiri ulimwengu wote mzima
[Hisani]
Tufe: Mountain High Maps® Copyright © 1995 Digital Wisdom, Inc.