Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 2/22 kur. 11-13
  • Nawezaje Kuwa Rafiki ya Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nawezaje Kuwa Rafiki ya Mungu?
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ujuzi wa Kibinafsi wa Mungu
  • Mwenendo Mnyoofu Ni wa Lazima
  • Tafuta Washiriki Wazuri
  • Unaweza Kuwa Rafiki ya Yehova
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • Jizoeze Utawa Kuwa Lengo Lako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Yehova-Mtu Umjuaye Tu au Rafiki Yako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Je, Kuwa Rafiki ya Mungu Kutanisaidia?
    Amkeni!—1995
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 2/22 kur. 11-13

Vijana Huuliza . . .

Nawezaje Kuwa Rafiki ya Mungu?

“UAMINIFU-MSHIKAMANIFU.” “Ujitoaji wa kibinafsi.” Haya ni maneno ambayo kwa kawaida watu hutumia kuelezea ufungamano wao kwa marafiki wao wa karibu zaidi. Je, ulijua kwamba maneno hayo pia yaweza kueleza ufungamano kwa Muumba Mtukufu wa ulimwengu huu wote mzima wenye kutisha—kwamba Mungu mwenyewe aweza kuwa rafiki yako wa kibinafsi? Ndiyo, Biblia huzungumza juu ya kuwa na ujitoaji kimungu, na kwamba neno hilo halihusishi tu utii bali pia ufungamano wa kibinafsi kumwelekea Mungu, ukaribiano ambao hutokana na moyo wenye shukrani.

Makala zilizotangulia katika mfululizo huu zimeonyesha kwamba ufungamano kama huo unawezekana na ni wenye kufaa.a Lakini waweza kupataje uhusiano huu wa kibinafsi pamoja na Mungu? Si kitu fulani unachozaliwa nacho au unachorithi moja kwa moja kutoka kwa wazazi wenye kumhofu Mungu. Badala ya hivyo, ni kitu kinachokuja tu kutokana na jitihada ya kweli. Mtume Paulo alimwambia kijana Timotheo ‘awe akijizoeza mwenyewe ujitoaji-kimungu ukiwa shabaha yake.’ Ndiyo, alipaswa aweke jitihada ambayo mwanariadha huweka katika mazoezi! (1 Timotheo 4:7, 8, 10) Wapaswa kufanya vivyo hivyo ikiwa wataka Mungu awe rafiki yako. Lakini waweza kuanzaje kujizoeza kwa habari hiyo?

Ujuzi wa Kibinafsi wa Mungu

Kwa vile ujitoaji kimungu hutoka moyoni, ni lazima ujaze moyo wako na ujuzi wa Mungu. Kwa kusikitisha, vijana zaidi ya 500 walipoulizwa “Ni mara ngapi unasoma Biblia ukiwa peke yako?” asilimia 87 walisema ama “mara moja moja,” ama “mara chache sana,” ama “hawasomi kamwe.” Vijana wengi kwa wazi wafikiri kwamba kusoma Biblia hakusisimui na kunachosha. Lakini haipaswi kuwa hivyo hata kidogo! Fikiria: Kwa nini baadhi ya vijana hukariri tarakimu mbalimbali za michezo au hujifunza maneno ya nyimbo wazipendazo sana? Kwa sababu wanapendezwa na mambo hayo. Hali kadhalika, kujifunza Biblia hupendeza ikiwa wajitia ndani yayo kabisa. (1 Timotheo 4:15) Mtume Petro alisihi: “Fanyizeni hamu sana ya maziwa yasiyoghushiwa yaliyo ya neno.” (1 Petro 2:2) Ndiyo, wapaswa ufanyize, au ukuze tamaa kama hiyo katika Maandiko. Hii yaweza kuhitaji jitihada, lakini manufaa yastahili jitihada hiyo.b

Faida moja ya kusoma na kujifunza Neno la Mungu na fasihi zenye msingi wa Biblia ni kwamba kutafunua “uzuri wa BWANA.” (Zaburi 27:4) Kijana mmoja Mkristo aitwaye Amber alifanya kuwa mradi wake kusoma Biblia yote. Huu ulimchukua karibu mwaka mmoja. “Sidhani kama kuna mambo mengi katika maisha yangu ambayo huhitaji wakati na jitihada kubwa na kuleta thawabu nyingi,” alieleza Amber. “Nilipokuwa nikisoma Biblia, nilihisi kana kwamba Yehova ameniweka katika mapaja yake kama baba na kunifundisha. Nilijifunza mengi sana kuhusu Yehova—mambo ambayo yalifanya nimkaribie zaidi na kutaka kumhofu kwa maisha yangu yote.”

Usomapo Biblia, wajifunza matukio mengi ambayo Mungu kwa uaminifu-mshikamanifu aliwategemeza marafiki zake. (Zaburi 18:25; 27:10) Wapata kwamba viwango vyake wakati wote ni bora na ni kwa manufaa yetu ya kudumu. (Isaya 48:17) Kusoma kuhusu sifa zisizo na kifani za Mungu, kama vile upendo na busara, hukuchochea kutaka kumwiga. (Waefeso 5:1) Ili habari kama hizo zichochee moyo wako, wapaswa kutafakari pia. Usomapo, jiulize: ‘Hili laniambia nini kuhusu Yehova? Ninaweza kulitumiaje katika kufikiri na matendo yangu? Hili laonyeshaje kwamba Mungu ni rafiki bora zaidi ambaye ningeweza kupata?’

Ujuzi uupatao kuhusu Mungu kupitia funzo la binafsi na la kutaniko utakusaidia kuwa karibu naye katika njia nyingine. Methali ya Kifaransa husema: “Marafiki wa kweli hufikiri sawa.” Lakini wawezaje ‘kufikiri sawa’ pamoja na Mungu? Kijana Denise aeleza: “Kadiri ujifunzapo na kufanya utafiti juu ya jambo fulani, ndivyo upatapo kujua zaidi maoni ya Yehova juu ya jambo hilo. Husaidia kujua jinsi ahisivyo juu ya jambo fulani.”

Mwenendo Mnyoofu Ni wa Lazima

Mungu huchagua kuwa marafiki zake wale tu ambao huheshimu viwango vyake vya maadili. “Siri yake ni pamoja na wanyofu,” lasema Mithali 3:32. Kijana ajitahidiye kuwa mnyoofu ‘ataenda katika sheria ya BWANA.’ (2 Wafalme 10:31) Mwenendo kama huo waweza kumleta mtu karibu na Mungu kwa kadiri gani? Yesu Kristo alisema: “Baba yangu atampenda, nasi hakika tutakuja kwake na kufanya kao letu pamoja naye.” (Yohana 14:21-24) Picha ya kuchangamsha moyo kama nini! Wazia, watu wawili wakuu zaidi katika ulimwengu wote mzima wakitoa uangalifu wao wa kudumu na utunzi kwa mwanadamu! Hilo litatukia kwako ikiwa utakuwa mwangalifu kutembea katika sheria ya Yehova.

Je, kuwa mnyoofu humaanisha kwamba wapaswa kuwa mkamilifu? Hapana hata kidogo! Kufanya makosa kwa sababu ya udhaifu hakumaanishi kwamba umeyaacha ‘mapito ya maagizo ya Mungu.’ (Zaburi 119:35) Fikiria kile ambacho Biblia hutuambia kuhusu mfalme Daudi. Ingawa alikuwa rafiki mwaminifu-mshikaminifu wa Mungu, alifanya makosa mazito kwa sababu ya udhaifu. Hata hivyo, Yehova alisema kwamba alitembea “kwa ukamilifu wa moyo, na kwa adili.” (1 Wafalme 9:4) Wakati wote Mfalme Daudi alionyesha toba ya kuhisiwa moyoni kwa kosa lolote alilofanya na alijitahidi sana kufanya kile kimpendezacho Mungu.—Zaburi 51:1-4.

Ingawa Daudi alimpenda Mungu, alijua jinsi ilivyo vigumu mara nyingine kufanya jambo lililo sawa. Ndiyo maana alimsihi Mungu: “Uniongoze katika kweli yako.” Ndiyo, alikuza hofu ifaayo ya kutomwudhi Mungu. Kwa kufaa Daudi angeweza kusema: “Siri ya BWANA iko kwao wamchao.” (Zaburi 25:5, 14) Hii si hofu mbaya bali ni kicho cha kina kirefu kwa Muumba na hofu yenye kufaa ya kutomchukiza. Hofu ya kimungu ni msingi ambao mwenendo ufaao unategemezwa. Kwa kutoa kielezi, fikiria kielelezo cha kijana mmoja Mkristo aitwaye Joshua.

Joshua alipokea ujumbe kutoka kwa mwanashule mwenzi ukisema kwamba alimpenda na alitaka kuwa na “uhusiano wa kimapenzi” pamoja naye. Joshua, japo alivutiwa naye, alitambua kwamba uhusiano na asiye mwamini ungeweza kuongoza katika ukosefu wa adili na ungeharibu urafiki wake pamoja na Yehova. Basi alimwambia waziwazi kwamba hakupendezwa! Baadaye alipomwambia mama yake jinsi alivyoshughulikia hali hiyo, mama huyo alisema kwa ghafula bila ya kufikiri: “Aa, Joshua, labda uliumiza hisia zake!” Joshua alijibu: “Lakini, mama. Ni afadhali niumize hisia zake kuliko kumwumiza Yehova.” Hofu yake ya kimungu, hofu ya kutomchukiza Rafiki yake wa kimbingu, ilimsukuma kudumisha mwenendo mnyoofu.

Tafuta Washiriki Wazuri

Hata hivyo, kijana mmoja aitwaye Lynn, aliendelea kuingia katika matata. Tatizo lilikuwa nini? Alikuwa anaandamana na washiriki wabaya. (Kutoka 23:2; 1 Wakorintho 15:33) Suluhisho likawa nini? Kutafuta marafiki wapya! “Ikiwa una marafiki karibu nawe ambao wanampenda Yehova,” alimalizia Lynn, “hukusaidia kuendelea kuwa na dhamiri iliyo chonjo na kuepuka matata. Wanapoonyesha chuki yao kubwa kwa makosa, jambo hilo linakufanya uhisi vivyo hivyo.”

Kwa kweli, chaguo lako baya la marafiki laweza kuwa ndicho kipingamizi kikubwa zaidi cha kuwa na urafiki pamoja na Mungu. Ann mwenye umri wa miaka 18 alikiri: “Washiriki wako wana uvutano mkubwa kwako. Baada ya muda fulani utakuwa kama wao. Watakuvuta ufikiri kama wao. Mazungumzo yao yaweza kuwa sana sana juu ya ngono. Yaweza kukufanya uwe mdadisi. Wajiuliza ngono ikoje.” Ann alijifunza hili kupitia somo chungu. Yeye asema: “Ninajua uvutano wa washiriki wabaya. Nilijihusisha katika ukosefu wa adili na nilipata mimba nikiwa na umri wa miaka 15.”

Hatimaye Ann alitambua ukweli wa maneno ya Biblia: “Kwa hiyo, yeyote yule atakaye kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya mwenyewe kuwa adui ya Mungu.” (Yakobo 4:4) Ndiyo, Ann alitaka kuwa—alikusudia kuwa—rafiki ya ulimwengu. Lakini hili lilimsababishia tu mfululizo wa maumivu ya moyoni. Kwa uzuri, Ann aliacha kujiendesha kipumbavu. Alihisi sikitiko kubwa sana kutokana na mwendo wake akatafuta msaada kutoka kwa wazazi wake na wazee wa kutaniko lake. Pia alitafuta marafiki wapya. (Zaburi 111:1) Kutokana na jitihada kubwa kwa upande wake, Ann aliweza tena kuwa rafiki ya Mungu. Sasa, miaka mingi baadaye, yeye asema: “Uhusiano wangu na Mungu ni wa karibu zaidi.”

Kupitia funzo la binafsi la Biblia, kutafakari, mwenendo mnyoofu na washiriki wafaao, wewe pia waweza kusitawisha urafiki wa karibu na Mungu. Hata hivyo kudumisha urafiki huo ni jambo jingine. Inawezekanaje kufanya hivyo japo magumu na udhaifu wa kibinafsi? Makala ya wakati ujao katika mfululizo huu itazungumzia jambo hili.

[Maelezo ya Chini]

a Ona matoleo ya Amkeni! ya Julai 22 na Novemba 22, 1995.

b Ona “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Nisome Biblia?” katika toleo letu la Agosti 8, 1985, (Kiingereza).

[Picha katika ukurasa wa 13]

Je, washiriki wangu watanisaidia kuwa rafiki ya Mungu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki