Jinsi ya Kushughulika na Hisia
JE, WAKATI huu unamtunza mpendwa wako aliye mgonjwa sana? Ikiwa ndivyo, huenda unapatwa na hisia zenye kuvuruga na zenye kuogopesha. Unaweza kufanya nini? Fikiria hisia ambazo baadhi ya watunzaji hung’ang’ana nazo na madokezo yenye kutumika ambayo yamewasaidia kukabili hali.
Aibu. Pindi kwa pindi, tabia ya mtu ambaye ni mgonjwa yaweza kukuaibisha mbele ya watu wengine. Lakini kwa kuwaeleza marafiki na majirani hali ya ugonjwa wa mpendwa wako kwaweza pia kuwafanya kuwa wenye “hisia-mwenzi” na subira. (1 Petro 3:8) Ikiwezekana, zungumza na familia ambazo pia ziko katika hali kama yako. Huenda aibu isiwe kubwa sana mnapoelezeana mambo mliyojionea. Sue aeleza jambo lililomsaidia: “Nilimsikitikia sana babangu—hiyo ilifanya nisione aibu yoyote. Na ucheshi wake pia ulisaidia.” Ndiyo, ucheshi—wa mgonjwa na wa wale wanaomtunza—ni chombo bora cha kuondoa mikazo ya kihisia moyo.—Linganisha Mhubiri 3:4.
Hofu. Kutojua hali ya maradhi hayo kwaweza kuogopesha kwelikweli. Ikiwezekana, tafuta ushauri wa wataalamu juu ya kile utakachotarajia ugonjwa huo uzidipo kuwa mbaya. Jifunze jinsi ya kuandaa utunzi chini ya hali hizo. Kwa Elsa, mojawapo ya mambo muhimu zaidi katika kukabiliana na hofu yake lilikuwa kuzungumza na watunzaji wengine na wauguzi wa makao ya kutunzia walio wagonjwa kuhusu kile atakachotazamia hali ya mgonjwa izidipo kuwa mbaya. Jeanny ashauri hivi: “Kabili na kudhibiti hofu zako. Hofu ya kile kiwezacho kutukia mara nyingi ni mbaya kuliko kile kitakachotukia kihalisi.” Dakt. Ernest Rosenbaum apendekeza kwamba chochote kile kinachozisababisha, hofu zako zapaswa “kuzungumziwa zizukapo.”—Linganisha Mithali 15:22.
Huzuni. Si rahisi kushughulika na huzuni, hasa katika hali za utunzaji. Unaweza kuhuzunikia kupoteza mwandamani, hasa ikiwa mpendwa wako aliye mgonjwa hawezi kuongea tena, kusikiliza vizuri, au hata kukutambua. Wengine hawawezi kuelewa hisia kama hizo mara moja. Kuzungumza juu ya huzuni yako na rafiki mwenye ufahamu ambaye atakusikiliza kwa subira na kwa hisia-mwenzi kwaweza kukutuliza sana.—Mithali 17:17.
Hasira na Mfadhaiko. Hizo ni matokeo ya kawaida ya kutunza mtu aliye mgonjwa sana ambaye mwenendo wake waweza kuwa mgumu nyakati nyingine. (Linganisha Waefeso 4:26.) Tambua kwamba mara nyingi ni maradhi, wala si mgonjwa, ambayo yanasababisha tabia hiyo yenye kuleta mkazo. Lucy akumbuka: “Nilipokuwa nimekasirika kabisa, nilikuwa nikilia. Kisha ningejaribu kujikumbusha hali na ugonjwa wa huyo mgonjwa. Nilijua kwamba mgonjwa alihitaji msaada wangu. Hilo lingenisaidia kuendelea kumtunza.” Ufahamu wa kina kama huo waweza kukufanya ‘usiwe mwepesi wa hasira.’—Mithali 14:29; 19:11.
Hatia. Hisia za hatia ni za kawaida sana miongoni mwa watunzaji. Hata hivyo, uwe na hakika kwamba unafanya kazi muhimu lakini iliyo ngumu sana. Kubali ukweli wa kwamba si sikuzote utaitikia kwa ukamilifu kwa neno na kwa tendo. Biblia yatukumbusha: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyu ni mtu mkamilifu, awezaye kuuongoza kwa hatamu mwili wake wote pia.” (Yakobo 3:2; Waroma 3:23) Usiruhusu hisia zozote za hatia zikuzuie kuchukua hatua ifaayo sasa. Unapohisi umekasirika juu ya jambo ambalo ulisema au kitu ulichofanya, yaelekea utapata kwamba kusema “pole” kutafanya wewe na mgonjwa wako kuhisi afadhali. Mtu mmoja aliyetunza mtu wa ukoo aliyekuwa mgonjwa alishauri hivi: “Fanya yote uwezayo chini ya hali hizo.”
Mshuko-Moyo. Mshuko-moyo ni wa kawaida sana—na inaeleweka—katika familia zinazokabili magonjwa mabaya. (Linganisha 1 Wathesalonike 5:14.) Mtunzaji anayepatwa na mshuko-moyo aeleza kile kilichomsaidia: “Wengi walikuwa wakitushukuru kwa kuandaa utunzaji. Maneno machache tu ya kutia moyo yaweza kukuimarisha sana uendelee mbele unapokuwa umechoka sana au umeshuka moyo.” Biblia yataarifu hivi: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha, bali neno jema huufurahisha.” (Mithali 12:25) Wengine huenda wasitambue uhitaji wako wa kitia moyo sikuzote. Hivyo, nyakati nyingine, huenda ukalazimika kwanza kutaja “uzito” ulio moyoni mwako ili upokee “neno jema” la kitia moyo kutoka kwa wengine. Ingawa hivyo, hisia za kushuka moyo zikidumu au kuwa kali zaidi, ni afadhali umwone daktari.
Kutoweza Kusaidia. Huenda ukahisi huwezi kusaidia unapokabili maradhi yenye kulemaza. Kubali uhalisi wa hali yako. Tambua upungufu wako—huwezi kudhibiti afya ya mgonjwa, lakini unaweza kuandaa utunzaji mwororo. Usijitazamie kuwa mkamilifu, wala usitazamie mgonjwa wako au wategemezaji wako kuwa wakamilifu. Kuwa na fikira zilizosawazika hakupunguzi tu hisia za kutoweza kusaidia bali pia hupunguza mzigo wa kazi. Kwa hekima, wengi ambao wametunza mpendwa washauri: Jifunze kukabili hali siku kwa siku.—Mathayo 6:34.
[Blabu katika ukurasa wa 8]
“Kabili na kudhibiti hofu zako. Hofu ya kile kiwezacho kutukia mara nyingi ni mbaya kuliko kile kitakachotukia kihalisi”
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
Maneno Yenye Kutia Moyo Kutoka kwa Watunzaji
“USISONONESHWE na mawazo yasiyofaa kujihusu. Hayo ni ya kawaida katika hali kama hizo. Kwa wazi hupaswi kuficha hisia zako kamwe. Zungumza na mtu kuhusu jinsi unavyohisi, na ukiweza, chukua likizo—nenda kwa muda fulani—ili uweze kuhisi umeburudika.”—Lucy, ambaye kazi yake katika kliniki imehusisha kusaidia idadi fulani ya watunzaji na wagonjwa vilevile.
“Ikiwa kuna washiriki wa familia au marafiki ambao wanapatikana nao wako tayari kusaidia, acha wasaidie. Ni muhimu kwamba ushiriki mzigo huo na wengine.”—Sue, aliyemtunza baba yake kabla ya baba kufa kwa maradhi ya Hodgkin.
“Jifunze kuwa mcheshi.”—Maria, aliyesaidia kutunza rafiki yake mpendwa aliyekufa kwa kansa.
“Dumisha nguvu za kiroho. Mkaribie Yehova, na usali bila kukoma. (1 Wathesalonike 5:17; Yakobo 4:8) Yeye huandaa msaada na faraja kupitia roho yake, Neno lake, watumishi wake wa kidunia, na ahadi zake. Jaribu kuwa mwenye utaratibu mzuri kwa kadiri iwezekanavyo. Kwa kielelezo, hufaa kutengeneza ratiba za dawa na orodha za wasaidizi.”—Hjalmar, aliyemtunza ndugu-mkwe wake aliyekuwa akifa.
“Jifunze yote uwezayo kuhusu hali ya ugonjwa wa mgonjwa wako. Kufanya hivyo kutakusaidia kujua jambo la kutarajia kutoka kwa mgonjwa wako na kwako wewe mwenyewe na jinsi ya kutunza mgonjwa wako.”—Joan, ambaye mume wake ana maradhi ya Alzheimer.
“Tambua kwamba wengine wamekabili hali hiyo kabla ya wewe na kwamba Yehova aweza kukusaidia kukabiliana na chochote kile kitakachotokea.”—Jeanny, aliyemtunza mume wake kabla ya mume kufa.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Ili kutuliza hofu zako, jaribu kujua kwa kadiri uwezavyo kuhusu ugonjwa huo
[Picha katika ukurasa wa 9]
Kuzungumza na rafiki mwenye ufahamu kwaweza kukutuliza sana