Mikusanyiko ya Rumania Yafanywa Japo Upinzani
Mkusanyiko wa Kimataifa wa “Wajumbe wa Amani ya Kimungu” wa Mashahidi wa Yehova ulipangwa kufanywa katika Bucharest, Rumania, tokea Julai 19 hadi 21, 1996. Wajumbe wapatao 40,000, kutia ndani maelfu kutoka nchi nyingine, walipanga kuzuru jiji hilo kuu na maridadi la Ulaya lenye wakazi milioni mbili. Stediamu ya Kitaifa, yenye uwezo wa kutoshea watu 60,000, ilikuwa imehifadhiwa kwa ajili ya pindi hiyo. Lakini, Juni 24, maofisa wa Rumania waliopashwa habari zisizo sahihi walikataa kutoa idhini ya kufanya mkusanyiko.
Mashahidi wa Yehova walijaribu sana amri hiyo ya kufutilia mbali mkusanyiko wao ibatilishwe, lakini hawakufanikiwa. Basi, ikawa lazima mipango ibadilishwe ili maelfu kadhaa ya wajumbe wa kigeni walioalikwa kutoka nchi kadhaa za Ulaya, Amerika Kaskazini, na Japani waweze kuhudhuria mkusanyiko katika Budapest, Hungaria, tokea Julai 12 hadi 14. Mabadiliko hayo ya dakika za mwisho yalitokeza gharama kubwa, kutatanishwa, na kutamaushwa kwa wengi.
Lakini ni nini kingepangwa kwa ajili ya wajumbe wa hukohuko Rumania? Maofisa katika majiji ya Cluj-Napoca na Brasov walionwa, na hatimaye iliwezekana kufanya mikusanyiko huko, tokea Julai 19 hadi 21. Hata hivyo, Warumania wengi hawakuweza kufika Cluj-Napoca au Brasov. Kwa hiyo, mikusanyiko mingine miwili ilifanywa Septemba 13 hadi 15, mmoja katika Baia-Mare na mwingine katika Bucharest.
Kwa nini mkusanyiko wa awali wa Bucharest ulifutiliwa mbali? Na ni nini kilichofanya maofisa wengine baadaye wabadili mawazo yao, ili mikusanyiko ifanywe katika Rumania, kutia ndani na mkusanyiko uliofanywa Bucharest?
Ni Nani Waliochochea Upinzani?
Wakati wa mkusanyiko wa kimataifa katika Budapest, gazeti la habari la Hungaria Színes Vasárnap lilisema hivi kuhusu Mashahidi wa Yehova: “Awali walikuwa wamepanga kufanya mkutano wao wa kimataifa wa kila mwaka Bucharest, lakini kwa sababu ya upinzani wa Wakristo Waothodoksi, maofisa wa Rumania hawakuwapa Mashahidi wa Yehova idhini ya kufanya huo mkutano.” Jambo la kwamba ni kanisa lililochochea huo upinzani likaja kujulikana sana. Kwa mfano, Times Union, ambalo ni gazeti la Albany, New York, Marekani, liliripoti hivi: “Mkuu wa Othodoksi Teoctist alionya waamini wa Othodoksi walinde dhidi ya kile alichokiita itikadi za ‘kizushi’ za Mashahidi wa Yehova.”
Je, hizo ripoti za upinzani wa makasisi dhidi ya mkusanyiko zilikuwa za kweli? Mnamo Juni, wakazi wa Bucharest walianza kuona vibandiko jijini kote kwenye majengo ya kanisa, kuta za majengo, na katika reli za chini ya ardhi, ambavyo vilichongea Mashahidi wa Yehova. Kibandiko kimoja chenye kichwa “KWA WARUMANIA WOTE!” kiliuliza: “Je, sasa Rumania inahitaji mkusanyiko wa kimataifa wa Wayehova . . . Julai 19-21? Enyi Wakristo—na tupinge mkusanyiko huu wa kishetani!”
Kibandiko kingine kilichokuwa na kichwa “Jihadharini na HATARI YA WAYEHOVA!” lilikazia: “Mashahidi wa Yehova hupigana na Ukristo . . . Nia yao ni kugawanya watu wetu na kusababisha ugomvi wa kidini. . . . ENYI WARUMANIA WOTE, pingeni mkusanyiko huu!”
“MWITO WA KUCHUKUA HATUA” kilikuwa kichwa cha kibandiko kingine. “Udugu wa Othodoksi ya Rumania . . . unawaalika waumini wote wa Othodoksi kwenye mkutano wa kuteta, utakaofanywa Jumapili, Juni 30.” Kibandiko hicho kilimalizia: “Tutaomba wenye mamlaka wafutilie mbali mkusanyiko huo wa kishetani. NJOONI ILI TUWEZE KUTETEA IMANI YA BABU ZETU. Mungu na atusaidie!”
Makasisi hata walichapisha na kugawanya trakti ambayo ilidai kwamba Mashahidi wa Yehova ni “shirika la kisiasa la farakano la kikomunisti.” Lakini hilo pia ni uwongo mkubwa, na labda Warumania wengi wanajua hivyo. Wao wanajua kwamba Mashahidi wa Yehova walinyanyaswa na mara nyingi kufungwa na Wakomunisti katika miaka ambayo imepita.
Jinsi Mitazamo Ilivyoathiriwa
Mateto ya kutoka ndani na nje ya Rumania upesi yakaanza kupinga mashambulizi yenye kuchochewa na kanisa, na maofisa wa serikali waliweza kuona kwamba ni sawa kuwapa Mashahidi mapendeleo ambayo wengine walipewa. Gazeti la habari la Bucharest Flagrant, lilitabiri hivi: “Mwelekeo huu wa uadui, uhasama, na chuki dhidi ya mkusanyiko huu wa kwanza wa kimataifa utatokeza matokeo yaliyo kinyume cha yanayotarajiwa. Badala ya kufanya watu wachukie Mashahidi, hatua hiyo itachochea upendezi, udadisi, uvumilivu, na huruma za watu.”
Utabiri huo ukawa kweli kabisa! Washiriki wengi wa Kanisa Othodoksi waliandika au kupiga simu kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Bucharest na kusema jinsi walivyoudhika na hatua ambazo makasisi wao walichukua. Watu wenye habari wanajua kwamba Mashahidi wa Yehova kamwe hawako kama Kanisa Othodoksi la Rumania linavyowaonyesha kuwa.
Marius Milla, akiandika katika gazeti la habari la Rumania Timishoara, la Julai 6, 1996, alisema hivi: “Nina hakika kwamba asilimia 99 kati ya wale walioshutumu sana Wayehova hawakuwa na upendezi wa kutosha wa kuzungumza nao au wa kuhudhuria mojawapo ya mikutano yao.” Aliongezea: “Lingekuwa jambo bora zaidi kama sisi, waamini wa Othodoksi, tungehangaikia zaidi boriti iliyo katika macho yetu na kuacha unyasi katika jicho la jirani yetu ukahukumiwe na Mungu.”—Mathayo 7:3-5.
Kisha Bw. Milla akanukuu hotuba ambayo wakili maarufu wa karne ya kwanza Gamalieli alitolea viongozi wa kidini waliokuwa wakipinga wafuasi wa Yesu: “Msijiingize katika mambo ya watu hawa, bali waacheni; (kwa sababu, ikiwa mpango huu au kazi hii ni kutoka kwa wanadamu, itapinduliwa; lakini ikiwa ni kutoka kwa Mungu, hamtaweza kuwapindua;) ama sivyo, huenda mkaonwa kuwa wapiganaji dhidi ya Mungu kwa kweli.” (Matendo 5:38, 39) Kwa umalizio, Milla akaandika: “Mtazamo wetu si wa kidemokrasi, si wa kibiblia, na ni wenye kuvuruga jamii.”
Punde si punde, uchambuzi dhidi ya kufutiliwa mbali kwa huo mkusanyiko ukaanza kuja kutoka sehemu nyingine za Ulaya na Marekani. Halmashauri ya Helsinki ya Rumania ilitoa taarifa kwa vyombo vya habari ikishutumu “msimamo wa wazi uliochukuliwa na Mkuu Teoctist, ambaye ni mwakilishi wa Kanisa Othodoksi la Rumania, dhidi ya ‘Mashahidi wa Yehova.’”
Ilitukia kwamba Hillary Clinton, mke wa rais wa Marekani, alikuwa akizuru Rumania wakati huo. Balozi wa Marekani katika Rumania, Alfred Moses, alieleza sababu iliyofanya Bi. Clinton asiingie ndani ya Kanisa la Kretzulescu la karne ya 18 kama alivyokuwa amepanga: “Uhuru wa kidini ni kanuni iliyowekwa na Katiba ya Marekani, na vilevile Katiba ya Rumania. Kuwapo kwa vibandiko katika majengo ya kanisa ambavyo vinaonyesha ukosefu wa ustahimilivu wa kidini hakupatani na demokrasi yenye kukubali wingi na pia hakupatani na makusudi ya ziara ya Bi. Clinton katika Rumania.”
Uthibitisho wa Utegemezo wa Mungu
Mashahidi wa Yehova walipata kufanya mikusanyiko katika jiji la Cluj-Napoca zamani, na maofisa wa huko waliwakaribisha tena waliponyimwa ruhusa ya kutumia Stediamu ya Kitaifa katika Bucharest. Lakini, ilikuwa imebaki juma moja tu kabla ya mkusanyiko uliokuwa umepangwa kuanza ndipo mkataba wa kutumia stediamu katika Cluj-Napoca ulipotiwa sahihi. “Iliwezekanaje kupanga mkusanyiko mkubwa hivyo kwa muda mfupi hivyo?” ripota mmoja alitaka kujua.
“Sisi ni tengenezo lenye muungano,” akaambiwa. “Tumezoea kufanya mikusanyiko. Lakini, zaidi ya yote, Mungu wetu Yehova anatutegemeza.”
Kwa kweli, ilikuwa ni msaada wa Yehova na utegemezo wake kwamba mambo mengi yalitimizwa kwa kipindi kifupi sana. Ebu wazia watu zaidi ya 20,000 wakikusanyika kwa siku tatu baada ya kujulishwa kwa muda mfupi sana! Kilele cha hudhurio kilikuwa 22,004, na 799 wakabatizwa. Gazeti la habari Adevărul de Cluj liliripoti hivi baada ya mkusanyiko: “Wazo unalopata kwa watu hawa ni kwamba sikuzote wao hutabasamu nao hufanya mambo yao yote kwa nafsi yote. Umoja wao ni wenye kuvutia . . . Walionyesha nidhamu ya hali ya juu kwa jinsi walivyoenenda nao walikuwa safi sana.”
Kilichotukia Brasov hasa kilivutia sana, kwa kuwa kibali cha kufanya mkusanyiko kilitolewa siku kadhaa tu kabla ya mkusanyiko uliopangwa kuanza! Na bado, watu 7,500 walipata malazi katika nyumba za watu binafsi. Shahidi mmoja aliposema na mmoja wa majirani wake, hao majirani walikaribisha wajumbe 30. Na kutaniko moja la Mashahidi katika Brasov lilikuwa na wajumbe 500 waliokaa nao. Wajumbe wengine walikaa katika mahema karibu na mahali pa mkusanyiko; na mvua iliponyesha, watu wenye ukaribishaji wageni walio katika nyumba zilizo karibu wakaja na kuwaalika wakae nao katika nyumba zao.—Linganisha Matendo 28:2.
Utendaji wa Mashahidi wa Yehova umewekewa masharti katika Bulgaria ambayo hasa ni ya Othodoksi, nchi hiyo inapakana na Rumania upande wa kusini. Wakati basi zilizojaa Mashahidi wa Bulgaria ziliposhika njia ya kwenda Bucharest, maofisa fulani wa forodha yaonekana tayari walijua kuhusu badiliko la mahali pa mkusanyiko. Katika Brasov jumla ya Wabulgaria 1,056 walifurahia programu yote katika lugha yao wenyewe. Kwa ujumla, watu 12,862 walihudhuria mkusanyiko wa Brasov, na 832—66 kati yao wakiwa Wabulgaria—walibatizwa.
Mnamo Septemba iliwezekana kupanga mikusanyiko midogo katika Baia-Mare na Bucharest kwa ajili ya wale ambao hawangeweza kwenda Cluj-Napoca na Brasov. Jumla ya hudhurio ilikuwa 5,340 katika mikusanyiko hii miwili ya ziada, na 48 wakabatizwa. Basi, katika mikusanyiko ya kiangazi ya “Wajumbe wa Amani ya Kimungu” katika Rumania, jumla ya hudhurio ilikuwa 40,206 na 1,679 wakabatizwa. Kwa kweli Yehova anabariki wale wanaojaribu kumtumikia katika Rumania!
Mwakilishi wa Mashahidi wa Yehova katika Bucharest alisema: “Kwa majuma matatu, tumepata utangazaji unaotoshana na ushahidi wa miaka mingi kotekote nchini. Mbinu ambayo Kanisa Othodoksi la Rumania ilidhani kwamba ingetuzuia kwa hakika imeeneza habari njema.”
[Picha katika ukurasa wa 24]
Bucharest ni jiji maridadi la kisasa
[Picha katika ukurasa wa 25]
Vibandiko vilivyochongea Mashahidi wa Yehova
[Picha katika ukurasa wa 26]
Wenye kutaka kubatizwa katika Bucharest
[Picha katika ukurasa wa 26]
Katika Brasov, ambako kibali cha kufanya mkusanyiko kiliidhinishwa siku kadhaa tu kabla ya mkusanyiko
[Picha katika ukurasa wa 26]
Kilele cha hudhurio kilikuwa 22,004 kwenye mkusanyiko katika Cluj-Napoca