Kupata Nafuu
BAADA ya kupatwa na mshiko wa moyo, ni kawaida kwa mtu kuwa mwoga na mwenye hangaiko. Je, nitapatwa na mshiko mwingine wa moyo? Je, nitalemazwa au nitashindwa kufanya mengi kwa sababu ya maumivu na kupoteza nguvu na nishati?
John, aliyetajwa katika makala yetu ya pili, alitumaini kwamba kadiri wakati ulivyopita, hali yake ya kusikia vibaya kila siku na maumivu ya kifua yangepungua. Lakini baada ya miezi michache, yeye alisema: “Bado hayajapungua. Hilo, pamoja na kuchoka kwa urahisi na kucheza-cheza kwa moyo wangu, hunifanya nijiulize daima, ‘Nitapatwa na mshiko mwingine wa moyo?’”
Jane, kutoka Marekani, aliyekuwa mjane mchanga wakati alipopatwa na mshiko wa moyo, alikiri: “Nilifikiri kwamba singeishi au kwamba ningepata mshiko mwingine wa moyo na kufa. Nikawa na hofu kwa kuwa nilikuwa na watoto watatu wa kulea.”
Hiroshi, wa Japani, alisimulia: “Nilishtuka kuambiwa kwamba moyo wangu hauwezi kutenda kama ulivyofanya awali; uwezo wao wa kupiga ulipunguka kwa asilimia 50. Nilikuwa na hakika kwamba ningelazimika kupunguza baadhi ya utendaji wangu nikiwa mhudumu wa Mashahidi wa Yehova, kwa kuwa niliweza kufanya chini ya nusu ya yale niliyokuwa nikifanya.”
Mtu akosapo nguvu, vipindi vya kushuka moyo na hisia za kutofaa zaweza kumwingilia. Marie, mwenye umri wa miaka 83 ambaye ni Mwaustralia aliyejitoa kwa kazi ya kuhubiri kwa wakati wote ya Mashahidi wa Yehova, aliomboleza hivi: “Kushindwa kwangu kuwa mwenye utendaji kama hapo awali kulinihuzunisha. Badala ya kusaidia wengine, sasa nilihitaji msaada.” Katika Afrika Kusini, Harold alisema: “Nilishindwa kufanya kazi kwa miezi mitatu. Kile nilichoweza kufanya wakati huo kilikuwa tu kutembea-tembea katika bustani. Jambo hilo lilinifadhaisha sana!”
Upasuaji wa kutumia mishipa mingine ya kupitisha damu ulihitajika baada ya Thomas, wa Australia, kupatwa na mshiko wa pili wa moyo. Yeye alisema: “Siwezi kuvumilia maumivu sana, na kufanyiwa upasuaji mkuu kulinishinda hata kuwazia.” Jorge, wa Brazili, alisema hivi baada ya kufanyiwa upasuaji wa moyo: “Kwa sababu ya hali yangu mbaya ya kifedha, niliogopa kwamba ningemwacha mke wangu peke yake bila msaada. Nilihisi kwamba nisingeishi muda mrefu zaidi.”
Kupata Nafuu
Ni nini ambacho kimesaidia wengi wapate nafuu na kurudia hisia-moyo zao thabiti? Jane aonelea: “Nilipohisi hofu ya ghafula, sikuzote nilimwendea Yehova katika sala na kumtwika mzigo wangu na kumwachia.” (Zaburi 55:22) Sala husaidia mtu kupata nguvu na amani ya akili ambazo ni muhimu anapokuwa na mahangaiko.—Wafilipi 4:6, 7.
John na Hiroshi walishiriki katika programu za kuwafanya wapate nafuu. Mlo mzuri na mazoezi yaliimarisha mioyo yao, hivi kwamba wote wawili walirudia kazi. Nao walisema walipona kiakili na kihisia-moyo kwa sababu ya uwezo wa kutegemeza wa roho ya Mungu.
Kupitia utegemezo wa ndugu zake wa Kikristo, Thomas alipata moyo mkuu wa kukabili upasuaji. Yeye alisema: “Kabla ya upasuaji, mwangalizi mmoja alinitembelea akasali nami. Kwa njia ya kugusa moyo kabisa, aliomba Yehova aniimarishe. Usiku huo nilikazia akili sala yake na kuhisi nimebarikiwa sana kuwa na wazee kama yeye ambao hisia-mwenzi zao wakati wa vipindi hivyo vyenye kufadhaisha ndizo baadhi ya mambo yanayofanya mtu apate nafuu.”
Anna, kutoka Italia, alikabiliana na mshuko-moyo kwa njia hii: “Ninapokuwa nimeshuka moyo, mimi hufikiria baraka zote ambazo tayari nimepokea nikiwa mmoja wa watumishi wa Mungu na baraka ambazo zitakuja chini ya Ufalme wa Mungu. Jambo hilo hunisaidia kupata utulivu.”
Marie anashukuru sana kwa msaada wa Yehova. Familia yake imekuwa ikimtegemeza, naye asema: “Ndugu zangu na dada zangu wa kiroho, kila mmoja akiwa na kifurushi chake cha kubeba, waliweka kando wakati ili kunizuru, kunipigia simu, au kunitumia kadi. Ningeweza kuhuzunikaje huku nikionyeshwa upendo mwingi hivi?”
Hakuna Wapweke
Imesemwa kwamba moyo unaopona haupaswi kuwa mpweke. Utegemezo wa familia na marafiki hutimiza fungu kubwa zuri katika kupona kwa wale ambao mioyo yao ni lazima ipone kihalisi na kitamathali.
Michael, wa Afrika Kusini, alieleza hivi: “Ni vigumu kueleza wengine jinsi kukata tamaa kulivyo. Lakini niingiapo katika Jumba la Ufalme, hangaiko ambalo akina ndugu huonyesha hunichangamsha sana na kuniondolea huzuni.” Henry, wa Australia, pia aliimarishwa kwa upendo wa kina na uelewevu ambao kutaniko lilionyesha. Yeye alisema: “Nilihitaji sana maneno hayo mororo yenye kutia moyo.”
Jorge alithamini kina cha hangaiko ambalo wengine walionyesha kwa kusaidia familia yake kifedha mpaka alipoweza kurudia kazi yake. Olga, wa Sweden, vilevile alithamini msaada halisi ambao ndugu na dada wengi wa kiroho waliwapa yeye na familia yake. Wengine walimfanyia ununuzi, huku wengine wakisafisha nyumba yake.
Mara nyingi, wagonjwa wa moyo ni lazima wapunguze kushiriki katika utendaji waupendao sana. Sven, wa Sweden, asimulia: “Nyakati nyingine ni lazima niepuke kushiriki katika huduma wakati halihewa ni yenye upepo mno au ni baridi mno, kwa kuwa hiyo hutokeza mpindano wa moyo. Nathamini uelewevu ambao wengi wa Mashahidi wenzangu wameonyesha katika jambo hili.” Na anapolazimika kuwa kitandani bila kuondoka, Sven aweza kusikiliza mikutano kwa sababu akina ndugu kwa upendo humrekodia katika ukanda. “Wao hunijulisha kile kinachoendelea katika kutaniko, na hiyo hufanya nihisi kuwa mshiriki.”
Marie, ambaye hulala kitandani sikuzote, ahisi kwamba amebarikiwa kutembelewa na wale ambao anajifunza Biblia nao. Kwa njia hiyo yeye aweza kuendelea kuzungumzia wakati ujao mzuri ajabu ambao anatazamia. Thomas ni mwenye shukrani kwa hangaiko analoonyeshwa: “Wazee wamekuwa wenye fadhili sana nao wamepunguza migawo wanayonipa.”
Familia Zahitaji Utegemezo
Hali yaweza kuwa ngumu kwa washiriki wa familia kama ilivyo kwa mhasiriwa. Wao hupatwa na mkazo mwingi na hofu. Kuhusu hangaiko la mke wake, Alfred, wa Afrika Kusini, alionelea: “Niliporudi nyumbani kutoka hospitali, mke wangu alikuwa akiniamsha mara nyingi usiku kuona ikiwa ningali nilikuwa mzima, naye alikuwa akisisitiza nimwone daktari kila baada ya miezi mitatu nikapimwe.”
Mithali 12:25 yasema kwamba “uzito katika moyo wa mtu huuinamisha.” Carlo, wa Italia, asema kwamba tangu apatwe na mshiko wa moyo, mke wake mwenye upendo na utegemezo “ameshuka moyo.” Lawrence, kutoka Australia, alisema: “Mojawapo mambo ya kuangalia ni kwamba mwenzako anatunzwa. Mkazo waweza kuwa mkubwa zaidi kwa mwenzi wako.” Hivyo, twapaswa kukumbuka sikuzote mahitaji ya familia nzima, kutia ndani watoto. Hali hiyo yaweza kuwalemaza kihisia moyo na kimwili.
James, aliyetajwa katika makala ya pili, alikuja kuwa mnyamavu baada ya mshiko wa moyo wa babake. Yeye alisema: “Nilihisi kwamba singeweza kufurahia michezo tena kwa sababu nilifikiri kwamba mara nitakapofanya hivyo, jambo baya lingetokea.” Kumwambia babake hofu yake na kufanyia kazi kukuza uhusiano mzuri pamoja na wengine kulisaidia kuondosha wasiwasi wake. Katika pindi hiyo James alifanya kitu kingine ambacho kilikuja kuwa na uvutano mkubwa sana katika maisha yake. Yeye alisema: “Niliongeza funzo langu la kibinafsi la Biblia na utayarishaji wangu wa mikutano ya Kikristo.” Miezi mitatu baadaye aliweka wakfu maisha yake kwa Yehova naye akaonyesha wakfu wake kwa ubatizo wa maji. “Tangu wakati huo,” yeye asema, “nimesitawisha uhusiano wa karibu sana na Yehova. Kwa kweli nina mengi sana ya kumshukuru.”
Baada ya kupatwa na mshiko wa moyo, mtu hupata nafasi achunguze upya maisha yake. Kwa kielelezo, mtazamo wa John ulibadilika. Yeye alisema: “Unaona ubatili wa kufuatia mambo ya kilimwengu na kutambua jinsi upendo wa familia na marafiki ulivyo muhimu na jinsi tulivyo wenye maana sana kwa Yehova. Uhusiano wangu pamoja na Yehova, familia yangu, na ndugu na dada wa kiroho ni wa kutangulizwa hata zaidi sasa.” Akikumbuka masaibu yake, yeye aliongezea: “Siwezi kuwazia kukabiliana na hilo bila tumaini letu la wakati ambapo mambo haya yatakuja kurekebishwa. Ninaposhuka moyo, mimi hufikiria wakati ujao, na kile kinachotendeka sasa chawa kidogo tu.”
Wapatwapo na mishuko ya moyo wakati wanapopata nafuu, waokokaji hao wa mishiko ya moyo wana tumaini imara kwa Ufalme ambao Yesu Kristo alitufundisha kusali kuuhusu. (Mathayo 6:9, 10) Ufalme wa Mungu utaletea wanadamu uhai udumuo milele katika ukamilifu kwenye dunia iliyo paradiso. Kisha maradhi ya moyo na ulemazo mwingine wote utaondolewa milele. Huo ulimwengu mpya upo mbele tu. Kwa kweli, maisha bora zaidi yangali yanakuja!—Ayubu 33:25; Isaya 35:5, 6; Ufunuo 21:3-5.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Utegemezo wa familia na marafiki hutimiza fungu kubwa katika kupona