Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 1/22 kur. 10-12
  • Je, Niungame Dhambi Yangu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Niungame Dhambi Yangu?
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Hakuna Jambo Lililofichwa”
  • Kutaja
  • Kuwaambia Wazazi Wako
  • Kuwaendea Wazee ili Kutafuta Msaada
  • ‘Ninaogopa Kutengwa na Ushirika’
  • Kubali Sikuzote Nidhamu ya Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Je, Kuungama Dhambi Ni Takwa la Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Ukitenda Dhambi Nzito Unapaswa Kufanya Nini?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • Naweza Kuachaje Maisha Maradufu?
    Amkeni!—1994
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 1/22 kur. 10-12

Vijana Huuliza . . .

Je, Niungame Dhambi Yangu?

“Nimeaibika sana, sijui jambo la kufanya. Ninataka kwenda kwa wazazi wangu, lakini nimeaibika mno.”—Lisa.a

HIVYO ndivyo alivyoandika mwanamke mmoja mchanga aliyefadhaika. Alikuwa amejihusisha kimahaba na mtu asiye mwamini kwa kipindi cha miaka michache ambapo siku moja, akiwa amelewa kwa alkoholi, alifanya ngono naye.

Kwa kusikitisha, mambo kama hayo hutokea mara kwa mara, hata miongoni mwa vijana Wakristo. Kadiri tulivyo wachanga zaidi na wasio na uzoefu, ndivyo inavyoelekea kwamba tutafanya makosa mengi. Lakini ingawa si jambo kubwa kufanya kosa dogo, ni jambo zito kabisa kufanya kosa zito, kama vile ukosefu wa adili katika ngono. (1 Wakorintho 6:9, 10) Hilo litokeapo, kijana ahitaji msaada. Lakini tatizo ni kwamba si rahisi kwa mtu kuungama dhambi zake.

Msichana mmoja Mkristo alifanya ngono kabla ya ndoa. Aliamua kuungama kwa wazee wa kutaniko lake, hata akapanga tarehe ambayo angefanya hivyo. Lakini aliahirisha tarehe hiyo. Baadaye, aliisogeza tarehe mbele tena. Hatimaye, mwaka mzima ulikuwa umepita!

“Hakuna Jambo Lililofichwa”

Ikiwa umefanya dhambi nzito, wapaswa utambue kwamba kuficha si wazo la busara kamwe. Jambo moja lililo wazi ni kwamba kwa kawaida ukweli huja kujulikana. Akiwa mtoto mdogo, Mark alivunja pambo la kauri la ukuta. “Nilijitahidi kulishikanisha kwa gundi kwa uangalifu na kulirudisha mahali palo,” akumbuka, “lakini muda mrefu haukupita kabla wazazi wangu hawajagundua nyufa.” Ni kweli, wewe si mtoto tena. Lakini kwa kawaida wazazi wengi wanaweza kutambua watoto wao wanapokuwa na tatizo fulani.

“Nilijitahidi kuficha matatizo yangu kwa kusema uwongo,” akubali Ann mwenye umri wa miaka 15, “lakini nilifanya mambo yawe mabaya zaidi.” Mara nyingi, uwongo hufunuliwa. Na wazazi wako wagunduapo kwamba ulisema uwongo, yaelekea watakasirika—watakasirika zaidi kuliko kama ungeungama mwanzoni.

La maana hata zaidi, Biblia husema: “Kwa maana hakuna jambo lililofichwa ambalo halitakuwa dhahiri, wala kitu chochote kilichositiriwa kwa uangalifu ambacho hakitakuja kujulikana kamwe na ambacho hakitakuja kuwa wazi kamwe.” (Luka 8:17) Yehova hujua kile ambacho tumefanya na kile tunachofanya. Huwezi kujificha kutoka kwake kama vile Adamu alivyoshindwa kujificha. (Mwanzo 3:8-11) Baadaye, dhambi zako zaweza kufunuliwa kwa wengine.—1 Timotheo 5:24.

Kuficha kwaweza kukuumiza kwa njia nyingine pia. Mtunga-zaburi Daudi aliandika: “Niliponyamaza mifupa yangu ilichakaa kwa kuugua kwangu mchana kutwa. Kwa maana mchana na usiku mkono wako ulinilemea.” (Zaburi 32:3, 4) Ndiyo, mkazo wa kuficha siri waweza kutokeza madhara makubwa sana ya kihisia-moyo. Wasiwasi na hatia, pia hofu ya kufichuliwa, zaweza kukufanya ushuke moyo kabisa. Waweza kuanza kujitenga na marafiki na familia. Waweza hata kuhisi kwamba umekatiliwa mbali kabisa na Mungu mwenyewe! “Nilikuwa nimehangaika na dhamiri mbaya kwa sababu ya kumhuzunisha Yehova,” aliandika kijana aitwaye Andrew. “Ilinisumbua sana.”

Kutaja

Je, kuna njia yoyote ya kuondolewa kizaazaa hicho cha kihisia moyo? Ndiyo, ipo! Mtunga-zaburi alisema: “Nalikujulisha dhambi yangu, wala sikuuficha upotovu wangu. . . . Nawe ukanisamehe upotovu wa dhambi yangu.” (Zaburi 32:5; linganisha 1 Yohana 1:9.) Hali kadhalika Andrew alipata msaada wa kweli katika kuungama dhambi zake. Akumbuka: “Nilimfikia Yehova na nilisali kwa unyoofu ili kupata msamaha wake.”

Waweza kufanya vivyo hivyo. Sali kwa Yehova. Yeye ajua kile ambacho umefanya, lakini kwa unyenyekevu kiri kwake katika sala. Omba msamaha, usijizuie kwa sababu wahisi u mwovu sana kupata msaada. Yesu alikufa ili tuweze kufurahia uhusiano mzuri na Mungu ingawa hatujakamilika. (1 Yohana 2:1, 2) Pia waweza kuomba upate nguvu ili kufanya mabadiliko yahitajiwayo. Kusoma Zaburi 51 kwaweza kuthibitika kuwa kwenye msaada kimahususi katika kumfikia Mungu.

Kuwaambia Wazazi Wako

Hata hivyo, mengi zaidi yanahitajiwa zaidi ya kuungama tu kwa Mungu. Pia una wajibu wa kuwaambia wazazi wako. Wao wameamriwa na Mungu kukulea “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Wao waweza kufanya hivyo ikiwa tu wayajua matatizo yako. Tena, kuwaambia wazazi wako laweza kuwa jambo lisilo rahisi au la kupendeza. Lakini baada ya itikio lao la kwanza, yaelekea wataweza kudhibiti hisia-moyo zao. Hata waweza kufurahi kwamba umewaamini kiasi cha kufunua tatizo lako kwao. Kielezi cha Yesu cha mwana mpotevu chaeleza juu ya kijana mwanamume ambaye aliangukia ukosefu wa adili katika ngono. Lakini hatimaye alipotubu, baba yake alimkaribisha kwa uchangamfu! (Luka 15:11-24) Bila shaka wazazi wako watakusaidia pia. Zaidi ya yote, wao bado wanakupenda.

Kweli, waweza kuhofu kwamba utawaumiza wazazi wako. Lakini kuungama dhambi siko kuwaumizako wazazi wako; bali kufanya dhambi ndiko huwaumiza! Kuungama ni hatua ya kwanza ya kutuliza umizo hilo. Ann, aliyetajwa mwanzoni, aliwaambia wazazi wake na baadaye alipata kitulizo kikubwa sana.b

Bado kipingamizi kingine katika kuungama ni aibu na fedheha. Mwandishi mwaminifu Ezra hakuwa amefanya dhambi, lakini alipoungama dhambi za wenzi wake Wayahudi, alisema: “Nimetahayari, naona haya kuinua uso wangu mbele zako, Mungu wangu.” (Ezra 9:6) Kwa kweli ni jambo la kufaa kuhisi aibu ufanyapo kosa. Huonyesha kwamba dhamiri yako bado inafanya kazi. Baadaye hisia hizo za aibu zitapungua. Andrew alieleza hilo namna hii: “Ni jambo gumu sana na fedheha kuungama. Lakini kujua kwamba Yehova atasamehe kabisa ni kitulizo.”

Kuwaendea Wazee ili Kutafuta Msaada

Ikiwa wewe ni Mkristo, jambo hilo haliishi tu kwa kuwaeleza wazazi wako. Andrew asema: “Nilijua nilipaswa kupeleka tatizo langu kwa wazee wa kutaniko. Ilikuwa kitulizo kama nini kujua kwamba walikuwa tayari kunisaidia!” Ndiyo, vijana miongoni mwa Mashahidi wa Yehova waweza na wapaswa kwenda kwa wazee wa kutaniko ili kupata msaada na kitia-moyo. Lakini kwa nini huwezi kusali tu kwa Yehova na kuachia mambo hapo? Kwa sababu Yehova amekabidhi wazee daraka la ‘kufuliza kulinda juu ya nafsi zenu.’ (Waebrania 13:17) Wao waweza kukusaidia kuepuka kuingia katika kosa tena.—Linganisha Yakobo 5:14-16.

Usijidanganye kwa kusababu kwamba waweza kujisaidia. Ikiwa wewe ni mwenye nguvu kiasi cha kufanya hivyo, je, kweli ungeingia katika dhambi? Kwa wazi unahitaji kutafuta msaada kutoka kwa mtu mwingine. Andrew alifanya hivyo kijasiri. Shauri lake ni nini? “Ninamtia moyo mtu yeyote ambaye ameingia katika dhambi nzito, au alihusika katika dhambi nzito, kufungua moyo wake kwa Yehova na kwa mzee.”

Lakini utamfikiaje mzee? Mchague mmoja ambaye unastarehe naye kwa kadiri fulani. Unaweza kuanza kwa kusema: “Ninataka kuongea juu ya jambo fulani” au “nina tatizo” au hata “nina tatizo na ninahitaji msaada wako.” Kuwa kwako mnyoofu na wazi kutaonyesha kwa wazi kutubu kwako na tamaa yako ya kubadilika.

‘Ninaogopa Kutengwa na Ushirika’

Vipi kuhusu uwezekano huo? Ni kweli kufanya dhambi nzito kunamweka mtu katika hali ya kuweza kutengwa na ushirika, lakini si lazima. Kutenga na ushirika ni kwa wale wakataao kutubu—ambao kwa shingo ngumu wakataa kubadilika. Lasema Mithali 28:13: “Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema.” Ukweli kwamba umewafikia wazee ili kutafuta msaada ni uthibitisho wa tamaa yako ya kutaka kubadilika. Kimsingi wazee ni waponyaji, si watoa adhabu. Wao wana wajibu wa kushughulikia watu wa Mungu kwa fadhili na heshima. Wao wataka kukusaidia ‘kufanyia miguu yako mapito yaliyo manyoofu.’—Waebrania 12:13.

Kwa kweli, hila au kosa zito la muda mrefu lihusikapo, usadikisho wa “kazi zinazofaa toba” waweza kukosekana. (Matendo 26:20) Mara nyingine kutenga na ushirika hutokea. Na hata ikiwa mwenye kutenda dhambi ni mwenye kutubu, wazee wana wajibu wa kutoa nidhamu ya aina fulani. Je, wapaswa uwe na hasira au mwenye uchungu kuhusu uamuzi wao? Katika Waebrania 12:5, 6, Paulo asihi: “Mwana wangu, usipuuze nidhamu kutoka kwa Yehova, wala usizimie wakati usahihishwapo naye; kwa maana ambaye Yehova ampenda humtia nidhamu; kwa kweli, yeye humpiga mijeledi kila mtu ambaye yeye ampokea kuwa mwana.” Nidhamu yoyote upokeayo, uione kuwa ni uthibitisho kwamba Mungu akupenda. Kumbuka, toba ya kweli itakurudishia uhusiano wa kufaa pamoja na Baba yetu mwenye rehema, Yehova Mungu.

Inataka ujasiri kukubali makosa yako. Lakini kwa kufanya hivyo, waweza kunyoosha mambo si na wazazi wako tu bali na Yehova Mungu mwenyewe. Usiruhusu hofu, kiburi, au fedheha zikuzuie kutafuta msaada. Kumbuka: Yehova ‘atasamehe kabisa.’—Isaya 55:7.

[Maelezo ya Chini]

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b Kwa maelezo kuhusu kuwafikia wazazi wako, ona sura 2 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

‘Natia moyo wote ambao wametenda dhambi wafungue mioyo yao kwa Yehova.’—Andrew

[Picha katika ukurasa wa 11]

Kuungama kwa wazazi wako kwaweza kufanya upate nguvu ya kiroho tena

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki