Ni Dini Gani Inayokubaliwa na Mungu?
KWA kuhuzunisha, chuki za kidini za Ufaransa ya karne ya 16 hazikukoma. Katika karne iliyofuata, ubaguzi wa kina uligawanya Ulaya, huku Wakatoliki na Waprotestanti wakienda tena vitani wakati wa Vita vya Miaka Thelathini (1618-1648). Katika jina la Mungu, waliodai kuwa Wakristo walianzisha upya machinjano yao makatili.
Chuki na mauaji ya kidini hayajakoma. Wakatoliki na Waprotestanti hivi majuzi wamechinjana katika Ireland na washiriki wa dini za Othodoksi na Katoliki ya Kiroma wamefanya vivyo hivyo katika eneo la ile iliyokuwa Yugoslavia. Na hata ionekane kuwa jambo lisiloaminika kadiri gani, wakati wa Vita ya Ulimwengu ya 1 na 2, Wakatoliki na vilevile Waprotestanti waliua maelfu ya washiriki wa dini zao wenyewe katika nyanja za mapigano. Je, kuna uteteaji wa haki wa mauaji haya? Maoni ya Mungu ni nini?
Jitihada za Kujitetea
Kile 1995 Britannica Book of the Year hutaarifu hivi: “Vikundi kadhaa vya watu vilijaribu kujitetea kitheolojia katika 1994.” Zaidi ya miaka 1,500 iliyopita, jaribio kama hilo la kutetea mauaji lilifanywa na mwanafalsafa Mkatoliki “Mtakatifu” Augustine. Kulingana na New Catholic Encyclopedia, yeye “alikuwa mwanzilishi wa nadharia ya vita vyenye haki,” na ensaiklopedia hiyo hutaja kwamba kufikiri kwake ‘kuna uvutano hata katika siku za kisasa.’
Makanisa Katoliki, Othodoksi, na Protestanti yameruhusu, na hata kuendeleza, mauaji katika jina la Mungu. Ingawa rekodi ya dini hizo imejaa damu, rekodi ya dini nyinginezo nyingi kotekote ulimwenguni si nzuri. Basi, wawezaje kutambulisha watu ambao wanafuata ibada ya kweli?
Si kwa kusikia tu kile wanachodai kuamini. Kuhusu jambo hilo, Yesu Kristo alionya hivi: “Jihadharini na manabii wasio wa kweli ambao huja kwenu wakiwa wamejificha kama kondoo lakini ndani ni mbwa-mwitu wenye kulafua. Mtaweza kuwajua kwa matunda yao. . . . Mti timamu hutokeza matunda mema lakini mti uliooza matunda mabaya. . . . Mti wowote ambao hautokezi matunda mema hukatwa na kutupwa motoni.” (Italiki ni zetu.)—Mathayo 7:15-20, The New Jerusalem Bible.
Wajulikana kwa Matunda Yao
Mamilioni ya watu wenye kufuatia haki wanatambua kwamba dini za ulimwengu ni ‘miti iliyooza’ ambayo imetokeza “matunda mabaya,” kihususa, kwa kuendeleza vita vyenye umwagikaji wa damu. Katika Biblia milki ya ulimwengu ya dini zisizo za kweli hufafanuliwa kuwa kahaba wa kiroho aitwaye “Babiloni Mkubwa.” Biblia husema kwamba “katika yeye ilipatikana damu ya manabii na ya watakatifu na ya wote wale ambao wamechinjwa juu ya dunia.”—Ufunuo 17:3-6; 18:24.
Hivyo, badala ya kukubali vita ambavyo vimebarikiwa na viongozi wa kidini, Mungu hivi karibuni atatekeleza hukumu juu ya zile dini ambazo zimeua kimakusudi katika jina lake. Atafanya hivyo kwa utimizo wa unabii wa Biblia: “Kwa mtupo wa kasi sana atavurumishwa chini Babiloni lile jiji kubwa, na hatapatikana tena kamwe.” Tukio hilo lenye kufurahisha litakapotukia, Mungu atakuwa “ametekeleza hukumu juu ya kahaba mkubwa” na atakuwa “amelipizia kisasi damu ya watumwa wake mkononi mwake.”—Ufunuo 18:21; 19:2.
Watu ambao huchukizwa na mauaji yote ambayo yameendelea katika jina la Mungu huenda wakajiuliza ikiwa kuna Wakristo ambao kwa hakika huishi kwa kupatana na unabii wa Biblia usemao: “Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.” (Isaya 2:4) Je, wewe wajua watu wanaomhofu Mungu kikweli ambao wamekataa vita?
Dini Inayokubaliwa na Mungu
Uchunguzi wa mahusiano ya kijamii wenye kichwa “Habari Zaidi Kuhusu Kutetea Jeuri,” uliochapishwa na Chuo Kikuu cha Michigan, ulitaarifu hivi: “Tangu kuanza kwa karne hii, Mashahidi wa Yehova wamedumisha daima msimamo wao usio na jeuri wa ‘Kutokuwamo kwa Kikristo’ kupitia vita viwili vikubwa na mapigano yaliyofuata ya kijeshi ya kipindi cha ‘Vita Baridi.’” Ukitambulisha sababu ya Mashahidi kuendelea kutokuwamo, uchunguzi huo ulisema hivi: “Mafundisho ya Mashahidi wa Yehova hutokana na usadikisho wao kwamba Biblia ni neno lililopuliziwa la Mungu.”
Ndiyo, Mashahidi wa Yehova huishi kulingana na Biblia, ambayo hufundisha: ‘Watoto wa Mungu na watoto wa Ibilisi ni dhahiri kwa jambo hili: Kila mtu ambaye haendelezi uadilifu hatokani na Mungu, wala yeye ambaye hapendi ndugu yake. . . . Twapaswa tupendane; si kama Kaini, ambaye . . . alimchinja ndugu yake.’—1 Yohana 3:10-12.
Mara nyingi Mashahidi wa Yehova wameelekeza uangalifu wa watu kwenye hatia ya damu ya dini za ulimwengu. Pia wamerudia ombi la uharaka la Biblia: “Tokeni kwake [Babiloni Mkubwa], watu wangu, ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake, na ikiwa hamtaki kupokea sehemu ya tauni zake. Kwa maana dhambi zake zimetungamana pamoja hadi mbinguni, na Mungu amekumbuka matendo yake yasiyo ya haki.”—Ufunuo 18:4, 5.
Watu wengi wenye moyo mweupe wanatii mwito wa kutoka kwa milki ya ulimwengu ya dini zisizo za kweli. Ikiwa washangazwa sana na mauaji yanayofanywa katika jina la dini, twakualika uwasiliane na mtu aliyekupa gazeti hili au uandike kwa kutumia mojawapo anwani zilizoandaliwa kwenye ukurasa 5. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia ujifunze kuhusu ahadi ya Biblia ya ulimwengu mpya mwadilifu, ambao katika huo hakutakuwa na vita tena kamwe.—Zaburi 46:8, 9; 2 Petro 3:13.
[Picha katika ukurasa wa 10]
“Wao hutangaza hadharani wamjua mungu, lakini wao humkana yeye kwa kazi zao.” TITO 1:16