Upendo Wetu kwa Bustani
JE, WEWE hufurahia utulivu wa bustani maridadi ukiwa kimbilio kutoka kwa kelele na hekaheka za maisha? Je, bustani tulivu zenye nyua, maua, miti yenye vivuli, na vidimbwi ndizo mazingira ambayo wewe hupendelea kufanyia mandari na familia yako au kutembea-tembea na rafiki yako? Ndiyo, bustani ni yenye kutuliza, kuburudisha, starehefu, na hata yenye kuponya kama nini!
Ingawa huenda wengine wasipendelee kutunza bustani, labda kwa kukosa wakati, sisi sote hufurahia sana rangi, manukato, kelele, na matunda ya bustani. Thomas Jefferson—ambaye alikuwa msanifuujenzi, mwanasayansi, wakili, mvumbuzi na pia rais wa Marekani—alipenda bustani. Aliandika: “Hakuna kazi inayonipendeza sana kuliko kutunza dunia. . . . Bado nimejitoa kutunza bustani. Na ingawa mimi ni mzee kwa umri, mimi ni mtunza-bustani kijana.”
Watu wengi wana maoni kama yake. Kila mwaka mamilioni ya wageni humiminikia bustani maarufu za ulimwengu—Bustani za Kew (zile Royal Botanic Gardens), Uingereza; bustani zilizo Kyoto, Japani; bustani za Makao ya Kifalme ya Versailles, Ufaransa; Bustani za Longwood, Pennsylvania, Marekani, tukitaja chache tu. Nchi nyingi pia zina maeneo ya majiji ambamo nyumba, zikiwa kandokando za barabara zenye miti, zimezingirwa na vichaka, miti, na maua yenye rangi nyingi sana—kama paradiso ndogo.
Bustani Zaweza Kuendeleza Afya Nzuri
Imeonekana kwamba wanadamu wanapochangamana na ulimwengu wa mambo ya asili, afya zao zaweza kuboreka, ingawa kuchangamana ni kuona tu maua, miti, vichaka, na ndege dirishani. Jambo hilo lilifanya hospitali moja ya New York City kupanda bustani kwenye paa yayo. “Ilipokewa kwa shangwe,” asema ofisa mmoja wa hospitali hiyo. “Hiyo imechochea sana wagonjwa na wafanyakazi. . . . Tunaona kwamba itasaidia sana kiafya.” Kwa kweli, uchunguzi mbalimbali waonyesha kwamba watu wanaweza kunufaika kimwili, kiakili, na kihisia-moyo kwa kutumia hisi zao kwenye mambo ya asili.
Isitoshe, mtu ambaye ana mtazamo wa kiroho huenda akahisi kuwa karibu zaidi na Mungu akiwa katikati ya uumbaji Wake. Jambo hilo kuhusu bustani laweza kufuatiliwa hadi nyuma kwenye bustani ya kwanza kabisa duniani, Bustani ya Edeni, ambako Mungu aliwasiliana na binadamu kwa mara ya kwanza.—Mwanzo 2:15-17; 3:8.
Bustani inapendwa kotekote duniani. Na kama tutakavyoona jambo hilo ni la maana. Kabla ya kuzungumzia jambo hilo, twakualika “kutembea” kwenye bustani chache za kihistoria ili uone jinsi watu wanavyotamani sana Paradiso.